Dar es Salaam
Na Mathayo Kijazi
Parokia ya Mtakatifu Peter Claver – Mbezi Louis, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, imeadhimisha Jubilei ya Miaka 25, huku Waamini wakiaswa kuepuka dhuluma, kutafuta ukubwa, umaarufu na kutambulika katika jamii.
Askofu Mkuu wa Jimbo hilo, Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Jubilei hiyo, alisema kwamba:
“Hayo ni mahangaiko makubwa ya wanadamu, kupambana kupata ukuu, kupambana kupata umaarufu, kupambana kuwapiku wengine. Na katika kupambana huko, tunaweza tukatendeana visivyo, tukadhulumiana, tukakanyagana, tunaweza tukakuta mtu anatembea juu ya mabega na vichwa vya wengine ili aonekane, atambulike, aheshimike. Ukuu wa kweli hauji kwa kuwapiku wengine, ukuu wa kweli hauji kwa kuwakanyaga wengine,” alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.