Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

Waamini wa Parokia ya Bikira Maria Consolata, Kigamboni, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakiwa katika Sherehe ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Jubilei ya Miaka 50 ya Parokia hiyo iliyoanzishwa mwaka 1973. (Picha zote na Yohana Kasosi)

Wafanyakazi wa Tumaini Media wakifanya Ibada fupi  kwenye Kaburi la aliyekuwa Mkurugenzi wa Tumaini Media, Padri Paul Peter Haule, katika eneo la Makaburi ya Mapadri yaliyoko kwenye Kituo cha Hija Pugu, wakati wa ziara yao ya kiroho ya kutembelea makaburi ya waliokuwa wafanyakazi wenzao.

MWANZA

Na Paul Mabuga

Zamani ukitaka kuijua jamii tunayoisha hapa Bongoland, ilikuwa unatakiwa kutafuta kile kilichomo ndani ya vyombo vya habari, lakini kwa sasa siyo tena kwani huko yamejaa maisha ya kuigiza, bali unatakiwa kupanda daladala na hutanyimwa tafsiri ya namna tunayoishi.
Ndani ya daladala utasikia hapendwi mtu kwa kuwa huko mitaani ndiyo mtindo wa maisha uliopo kwami kinachotawala upendo ni pesa.
Utajua jamii inahalalisha udhalimu kwa kuwa kitanda hakizai haramu na tukiandaa vikao vya harusi vinaendelea mwaka mzima, lakini mafunzo ya wanandoa  tunatamani hata yawe wiki mbili!
Ukizama kwenye vyombo vya habari utaona kila mtu anajua, anakosoa na hata anajadili masuala ambayo yapo juu ya upeo wake, ni kama vile wote wa shahada.
Kila mtu anaonesha maisha ya kuigiza kuliko hali halisi na ukiwatathmini watu kwa yale unayosoma, kusikia na kutazama unaweza kushindia matango pori na kupata uwelewa usio sahihi.
Unapanda daladala kutoka Buswelu kwenda Kemondo katika Jiji la Mwanza, dereva ndiye DJ, na anaweka muziki anaoutaka huku sauti ikiwa juu, abiria wanasikilizana kwa shida, hasa kwa kuwa kila viti viwili, vitatu ni kama Bunge kamili kwani kila seti ina mada ya mjadala  inayoendelea nao.
Wimbo ulioingia zamu ya kupigwa unashusha kutokana na aina ya beti zake ambazo hazina staha kwa waungwana, abiria wanalalamika kwa sauti kubwa na maneno ya beti na wanaomba dereva apunguze sauti, na mzee mmoja anatasema, “angalieni [dereva] alivyonyoa kiduku, kichwa kimekuwa kama mjusi wa rangi!” Dereva anazima kabisa muziki kwa hasira, ni kama abiria wanaifurahia hali ile.
Kiti cha nyuma ni kama mama na wenzake walikuwa wakisubiri muda huo, kwa maneno yake anaonekana kama ni mjasiriamali mdogo na anawaambia wenzake juu ya mumewe ambaye ameondoka kwake na kwenda kukaa kimada kwa mama ntilie.
“Yaani alianza kuwa anachukua nguo moja moja anakwenda na anarudi, na nikaja kugundua hilo na wakati nafikiri nini cha kufanya akaja   ananiambia ana safari na anataka kuchukua begi ambalo nilinunua mimi, nikamwambia we nenda ulikotamani na vitu vyangu pamoja na nguo nilizokununulia acha,’’ anasema Mama yule.
Wenzake wawili katika mjadala huo, wanaonekana kumuunga mkono na wanasema wa namna hiyo hafai!
Inabidi kushangaa, yaani inaonekana kama vile kuachana ni kama kwenda kununua parachichi Manzese na unajihoji hivi hawa huwa hawangalii “Nyumba Amninifu” ya Tumaini TV! Kwa hakika wakiangalia wanaweza kubadili fikra.
“Asikubabaishe huyo, kwa mama ntilie kafuata mapochopocho, akichoka aende zake akafie mbali, hawa ndiyo wale tunaosema wana tabia kama kipepeo, wanatoka ua moja hadi jingine!” kwa lugha ya mjini wanasema walikuwa wanamjaza.
Ni wazi huyu mama hakutayarisha kumtambua mwenza wake, ikiwa ni pamoja na kufahamu wasifu wake wa ndani na nje na kuvitawala vichocheo vinavyomuongoza, [male instincts].
Angepata mafundisho ya ndoa yanayoakisi hali halisi [Biological response] na siyo nadharia za kufikirika bila shaka angeweza kuimudu hali hiyo na ndoa ingeokolewa na hasa kama ingekuwa Takatifu.
Lakini pia ni tatizo hata kwa mwanaume! kwani inaonekana ameingia katika taasisi hiyo takatifu kama vile alikuwa anakwenda disco. Tena diisco toto lile linalopigwa mchana na saa 12 jioni mwisho ili watoto warudi nyumbani.
Kwa bahati mbaya kamati za sherehe za harusi ambazo hudumu hata kwa maandalizi ya mwaka mzima, huwa hazioni kama mafunzo kwa wanandoa ni jambo muhimu na hata halipangiwi bajeti.
Ukienda kwa kile kinachoiwa kitchen party huko mitaani kwetu, na ukasikia wanachokisema ‘masomo’, kama hujapata kiu kwenye baridi kali basi wewe ni mtu tofauti.
Tunaigiza maisha kwa sababu, vijana hawatayarishwi vilivyo katika kuishi kwenye taasisi ya ndoa. Kuna jamaa wameoana miaka mingi na bahati nzuri baada ya kulia kwa kipindi kirefu sasa wamepata mtoto!
Kuoneshwa hawjatayarishwa vya kutosha, hata jina walilompa mtoto wamelitoa kwenye filamu ya katuni. Na kanisani hawakosi kila Dominika.
Mama hajui hata kunyonyesha anategemea aangalie kwenye mitandao, matokeo yake mtoto alimaliza siku kadhaa bila kushiba kwa kuwa alikuwa hawekwi mkao wa kunyonya.
Mtoto alikaribia kupata ulemavu kwa kuwa kwenye mitandao wanakataza kumrusha mtoto atakuwa taahira na alikuwa hata hanyooshwi viungo. Ni hatari!
Yaani vijana wanaojitayarishwa kwa ajili ya ndoa wanataka waishi kama wanayoyaona kwenye runinga, bila kujua kwamba sehemu kubwa wa yale wanayotazama ni maigizo.
Matokeo yake wanakosa kujitambua na umakini na hivyo wanakutana na mazingira yanayowataka kuishi maisha halisi matokeo yake wanakwama.
Wanataka waishi kama wasanii wa muziki ambao nao pia hawaishi maisha yao halisi, kwani kilichopo kwenye vyombo vya habari ni tofauti na yale yaliyopo kwenye familia zao.
Wanapata taarifa ambazo zimepakwa rangi za kupendeza kuliko hali halisi.
Na kimsingi hata wabunge na viongozi wengine wangekuwa wanapanda daladala wangetuwakilisha vilivyo.

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliwaletea Historia ya Dini ilivyokuwa wakati wa Mapinduzi ya Viwanda (Industrial Revolution) barani Ulaya. Leo tunawaletea Misingi na Haki ya Mafundisho ya Kijamii ya Kanisa. Sasa endelea…

Mwaka 1967 Papa Paulo VI (1963-1978: wa 262) alitoa barua yake ya Kichungaji “Populorum Progressio,” yaani ‘Maendeleo ya Binadamu’. Licha ya mengine, alisisitiza kwamba hakuna maendeleo ya kweli, kama siyo ya binadamu wote.
Anasisitiza juu ya wajibu wa mataifa tajiri kusaidia yale maskini. Wakati wa kuadhimisha miaka 80 tangu itolewe barua ya Rerum Novarum Mei mwaka 1891, Papa Paulo VI alitoa barua ya Kitume mwezi Mei 1971 “Octogesima Adveniens”, yaani ”Ujio wa Miaka Themanini”.
Katika barua hiyo, aliongelea hasa hali duni katika miji. Tarehe 26 Oktoba 1975 alitoa barua nyingine ya “Evangelii Nuntiandi”, yaani “Utangazaji wa Injili”, ikiadhimisha miaka 10 ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano (1962-1965), alisisitiza kwamba kazi ya Kanisa ni kupigana dhidi ya uonevu na udhalilishaji.
Papa Yohana Paulo II (1978-2005: wa 264) alitoa barua mbili kukazia mafundisho hayo ya Kanisa juu ya jamii. Mwaka 1981 ikiwa miaka 90 tangu barua ya Rerum Novarum, aliandika barua ya kitume ya “Laborem Exercens” akisisitiza kwamba haki binafsi ya kuwa na mali haipashwi kuathiri umma, yaani haki ya wote kuwa na mali au kukiuka haki za jamii.
Papa Yohana Paulo II alirudia mawazo hayo kwa mkazo zaidi, hasa akikosoa ubepari uliopindukia, na ujamaa hasi katika barua yake nyingine ya kitume “Centesimus Annus” ya mwaka 1991, akiadhimisha miaka 100 ya Rerum Novarum.
Kwa namna hii, unaonekana umuhimu wa barua ya Papa Leo XIII (1878-1903: 256) iliyolitoa Kanisa katika makucha ya mabepari bila kuiingiza katika utumwa wa wajamaa hasi, au ukomunisti. Kabla Papa Yohana Paulo II hajafariki mwaka 2005. ulitolewa muhtasari (Compendium) ya Mafundisho ya Kanisa juu ya jamii.
Papa Benedikto XVI (2005 -2013: wa 265) akifuata katika nyayo za watangulizi wake, mwaka 2009 alitoa barua ya Kitume “Caritas in Veritate”, yaani “Upendo katika Ukweli”.
Licha ya kusisitiza yale yaliyosemwa na watangulizi wake, pia aliisifu hasa barua ya kitume ya Papa Paulo VI ya mwaka 1967” Populorum Progressio” kwa kuongelea, siyo tu juu ya maslahi ya wafanyakazi, bali pia juu ya maendeleo ya binadamu mzima (Integral Developoment).
Papa Benedikto XVI alikosoa sana ubepari, akiuona kukosa utu na kuwa na ubinafsi wa kujitafutia faida kutoka kwa wengine bila kuona wajibu wa kurudisha vilevile kwa jamii. Alisisitiza juu ya haki za jamii kuzidi haki za mtu binafsi kupata faida. Alilaumu ubepari kwa madhara ya siki hizi, yakiwemo vilevile balaa la madawa ya kulevya.
Papa Fransisko (wa sasa: 2013: wa 266), mafundisho yake yote ni juu ya upendo na kujali. Mwaka 2016 alitangaza mwaka wa Huruma ya Mungu na Upatanisho. Mafundisho yote ya wakati huo yalikuwa Mungu atakuhurumia, nawe ukiwahurumia wengine.
“Kuweni na Huruma kama Baba yenu wa Mbunguni alivyo na Huruma.” Katika barua yake ya Kitume “Evangelium Gauduim” au “Furaha ya Injili” ya mwaka 2013, anasihi serikali mbalimbali na vyombo vya kimataifa vya fedha kuhakikisha kuwa watu wanapata haki za msingi, yaani kazi, afya na elimu.
Anakubali haki ya serikali kuingilia uchumi kwa wema wa umma. Anapinga utamaduni wa kuabudu fedha na kuacha soko huria kwa faida ya wachache, wakati wengi wanakuwa fukara. Analaami utofauti unaoongezeka kati ya walionacho na wasionacho.
Katika barua nyingine ya Kitume ya mwaka 2015 “Laudato Si”, ambayo ilipokelewa vizuri sana na watu wa rika na Imani mbalimbali, anaongelea siyo tu juu ya haki ya wanyonge, bali na ulazima wa kutunza mazingira, na kulaani matumizi mabaya ya nyenzo za dunia kwa sababu ya ulafi.
Aliongeza barua nyingine mbili akisisitiza juu ya upendo na kujali; “Gaudete et Exultate” yaani “Furahini na Kushangilia” ya mwaka 2018 na “Fratelli Tutti”, yaani “Sote ni Ndugu”, ya mwaka 2020.
Kanisa katika mafundisho yake ya kijamii katika miaka hii yote, imesisitiza juu ya mambo yafuatayo:

1.    Haki ya Uhai:
    Maisha ya binadamu ni matakatifu tangu kutungwa mimba hadi kifo. Kila binadamu siyo tu ana haki ya kuishi, bali pia ana haki ya kupata heshima. Katika mafundisho yake yote, Kanisa linasisitiza kwamba kila binadamu ameumbwa katika sura ya Mungu, na watu wote wana haki sawa mbele ya Mungu, na hivyo wanastahili heshima.

2.    Auni (Subsidiarity):
    Hii ilisisitizwa hasa kuanzia na barua ya Papa Pio XI ya Quadragesimo Anno mwaka 1931. Madaraka ya juu yasichukue kile ambacho madaraka ya chini yanaweza, na yana haki nacho. Mkubwa asaidie kile ambacho mdogo hawezi peke yake kufanya, la sivyo unamnyang’anya heshima na juhudi zake.

3.    Mshikamamno na kufanya juhudi kwa wema wa wote (Common Good):
    Watu hatuko kisiwa, hivyo lazima kusaidiana kama binafsi, kama junuiya, na kama mataifa.

4.    Upendo ndio upeo wa yote:
    Hapa siyo upendo wa kihisia, bali ni upendo wa kweli wa kujitoa kwa ajili ya wengine.
    Hayo maagizo manne yanakuwa msingi wa haki na wajibu katika Mafundisho ya Kanisa juu ya jamii kama haki ya kupata kazi; haki ya familia; haki ya uhuru wa kuabudu na kuwasiliana; utunzaji wa mazingira; haki ya kuwa na mali binafsi; kujali maskini; na wasiojiweza.

Masista na Waamini wa Parokia ya Mtakatifu Ambrose Tagaste, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakiwa katika Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, iliyofanyika parokiani hapo.

Baadhi ya Vijana waliopata Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, wa parokia ya Mtakatifu Ambrose Tagaste, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakiwa kanisani wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti hiyo.

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, (aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja na Mapadri wa Parokia ya Mtakatifu Ambrose Tagaste, na Viongozi wa Halmashauri ya Walei wa Parokia hiyo, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Kipaimara. (Picha zote na Yohana Kasosi)

DAR ES SALAAM

Na Arone Mpanduka

Tayari mwili wake umelala katika makaburi ya Kijiji cha Mpute huko mkoani Lindi, huku akiacha mabaki ya mtekenyo wa ala tamu za gitaa kwenye masikio ya mashabiki wake wa muziki wa dansi.
Ni ala za tamu na chungu,kwani kila shabiki anayekumbuka jinsi gitaa lilivyotekenywa kwenye wimbo maarufu wa ‘Kisa cha Mpemba’, ama ‘Bwana Kijiko’, anabaki kuwa na huzuni.Mtu huyu si mwingine bali ni marehemu Adolf Mbinga, mtaalamu wa kucharaza gitaa la solo na rhythm.
Mbinga ambaye alizaliwa mwaka 1967, alianza kuupenda muziki tangu akiwa kijijini kwao Mpute ambako mara kadhaa alikuwa akitumika kama miongoni mwa washereheshaji kwenye shughuli za jando, mwanzoni mwa miaka ya 1980.
Alikuwa akitumia sana gitaa la asili lililofungwa na kamba na nyaya katika shughuli hizo za jando.
Baadaye mwaka 1988 akajiongeza na kujiunga na Bendi ya Mondomondo huko Nachingwea.Mwaka 1989 akatua Dar es salaam akitokea ‘bush’ na kujiunga na Bendi ya Biko Stars na hakudumu, kwani mwaka 1992 akatimkia Bendi ya Carnival, na kupewa gitaa la rhythm.
Baadaye akapita bendi zingine nyingi, ikiwemo Diamond Sound, Twanga Pepeta, Mchinga Sound, na nyingine nyingi, ikiwemo Sikinde.
NEEMA
Huu ni wimbo wa kwanza kwa Mbinga kutunga katika maisha yake ya muziki akiwa na bendi ya Diamond Sound. Hiki pia ni kisa cha kweli ambacho kilimtokea mwenyewe wakati akiishi geto pale Kinondoni. Alimpata msichana kwa lengo la kuishi naye, lakini alimkimbia kwa sababu hakuwa na pesa.
Wimbo huo aliutunga mwaka 1996 akiwa na Diamond Sound, maarufu kama wana Kibinda Nkoi, ambao miaka hiyo ndiyo walioanza kuichangamsha nchi kwa miziki ya dansi la kizazi kipya.
KISA CHA MPEMBA
‘Kisa cha Mpemba’ ni miongoni kwa nyimbo maarufu kutunga akiwa Twanga Pepeta, na uliompa umaarufu. Wimbo huu ulitengenezwa mwaka 1998 katika studio za MJ Records (Master J). Hiki ni kisa cha kweli kabisa ambacho kilitokea Tabata ambapo Mbinga alishuhudia purukushani ya muuza duka mmoja (Mpemba) aliyepata sekeseke kutoka kwa jamaa ambaye mkewe alikuwa anapewa vyakula vingi kutoka duka la Mpemba huyo, kuliko thamani ya pesa aliyoacha.
Mbinga akatumia kisa hicho na kutengeneza wimbo ambao ndani yake aliongeza vionjo.
MTUHUMIWA
Mtuhumiwa si wimbo bali ni jina la utani alilopewa na wenzake mara baada ya kuiasi bendi ya Mchinga Sound.
Ikumbukwe kwamba mwaka 2000, Mbinga aliondoka ghafla katika bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’ na kwenda kumshawishi Mheshimiwa Mudhihiri Mudhihiri ambaye alikuwa Waziri kwa wakati huo, aanzishe bendi yake ambaye naye alikubali na kununua vifaa vya muziki.
Baada ya ushawishi huo kukubalika, ndipo wakaunda bendi ya Mchinga Sound ambayo ndani yake alikuwemo Mbinga mwenyewe, Mwinjuma Muumini, Deo Mwanambilimbi, Roshi Mselela, Rogart Hega Katapila, na wengine wengi.
Mbinga alitoka na tungo iitwayo ‘Kidomodomo’ambayo aliitunga akiwa Twanga Pepeta na kwenda kuirekodi Mchinga, na kufuatiwa na nyimbo zingine nzuri kama Kisiki cha Mpingo, na Fadhila kwa Wazazi.
Nyimbo zote za Mchinga Sound, kazi za kurekodi gitaa la solo na rhythm zilifanywa studio na Mbinga mwenyewe.
Wakati Mchinga Sound ilipokolea na kuwa maarufu nchini, ghafla Mbinga ambaye alikuwa kiongozi mkuu, aliondoka kwenye bendi hiyo na kurudi Twanga Pepeta. Kwa tafsiri nyingine ni kama alimuacha kwenye mataa Mheshimiwa Mudhihiri asijue nini cha kufanya, hasa ikizingatiwa alikuwa hajui lolote kuhusu masuala ya muziki, ikiwemo kuongoza bendi.
Hicho ndicho kikawa chanzo cha bendi hiyo kuvunjika na kusambaratika, kwani wanamuziki wengine wote waliondoka na kwenda kwenye bendi zingine.
Aliporudi Twanga Pepeta, wanamuziki wenzake walimpa Mbinga jina la mtuhumiwa wakiamini kwamba Mheshimiwa Mudhihiri alimtuhumu kwa usaliti wa bendi ya Mchinga Sound.
Hivyo, Mbinga ameondoka duniani akiwa ameacha majina ya utani ya ‘Mtuhumiwa’ na ‘Chinga One’.Jina la Chinga One lilitokana na kabila lake la Kimakonde.
KIFO CHAKE
Mwanzoni mwa mwaka huu, Mbinga aligundulika kwamba anaumwa mara baada ya ndugu, jamaa na marafiki kubaini kutetereka kwa afya yake.
Inaelezwa kwamba alikuwa akiumwa kwa muda mrefu ugonjwa ambao mwenywe hakutaka kuuweka hadharani, lakini aliwaficha hata ndugu na jamaa hadi kufikia katika hali mbaya.Jambo baya zaidi, alikuwa hataki kutumia dawa alizokuwa anapewa hospitalini.
Kufuatia hali yake kuwa mbaya zaidi, ilifikia hatua ikabidi asafirishwe kurudishwa kijijini kwao Mpute, ambako usiku wa Juni 15 mwaka huu, alifariki dunia na kuzikwa Juni 17.

LONDON, England
Dillian Whyte yuko tayari kwa mechi ya marudiano na mpinzani wa uzito wa juu wa Uingereza, Anthony Joshua, katika ukumbi wa O2 Arena, Agosti 12 mwaka huu, lakini kifungu cha marudiano ya pambano hilo, ni mazungumzo magumu.
Whyte ambaye ni mwana masumbwi mahiri na alimshinda Joshua, kabla ya AJ kumshinda mwaka 2015 na sasa Whyte bado anataka nafasi ya kulipiza kisasi hasara hiyo.
Whyte alianza tena mazungumzo wiki jana baada ya kumpinga kwa maneno promota Eddie Hearn kuhusu kukatika kwa mawasiliano kuhusu mechi ya marudiano inayotarajiwa kuwa kubwa, ambayo inatarajiwa kuandaliwa katika uwanja wa The O2 mnamo Agosti 12.
Whyte ana ushindani wa muda mrefu na Joshua na alimshinda AJ kama mwanariadha, kabla ya Joshua kushinda medali ya dhahabu ya Olimpiki huko London mwaka 2012.
Na Joshua tayari amekuwa akihusishwa na pambano linalotarajiwa kupigwa na Deontay Wilder, litakalofanyika Mashariki ya Kati baadaye mwaka huu.

Nottingham, England
Andy Murray anajiandaa kwa Wimbledon yake ya 15, itakayoanza Julai 3 mwaka huu, huku nyota huyo mwenye umri wa miaka 36, lakini hatazami kustaafu hivi karibuni.
Andy Murray anatumaini Wimbledon ya mwaka huu haitakuwa yake ya mwisho, akisema kwamba anataka kujituma kwa kucheza kwa kiwango cha juu sana kabla ya kutundika daluga lake.
Murray alitolewa katika robo fainali na Sam Querrey huko Wimbledon mnamo 2017, na kazi yake ilionekana kuwa mwisho baada ya kutolewa kwenye Australian Open mnamo mwaka 2019, lakini upasuaji wa kurekebisha nyonga yake ulimpa nafasi ya pili mchezaji huyo wa zamani wa Ulimwengu.
Ushindi wa mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 36 katika michuano ya hivi majuzi ya Nottingham Challenger, ulimpeleka kwenye cheo chake cha juu zaidi tangu upasuaji wake wa nyonga akiwa nambari 38 duniani.
Murray aliorodheshwa katika nafasi ya 839 duniani mnamo Julai 2018 alipopata nafuu baada ya upasuaji wake wa kwanza wa nyonga, kushindana na Grand Slams tena kulionekana kuwa tumaini la kusikitisha, lakini amepambana, na sasa ana matumaini makubwa ya kushindana tena katika daraja la juu la mchezo huo.