Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha
Makala

Makala (58)

TAFAKARI SOMO LA INJILI DOMINIKA YA 19

Amani na Salama!
“Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye, hataona kiu kamwe.” Haya ndiyo maneno ya hitimisho la somo la Injili ya Dominika iliyopita. Yesu anajitambulisha kwa wasikilizaji wake kwa namna ambayo iliwakwaza, ni maneno yaliyoweka imani yao njia panda, na hapa ndipo tunaona wasikilizaji wake ambao Mwinjili anawatambulisha kama “Wayahudi,” walimnung’unikia Yesu kutokana na maneno hayo.
Wayahudi waliamini kuwa na ukweli wote, na ndiyo Torati na Manabii. “Atamlisha mkate wa ufahamu, na kumnywesha maji ya hekima.” (Yoshua bin Sira, 15:3) Hivyo, ndiyo kusema kuwa mkate wa uzima ni Neno la Mungu ambalo Wayahudi waliamini kuwa nalo katika ukamilifu wake, ndiyo Torati na Manabii na Vitabu vingine vya Maandiko Matakatifu.
Kwao ilikuwa ni makwazo makubwa, kwani Yesu leo anajitambulisha kuwa ni Yeye aliye mkate wa uzima wa milele utokao mbinguni, ni kwa kulisikiliza na kulishika Neno lake, kila mwenye njaa na kiu atashibishwa, na hivyo hataona njaa wala kiu tena.
Wayahudi walishindwa kuupokea utambulisho wa Yesu kama chakula cha uzima, na wakabaki kumwona kama mwana wa Yusufu tu, na tena waliyemfahamu vyema hata kazi na ujira wake kuwa ni ule duni kabisa, na zaidi sana hata mama yake pia walimfahamu. Ni watu waliomfahamu vyema na vizuri, na kwa nini basi anajitambulisha na kujifananisha kuwa ni Mungu, ni kutoka mbinguni?
“Wakasema, huyu siye Yesu, mwana wa Yusufu, ambaye twamjua babaye na mamaye? Sasa asemaje huyu, ameshuka kutoka mbinguni?” Na tunasikia manung’uniko haya hawakumwelekezea Yesu, bali yalikuwepo baina yao, miongoni mwao, kati yao wenyewe.
Kunung’unika siyo kitendo kile cha kulalamika tu. Naomba kieleweke, na Mwinjili anakitumia kitenzi hicho kuonesha mkwamo wao wa kiimani, kukwazika na kujikwaa kwao kwa fundisho lenye utambulisho mpya kumhusu Yesu, utambulisho ambao unamfunua Yesu kuwa si tu mwanadamu kweli, bali pia ni Mungu kweli, ametoka kwa Mungu, amekuja kuifunua katika ukamilifu sura halisi ya Mungu. Kwao haikuwa jambo rahisi na lenye kueleweka kuwa kwa njia ya Yesu, hekima ya Mungu imejimwilisha na kukaa kati yao, na kuwa katikati yao. Soma zaidi Tumaini Letu.

Amani na Salama! Tumekuwa tukisoma na kutafakari Injili ya Marko, leo Liturjia inatualika kugeukia Injili ya Yohane na hasa sura ile maarufu ya sita, juu ya Yesu kama chakula cha uzima. Mwaka B wa Kiliturjia wa Kanisa kwa kawaida tunasoma Injili ya Marko, lakini Liturjia ya Mama Kanisa ameingiza pia Injili ya Yohane sura ile ya sita kwa Dominika tano mfululizo. Injili ya Marko inatupa masimulizi mawili juu ya muujiza wa Yesu kulisha makutano mikate. Na ndipo tunaona kwa jinsi anavyotoa mkazo na msisitizo huo, hapo Mama Kanisa ameona ili kupata mafundisho ya kina hatuna budi kugeukia sura ya sita ya Injili ya Yohane. Leo tunasikia juu ya muujiza ule wa kugawa mikate kwa watu wengi, na baadaye zaidi katika dominika zijazo tutasikia juu ya mafundisho ya Yesu mkate wa uzima, aliyoyatoa akiwa katika sinagogi la Kapernaumu.
Ni vema ili kupata ujumbe kusudiwa wa Mwinjili Yohane, badala ya kuwahi kuhitimisha juu ya fundisho la Yesu la Ekaristi Takatifu, ambalo kwa kweli linagusiwa sio mwanzoni mwa sura ile ya sita bali mwishoni kabisa, hivyo niwaalike kusoma na kubaki na kile ambacho kipo mbele yetu ili kukwepa kupotoka au kupata maana inayokuwa siyo ile inayokusudiwa na Mwinjili.
Kati ya miujiza iliyofanywa na Bwana wetu Yesu Kristo, ni muujiza huu wa kugawa mikate unaosimuliwa mara nyingi zaidi na Wainjili wote wanne. Wainjili wote haidhuru mara moja wanatupa masimulizi ya muujiza huu, na Wainjili Matayo na Marko wanasimulia mara mbili juu ya muujiza huu, hivyo kufanya masimulizi juu ya kugawa mikate kuwa sita.
Na ndio hapo tunaweza kujiuliza, kwa nini Kanisa lile la mwanzo linatoa msisitizo mkubwa kabisa juu ya muujiza huu? Yesu alitenda miujiza mingine mingi tena mikubwa zaidi, lakini kwa nini Wainjili wote wanne wanatoa mkazo na msisitizo mkubwa kwa muujiza huu? Na kama ndivyo, kwa nini basi miujiza mingine inasimuliwa mara moja peke yake tofauti na muujiza huu wa leo?
Muujiza wa mikate kama unavyosimuliwa na Mwinjili Yohane ni tofauti na jinsi inavyosimuliwa na Wainjili wengine. Na ndio mwaliko wangu leo kujaribu kuingia ndani ya Injili hii ili tuweze kwa pamoja kuchota ujumbe unaokusudiwa kwetu. Na ndio tunaona pia Mama Kanisa ameingiza sura ile ya sita ya Injili ya Yohane kwa Dominika tano mfululizo, ili tuweze kuchota mafundisho ya kina kabisa juu ya utambulisho wa Yesu kama mkate wa uzima.
Tafakari hizi zitusaidie na kutusindikiza tunapoelekea kwenye kilele cha Kongamano la Ekaristi Takatifu Kitaifa hapo Septemba katika Jimbo Kuu la Dar es Salaam. Yesu wa Ekaristi Takatifu ni nani haswa katika maisha yako na yangu, katika maisha ya kila mwamini na kwa Kanisa kiujumla. Mababa wa Mtaguso wa II wa Vatikano wanatualika kuona Ekaristi Takatifu kama chemuchemu na kilele cha maisha ya Kanisa. Ni Ekaristi Takatifu inayolifanya Kanisa liwepo, na Kanisa linadumu hata ukamilifu wa dahari kwa kuadhimisha Ekaristi Takatifu.
Kwanza yafaa kutambua kuwa Mwinjili Yohane hauiti kama muujiza bali kama ishara, na pia hatusikii moja kwa moja kuwa Yesu aliifanya mikate na samaki kuwa mingi na wengi ili kuwatosha watu wote, na badala yake ni mikate ile ile na samaki wale wale kidogo waliwekwa kwa ajili ya wote mpaka kila mmoja akapata kadri ya haja na mahitaji yake na hata kusaza.
Na bado wakaweza kukusanya mabaki vikapu kumi na viwili vya mikate, ndio kusema waliweza kupata kila mmoja na bado hawakuweza kumaliza chote kilichowekwa mbele yao. Hivyo tunaona mara moja msisitizo wa somo la Injili ya leo haupo katika ongezeko la mikate wala samaki, na badala yake moyo na roho ile ya kushirikiana kidogo kinachokuwepo kwa wote kadri ya uhitaji wa kila mmoja wetu.
Falsafa ya ulimwengu wa leo ni kuwa na kila kitu kwa wingi katika maisha, iwe ni pesa, afya, elimu, miaka ya kuishi, marafiki, mafanikio, na kadhalika na kadhalika. Na huu ndio ugonjwa wa wengi wetu, wa kujikusanyia, wa kujilimbikizia, wa kujijali na wenye kutaka na kusaka zaidi na zaidi. Ugonjwa huu wa kujilimbikia unaakisi hasa utamaduni wa kifo, unaotokana na maisha yenye kujaa hofu ya kifo, na ndio dalili ya wazi ya kukosa imani, kwani tunakuwa watumwa wa vitu na mali na badala ya kuwekeza katika upendo kwa Mungu na kwa jirani.
Somo la Injili ya leo, Yesu anatufundisha juu ya ugonjwa huu wa kujilimbikizia na kujikusanyia kila kitu, ugonjwa wa kutaka zaidi na zaidi katika maisha, ni njaa ya vitu na mali.Yesu leo anatupa dawa ya ugonjwa wetu huu, dawa ambayo ni kinyume kabisa na mantiki na utamaduni na falsafa ya ulimwengu wetu, Yesu leo anatuonesha njia salama na sahihi ya ugonjwa wa ubinafsi na umimi ni ile ya kushirikiana sote kwa pamoja bila ubaguzi kidogo kinachokuwepo mbele yetu.
Pasaka, ndiyo sikukuu ya Wayahudi ilikuwa karibu. Mwinjili Yohane anatuonesha ni wakati gani Yesu alitenda ishara ile. Ndio kusema mazingira yalikuwa ni pale walipokumbuka kukombolewa kwao kutoka utumwani Misri.
Ndiyo kusema Mwinjili anajaribu kuoanisha na kuhusianisha tukio la ishara ya mikate, pamoja na tukio la kihistoria la kutoka utumwani Misri. Yesu leo anavuka kama vile Musa alivyowavusha Wanawaisraeli katika bahari ile ya Shamu, na ndipo tunaona leo hakuna chombo kinachotajwa kumvusha Yesu.
Kama vile Musa alivyowaongoza watu wengi, ndivyo na Yesu leo wanamkusanyikia watu wengi na hapo anatenda ishara kama vile Musa nyakati za kuwakomboa Wanawaisraeli. Mara mbili Yesu anapanda juu mlimani, ni kama Musa alivyokuwa akipanda juu mlimani na huko kupokea maagizo ya jinsi ya kuliongoza taifa lile teule.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

”Zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni muhimu sana katika kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuendeshwa kwa misingi ya kidemokrasia”.
Kauli hii ilitolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika hotuba yake ya  uzinduzi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura  Mkoani Kigoma uliofanyika kwenye uwanja wa Kawawa katikaka Manispaa ya Kigoma  - Ujiji, Julai 20, 2024.
Uboreshaji huo utafanyika katika mizunguko 13, na mzunguko wa kwanza unahusisha Mikoa mitatu ya Kigoma, Tabora na Katavi, kisha Geita na Kagera, ikifuatiwa na Mwanza, Shinyanga na baadae Mara, Simiyu na sehemu ya Mkoa wa Manyara.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa zoezi hilo lina lengo la kuhakikisha wananchi wote wenye sifa wanapata na kutumia haki yao ya kikatiba ya kupiga kura kama ilivyobainishwa kwenye Ibara ya 5 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
”Vile vile, umuhimu wa zoezi hili unatokana na ukweli kwamba hii ni hatua muhimu ya maandalizi ya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika mwaka 2025 hapa nchini. Pia kutokana na uwepo wa kundi kubwa la wananchi waliopata sifa ya kiumri tangu uchaguzi uliopita, zoezi hili ni muhimu kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya”.
Akieleza kuhusu umuhimu zoezi hilo Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa maboresho ya daftari la mpiga kura, mbali ya kuandikisha wapiga kura wapya, pia yanalenga kutoa fursa muhimu kwa wapiga kura ambao kwa sababu moja au nyingine, kadi zao za mpiga kura zimepotea au kuharibika, au wamehama kutoka eneo moja la uchaguzi kwenda jingine waboreshewe taarifa zao ili wawe na sifa za kuwawezesha kupiga kura katika uchagu ujao wa Rais, Wabunge na Madiwani.
Aliwataka wote waliohama kutoka kwenye vituo vyao vya kupigia kura au kupoteza  kadi zao, kufika kwenye vituo vya kuandikisha wapiga kura ili kuboresha taarifa zao na kupatiwa kadi mpya zitakazowawezesha kupiga kura.
Alisisitiza kuwa kwa mujibu wa Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022; inakadiriwa kuwa jumla ya wapiga kura wapya 5,586,433 wataandikishwa, wakiwemo waliotimiza umri wa miaka 18 katika kipindi cha kuanzia mwaka 2020 baada ya uchaguzi mkuu uliopita, na ambao watatimiza umri huo ifikapo tarehe ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. ”Kwa mujibu wa taarifa za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, inakadiriwa kuwa wapiga kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao”.
Idadi hii siyo ndogo kwenye zoezi la kupiga kura. Hivyo, nitoe rai kwa kila mpiga kura aliyeandikishwa mwenye uhitaji wa kuboresha taarifa, iwe kwa kurekebisha taarifa au kuhama kutoka eneo moja la uchaguzi kwenda lingine, asisite kufika katika kituo cha kuandikisha, kwani Tume imeshajipanga ili kuhakikisha wananchi wote wanafikiwa.
Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa ili kufanikisha zoezi hili, kila Mtanzania, Asasi za Kiraia, Vyama vya Siasa, Jeshi la Magereza na Vyuo vya Mafunzo, Vyombo vya Habari, Mawakala Vyama vya Siasa na Watendaji wa walioteuliwa na Tume, wanapswa kutimiza wajibu wao ili zoezi hili liweze kufanikiwa.
Wajibu wa kila Mtanzania:
Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa kila Mtanzania ashiriki katika usimamizi wa suala hilo, kwani wanaotakiwa kuandikishwa ni raia wa Tanzania tu wenye sifa zilizobainishwa kwa mujibu wa sheria. ”Wananchi ni watambuzi wa kwanza, niwasihi sana tuwe wazalendo, huu ni wajibu wa raia wa Tanzania kuhakikisha wanaoandikishwa ni Watanzania tu”.
Jeshi la Magereza, vyuo vya Mafunzo na Uhamiaji:
Hapa Waziiri Mkuu anasema kuwa, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa pamoja na Uchaguzi Mkuu, umeongeza kundi jingine ambalo ni wafungwa wanaotumikia vifungo vya chini ya miezi sita gerezani, au kwenye vyuo vya Mafunzo na mahabusu hawa wote watapata nafasi ya kupiga kura. Hivyo Jeshi la Magereza na upande wa Zanzibar Vyuo vya Mafunzo wanawajibika kuweka miundombinu wezeshi ili Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi iweze kutekeleza wajibu huo kwa ufanisi.
Aidha, Jeshi la Uhamiaji liwajibike kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kuwatambua na kutoa taarifa za uwepo wa mtu au watu ambao sio raia wa Tanzania, walioandikishwa tayari, au wanaopanga kwenda kuandikishwa, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa mapema dhidi yao.
Wajibu wa Vyama vya Siasa  Majaliwa anatoa rai kwa viongozi wa Vyama vya Siasa kuhakikisha mawakala wao wanatoka kwenye mitaa, Kijiji na shehia husika ili waweze kutimiza wajibu wao wa kisheria wa kuwatambua watu wenye sifa za kuandikishwa kuwa wapiga kura.
Mawakala wa Vyama vya Siasa:
Anasema kuwa kwa upande wa mawakala watakaoteuliwa na Vyama vya Siasa, wanao wajibu wa kutambua watu wenye sifa za kuandikishwa wanaofika kwenye vituo kwa ajili ya kuandikishwa kuwa wapigakura.
Watendaji walioteuliwa na Tume:
”Ninawasihi sana watendaji walioteuliwa na kuanzia ngazi ya Mkoa, Jimbo, Kata na Kituo cha kuandikisha wapiga kura kuwa waadilifu, na watangulize uzalendo kwa kutotoa fursa kwa watu ambao hawana sifa za kushiriki katika uboreshaji. Kila mmoja ajitume, afanye kazi kwa weledi na kutumia lugha nzuri kwa wananchi wanaokuja kujiandikisha”.
Taasisi na Asasi za Kiraia
Anasema kuwa eneo jingine muhimu ni suala la utoaji wa elimu ya mpiga kura, ambapo alizitaka taasisi na asasi zote zilizopewa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura kutekeleza zoezi kwa weledi, na wasiingize vitu ambavyo havitakiwi, na ambavyo havipo kwenye makubaliano.
”Wakati wa zoezi hili la uboreshaji daftari la mpiga kura, , hakikisheni mnatekeleza kazi zenu kwa kuzingatia masharti ya vibali na miongozo iliyotolewa na itakayotolewa na Tume. Ni vema wakati wote taasisi ziepuke kufanya masuala ambayo hayamo kwenye miongozo waliyopewa kwa mujibu wa vibali vyao”.
Vyombo vya Habari:  Alisema kuwa Vyombo vya Habari vinao wajibu wa kutumia kalamu zao, kuwakumbusha wadau wa uboreshaji kutumia taratibu zilizoainishwa kwenye sheria, kanuni na miongozo, kutatua au kuwasilisha malalamiko iwapo kutajitokeza changamoto ya aina yoyote wakati wa uendeshaji wa zoezi hili.
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa aliwahakikishia Watanzania kuwa  Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amedhamiria kuhakikisha kuwa Uchaguzi unakuwa wa huru na haki.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Ummy Nderiandanga, alisema kuwa uzinduzi wa uandikishaji na uboreshaji, mchakato huo umeshirikisha wadau mbalimbali wa uchaguzi, ikiwa ni utekelezaji wa falsafa ya 4R za Rais  Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Tume imekutana na wadau wa makundi mbalimbali kama vile Vyama vya Siasa, Asasi za Kiraia,Viongozi wa Dini, Makundi Maalum kama vile Vijana, Wanawake na Watu wenye Ulemavu. Lengo ni kuhakikisha kuwa mchakato huu unakuwa shirikishi kwa Watanzania wote bila kujali itikadi za Vyama vya Siasa au Dini”
Naye Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Jacobs Mwambegele alisema kuwa jumla ya vituo 40,126 vitatumika katika Zoezi la Uboreshaji wa Daftari, ambapo kati ya hivyo, vituo 39,709 vipo Tanzania Bara, na vituo 417 vipo Tanzania Zanzibar.

UNGUJA

Na Paul Mabuga

Unaweza kusema kuwa kijiji cha Paje kule Unguja  ni mahali ambapo tamaduni zinapambana ili kuleta moja inayowakilisha mchanganyiko wa watu wanaoishi hapo wakiwa ni wageni wa muda kama watalii, wengine walioamua kuhamia,  na pia wenyeji.

Wakati maeneo mengine ya Unguja, kama Tumbatu na Makunduchi yakipambana na kuhifadhi tamaduni na hasa mila, desturi na historia, Paje inazidi kukaribisha na kukumbatia mchanganyiko wa amali hizo za maisha na kupata kile kinachoitwa ‘cultural amalgamation’.

Ni rahisi kutambua hili, kwani unapokuwa pale Unguja, utashuhudia mji ukijitambulisha kwa mavazi, ambayo kwa akina mama, kama siyo baibui, basi ni nguo ndefu inayofunika mwili na kichwa, huku wanaume wakiwa katika kanzu, ama hata kama ni shati na suruali, kibagarashia  na makubasi, basi ni katika mtindo unaoashiria ustaarabu wa Kizanzibari.

Lakini ukipanda zile daladala za mbao na kusafiri kwa saa nzima hadi  Paje, utakaribishwa mji unaonekana mkiwa umepoa kwa mchana lakini wenye mambo makubwa kinapoingia kiza. Pamoja na kuwa ni kama kijiji, lakini kuna hoteli zaidi ya 35, hizi zote pamoja na malazi na chakula, lakini pia zinatoa burudani mbali mbali kwa watalii, wahamiaji na wenyeji pia.

Paje inapendelewa na wageni wengi wakiwemo watalii, kutokana na fukwe yake kuwa mahali salama kwa kuogelea, na hata kutiara  kwenye maji [kiteboating] na kuwepo kwa maji ‘meupe’.  Wingi wa migahawa na hoteli pia unawafanya  wageni kuvutiwa ma machaguo kulingana na uwezi wao kifedha. Wapo wanaoona heri wafanye huko makazi na kwenda kutembelea vuvutio vya Unguja, na kurudi huko kwa malazi.

Kutokana na mazingira haya, kuna wahamiaji wengi wameingia Paje kwa ajili ya ajira katika sekta ya huduma na biashara, wao ukichanganya na watalii na wenyeji, unapata mchanganyiko wa tamaduni ambazo ni dhahiri kupitia mavazi, lugha na mitindo ya maisha. Mavazi unayoyaona Paje ni nadra kuyaona katika miji kama Unguja, Makunduchi ama Wete.

Katikati ya kuchangamka huko akina mama wameanzisha kikundi cha ujasiriamali ili kufaidika na fursa katika kijiji cha Paje. Walikianzisha mwaka 2011, na wanakiita ‘Furahia Mwanamke’, na wanajishughulisha na kuzalisha na kuuza zao la baharini la mwani.

“Nimefanya kazi kwa miaka 40, lakini tangu tumejiunga na kikundi, niseme tu, mazingira ya biashara ni mazuri, na karibu sisi hivi siyo tegemezi tena, maana mwani una soko kutokana na thamani yake ya virutubisho muhimu,” anasema Hifadhi Ally, mmoja wa wanachama wa kikundi.

Akina mama hawa wameweka hata duka lao hapo Paje, wakiuza bidhaa mbali mbali zinazotokana na mwani, ikiwa ni pamoja na unga, ambao thamani yake inafika hadi shilingi elfu arobaini kwa kilo moja, mafuta ya kupaka, sabuni, pamoja na dawa za mafua.

“Kuna changamoto kadhaa katika biashara zetu, ikiwa ni pamoja na magonjwa kwa mmea wenyewe, na wakati mwingine bei kupungua. Ilifika hadi shilingi 50,000 kwa kilo, lakini sasa hivi bei imeteremka. Ila tunashukuru tunasomesha watoto, na hata tuna mashine ya kusaga mwani,” anasema mwanachama mwingine wa kikundi hicho,Tano Hassan.

Artifisha Abdul Harim, yeye amepata ajira ya kuuza duka la bidhaa za mwani la umoja wa akina mama hawa ambao anasema kwa idadi wapo 34. Katika duka hilo kuna bidhaa nyingi za mwani na kinachovutia kuna mwani wenye rangi nyekundu, mwingine kijani na ipo ya rangi nyeupe pia. Na hizi rangi ni za mimea yenyewe.

Mwani wanaupanda baharini na hutegemea kupwa na kujaa kwake, na kwamba wakati mwingine katika jua kali, kilimo chao huathiriwa. Wanasema kwamba kwa sasa kilimo hicho kimekuwa na faida kidogo kutokana na gharama yake ya uzalishaji kuwa kubwa.

Licha ya malalamiko haya kutokana na akina mama hawa, lakini bado Zanzibat ni nchi ya nane duniani kwa uzalishaji wa zao hilo, na katika hali ya ubora. Na wanakikundi wana msemo wao kwamba “mwani ni pesa, mwani ni chakula, mwani ni zawadi kutoka kwa Mungu.”

“Mwani una sifa nyingi. Sabuni ya mwani ni nzuri kwa watoto na hata kupaka kabla ya kunyoa nywele ama ndevu kwa kuwa inafanya mwili kuwa laini. Pia karajina [unga wake] Unaweza kuchanganywa kwenye sharubati [juisi], tambi, chachandu, kachumbari na kuleta ladha ya kuvutia,” anasema Artifisha.

Paje inajiweka mahala pema, kwani wakati akina mama hawa wanachangamka na mwani, huku utalii nao ukichagiza biashara, lakini pia una nafasi katika maendeleo ya uchumi wa bluu, ambao serikali ya Zanzibar imeiweka kama ajenda yake ya kipaumbele.

Kilimo cha mwani ambacho kwa sehemu kubwa kinaendeshwa na akina mama,  kinatajwa katika na ripoti ya umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara kuwa kimechangia pakubwa katika kuifanya Zanzibar kuelekea kuyafikia Malengo ya Milenia ambayo, pamoja na mambo mengine, yanalenga kupambana na umaskini, na hivyo kuboresha hali za wanawake na watoto.

Mafanikio haya yanapatikana ingawa ripoti hiyo inaonesha kuwa kuna kushuka katika rekodi kwa uzalishaji wa mwani kutoka tani 178,000 mwaka 2016 hadi 81,000 ilipofika mwaka 2021. Lakini hata hivyo, bado zao hilo limeendelea kuwa na mchango mkubwa, huku likitoa ajira kwa akina mama zaidi ya 400 visiwani humo.

Ukiacha Paje, kuna kijiji kinaitwa Makunduchi, huko utamkuta Bibi Nali Kombo! Yeye anakuonesha kuwa unahitaji kujifunza Kiswahili, kwani akikusemesha anakutaka uitikie ‘enhee’, na wala siyo kuitikia kwa kichwa ama kuguna, huko ni kukosa nidhamu.

“Hano pa, swalaa swalaa hiyo” anakuambia, pengine akimaanisha, ‘ameamka alfajiri’, na zaidi anakujibu kwa swali lako la kutaka kujua jinsi huduma bora za afya zilivyomsaidia kupambana na shinikizo kubwa la damu, “dawa maungoni zinaingia, upo!” Anakuona kama unazubaa kidogo, kisha anakuambia, “ useme enhee!”

HISTORIA YA KANISA

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita tuliwaletea mada ya historia ya uinjilishaji katika nchi ya Rwanda. Leo tunaendelea kuwaletea historia ya uinjilishaji nchini Burundi na Kongo Brazaville. Sasa endelea…

Wamisionari wa kwanza, Wamisionari wa Afrika, walifika Burundi kutokea Ujiji, Tanzania, mwaka 1879 wakingozwa na Padre Deniaud, na kufungua misioni Rumonge. Lakini mwaka 1881 kwa chuki ya Waarabu wakishirikiana na baadhi ay Waafrika, walimwua Padri na wenzake wawili. Hapo ikabidi misioni isitishwe. Sehemu ya Burundi walibaki Kibanga ukingoni mwa Ziwa Tanganyika.
Mwaka 1895 Burundi iliunganishwa na Vikariati ya Unyanyembe, Tanganyika.  Parokia za kwanza zilifunguliwa ni Muyinga mwaka 1898 na Mugera mwaka 1899. Historia ya mwanzo ya Burundi ilienda sambamba na historia ya Rwanda.
Mwaka (1912-1922), ziliunganisjwa katika Vikariati moja ya Ruvu, chini ya Askofu Hirth. Jamii ya Burundi ilikuwa na mshikamano mkubwa kuliko ule wa Rwanda. Vile vile kati ya watawala, licha ya Watutsi yalikuwepo makabila mengine mawili, Bahima ambao ni ukoo mmojawapo wa Watutsi, na Ganwa ambao ni Wahutu, lakini wa damu ya kifalme. Hii ilileta kidogo changamoto kati ya Watutsi.
Vile vile, kuna familia nyingi zaidi zenye damu mchanganyiko wa Kitutsi na Kihutu. Dini ilienea haraka zaidi Burundi kuliko Rwanda, baada ya Vita Kuu ya Pili (1939-1945) palikuwepo Wakatoliki 600,000 ambao walikuwa mara mbili ya wale wa Rwanda, na miaka kumi baadaye kabla ya Uhuru mwaka 1959 walishafikia Wakatoliki 1,200,000 ambao walikuwa asilimia 55 ya wakazi wote.
Miito ya Upadre ilikuwa michache, walipata Padre wa kwanza Mwafrika mwaka 1925 na Askofu wa kwanza Michael Ntuyahaga mwaka 1959.
Mauaji yaliyotokea Rwanda mwaka 1960 yalliwafanya Watutsi wa Burundi wajihami.  Mwaka 1962 chama cha Watusi UPRONA kilichukua madaraka Burundi ilipopata Uhuru chini ya mwana mfalme Rwagasore, ambaye bahati mbaya aliuawa miezi michache baadaye.
Ingawa katika uchaguzi wa mwaka 1965 Wahutu walishinda, lakini madaraka yalichukuliwa na Watutsi.  Wahutu walipoasi wakipigania haki yao, viongozi 131 wa Kihutu na Wahutu wengine waliuawa na Kanali Micombero wa kabila la Kitutsi.
Baadaye Micombero alimpindua mfalme Ntare V.  Wahutu walinyanyaswa sana. Mwaka 1972 Wahutu walijaribu kujikomboa na kuwaua Watusi 1200.  Watusi walilipiza kisasi kwa kuwaua zaidi ya Wahutu 120,000 wakianza na wasomi.  Zaidi ya waalimu na Makatekista 2,300 Wahutu waliuawa.
Kanisa nchini Burundi lilisimama imara katika majaribu haya, kuna Watutsi wengi walioteseka au kuuawa wakiwalinda Wahutu, na Wahutu vilevile wakiwatetea Watutsi, kati yao wakiwemo Mapadre na Watawa. Hata hivyo hata wale waliokuwa wanaua walikuwa Wakristo.
Mwaka 1976 Jean Baptist Bagaza alimpindua Micombero. Bagaza alichukia Kanisa Katoliki. Aliwafukuza Wamisionari 300, akawafunga Mapadre 20, akapiga marufuku misa za kila siku na vyama vya kitume na kufunga Seminari zote.
Hata hivyo Kanisa liliendelea likitumia ukomavu wa Waamini wake katika kueneza Dini. Kwa wastani Padri mmoja alliwahudumia waamini zaidi ya elfu kumi na tano. Huu ulikuwa wakati mgumu kwa Kanisa, lakini ulilikomaza na kuliimarisha.
Kumekuwepo na  Maaskofu shupavu kama Askofu Simon Ntamwana wa Bujumbura, Mhutu, ambaye alipoteza karibu ndugu zake wote kwa kuuawa na Watutsi lakini bado anapigania amani kwa upendo na utulivu bila kuwa na kisasi.
Mwaka 1987 Pierre Buyoya, naye Mtutsi, alimpindua Bagaza.  Buyoya alikuwa mtu mstaarabu; alifanya amani na Kanisa na kushirikiana nalo, akawaingiza Wahutu katika Serekali yake na kutayarisha uchaguzi mwaka 1993.
Kutokana na uchaguzi huo Mhutu, Melchior Ndadaye, akiongoza chama cha FRODEBU, alichaguliwa kuwa Rais, ila miezi michache baadaye aliuawa na Jeshi la Watutsi lililoasi.  Rais Mhutu aliyemrithi aliuawa katika ndege iliyotunguliwa Rwanda pamoja na Raisi wa Rwanda Habyarimana.
Katika vita vya wenyewe kwa wenyewe, maelfu ya Watutsi na malaki ya Wahutu waliuawa. Mwaka 1996, Buyoya kwa mara nyingine tena alishika madaraka ya serikali na kidogo kuleta hali ya utawala, ingawa mapigano yaliendelea kwa sababu vikundi kadhaa vya Wahutu viliingia vita vya msituni.
Mazungumzo ya maelewano yalisimamiwa kwanza na Mwalimu Julius Nyerere, Raisi mstaafu wa Tanzania, na baada ya kifo chake yakasimamiwa na Mzee Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika ya Kusini, ambayo mwaka 2000 yalianza kuzaa matunda, na mwaka 2003 vikundi vikuu vilitia sahihi ya kusitisha mapigano.
Katika uchaguzi wa mwaka 2005 alishinda na kiongozi  waasi Pierre Nkurunziza wa chama cha CNDD-FDD. Ila chama cha Paripehutu, bado kiko msituni kikipigana.
Katika vita hivi Kanisa lilihusika kama mtume wa amani na uelewano, na limejaribu kufanya juhudi nyingi kupatanisha raia. Mwaka 2010 kati ya wakazi milioni nane, asilimia 65 walikuwa Wakatoliki, Waislamu asilimia 10 na Waprotestanti asilimia 5. Asilimia 20 zilizobaki za watu wa dini za asili, wengi wao wakiwa wakereketwa Wakatoliki ambao bado hawajabatizwa.
Uinjilishaji Kongo Brazaville:
Akishindana na Stanley, Sarvagnon de Brazza, aliweza kusimika bendera ya Ufaransa Kaskazini, mwa Mto Kongo na kushika sehemu yote ya Kaskazini na hivyo kuunda koloni za Kifaransa karibu na Ekweta. Koloni hizo zilikuwa Kongo-Brazaville, Gabon, Ubangi Shari (ambayo sasa ni Jamuhuri ya Afrika ya Kati) na Chad. De Brazza alipofanywa mtawala baada ya mkutano wa Berlin, aliwaalika Shirika la Roho Mtakatifu kuunda Vikariati.
Kufikia mwaka 1883 Wamisionari wa Shirika la Roho Mtakatifu walikuwa na misioni imara kwenye mwambao na katika mji wa Brazaville. Augourd alipewa Uaskofu mwaka 1894, na alifanya kazi kubwa ya uinjilishaji hadi alipokufa mwaka 1921.
Wakazi wengi wa Kongo-Braza ni wa kabila la ‘Bakongo’, watu wa dini waliomwita Mungu ‘Nzambi’. Hata leo nyimbo zao nyingi hata za kiraia humtukuza huyo Mungu wao. Kabila hili liko vile vile Kongo Kinshasa. Kutoka n’gambo ya mto kule Kongo-Kinshasa walipokea Wamisionari Waprotestanti kutoka Sweden mwaka 1909.
Kanisa hilo liliendelea vizuri sana. Tangu mwaka 1961 linaongozwa na Waafrika na Waamini wao leo wana asilimia 10 ya wakazi wote. Vile vile, kutoka Kongo Kinshasa walipokea dini ya Wakristo Waafrika ya Kibanguisti.
Kule Kongo Braza vile kulizaliwa dini nyingine za Kikristo za Kiafrika kama dini ya ‘Mungu wa Mshumaa’, na nyingine ya kisiasa iliyotaka kumkomboa Mwafrika kutoka katika ukoloni. Dini hiyo ilianzishwa na Andre Matswa. Matswa alifia gerezani chini ya Wafaransa, lakini Waamini wake wanamwona kama Messiha na wanangojea ujio wake.
Vile vile palikuwepo dini ya ‘kujipiga na Msalaba’ iliyoanzishwa na mkatekista Mkatoliki, Victor Malanda’ ambayo Waamini wake walipakwa mafuta kwa ajili ya kuacha ushirikina. Pia palikuwepo na dhehebu la ‘Jeshi la Wokovu,’ ambao alama yao ni bendera. Dhehebu hili la Wokovu ambalo ni kama maaskari liko katika nchi nyingi hata hapa Tanzania.
Licha ya madehebu mengi, Wakatoliki waliongezeka sana ingawa hawakufadhiliwa sana na serikali kama wenzao wa Kongo-Kinshasa katika kufadhili shule. Mwaka 1960 Kanisa lilimpata Askofu wake wa kwanza Mwafrika, Theophile Mbemba ambaye mwaka 1964 aliteuliwa kuwa Askofu Mkuu wa Brazaville.
Wakati huo Wakatoliki kwa uelekeo au mashabiki walikuwa asilimia 52 ya wakazi wote, wakifuatiwa na Waprotestanti asilimia 27, Makanisa ya kiafrika asilimia 9. Ingawa asilimia ni kubwa, kati yao kuna wengi waliokuwa washabiki tu wa Ukristo bila kujiunga rasmi kwa kubatizwa. Katika Sensa walijiandikisha katika madhehebu hayo. Mwaka 1973 Kongo-Brazaville ilipata Kardinali wake wa kwanza Emile Biayenda.

MWANZA

Na Paul Mabuga

Upepo unavuma katika jua la saa nane, na miti iliyo karibu inatoa ukinzani,  hali hii inazalisha mvumo ulio sawa na wimbo mzuri unaopigwa kwa ala tupu! Hakika, hali hii ingeweza kuwa ya kufurahisha, lakini la hasha! Aron Malifweda [48], [siyo jina lake halisi kwa sababu za kitaaluma], zaidi ya kutafakari kila swali analoulizwa kwa ajili ya makala haya, huku akiwa ameketi kiambazani kwenye nyumba yake iliyo kwenye moja ya miji mdogo kanda ziwa, ni kama haoni wala kusikia kingine cha ziada katika mazingira yake.
Ni kwa sababu amechanganyikiwa na kuzama katika fikra zisizo na msaada wala  ufumbuzi, anaona ni kama ametengwa na jamii yake kutokana na hali aliyonayo, anachokitamani anaona kama ananyimwa, na hivyo kukata tamaa.
Alitaka awe na  watoto, ikashindikana kwa nguvu za kiume [syo rijali]. Lakini sasa anataka kuasili mtoto anakayerithi mali zake, lakini amepewa sharti, kwamba ni  lazima aoe na kuishi na mke.
“Unajua nimehangaika kwa  miaka mingi, iwe kwa madaktari hospitali, ama tiba asilia, lakini sikufanikiwa. Baadaye daktari mmoja ninayemwamini akaniambia kwamba siwezi kuondokana na hali hiyo nilipata huzuni sana siku hiyo, na nikaona dunia yote imeniangukia.
Nikifikira maisha ya kukaa bila mke wala watoto, nilikiona hata kifo kinaninyemelea! Nimehangaika hivii kwa zaidi ya miaka 15,” anasema Malifwedha, wakati akisimulia kisa chake cha sharti la kuhifadhiwa utambulisho.
Anasema kuwa kama suluhisho katika hilo, alishauriwa na daktari huyo kwamba atafute mtoto wa kuasili ndiye atakayekuwa  mrithi wa mali zake, jambo ambalo anaeleza kuwa  awali lilikuwa gumu, kwani wapo waliomkatisha tamaa kwa kumtishia kuwa anaweza kupata kijana, akamlea, lakini baadaye atakapokua, asimjali na kumkimbia akirejea katika familia yake ya uzao wa kibayolojia.
“Walikuwa wananiambia, Unaweza kupata mtoto wa kuasili na kumsomesha, lakini akifika chuo kikuu, akakukumbia na kukutelekeza,” anasimulia Malifwedha na kuongeza kuwa, “Baada ya ushauri wa Maafisa Ustawi wa Jamii katika eneo langu, nilipata moyo wa kuanza mchakato wa kupata mtoto wa kuasili, ambao. Licha ya jambo kwenda vyema, lakini sasa nimefikia pahala umekwama kutokana na sharti nililopewa, kwamba ni lazima nioe!”
Kwa mujibu wa Tovuti ya Wakala wa Uzazi na Vifo, kuasili watoto ni mchakato wa kisheria ambao huhamisha uwajibikaji wa mzazi kutoka kwa wazazi wa kuzaliwa kwa watoto, kwenda kwa wazazi  wa kuwalea. Kuasili mtoto kunaongozwa na sheria  ya kuasili mtoto, Sura Namba 335 Toleo la Mwaka 2002.
Na kwa mujibu wa sheria hiyo, mara mtoto anapoasiliwa, basi unajengwa uhusiano wa kudumu na wa moja kwa maoja kati yake na wazazi waliomuasili, na kwamba haki zote kutoka kwa wazazi wake wa kibayolojia [wa damu] zinafutika na kuhamia katika familia yake mpya. Pia, Wazazi wa damu nao haki zao kwa mtoto aliyeailiwa, nazo zinakoma.
Tukirejea kwa Malifedha, anaeleza kuwa baada ya kupata mtoto wa kuasili, na wazazi wake wa damu kutoa ridhaa chini ya usimamizi wa Maafisa Ustawi wa Jamii, na uchumguzi wa kina kufanyika katika kipindi cha miezi sita, alijaza fomu mbali mbali na taarifa za ufuatiliaji zikaandikwa, tena zikionesha kwamba ana mwenendo mzuri, na ana uwezo wa kuasili.
Bila shaka mchakato kama huu, kulingana na taratibu, baadaye ulihitaji idhinisho la mamlaka ya juu ya Ustawi wa Jamii. Kutoka hapo, hoja hupelekwa mahakamani mbele ya jaji, na  kama kutakuwa na kukidhi matakwa ya kisheria, basi, hutolewa amri ya kuasili, na mchakato huwa umekamilika. Hata hivyo, katika muda wote Maafisa Ustawi wa Jamii huendelea kufuatilia ustawi na maslahi ya mtoto.
Pengine kilichoonekana kuwa ni kikwazo kwa Malifwedha kwa mujibu wa sheria hiyo, ni kwamba mzazi wa kiume anayeishi pake yake haruhusiwi kumuasili mtoto wa kike, ama vingunevyo kuwe na mazingira mahsusi! Ingawaje hata huvyo  anaruhusiwa kuasili mtoto wake wa kiume. Na pia, kuwe na tofauti ya umri wa miaka  isiyopungua 21 kati ya mzazi anayeasili, na mtoto anayeasiliwa.
Tena basi, inaelekezwa katika kanuni za sheria hiyo kwamba katika mazingita yanayofaa, mtoto aliyeasiliwa, atakapofikisha umri wa miaka 14, ataelezwa hali ya kuasiliwa kwake na maafisa ustawi wa jamii katika eneo husika.
Kuhusu suala na kuoa Malifwedha anasema, “Nilikwenda kwa wanasheria, wakaniambia kuwa huyo mwanamke nikimuoa, atakuwa na haki zote kama mke kwenye mali zangu, hata kama itakuwa ni ndoa ya kudanganyia ili tu nipate kibali cha kuasili! Hilo nalo nkaliona gumu. Nikashauriwa niende kwa Wakurya,  eti huko ukioa mwanamke aliyezalia nyumbani, na ukishatioa mahari, watoto wanakuwa mali yako.”
Sadick Hunga ambaye ni Mwandishi wa Habari anayefanya kazi zake Mkoani Mara, na ambaye ni mmoja wa wanajumuia ya Wakurya wanaoishi Mkoani humo,  anasema katika mahojiano kwa njia ya simu kwamba, mila hiyo ipo katika jamii yake na imeendelea kuwepo, kwamba katika jamii hiyo, wakati wote watoto huwa ni mali ya mwanaume aliyelipa mahari.
“Huyu jamaa sisi tunamuambia karibu ‘tata’ [baba]! Yaani huku kwetu, kama mwanamke amezalia nyumbani, akaja mwanaume kumuoa, analipa mahali ya mke, mathalani ng’ombe sita, lakini baadaye atatakuwa kuwalipia watoto mahari nyingine inayoitwa ‘kuborora’, ambayo inaweza kufikia hadi ng’ombe wawili kwa kila mtoto, na kutokea hapo watoto hao wanakuwa mali yake daima dumu, hata wana umri mkubwa namna gani,” anasema Hunga.
Katika mtazamo mwingine Hunga anasema kuwa miongoni mwa jamii ya Wakurya, ikiwa mwanamke ameachana na mume wake, na  ikatokea akaolewa na mwanaume mwingine, basi, watoto wote watakaozaliwa katika familia mpya ni mali ya yule mume wa awali, “na hii imetokea majuzi huko Serengeti! Itaondoka tu ikiwa mume mpya atalipa mahari kurejesha iliyokwishakulipwa kabla.”
Wakati hali ikiwa hivi, Malifwedha bado yupo njia panda juu ya nini akifanye ili kukabiliana na hali hii, kwani ana malalamikio mengine. Anadai kwamba ndugu zake wanamtenga na hususan yanapokuja matukio kama harusi huwa hashirikishwi, na hilo linamuongezea mawazo! “Yaani utasikia tu kuna harusi huko, lakini hushirikishwi, huwa najiuliza, sijui wananionaje,” anasema.
Kuna changamoto nyingine pia, kwani Malifwedha akifikisha umri wa miaka 50, yaani katika kipindi cha miaka miwili ijayo, kwani suala la kuasili litakuwa na kipingamizi, kwani halitakuwa katika maslahi ya mtoto, na hususani katika maendeleo na makuzi yake. Na itakuwa ni kazi kubwa kujenga hoja dhidi ya pingamizi kama hizi kulingana na kanuni za kuasili.
Mrumbi wa masuala ya ndoa na muendeshaji wa kipindi cha ‘Ndoa Aminifu’ cha Runinga ya Tumaini, Paschal Maziku, anasema kwamba ndoa katika Kanisa Katoliki huwa ni kwa ajili ya manufaa ya wanandoa wenyewe, watoto wanaowalea na jamii kwa ujumla, na wala siyo kwa manufaa binafsi kama ilivyo katika jambo hili katika makala haya.
“Isitoshe, huyu bwana hawezi kuwa na ndoa, kwani ndoa huwa kati ya mwanamke na mwanaume rijali. Sasa jamaa na hali aliyonayo, haiwezekani, maana ndoa ili  ikamilike inahitaji kuwa ‘consummated’ [tendo la ndoa kufanyika ndani ya muda unaovumilia kwa busara ana kupatilizwa], kinyume na hapo inavunjwa”
Kuhusu, kuasili watoto, Maziku anasema, huko ni sawa na mtoto kuwa ‘displaced’ [kuwa pasipostahili],  na kwamba, “ni vema tukarejea katika mila zetu, kama ni yatima ama ana mazingira magumu, basi ndugu wa karibu, wajomba, mathalani baba wadogo na wengine, wachukue majukumu yao.”

Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliawaletea mada ya historia ya jinsi Uinjilishaji ulivyoingia nchi za Ethiopia, Eritrea na Somalia. Leo tunaendelea na historia ya Uinjilishaji katika nchi za Maghreb.. Sasa endelea…

Katika Kiarabu, nchi za Magharibi mwa Misri huitwa ‘Maghreb’. Nchi hizi ni pamoja na Libya, Tunisia, Algeria na Morroco. Zamani nchi hizi, hasa kwenye mwambao, zilikuwa za Kikristu hadi zilipotekwa na Waislamu katika karne ya saba. Pole pole Ukristo uligandamizwa na kupotea.
Ufaransa iliteka Algiers mwaka 1830 na kufanya Algeria nzima koloni lake, baadaye waliteka Tunisia mwaka 1881 na Morocco mwaka 1912. Libya ilitekwa na Waitaliani mwaka 1912 na kuipoteza kwa Waigereza wakati wa Vita Vikuu vya Pili, mwaka 1942.
Wakati wa ukoloni, Wakristo walikuwa na uhuru wa kuinjilisha, na waliongezeka hadi kufikia milioni moja na nusu. Hata hivyo, hawakuwa na mafanikio makubwa kati ya Waarabu Waislamu. Wengi wa waumini wao walikuwa Wazungu waliohamia kule.
Waarabu walioongoka hawakuzidi 10,000. Utume katika nchi hizo ulifanywa hasa na Wamisionari wa Afrika (Mapadre Weupe) waliokuwa na Makao Makuu yao kule Algiers, Algeria.
Utume wao mkubwa ulikuwa utume wa kuwepo kwa kuonyesha mfano na kufanya matendo mema. Walianzisha vyuo vya kujifunza lugha ya Kiarabu na Uislamu kwa wageni.
Mmisionari mwingine alikuwa Charles de Foucard aliyeanzisha Mabruda na Masista Wadogo wa Yesu. Wao wanajaribu kuishi katikati ya watu na kufanya kazi pamoja nao katika viwanda na sehemu nyingine.
Nchi za Maghreb zilipopata uhuru wake, Wazungu karibu wote bila kungoja kufukuzwa, walirudi Ulaya. Kadri siku zilivyopita, nchi hizi ziliweka sheria ngumu ya kuwabana Wakristo, na hivyo hata Wakristo Waarabu walikimbilia Ulaya na kufanya kazi huko. Hivyo katika nchi za Maghreb hadi leo, Ukristo ni kama haupo.
MOROCCO
Morocco ilipata uhuru wake bila matatizo mwaka 1956. Ingawa iliwekwa sheria ya kukataza Waislamu kuongoka kuwa Wakristo, uhusiano na Kanisa ulibaki mzuri. Tangu mwaka 1952 kuna monasteri ya Wabenediktini inayoendesha semina hasa juu ya Mahusiano ya Dini mbalimbali. Kati ya wakazi milioni 31, Wakristo ni asilimia 0.5, na Wakatoliki ni asilimia 0.2 tu.
ALGERIA
Algeria ilipata uhuru wake mwaka 1962 baada ya vita vikali vilivyodumu miaka 8. Kwa sababu wakati wa vita, Askofu Mkatoliki Etienne Duval alitetea haki za wazawa, baada ya uhuru Kanisa liliheshimiwa.
Hata hivyo, Wakatoliki 800,000 waliondoka wakabaki 80,000 tu. Ila, Mapadre na Watawa walibaki kuwahudumia watu bila ubaguzi. Kati ya wakazi milioni 34, Wakristo ni asilimia 0.9 na Wakatoliki ni asilimia 0.6 tu. Kuna majimbo manne, Mapadre 62 na Watawa wanawake 116.
TUNISIA
Tunisia ilipopata uhuru mwaka 1956, kwa makubaliano kati ya serikali ya Kiislamu na Wamisionari wa Afrika, alama na mambo mengi ya Kikristo katika mji wa Tunis yaliondolewa.
Kwa mfano, sanamu ya mwanzilishi wa shirika iliyokuwa katikati ya mji, ilipelekwa makaburini, Cathedral nzuri ilifanywa makumbusho, kati ya makanisa sabini, sitini na tano yalipewa kwa serikali kwa matumizi ya umma, hata na cheo cha Askofu Mkuu cha Kartago kilishushwa na kuwa Usimamizi wa Kitume.
Hata hivyo, waliimarisha urafiki na Rais wa Tunisia, Bourguiba, ambaye alianzisha uhusiano wa kibalozi na Vatikano. Wamisionari walibaki na chuo chao cha kufundisha Kiarabu kilicholeta mahusiano mazuri. Kati ya wakazi milioni 10, Wakristo ni asilimia 0.3 na Wakatoliki ni asilimia 0.2 tu. Mwaka 1996 Papa Yohane Paulo II (1978-2005), alitembelea Tunisia kuwatia moyo.
LIBYA
Libya ilipata uhuru wake mwaka 1951 kutoka kwa Waitaliani. Baada ya uhuru, idadi ya Wakatoliki ilishuka hadi kubakia 5,000 tu, na baadaye Wamisionari walifukuzwa, Wakopti nao walibakia wachache.
Baada ya mapinduzi ya Kanali Ghadafi, katika makubaliano na Vatikano, Kanisa lilibakiza kanisa moja tu kule Tripoli. Ila baadaye Gadafi aliwaalika Masista manesi kwenda kusaidia watu wake. Hata Masista Watanzania wa Shirika la Konsolata walikwenda huko. Kati ya wakazi milioni 5.4, Wakristo ni asilimia 2.1,   na Wakatoliki ni asilimia 0.3 tu.
Ingawa katika nchi nyingi za Maghreb kuna uhusiano wa kidiplomasia na Vatikano, hakuna uhuru wa kuabudu. Haiwezekani kujenga kanisa au kuhubiri dini kwa Waarabu Waislamu. Kwa Mwarabu kuongoka na kuwa Mkristo, ni kosa linaloadhibiwa kisheria, mahali pengine hata kuuawa.

DAR ES SALAAM

Na Pd. Dkt. Clement Kihiyo (TEC)

Mwaka wa Liturujia Leo ya Wokovu
1. Utangulizi:
Ishara na matendo yanayofanywa kwa wakati huwa njia ya wokovu kwetu. Mwaka wa Liturujia ambao pia huitwa mwaka wa Kanisa ni fumbo la Kristo. Ni kwa njia ya maadhimisho ya kumbukumbu takatifu ndani ya Mwaka wa Liturujia, ndipo tunapata wokovu. Katika Mwaka wa Liturujia, Fumbo zima la Kristo linafunuliwa; yaani, kutoka Umwilisho na kuzaliwa, na kutoka Kupaa hadi Pentekoste
Mama Kanisa Takatifu huchukulia wajibu wake kuadhimisha kwa kumbukumbu takatifu kazi ya ukombozi ya Bwanaarusi wake aliye Mungu, katika siku zilizopangwa katika mwenendo wa mwaka mzima. Kila juma, Kanisa katika siku aliyoiita “Dominika”, yaani “Siku ya Bwana”, linaadhimisha kumbukumbu ya ufufuko wa Bwana. Kwa namna ya pekee, linauadhimisha ufufuko huo pamoja na mateso yake yenye heri mara moja kwa mwaka katika Sikukuu ya Pasaka, iliyo kubwa kuliko maadhimisho yoyote (SC 102).
Katika mzunguko wa mwaka mzima, Mama Kanisa analikunjua fumbo la Kristo, tangu umwilisho na kuzaliwa, hadi kupaa mbinguni, mpaka siku ya Pentekoste na kungojea kwa tumaini lenye heri kurudi kwake Bwana. Anapokumbuka namna hii mafumbo ya ukombozi, Kanisa huwafungulia waamini utajiri wa uweza na mastahili ya Bwana wake. Kwa njia hii, uwepo wa mafumbo haya unakuwapo kwa nyakati zote, ili kutoka humo waamini waweze kuchota na kujazwa neema ya wokovu.
Mwaka wa Liturujia pia unawakilisha na kueneza tena  imani, maisha ya Kikristo na uwepo wa ukombozi wa Kristo na utajiri wa wokovu (SC. 102c). Mwaka wa Liturujia ni safari ya wokovu wa Kristo Mwenyewe na Kanisa lake (Lk, 24:15). Mwaka wa Liturujia sio mfuatano wa jumla wa siku na miezi, lakini unakuwa alama/ishara ya mfuatano ambao matukio ya neema yanatokea kama matukio ya wokovu kwetu hapa leo. Mwaka wa Liturujia ni wakati wa wokovu, ‘epifania’ ‘hic et nunc’ (hapa na sasa) kwetu.

2. Baadhi ya Mambo Makuu ya Mwaka wa Liturujia
2.1 Mwaka wa Liturujia ni Maadhimisho:
Matukio ya Mwaka wa Liturujia sio tu mifano ya kutafakari au kuiga uungu, lakini ni ishara zenye ufanisi za wokovu, ambao Kristo katika Utatu Mtakatifu, wamekamilisha kwa wokovu wa wanadamu. Mambo makuu ya ukombozi ni sisi kuadhimisha na kurithisha kwa kizazi kingine. Mwaka wa Liturujia una nguvu maalum ya kisakramenti na ufanisi wa kuimarisha maisha ya Kikristo.

2.2 Mwaka wa Liturujia Kuanzia Ufufuko:
Tukianzia na habari ya wanafunzi wa Emao (Lk 24:25-26); Yesu alieleza kisa chote kuanzia Ufufuko hadi Manabii. Ina maana kila kitu kinamhusu Kristo. “Bila ufufuko imani yetu haina maana” (1Kor. 15:13-17). Ufufuko ni chanzo na kitovu cha Mwaka wa Liturujia. Ufufuko ni siku ya Adamu Mpya (Rum. 11:5, Efe 2:5,8).
2.3 Siku ya Kwanza ya Juma-Dominika- Siku ya Bwana
Tangazo la ufufuko lilianza siku hii kwa amri ya Bwana (Mk.16.7, Mt. 28.7, Lk. 24.9). Ndipo wale wanawake wakatangaza ufufuko siku ile ile. Kwa hiyo, Dominika ni mwendelezo wa tangazo la Ufufuko. “Tunasherehekea Dominika kwa sababu ya Ufufuko Mtukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo, na tunafanya hivyo sio tu wakati wa Pasaka bali pia kila mzunguko wa juma, yaani kila Siku ya Kwanza ya Juma. Mtakatifu Augustino anaiita Dominika kwa usahihi kama Sakramenti ya Pasaka  (Taz . In Io. Tract . XX, 202: CCL 36,203), (SC 26, 184). Kwa Kanisa la Mashariki Dominika ni ‘Anastasimos hemera’, yaani, siku ya ufufuko.
Matendo ya kiliturujia si matendo ya kila mmoja peke yake, bali ni maadhimisho ya Kanisa, ambalo ni “sakramenti ya umoja”, yaani taifa takatifu linalokusanywa na kuratibishwa chini ya uongozi wa Maaskofu SC 26.
Kwa sababu hiyo matendo hayo ni ya mwili wote kabisa wa Kanisa, nayo huudhihirisha na kuuimarisha. Aidha, kila mmoja wa wanakanisa anahusika kwa namna tofauti, kadiri ya utofauti wa daraja, wa majukumu, na wa ushiriki kiutendaji
Matukio maalum ya kimungu siku ya Dominika pia yanaipa siku hii umaalumu wake. Maana yake:

i.    Roho Mtakatifu alitolewa kwa Wanafunzi siku ya Dominika (Pokeeni Roho Mtakatifu, wowote mtakaowaondolea dhambi wameondolewa),
ii.    Pentekoste ilikuwa siku ya Dominika,
iii.    Dominika ni siku ya Amani, siku ya Yubilei ya Roho Mtakatifu (Lk 4:18-19, Isa 61:1-3).
iv.    Kwa namna ya pekee, Dominika ni siku ya uumbaji mpya, siku ya Jua Jipya (Mal, 4:2).

2.4 Dominika ni Kitovu na Kiini cha Mwaka wa Liturujia:
Dominika ni Kitovu na Kiini cha Mwaka wa Liturujia kwa muktadha ufuatao:
Dominika ni siku ya Bwana. Wayunani wanaiita, “Kyriake Hemera”, ambapo kivumishi ‘Kyriake’ kinarejelea Kyrios, yaani Bwana aliyefufuka pamoja na Roho (1 Kor. 16:2, Mdo, 20:7, Ufu.1.10).
Dominika ni siku ya kimungu ya kumwadhimisha Bwana, siku kwa ajili ya kumega mkate na Neno, siku kwa ajili ya karamu na kwa ajili ya kukusanya sadaka kwa ajili ya maskini (2 Kor, 9:12, Rum. 15:27).
Dominika ni siku ya mwanzo wa uumbaji, ni siku ya nane baada ya ufufuko. Ni siku ya nane kwa sababu ni nje ya muda unaopimwa katika wiki. Siku ya nane ni siku ya Ekaristi. Hivyo, Dominika hugusa fumbo zima la wokovu. Inaleta pamoja na yenyewe ulimwengu wote wa mfano wa Kikristo. Inaangazia siku ya mwisho, siku ya Parousia.
Kwa hiyo, Dominika ni siku maalum na siku pekee  ya Bwana. Inaunda mwendelezo halisi wa adhimisho wa Kanisa kutoka Pentekoste hadi kurudi kwa Bwana. Maadhimisho mengine, isipokuwa kama yana umuhimu mkubwa, hayatapewa kipaumbele kuliko Dominika ambayo ndiyo msingi wa kweli na kiini cha Mwaka mzima wa Liturujia.
Kadri ya mapokeo ya Mitume, yanayopata asili yake katika siku ya ufufuko wa Kristo, Kanisa huadhimisha fumbo la Pasaka kila siku ya nane, katika siku ile iitwayo kwa haki kabisa Siku ya Bwana au Dominika. Katika siku hii Waamini wanapaswa kujumuika pamoja ili, wanaposikiliza Neno la Mungu na kushiriki Ekaristi, wafanye ukumbusho wa mateso, ufufuko na utukufu wa Bwana Yesu. Na pia watoe shukrani kwa Mungu “aliyewazaa upya katika tumaini lenye uhai kwa njia ya ufufuko wa Yesu Kristo katika wafu” (1Pet, 1:3). Kwa hiyo, siku ya Dominika ni Sikukuu ya kwanza ambayo ni lazima ielezwe vizuri na kuingizwa, kwa kadri inavyowezekana, katika maisha ya kidini ya Wakristo, ili iweze kuwa pia siku ya furaha na ya kuacha kazi. Maadhimisho mengine yasitiliwe mkazo sana, isipokuwa yale yenye umuhimu zaidi, kwa sababu siku ya Dominika ni msingi na kiini cha mwaka mzima wa Liturujia (SC. 106).

3. Fumbo na Mafumbo ya Kristo:
Imani ya Kikristo inaadhimisha Fumbo Kuu Moja la Pasaka, nalo ni  Fumbo la Kristo, aliyeteswa, akafa, akazikwa na kufufuka. Kanisa linaendelea kuadhimisha Fumbo hili kwa njia tofauti. Fumbo hili lilianza kufunuliwa katika Agano la Kale; na linatimizwa kihistoria katika maisha ya kidunia ya Kristo, na lipo katika mafumbo ya kisakramenti.
Fumbo la Pasaka huadhimishwa katika mwaka kwa njia tofauti, lakini katika utaratibu ule ule wa Neno, mwili na kikombe cha Yesu Kristo. Awamu tofauti za maadhimisho zinalenga kutufanya tuelewe vizuri Fumbo hilo. Katika uwezo wetu mdogo wa kibinadamu na kisaikolojia, hatuwezi kulielewa na kuliadhimisha hilo Fumbo kwa wakati mmoja na kuchota utajiri wa neema ya Fumbo hilo la Kristo”, kwa hivyo, Mwaka wa Liturujia unatupa muda wa kutosha wa kuliadhimisha na kuchota neema zake.
Kwa muktadha huu, katika kila Misa kuna Majilio, Noeli, Epifania, Alhamisi Kuu, Ijumaa Kuu, Pentekoste, Pasaka, Kupaa, na Watakatifu wote. Kwa hiyo, Mwaka mzima wa Kanisa ni Fumbo Moja, “ Sakramenti Paschale ” ambalo huadhimishwa kila Dominika.
Kutoka hili Fumbo Kubwa la Pasaka, linajigawa katika mafumbo kadhaa yanayorejelea matukio tofauti katika maisha ya Kristo, na ni ushiriki na ukuzaji wa Fumbo moja pekee la Pasaka, ambalo huanza kutoka Usiku Mtakatifu wa Ufufuo hadi wakati wa Pasaka hadi Pentekoste, Wiki Takatifu, Kwaresima, Wakati wa Kawaida, Majilio, Noeli hadi Epifania na Sikukuu mbalimbali.
Itaendelea toleo lijalo.

DODOMA

Na Bartholomew Wandi

Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 hauko mbali sana kuanzia sasa, kwani ukipiga hesabu umebaki takribani muda wa mwaka mmoja (1) na miezi kadhaa hivi. Wananchi wengi ambao watafikisha miaka kumi na minane wakati wa jukumu hili, waliofikisha miaka kumi na minane (18) tayari na zaidi, na wale ambao waliokuwa na sifa zote za kuandikishwa mwaka 2020, lakini kutokana na sababu zisizoweza kuzuilika walikosa nafasi ya kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, wataandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Awamu ya Kwanza na ya pili  ya uboreshaji.
Mpaka sasa mikoa yote 25 Tanzania Bara tayari ina watu ambao wanahitaji kuandikishwa kuwa wapiga kura wenye sifa nilizozielezea hapo juu.Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni hitaji la kisheria na Kikatiba pia. Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria kuandikisha wapiga kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na pia Madiwani Tanzania Bara.
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utakuwa mahsusi kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao zilizokosewa awali, waliopoteza kadi za kupigia kura, wenye kadi zilizoharibika ili waweze kupata kadi nyingine,  na wale ambao wanataka kuhama Jimbo au Kata kwenda Jimbo au Kata nyingine ili waweze kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kifungu cha 12 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inaeleza, “Mkurugenzi wa Uchaguzi ataweka, atatunza na kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililoanzishwa chini ya kifungu cha (1)”.
Kulingana na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, Kifungu cha 9 (2) inasema, “Bila kujali Masharti ya kifungu kidogo cha (1), na kwa kuzingatia uthibitisho wa umri , Mtanzania yeyote ambaye hajapoteza sifa chini ya Sheria hii au Sheria nyingine yoyote ya Bunge, na ambaye wakati au kabla ya tarehe ya Uchaguzi atatimiza umri wa miaka kumi na minane (18) atastahili kuandikishwa kuwa Mpiga Kura chini ya
Kifungu cha 13 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, pia inaeleza kwamba, “Tume itamwandikisha mtu yeyote Tanzania Zanzibar ambaye anastahili kuandikishwa kuwa mpiga kura katika Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano”.
Zaidi ya hayo, Ibara ya 5(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inafafanua, “Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane (18) anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti mengine ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi”.
Pamoja na hayo, pia Ibara ya 5(3)(a-d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inaeleza kuwa Bunge  litatunga sheria ya uchaguzi na kuweka masharti kuhusu kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika Daftari hilo, kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga kura na kupiga kura, utaratibu wa kumwezesha mpiga kura aliyejiandikishwa sehemu moja kupiga kura sehemu nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa utaratibu huo, na kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.
Marekebisho ambayo yanapaswa  kuingizwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni kuondoa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja, waliojiandikisha na huku wako chini ya umri wa miaka kumi na minane (18), waliofariki dunia  au kupoteza sifa ya kuwa wapiga kura kwa namna nyingine, kuwapa kadi za mpiga kura mpya waliopoteza kadi zao, kurekebisha taarifa za wapiga kura zilizokosewa awali,  na kuwaingiza waliofikisha umri wa miaka kumi na minane (18) na kuendelea.
Kifungu cha  16(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inasema, “Tume itakuwa na jukumu la kupanga muda na kupitia upya uandikishaji wa wapiga kura katika kila eneo la uchaguzi ndani ya jimbo”
Kwa mujibu wa kifungu cha 16 (5) cha  Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, inaeleza kwamba Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika mara mbili kwa miaka mitano (5), yaani baada ya Uchaguzi Mkuu kupita, na kabla ya siku ya uteuzi.
Uchaguzi Mkuu wa Mwisho ulifanyika Oktoba 28 mwaka, 2020, na sasa Tume ipo kwenye maandalizi ya kuboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Mchakato wa Uboreshaji huo wa Daftari umeanza kwa kukagua vituo vilivyotumika kuandikishia Wapiga Kura mwaka 2019/2020.
Uhakiki huo wa vituo hivyo vya kuandikishia wapiga kura, unalenga kuona kama kuna haja ya kuongeza vituo, kuona kama vilivyopo bado vinakidhi matakwa ya kisheria, na kufanya marekebisho mengine kama vile kubadilisha au kurekebisha majina ya vituo vilivyokosewa.
Matokeo ya uhakiki huo kwa Tanzania Bara yanaonesha kuwa, vituo vya kuandikisha wapiga kura vimeongezeka kutoka 37,814 hadi 40,126 ambapo kati ya vituo hivyo, 39,709 ni vya Tanzania Bara na vituo 417 ni vya Zanzibar.
Baada ya kazi ya kukagua vituo hivyo, Tume imefanya Uboreshaji wa majaribio (pilot) unaofanyika katika baadhi ya vituo vilivyoko kwenye halmashauri za Wilaya na Halmashauri za miji kwa  lengo la kujaribu kuona namna na jinsi vifaa vya uboreshaji vinavyofanya kazi katika mazingira tofauti, na kupata namna bora ya kufanikisha zoezi hili la uboreshaji.
Tume tayari imeshafanya uboreshaji wa majaribio katika kata ya Ikoma iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mkoani Mara na Kata ya Ng’ambo iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mkoani Tabora. Kata hizi zilichaguliwa ili kupata mazingira tofauti ya kijiografia, pamoja na idadi ya watu.
Uboreshaji huu wa majaribio umefanyika kwa mafanikio kutokana na kuboreshwa kwa vipuri na mfumo wa uandikishaji wa wapiga kura. Aidha, ilibainika kuwa betri mpya za BVR Kits zinao uwezo wa kuhifadhi chaji kwa muda mrefu, na hivyo zitaweza kukabiliana na changamoto ya nishati ya umeme katika baadhi ya maeneo ambayo hayana miundo mbinu hiyo.
Pamoja na mafanikio hayo kulikuwa na changamoto ndogo ya baadhi ya  wapiga kura kutokuwa na uhakika ama kukumbuka majina yao wanapokuja kurekebisha taarifa zao na hivyo kuchukua muda mrefu kituoni kutokana na kazi ya kutafuta majina yao kwa usahihi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi  itaendelea kuwaelekeza Wapiga Kura kuhakikisha wanakumbuka taarifa zao kwa usahihi ili waweze kuhudumiwa kwa haraka vituoni.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele wakati akiongea na Waandishi wa Habari Mjini unguja, Zanzibar, amesema kuwa uzinduzi rasmi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika Mkoa wa Kigoma tarehe 01 Julai, 2024.
Uboreshaji huo wa Daftari kwa Teknolojia ya BVR kwa mwaka huu 2024, hautakuwa tofauti na wa mwaka 2019/2020, ambao ulihusisha wananchi wote wapya wenye sifa za kuwa wapiga kura, waliohama jimbo au Kata, na ambao kadi zao zilipotea au kuharibika.
Wapiga kura ambao waliandikishwa mwaka 2015 na  2020 na wanazo kadi zao za kupigia kura na hazina matatizo yoyote, au hawajahama Jimbo/Kata kwenda Jimbo/Kata nyingine au hakuna mabadiliko yoyote ya mipaka ya kiutawala,  wanatakiwa pia kwenda katika vituo vya kuandikisha Wapiga Kura ili kuhakiki taarifa zao kwenye Daftari.
Kwa upande wa idadi ya Wapiga Kura watakaoandikishwa awamu hii, Tume imeshafanya makadirio kulingana na uandikishaji uliopita pamoja na matokeo ya Sensa ya watu na makazi uliofanyika mwezi wa Agosti mwaka huu, 2022.
Mhe. Jaji Mwambegele aliwaambia Waandishi wa Habari kuwa, makadirio ya Tume kwa kutumia ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ya Sensa ya Watu na Makazi, inatarajiwa idadi ya Wapiga Kura kuongezeka kufikia 34,746,638 kutoka 29,754,699 ya Wapiga Kura katika mwaka 2020, idadi hii itajumuisha wapiga kura wapya 5,586,433, sawa na asilimia 18.7 wanaotarajiwa kuandikishwa.
Pamoja na hayo, Mwnyekiti wa Tume anasema kuwa inakadiriwa Wapiga Kura 594,494 wataondolewa katika Daftari kwa kupoteza sifa na jumla ya Wapiga Kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao. Hawa watakaoboresha ni wale ambao taarifa zao zilikosewa au wamehama kutoka Kata au Jimbo moja kwenda eneo lingine la Uchaguzi, na wengine ni wale ambao kadi zao zimeharibika au zimepotea.
Hata hivyo, Uboreshaji wa safari hii hautofautiana sana na ule wa mwaka 2015 na 2020, kwani Teknolojia itakayotumika ni ile ile ya kuchukua alama za kibaiolojia yaani Biometric Voters Registration (BVR), pamoja na Android.
Aidha, mabadililiko yanayotazamiwa ni kwa upande wa kupunguza ukubwa na uzito wa BVR Kits ambapo awali wakati wa uboreshaji wa Dafrari wa mwaka 2014/2015 na 2019/2020 BVR zilikuwa na uzito wa kilo 35 lakini kwa uboreshwaji wa mwaka huu kwa 2024/2025, uzito umepunguzwa  hadi kufikia kilo 18 ambapo yapo masanduku mawili, moja ni kwa kuhifadhia mashine ya BVR Kits, na lingine ni kuhifadhia vifaa vingine vya kuunganishia BVR Kit hiyo ikiwemo kishikwambi kwa ajili ya kupigia picha ya Mpiga Kura na kuchukulia alama za vidole, ila vifaa hivi vitatoa huduma ile ile ya kuandikisha wapiga kura na kutoa kadi hapo hapo kituoni.
Mabadiliko mengine katika Uboreshaji wa Daftari ni Tume kuanzisha mchakato wa uboreshaji kwa njia ya mtandao (Online) ambapo mpiga kura anaweza kuanzisha mchakato huu wa awali kwa njia ya mtandao ili kurekebisha, au kubadilisha taarifa zake, kuhamisha taarifa zake kutoka kituo cha awali kwenda kingine, au anayetaka kufanya vyote kwa pamoja.
ITAENDELEA WIKI IJAYO.
Wapiga kura wanaotaka kuboresha taarifa binafsi na wanaohama vituo au vyote viwili kwa wakati mmoja, wanaweza kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zao kwa njia ya mfumo wa mtandao ‘online’ kuingia kwenye Tovuti ya Tume www.inec.go.tz kwa kutumia kompyuta au simu janja, kisha atabonyeza kiunganishi (link) iliyoandikwa Boresha Taarifa za Mpiga Kura, au atatumia anuani ya ovrs.nec.go.tz itakayompeleka moja kwa moja kuanzisha mchakato huo.
Katika mfumo huu, wapiga kura wanatakiwa kuingiza namba ya kitambulisho cha taifa (National Identity Number: NIN), namba ya kadi ya mpiga kura, namba ya simu anayotumia kwa sasa, na jina la Kata, kisha watapata ujumbe wenye namba za utambulisho (token namber) ambazo wataenda nazo kituoni ili kukamilisha taratibu za kupata kadi za mpiga kura.
Mwombaji ambaye ni mpya anatakiwa kwenda kituoni bila kuwa na kitambulisho cha aina yoyote kiinachomtambulisha ili aweze kupatiwa kadi ya mpiga kura. Mwaombaji huyu atakapofika kituoni atamwona Mwandishi Msidizi wa Kituo cha kuandikisha Wapiga Kura na  kuajaza fomu Na. 1,
Baada ya kujaza Fomu Na. 1, Mwombaji huyo Mpya atampatia Afisha Mwendesha Mashine ya Bayometriki (BVR Kits Operetor) ambaye ataingiza taarifa zake kwenye BVR Kit, atapigwa picha, atachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili  na kuweka saini na kupewa Kadi ya Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Kwa wapiga kura ambao walipoteza, kuharibika au kukosewa Kadi zao na ambao hawatajaza Online, watakapofika Kituoni, watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo , kisha Afisa Mwendesha Mashine ya Bayometriki ataingiza taarifa zao kwenye BVR Kit, akisha watapigwa picha, watachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili, na kuweka saini na mwishowe watapewa Kadi zao za Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Vile vile,, Wapiga Kura ambao wanataka kuhamisha taarifa zao, pia watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo ili kuomba kuhamishiwa taarifa zao kwenda Jimbo au Kata na Kituo kingine cha Kupigia Kura wakati wa Uchaguzi Mkuu, na Chaguzi nyingine Ndogo zitakazofuata baada ya Uchaguzi Mkuu kupita.
Aidha, Mtu anatakiwa aende mwenyewe kituoni na anatakiwa kujiandikisha mara moja tu. Ni kosa la jinai kwa mwananchi yeyote kwa makusudi kwenda kituoni na kujiandikisha zaidi ya mara moja. Mwaka 2015, Kwa Mkoa mmoja tu wa Njombe, Kanzi Data hiyo imeweza kung’amua wapiga kura zaidi ya 600 waliojiandikisha zaidi ya mara moja, na walichukuliwa hatua za kisheria.
Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024,  kifungu cha 114(1)(b) inaeleza kuwa “kwa kujua au ana sababu ya kuamini kuwa ameandikishwa katika eneo la Uchaguzi anaomba kuandikishwa kinyume na kifungu cha 25, na bila kufichua kwa Msimamizi wa Uchaguzi kujiandikisha kwake kwa awali katika eneo jingine la Uchaguzi atenda kosa na akitiwa hatiani atapaswa kulipa faini isiyopungua shilingi laki moja na isiyozidi shilingi laki tatu au kifungo cha muda usiozidi Miaka miwili au vyote kwa pamoja”.
Baada ya zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaandaa Daftari la Awali la Wapiga Kura na kupelekwa mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) kwa ajili ya wapiga kura kuangalia kama majina yao yamo kwenye Daftari.
Kama baadhi ya majina hayaonekani, Wapiga Kura watamweleza Mwandishi Msaidizi kutoonekana kwa majina hayo na Mwandishi Msaidizi ataandika majina ya Wapiga kura hao waliokosekana kwenye Daftari la Awali na kisha ataleta orodha hiyo ya Majina Tume kwa ajili ya kuingizwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Pamoja na hayo, dhumuni lingine la Tume kupeleka Daftari la Awali la Wapiga Kura mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) ni kuwapa fursa Wapiga Kura kuangalia kama kuna majina ya Wapiga Kura walioandikishwa na hawana sifa kisha watawawekea pingamizi kwa kujaza fomu Na. 3B na kumkabidhi Mwandishi Msaidizi fomu hiyo ambaye ataileta Tume kwa ajili ya Wapiga Kura hao ili wafutwe kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kama kweli hawana sifa.
Hata hivyo, Majina hayo yaliyowekewa pingamizi hayafutwi moja kwa moja kwenye Kanzi Data ya Tume badala yake yanahifadhiwa sehemu nyingine kwenye Kanzi Data ili kama mtu huyo ana ushahidi wa kutosha kuwa ana sifa za kutosha kuandikishwa na kubaki kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura anarudishwa mara moja, Machapisho mbalimbali ya Elimu ya Mpiga Kura ya uhamasishaji ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yatasambazwa nchi nzima  ili kuwaelimisha Wapiga Kura kuwa na uelewa na mwamko wa kujiandikisha kwa wingi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga kura.
Mchapisho hayo pia yanasistiza Wapiga Kura kutunza Kadi zao za kupigia kura na hatimaye kujitokeza kwa wingi kupiga Kura kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2025 utakapowadia na Chaguzi Ndogo zitakazofuata  na kila mmoja anatakiwa awe na Kadi yake ya kupigia kura.
Tume pia katika uhamasishaji wake wa Uboreshaji wa Daftari itatumia vyombo mbalimbali vya habari kama Magazeti, Radio kubwa na Radio za Kijamii, TV, INEC TV ONLINE, Tovuti ya Tume na Mitandao ya Kijamii, machapisho yakiwemo mabango, vijitabu na vipepeperushi, gari la Elimu ya Mpiga Kura na kushirikisha wadau kwa kutoa vibali kwa taasisi na asasi za kiraia.
Mwandishi wa Makala haya ni Afisa Habari Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) Simu  0754203015.

Dar es Salaam

Na Edvesta Tarimo

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia (World Bank -2023), inakadiriwa kuwa uzalishaji wa taka utaongezeka kwa 70% kutoka tani bilioni 2.01 hadi bilioni 3.40 ifikapo mwaka 2050.
Kulingana na ripoti ya taarifa ya kiuchumi ya Urejelezaji wa Marekani
(U.S Recycling Economic Information - REI), San Francisco, Marekani, ni jiji la kijani kibichi hasa, na linatajwa kama kinara kwa urejeshaji wa taka (recycling), kwa zaidi ya asilimia 80 ya taka zake.
Urejelezaji wa taka na mifumo mizuri ya kushughulika na majitaka, utasaidia kuongeza ajira, kuongeza viwanda vidogo vidogo, kuongeza teknolojia mpya, pamoja na kipato ambacho kimekuwa kikipotea, ikiwa ni pamoja na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.
Majiji mengine yanayofanya vizuri kwenye urejeshaji wa takataka ni pamoja na Curitiba - Brazil, iliyofanikiwa kwa asilimia 70, pamoja na Vancouver-Canada, waliofanikiwa kwa asilimia 60 wakiwa na lengo la kufikia asilimia 100 ifikapo mwaka 2040.
Wanafanyaje? Kwa kushikamana na mipango madhubuti ya kuchakata taka na sera ya kulipa fedha kadri wakazi wake wanavyotupa taka zisizoweza kutumika tena, huwafanya wananchi wawe na ufahamu zaidi wa mazingira, hasa kuhusu bidhaa wanazonunua katika kuepuka kulipishwa fedha zaidi za taka.
Nini kifanyike kukabiliana na hili?
Jiji la Dar es salaam ambalo linatajwa kuwa kitovu cha biashara, lenyewe linakadiriwa kuzalisha zaidi ya tani 4,252 za taka kwa siku moja. Kati ya taka hizo, ni asilimia 50 tu ndizo zinazopokelewa kwenye maeneo maalumu, nyingine zikisalia na kutupwa kwenye mitaro, maeneo ya wazi, na hata barabarani.
Hapa Tanzania, baadhi ya wadau wa mazingira wamekuja na mpango mkakati wa kuweka mazingira katika hali safi kwa kukusanya takataka, na kwa kupita baadhi ya masoko katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kama vile Ilala, Buguruni. n.k.
Alpha Ntibachunya  ameamua kushiriki katika utunzaji wa mazingira kwa kuanzisha kampuni ya LIMA ya kurejeleza taka ngumu katika matumizi mengine, badala ya kutupwa na kuchafua mazingira.
Ntibachunya anasema kuwa yeye na mwenzake walifanya utafiti wa kujua takataka zinazotupwa zinapelekwa wapi baada ya kukusanywa, na baada ya utafiti, waligundua kuwa kuna fursa nyingi zinazopatikana kwenye takataka.
“Kilichotupelekea tukaanzisha huu mradi, tulikaa tukafanya utafiti na kugundua kwamba kuna changamoto, baada ya hapo tukapata wazo linguine, tukaja na wazo hili la kuzalisha chakula cha kulishia mifugo, na mbolea ambayo tulitazama zaidi wakulima wadogo, hasa wa vijijini,” anasema Ntibachunya.
Anaongeza kusema kuwa njia mbili tofauti wanazotumia katika kukusanya taka, kwa kwenda sokoni, mfano soko la matunda Buguruni, hotelini na kutumia njia ya boksi hai ambalo hupeleka majumbani mwa watu kwa ajili ya kukusanyia mabaki ya vyakula majumbani mwa watu, kisha wanakwenda kuzichukua na kwenda kuzichakata.
Anasema kuwa wametumia changamoto ya mlundikano wa takataka katika maeneo tofauti tofauti katika jiji kugeuza kuwa sehemu ya kujipatia ajira, na kuajiri vijana wengine katika kukusanya na kuzichakata na kuwa chakula cha kulishia mifugo, na mbolea ambayo ni halisia isiyokuwa na makemiko ya aina yoyote.
Ntibachunya anasema kwamba uchakataji wa taka katika matumizi mengine umekuwa mchango mkubwa wa nafasi ya ajira kwa vijana wengi, kwani uzalishaji wake hauhitaji kiwango cha elimu, bali utayari wa kijana wa kuelekezwa kufanya kazi hiyo.
Kuchakata taka kunanufaisha mazingira, na kunatoa ajira kwa vijana, kunakuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla. Kwa kutenganisha taka zinazoweza kutumika tena kama karatasi, nguo chakavu, glasi, plastiki, aluminium na mabaki ya vyakula na taka za elektroniki, watumiaji wanaweza kusaidia kuunda kijani kibichi kwenye majiji makubwa duniani.
Anitha Erasmi ni mama wa watoto wanne, anasema kuwa uchakataji wa taka umekuwa sehemu yake ya kujipatia kipato cha kuendesha maisha ya familia yake, licha ya ndugu kumwona kama amechanganyikiwa.
“Mwandishi, ndugu zangu na jamii, iliniona kama chizi, lakini mimi sikujali kwa sababu mjini kama huna kazi, ukichagua kazi utashindwa kuishi. Nakusanya mamboga mboga nazipeleka kuziuza, napewa pesa,” anasema Anitha.
Philbert Alphonce mkazi wa Goba jijini Dar es Salaam, anasema kwamba amekuwa anakikusanya taka ngumu kutoka soko na kuzipeleka sehemu wanakozichakata na kuzirejelesha katika matumizi ya kulisha baadhi ya mifugo, na pia mbolea asilia ambayo hutumiwa na wakulima wadogo wadogo kuweka kwenye mashamba ya mboga na maua.
Alphonce anasema amekuwa akiendesha familia yake ya mke na watoto wawili kupitia kazi yake ya ukusanyaji wa mabaki ya mbogamboga na kwenda kuziuza, ambapo kwa wiki anakwenda sokoni mara mbili, huku siku nyingine akizitumia kwa shughuli zake nyingine.
NEMC,Wadau watoa neno
Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (National Environment Management Council – NEMC), Dk. immaculate Sware Semesi anasema NEMC, na taasisi ya mazingira, kituo cha Sayansi cha Mazingira (Centre for Science and Environment - CSE), kutoka India, wamekutana nchini Tanzania kujenga uelewa wa nini kifanyike katika taka ngumu, kuchukua takwimu ni taka kiasi gani zinazalishwa na zinatunzwaje, ili ziwe fursa badala ya kuwa uchafuzi wa mazingira.
Dk.Semesi anasema sambamba na hilo, kutambua ni teknolojia gani itumike ili kufanya taka zisiwe kero katika manispaa na jiji, bali ziwe fursa ya kuzalisha ajira au nishati kutokana na taka.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila katika moja ya hotuba yake alisema kwamba anaiona fursa kubwa kwenye wingi wa taka hizo, na tayari alisafiri mara moja kwenda kwenye jiji la Bursan nchini Korea Kusini kujifunza namna wenzetu walivyofanikiwa kwenye urejelezaji wa taka, na kuzifungamanisha na fursa kwa vijana wa rika mbalimbali.
Chalamila anasema kwamba jiji la Dar es salaam linaweza kuwa mfano kwa majiji mengine nchini Tanzania na Afrika Mashariki kwa fursa ya ajira kwa njia ya urejeleshaji wa taka, endapo juhudi za makusudi zitachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa vitendo.
Anaongeza kuwa urejelezaji wa taka (recycling) ni mchakato wa kutibu taka kwa lengo la kuokoa malighafi zilizopo ndani ya taka na kuzirejesha kwenye matumizi ya kiuchumi.
Vifaa vya kielektroniki kama simu na kompyuta hurejelezwa na kutumika tena katika kutengeneza matofali, saruji na vyombo vipya vya glasi.
Taka za kaboni kama maganda ya matunda na mbogamboga, zinatumika kutengeneza mbolea na karatasi zikirejelezwa na kutumika kama makasha ya mayai na vifungashio vya bidhaa mbalimbali.
Ripoti ya Benki ya Dunia kuhusu maendeleo ya miji, inaonesha kuwa Afrika huzalisha tani milioni 70 za taka kwa mwaka.
Wakati huu ambapo ongezeko la watu wanaohamia mijini linaongezeka kwa kiasi kikubwa, Benki ya Dunia inasema kuwa kufikia mwaka 2025, uzalishaji wa taka huenda ukafikia tani milioni 160 kwa mwaka.
Tafiti zinasema kwamba ni rahisi kutengeneza bidhaa kutoka nyenzo zilizorejelezwa, kwani bidhaa kama ya aluminium iliyorejelezwa inaweza kuandaliwa tena na kuuzwa kwa bei nusu, kutokana na kuhitajika nishati kidogo ya kuchakata aluminium iliyorejelezwa, kuliko kutumia aluminium mbichi ya kiwandani inayotumika kwa mara ya kwanza.
Urejelezaji pia huepusha gharama ya utupaji wa taka kwenye dampo na vichomaji (incinerators), kwani baada ya kuanza kwa urejelezaji, dampo chache zitahitajika, na ardhi zaidi zilizokuwa zimetengwa kuhifadhi taka huweza kutumika kiuchumi.
Aidha, mapato ni sehemu nyingine aliyoiona Chalamila, kwani urejelezaji huimarisha tasnia ya uchakataji, na hivyo kutengeneza nafasi mpya za kazi kwenye viwanda vidogo vitakavyoundwa, kama viwanda vya chuma, karatasi, glasi, pamoja na ajira kwenye vituo vya ukusanyaji taka, na hata warejeshaji husika.
Utafiti wa U. S Recycling unaonesha kuwa nguvukazi ya kuchakata na kutumia tena malighafi zinazotokana na taka, imekuwa kubwa zaidi kwenye mataifa mengi, zaidi ya nguvukazi inayotumika kwenye uchimbaji wa madini na usimamizi wa taka zisizorejelezwa.Mashirika yanayorejeleza taka, huzalisha takribani dola bilioni 240 kwenye mapato ya kila mwaka.
Huko Carolina kusini pekee, zaidi ya wafanyakazi 15,000 na dola za Marekani milioni 69 za ushuru, hutokana na uchakataji wa taka, huku Carlifonia urejelezaji wa taka ukiajiri watu 85,000.
Kila mwaka, dunia inageuka kuwa makao ya takribani tani bilioni 2.01 za taka ngumu, na idadi hiyo inatarajiwa kufikia bilioni 3.40 miaka 30 ijayo, sawa na ongezeko la 70%.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, (World Bank – WB), mataifa yenye kipato cha juu inaonesha kwa siku kuna ongezeko la 19%, huku mataifa yenye uchumi wa kati na chini, ukiongezeka kwa 40% au zaidi.

Page 3 of 5