DAR ES SALAAM
Na Deus Helandogo
Uongozi wa klabu ya soka ya Simba kupitia kwa Meneja wake Ahmed Ally, umefunguka sakata la kuachana ghafla na mshambuliaji wao Fredy Michael, ambaye amedumu ndani ya klabu hiyo kwa miezi michache tu.
Ahmed Ally aliweka wazi kwamba sababu za kuachana na nyota huyo ni kutokana na kuwa alishindwa kufundishika, mara baada ya kocha wao Fadlu Davis kumfanyia mazoezi mengi na kuzungumza naye, lakini bado kiwango chake kilikuwa hakiridhishi.
Ahmed alisema kuwa moja kati ya wachezaji ambao wao kama uongozi walikuwa wanafikiri a kuwa atakuwa kiongozi kwa wachezaji wengine, ni yeye, lakini kutokuwa timamu kimwili kumesababisha kocha kuomba kutafutiwa mchezaji mwingine.
Alisema pia kuwa wakati wa maandalzi ya msimu mpya wa ligi walipoweka kambi kule Misri, kocha Fadlu alikuwa akimfuatilia na kuzungumza naye mara kwa mara, lakini bado hakuwa katika utimamu wa mwili.
“Kocha alizungumza naye mara kwa mara tangu alipowasili kambini lakini hakuweza kufanya zaidi atu alikuwa akishuka kila siku na ndiyo maana kocha alitaka kutafutiwa mchezaji mwingine haraka zaidi, ndipo tukamtafuta mwamba Christian Lionel Ateba”, alisema Ahmed.
Alisema pia kwamba suala la kuachana na Fredy, ni kutokana na matakwa ya kocha na ni kutokana na kutopedezwa na kiwango chake alichoonyesha kwenye mazoezi laini. Kwa sasa wamemalizana naye na hivyo wanaanza upya.
Aidha, alizungumzia juu ya kulidhishwa na kikosi chao, huku akiweka wazi kuwa msimu huu, pamoja na kuwa wanajenga timu, lakini wana mipango ya kuchua ubingwa msimu huu na kurudisha ufalme wao ambao waliupoteza kwa watani zao Yanga, lakini watahakikisha wanafanya vyema.
Mpaka sasa, klabu ya Simba imefanikiwa kucheza michezo miwili ya ligi dhidi ya Tabora United na Fountaine Gate na kufanikiwa kubeba alama zote 6 na kujikusanyia mabao 7 wakiwa juu katika msimmo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
Papa Fransisko katika tafakari yake, Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho, tarehe 15 Agosti 2024 anasema, Mama Kanisa anawaalika watoto wake kumtafakari Bikira Maria baada ya kupashwa habari kuwa atakuwa ni Mama wa Mungu aliondoka, akaenda hata nchi ya mlimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elizabeti, binamu yake! Rej Lk, 1: 39-56. Shuhuda wa furaha, matumaini na uzima wa milele.
Ilikuwa ni tarehe Mosi, Novemba 1950, katika Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu, Papa Pio wa kumi na mbili (1939-1958: wa 260) katika Waraka wake wa kitume.
“Munificentimus Deus” yaani “Mungu Mkarimu” alipotangaza kwamba, “Bikira Maria, Mama wa Mungu ambaye daima ni Bikira, amepalizwa mbinguni mwili na roho baada ya kuhitimisha safari yake ya hapa duniani,” kuwa ni fundisho tanzu la imani ya Kanisa Katoliki.
Hii ilitokana na sababu kwamba tangu mwanzo kabisa, Kanisa limekuwa linamwadhimisha Mama Bikira Maria kama Eva mpya, huku akihusishwa na Adam mpya, Mwanaye Bwana wetu Yesu Kristo.
Kumbe, kwa maneno mengine, Sherehe hii inapata chimbuko lake katika Mapokeo ya Kanisa, na hasa zaidi wakati wa Maadhimisho ya Mtaguso wa Efeso uliofanyika mwaka 431, ulipotamka kuwa Bikira Maria ni Mama wa Mungu, “Theotokos.”
Waamini wa Kanisa la Mashariki kwa miaka mingi walikuwa wanaiadhimisha Sherehe hii ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho, kama kielelezo cha kulala usingizi wa amani “Dormitio,” na wataalam wengine wakaongeza kusema, “Somnum Mariae.”
Hii ni Sherehe inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila Mwaka ifikapo tarehe 15 Agosti.
Mwili wa Bikira Maria uliokuwa umekingwa na dhambi ya asili, ukapalizwa mbinguni, hiki ni kielelezo makini cha imani ya watu wa Mungu kama alivyokiri Mtakatifu Yohane Paulo II (1978-2005 wa 264) mnamo mwaka 1997.
Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake, Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho, tarehe 15 Agosti 2024 anasema, Mama Kanisa anawaalika watoto wake kumtafakari Bikira Maria baada ya kupashwa habari kuwa atakuwa ni Mama wa Mungu, aliondoka, akaenda hata nchi ya mlimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elizabeti, binamu yake! Rej Lk, 1: 39-56.
Taarifa kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu, ili kumsukuma kuondoka kwa haraka, kwenda kutangaza na kushuhudia ile furaha iliyomwilishwa katika huduma.
Tangu wakati huo, Bikira Maria alianzisha mchakato wa kumfuasa Mwanaye Mpendwa Kristo Yesu, kama mfuasi halisi wa Ufalme wa Mungu, akadiriki hata kusimama chini ya Msalaba, na hatima ya hija hii ya maisha ya kiroho ni Kupalizwa kwake mbinguni, ambako huko juu mbinguni wanaendelea kufurahia pamoja na Kristo Yesu, maisha ya uzima wa milele.
Bikira Maria ni mfano wa mwamini anayesoma alama za nyakati, akawa tayari kufuata nyayo za Mwanaye mpendwa, akakutana na wafuasi wa Kristo Yesu, na baadaye safari yake ya kutangulia kwenda mbinguni, kwenye utukufu wa Baba wa milele.
Huu ni mwaliko kwa waamini kutambua kwamba maisha yao huku bondeni kwenye machozi, ni safari endelevu itakayofikia hatima yake kwa kukutana na Kristo Yesu, huko mbinguni.
Waamini wanahamasishwa kuhakikisha kwamba wanatunza moyoni mwao, kwamba Mwenyezi Mungu amewaumba, ili hatimaye, waweze kuwa na furaha ya uzima wa milele na kwamba, ndoto yake ni kuwachukua waja wake wote, ili wakaishi naye katika maisha ya uzima wa milele.
Safari ya maisha ya binadamu ni sehemu ya mpango wa upendo wa Mungu kwa binadamu. Hii ni hija inayowaongoza siku hadi siku, ili kukutana na Mwenyezi Mungu, chemchemi ya furaha isiyokuwa na mwisho; furaha ambayo amewaandalia waja wake.
Baba Mtakatifu Fransisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanarutubisha safari hii kwa matumaini na hasa pale, wanapokumbana na magumu pamoja na changamoto za maisha.
Maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni Mwili na Roho, iwe ni fursa makini kwa Waamini kujiuliza swali la msingi, ikiwa kama katika safari ya maisha yao hapa duniani, wanaendelea kuirutubisha kwa matumaini, kwa kutambua kwamba, mwisho wa safari yao, yuko Kristo Yesu anayewangoja.
Au katika safari hii ya maisha, tayari wamekwisha “kubweteka?” Je, Waamini wanakumbuka kwamba wameumbwa kwa ajili ya kufurahia maisha ya uzima wa milele; kwa kuwapenda na kuwathamini ndugu na jirani au Mwamini amejikuta akiwa amezama zaidi katika uchoyo na ubinafsi, na hatimaye kuzama katika malimwengu?
Mwishoni mwa tafakari yake, Baba Mtakatifu Fransisko amewaalika Waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kumwangalia, na hatimaye, kumwomba Bikira Maria ili aweze kuwaombea, ili kamwe wasisahau kwamba hatima ya maisha yao ni furaha na matumaini ya uzima wa milele. “Macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika Watakatifu jinsi ulivyo.” Efe 1:18.
Katika hatua nyingine, Kardinali Pierbattista Pizzaballa, O.F.M. Patriaki wa Yerusalemu na Mlinzi Mkuu wa Nchi Takatifu na Mlima wa Sion, katika Maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa mbinguni Mwili na Roho, yaliyofanyika kwenye Kanisa Kuu la Mateso lililoko kwenye Mlima wa Mizeituni ulioko Mashariki mwa mji wa Yerusalemu.
Papa Fransis alitumia fursa hii kwa ajili ya kuombea amani duniani, lakini zaidi huko Mashariki ya Kati.
Katika mahubiri yake amewaalika Waamini kumtafakari Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni mwili na roho kama zawadi kubwa kutoka kwa Mungu, changamoto kwa Walimwengu ni kuondokana na : vita, ghasia, machafuko; Utumwa mamboleo na biashara ya ubidhaishaji wa maumbile ya binadamu unaoendelea kudhalilisha: utu, heshima na haki msingi za binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, pamoja na ukoloni mamboleo.
Bikira Maria, Mama wa Yesu akiwa amekwisha kutukuzwa mbinguni mwili na roho, ni sura na mwanzo wa Kanisa ambalo litapata utimilifu wake katika ulimwengu ujao. Kadhalika anang’aa duniani kama alama ya hakika ya matumaini na ya faraja kwa taifa la Mungu lililo safarini, mpaka siku ya Bwana itakapokuja. LG 68.
Amezungumzia kuhusu madhara ya vita yanayowatumbukiza watu katika umaskini wa kisiasa, kiuchumi na kijamii, kwa kusigina, uhuru, utu, heshima na haki zao msingi. Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni, awaombee Walimwengu haki, amani na upatanisho.
MWANZA
Na Paul Mabuga
Maureen Mwanawasa, Mke wa Rais wa zamani wa Zambia, Levy Mwanawasa [2002 – 2008], amefariki Agost 13, 2024, jijini Lusaka nchini humo baada ya kuugua kwa muda mfupi. Kama ulipata nafasi ya kumfahamu, bila shaka utajiuliza kwa nini akina mama huku kwetu wanashindwa kuwashawishi wanaume wanne wao kwenda kanisani hasa baada ya kuonekana mahudhurio yao ni hafifu na yenye kulalamikiwa.
Fikiria mama wa ‘kibongo’ anaweza kumshawishi mume wake, kulipia hadi shilingi elfu 30 ama hata hamsini, kwa ajili ya kusuka nywele ili apendeze, ama anunulie gauni la mtoko la hadi shilingi 60,000/- na kumsaidia marejesho ya mikopo ya kausha damu, lakini anashindwa kumbembeleza mwanaume ahudhurie kanisani, jambo ambalo hata hivyo haligharimu fedha yoyote.
Safari yangu ya kukutana na Maureen Mwanawasa ilianzia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Keneth Kaunda jijini Lusaka, ambapo wakati natoka nje nikiwa miongoni mwa wageni waliowasili, nilipokelewa na mzee mmoja raia wa Tanzania. Nilishangaa baada ya kuwa licha ya mzee huyo kunizidi umri, lakini alipokea begi langu ambalo lilikuwa mzigo wangu pekee, na kunielekeza kwenye gari ndogo tukielekea katikati ya jiji la Lusaka. Juhudi zangu za kukataa mzee huyu kunibebea mzigo ili kulinda mila za Kiafrika, zilizogonga mwamba.
Hapo safari ikawa moja kwa moja hadi katika hoteli ya Pamodzi [yaani pamoja] ambayo baadaye niliambiwa kuna Marais na Wakuu wa Nchi 14 wanalala hapo, na ndiyo maana ulinzi ulikuwa mkali. Nikajisemea kimya kimya, itakuwaje siye kwa mazoea ya kabila letu kwamba ukinywa hata kabia kamoja, unaanza kuimba. Lakini kwa bahati, mratibu wa mambo akaniambia, “Bwana mdogo twende huku.’’ Nikapelekwa hoteli nyungine jirani ambayo nayo ilikuwa kubwa. Hii ilikuwa ni Agosti 15, 2007.
Jioni hiyo kukawa na zoezi ambapo watu wote waliokuwa wanatarajia kuingia katika vikao vya Marais na wakuu wa Nchi katika Jumuiya ya Nchi zilizo Kusini mwa Afrika [SADC], walitakiwa kufika katika kituo maalum, ambapo baada ya kuhakikiwa, walipigwa picha na kupewa Kitambulisho maalum. Hakuna aliyekuwa akiachwa kwenye hatua hii, isipokuwa mabwana wakubwa.
Wakati nimefikia hatua ya kupigwa picha, akaingia mama mmoja aliyevaa kitamaduni, na baadaye nikabaini kuwa ni mmoja wa wafanyakazi katika Ikulu wa King Mswati lll wa Eswatini. Kwa heshima yake na kwamba anatoka katika familia ya kifalme, jambo ambalo inaelekea Wazambia wanalijali, nikaambiwa nimpishe ahudumiwe kwanza yeye. Nikafanya hivyo, na mimi baadaye nikapata kitambulisho changu.
Asubuhi wakati nakwenda kwenye mkutano, ile naingia geti la kwanza, nikakutana na askari ambaye baada ya kutambua kuwa ninatoka Tanzania, akanionesha kitambulisho cha mmoja wa Mawaziri wa huku kwetu ambacho kumeokotwa. Akaniuliza, unamjua huyu na mimi nikamwambia, naam namjua ni mmoja wa mawaziri wetu, na akanionya, mtafute umpe hiki kitambulisho, vinginevyo hataingia humo ndani. Niliifanya kazi hiyo na baadaye kumkabidhi kitambulisho chake.
Wakati wa mapumziko, nilifanikuwa kuwa karibu na aliyekuwa Rais wa Namibia, Hifikipunye Pohamba, jamaa mrefu hivi, baada ya kumsalimia kwa Kiingereza na kuonesha nia ya kufanya naye mahojiano, aliinama na kusoma kutambulisho changu ambacho kilikuwa kikionesha pia ninatoka nchi gani. Baada ya kugundua ninakotoka akabadili lugha na kuniambia kwa Kiswahili, “habari za Dar es salaam, vipi Buguruni, mambo poa” Wakati naendelea kutafakari hatua ya kufuata, akaanza kuondoka na kuniaga. “Haya bwana, kazi njema!”
Jioni wakati wa mpango wa kazi, nikaitwa na mkuu wangu, nakwambiwa kuwa siku inayofuata, nitaambatana na wake wa Marais na Wakuu wa Nchi ambao watakuwa katika ziara wakiongozwa na mwenyeji wao, Mke wa Rais wa Zambia Maureen Mwanawasa. Siku hiyo ilipofika, tulianza ziara tukiwa katika mabasi mawili, moja likiwa la hao akina Mama Waheshimiwa na jingine la watu waliokuwa kwenye kazi mbali mbali, tukiwemo wanahabari wachache.
Tulipomaliza ziara iliyochukua hadi muda wa mchana, tulirudi katika hoteli ya Pamodzi, ambapo kulikuwa na maonesho ya bidhaa mbali mbali zinazozalishwa na wanawake nchini humo, ikiwa ni pamoija na vito. Mama Maureen hakusita kuwaambia kwa lugha yao akina mama wale, wafanye biashara, kwani hao waliowatembelea ni wake wa Marais. Nilitafsisriwa hicho alichokisema na mwandishi wa gazeti moja la nchini humo.
Baada ya ziara hiyo, akina mama hao wakawa na kikao chao, Mama Maureen Mwanawasa ambaye alikuwa Mwenyekiti wao, alisimama na kuwaambia juu ya ajenda muhimu, iliyohusu azimio lao la kutaka wanawake kupewa nafasi ya madaraka katika kile kinachojulikana kama hamsini kwa hamsini, yaani kama mkakati wa kijinsia wanawake wapewe nafasi katika ngazi mbali mbali katika kiwango cha uwiano sawa na wanaume.
Cha kufurahisha ni kwamba aliwaambia kesho yake watawasilisha hoja, na kwamba kila mmoja aitangulize hoja hiyo kwa mwenzi wake. Na inawezekana kila mmoja aliwasilisha hoja hiyo, maana ilipowasilishwa na Mama Maureen Mwanawasa siku iliyofuata mbele ya Wakuu wa Nchi, hakukuwa na mjadala bali Viongozi hao walipiga makofi kama ishara ya kuiunga mkono, na ikapita, na kuanzia hapo imekuwa ajenda ya kudumu katika Nchi hizo.
Ukiacha hilo, lakini Maureen Mwanawasa amekuwa na ushawishi mkubwa katika mambo mbali mbali enzi ya uhai wake, ikiwa ni pamoja na harakati ya kupambana na umaskini, na pia akiongoza Wake wa Marais na Wakuu wa Nchi katika Jumuiya ya SADC katika kupambana na madhira ya UKIMWI na Virus vya UKIMWI.
Ni Mwanamke ambaye alitumia nguvu ya ushawishi wake katika kupeleka ajenda. Anasifika pia katika kuendesha kampeni za kisiasa kupigania ushindi wa mume wake katika chaguzi.
Maureen alizaliwa April 28. Mwaka 1963 katika eneo la Kabwe nchini Zambia. Aliolewa na Mwanasheria Levy Mwanawasa Mei 07, 1987. Mumewe alifariki mwaka 2008 akiwa madarakani, na Mwenyezi Mungu aliwajalia watoto wanne, ambapo watatu ni wa kike na mmoja ni wa kiume.
Kwa njia ya ushawishi wa akina mama kwenye hamsini kwa hamsini, dada zetu, shemeji zetu, shangazi na mama zetu wanashindwaje kuwashawishi wanaume kushiriki kwenda kanisani? Kwa nini nguvu hii ambayo haihitaji rasilimali fedha, haitumiki kupunguza changamoto hii, ambayo inaelekea kuwa sugu?
Kuna wakati ukihudhuria kanisani, unakuta uwiano ni wanawake kuwa theluthi mbili na wanaume theluthi moja. Unakaa kwenye jumuia unakuta ni wanawake na watoto, labda na mwanume mmoja. Kama akina mama wanaweza kuzengea fedha ya kucha, nywele na marejesho wanashindwaje kuwashawishi wanaume kwende kanisani?
Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Yohane Paulo ll, Buyuni, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es salaam, Padri Bartazari Minde akibariki vipaji wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Bikira Maria, iliyoadhimishwa hivi karibuni parokiani hapo.
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo akikata utepe Hospitali ya Saratani ya Good Samaritan iliyopo katika Jimbo Katoliki la Ifakara. Wa pili kulia ni Askofu wa Jimbo Katoliki la Ifakara, Mhashamu Salutaris Libena (mwenye miwani) na kushoto kwa Kardinali ni Mhashamu Lazarus Msimbe, Askofu wa Jimbo Katoliki la Morogoro. (Picha na Michael Ally)
Baadhi ya Waamini wa Parokia ya Mtakatifu Yohane Paul II, Buyuni, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakiwa katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Bikira Maria iliyoadhimishwa parokiani hapo.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu, akiongoza Sala wakati wa utoaji wa Daraja Takatifu la Upadri kwa Shemasi Peter Masaga (aliyelala kifudifudi), wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu, iliyofanyika Parokia ya Mtakatifu Gaspar Del Bufalo, Mbezi Beach, jimboni humo. (Picha na Yohana Kasosi)
Padri Peter Masaga akipokea zawadi kutoka kwa Viongozi wa Halmashauri ya Walei wa Parokia ya Mtakatifu Gaspar Del Bufalo, Mbezi Beach Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, iliyofanyika hivi karibuni parokiani hapo. (Picha na Yohana Kasosi)
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu (katikati aliyeshika fimbo ya Kichungaji) na Mapadri, wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Halmashauri ya Walei wa Parokia ya Mtakatifu Maria Salome, Kimara, Jimboni humo.
VATICANCITY, Vatican
Baba Mtakatifu Fransisko amekumbusha Wenyeheri wapya, Wamisionari Waxaveri wa Kiitaliano waliotangazwa kuwa wenyeheri Agosti 18, mwaka huu, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC.
Baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Baba Mtakatifu Fransisko alisema kuwa kutangazwa kwa Wenyeheri hao kutakuwa kitulizo cha vita nchini DRC,
“Kifo chao cha kishahidi kilikuwa kilele cha maisha yaliyotumiwa kwa ajili ya Bwana, na kwa ajili ya ndugu zao…mfano wao na maombezi yao yatie moyo njia za upatanisho na amani kwa manufaa ya watu wa Congo,”alisema Baba Mtakatifu Fransiko.
Baba Mtakatifu Fransisko alikumbuka tukio la kutangazwa Wenyeheri wapya katika nchi ya Afrika na kueleza kwamba:
“Huko Uvira katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Luigi Carrara, Giovanni Didoné na Vittorio Faccin, Wamisionari Waxaveri wa Kiitaliano, walitangazwa kuwa Wenyeheri, pamoja na Albert Joubert, Padre wa Congo, waliouawa katika nchi hiyo Novemba 28, 1964.
Baba Mtakatifu aliendelea kutazama hali halisi ya ulimwengu wa vurugu kama kawaida yake, alisema: “Na tunaendelea kuomba kwamba njia za amani ziweze kufunguliwa katika Mashariki ya Kati - Palestina, Israel - na vile vile katika Ukraine inayoteswa, Myanmar na katika kila eneo la vita, kwa kujitolea kwa mazungumzo na majadiliano na kujiepusha na kujibu kwa vitendo vya vurugu.
Aliwaasalimia Waamini wote kutoka Roma na Mahujaji waliotoka Italia na nchi mbalimbali. “Hasa ninawasalimu wale wanaotoka Jimbo la Mtakatifu Paulo nchini Brazili; na pia Masista wa Mtakatifu Elizabeth.
“Ninatuma salamu zangu na baraka zangu kwa wanawake na wasichana waliokusanyika katika Madhabahu ya Maria wa Piekary Šlskie huko Poland, na ninawatia moyo kushuhudia Injili kwa furaha katika familia na katika jamii.”
Aidha, Baba Mtakatifu Fransisko aliwasalimu watoto wa Parokia ya Moyo Safi wa Bikira Maria kutoka Roma. Hatimaye amewatakia Dominika njema, huku akiwaomba wasisahau kumuombea. Mlo mwema, mchana mwema na kwaheri ya kuonana.
MTWARA
Na Ibrahim Munanka – SJMC
Maaskofu wa Makanisa ya Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kusini Mashariki na Kanisa la Anglikana Tanzania Dayosisi ya Lindi –Masasi wamesema kuwa kazi ya Uinjilishaji katika maeneo hayo inakabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa Wachungaji na rasilimali fedha.
Wakizungumza na gazeti Tumaini Letu katika mahojiano maalumu yaliyofanyika mkoani Mtwara hivi karibuni, Viongozi hao wa Dini waliyoko katika Mikoa ya Lindi na Mtwara, akiwemo Askofu Yeriko Ngwema wa Kanisa la KKKT Dayosisi ya Kusini Mashariki (Mtwara na Lindi), na Askofu Dk. James Almas wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Dayosisi ya Masasi, waliwataka Wakristo waishio mijini kushiriki kikamilifu kuunga mkono juhudi za uinjilishaji katika maeneo ya misioni, ambako bado kuna changamoto kubwa za kimisionari na kiroho.
Wachungaji bado tatizo katika Uinjlishaji:
Kwa upande wake, Askofu Yeriko Ngwema alisema kuwa wanakabiliwa na uhaba wa Wachungaji na changamoto za kifedha ambazo zinakwamisha mipango ya maendeleo ya Kanisa katika maeneo hayo.
Alifafanua kuwa eneo hilo lina Makanisa 15 pekee na Wachungaji ni wachache kiasi kwamba mmoja analazimika kusafiri kutoka kituo kimoja cha kazi hadi kingine kuendesha ibada kwa waamini.
“Wakati mwingine, Mchungaji mmoja anaweza kuendesha ibada katika vituo vitatu tofauti kwa siku moja,” alisema Askofu Ngwema.
Aliongeza kuwa historia ya Ukoloni na Dini zilizotangulia katika maeneo hayo zilileta ugumu kwa watu kupokea mafundisho mapya ya Kikristo.
Kwa upenda wake, Dean Geofrey John Mposola, Msaidizi wa Askofu Ngwema, alisema kwamba uinjilishaji katika vijiji ni muhimu zaidi.
Alieleza kuwa Wakristo mijini wanapaswa kuiombea misioni ili kuwasaidia wale wanaopinga Injili, ili waipokee.
“Huku vijijini kuna utajiri mkubwa wa watu ambao hawajawahi kuipokea Injili, ni jukumu letu kufika huko,” alisema Dean Mposola.
Mchungaji ahudumia makanisa mengi:
Naye Askofu Dk. James Almas wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Dayosisi ya Masasi, alisema kuwa changamoto zinazolikabili kanisa lake kwenye maeneno hayo, linajumuisha eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 68,000.
Askofu Almas alisema kuwa licha ya juhudi za kuhubiri Injili kupitia mikutano ya nje na semina za ndani, changamoto za kiuchumi zimeathiri maendeleo ya Kanisa hilo.
“Uchumi wa eneo hili ni mgumu kutokana na hali ya hewa isiyotabirika, mvua zinaponyesha sana au kutoponyesha kabisa, mazao yanaharibika, na hii inaathiri uwezo wetu wa kuwatunza Wachungaji,” alisema Askofu Almas na kuongeza,
“Kwa sasa, matunzo ya wachungaji yamekuwa magumu sana, hali ambayo inawafanya wengi kushindwa kumudu mahitaji yao ya kimsingi….
“Licha ya changamoto hizo, Dayosisi ya Masasi imepiga hatua katika uinjilishaji, ambapo mwaka 2023, Idara ya Wanawake ilieneza Injili vijijini, na watu wanane kutoka madhehebu mengine ya dini walibatizwa na kuwa Wakristo.
Semina zasaidia kueneza Injili Vijijini:
Askofu Almas alisema kuwa jitihada hizo ni matokeo ya juhudi kubwa za semina za ndani kwa Waamini na mikutano ya Injili.
Askofu Almas alibainisha pia kuwa malengo makuu ya dayosisi ni kuongeza watumishi wa Injili, hasa wanawake na vijana, pamoja na kujitegemea kiuchumi.
Alieleza kuwa wameanza kuwaandaa wanawake wawili kwa ajili ya kupata Diploma ya Theolojia, na wengine 12 wakiwa na Vyeti kutoka vyuo mbalimbali kama Bunda Bible College na Nairobi Salvation Army.
Hata hivyo, changamoto ya ukosefu wa wataalamu wa ujenzi imekuwa kikwazo kikubwa, kwani Kanisa linajitahidi kukamilisha ujenzi wa makanisa makubwa 72, lakini hakuna watu wenye ujuzi wa kuyajenga mpaka kufikia hatua ya kupaua.
“Tunawaomba Wakristo wenye ujuzi mbalimbali kujitolea kusaidia katika kazi hii kwa ajili ya ufalme wa Mungu,” alisema Askofu Almasi.
Wakristo wanapaswa kukumbuka agizo kuu la Bwana Yesu Kristo, lililopo katika Injili ya Mathayo, 28:19, linalowataka kwenda na kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wa Bwana Yesu Kristo kwa mafundisho na kwa kuwabatiza. Wito huu unawataka kutoka mahali walipo na kuwaendea watu kwa mali na vipawa, pamoja na nguvu.
DAR ES SALAAM
Na Mathayo Kijazi
Vijana wanapopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, wametakiwa kusimama imara, kujitambua na kuelewa wajibu wao wa kuishi maisha bora ya Imani Katoliki kama walivyofundishwa.
Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba OSA, wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 166 katika Parokia ya Mtakatifu Agustino – Ukonga, jimboni humo.
Askofu huyo alisema kuwa dhambi ni kikwazo katika ubinadamu, ambacho kinawafanya watu wawe vipofu na kushindwa kumwona Mungu katika maisha yao.
“Kwa hiyo ndugu zangu tutambue kwamba dhambi ni kikwazo katika ubinadamu, ambacho kinawafanya watu wawe vipofu na washindwe kumwona Mungu. Tuishi maisha ya kumpendeza Mungu,” alisema Askofu Musomba.
Vile vile, aliwasihi vijana waliopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kuepuka kuyumbishwa, huku akiwasisitiza kubaki katika imani yao Katoliki kwani wao wamekuwa ni Askari hodari wa Kristu.
Aliwaagiza Wazazi, Walezi na Waamini wote kwa pamoja, kushirikiana katika kusimamia malezi ya vijana hao, kwani kwa kufanya hivyo, Kanisa litapata watendaji walio bora.
Katika homilia hiyo Askofu Musomba pia aliwasihi Waamini kutokuisaliti imani yao na kutokuionea haya, akisema kwamba kufanya hivyo, ni kupotea katika imani.
Pia, alisisitiza kuepuka kiburi na majivuno katika mazingira wanayoishi, akiwasisitiza kuguswa na Roho Mtakatifu pamoja na kusikiliza kila wanachoelezwa.
“Epukeni kiburi na majivuno, kwamba bila mimi, hiki hakiwezi kufanyika. Jitahidini kuishi maisha ya kuguswa na Roho Mtakatifu huku mkisikiliza kila mnachoelezwa,” alisema Askofu Musomba.
Aliwataka Waamini kutambua kwamba ni wajibu wao kuiishi pamoja na kuishuhudia imani siku zote za maisha yao, kwani wao ni sura na mfano wa Mungu.
Katika hatua nyingine Askofu Musomba aliwashukuru Waamini wa Parokia ya Ukonga kwa ukarimu waliouonyesha kwake, kwani hiyo imemfanya ajihisi kuwa yuko nyumbani.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri James Mweyunge alisema kuwa alipo Askofu, ndipo Kanisa lilipo, hivyo ni furaha kwao kusali pamoja na Askofu katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu.
Padri Mweyunge aliwashukuru walimu (Makatekista) waliowafundisha vyema vijana hao hadi wameweza kufahamu mambo mengi yanayohusu Imani Katoliki.
IFAKARA
Na Celina Matuja
Wakati Serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa, Mbunge wa Jimbo la Rufiji, kutangaza rasmi kuanza kwa mbio za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27 mwaka huu, Askofu wa Jimbo Katoliki la Ifakara, Mhashamu Salutaris Libena, ametoa ya moyoni.
Uchaguzi huo ni muhimu kwani utatoa fursa kwa wananchi kuwachagua Viongozi wa mitaa na vijiji, na ni maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wa mwakani.
Askofu Libena alisema hayo hivi karibuni katika Mahojiano Maalumu na gazeti Tumaini Letu ofisini kwake Jimboni Ifakara, kuhusu uchaguzi huo.
Alisema kwamba ni muhimu kwa Waamini wote kujitokeza kushiriki katika masuala ya kitaifa kwa kuwa ni haki ya kila raia Mtanzania, bila kujali dini, ili kupata viongozi wazuri na wanaowataka kwa maendeleo yao.
Askofu Libena aliwataka Waamini wa Jimbo hilo kujitokeza kwa wingi kujiandikisha, kugombea kupiga kura, kugombea na kushiriki katika Uchaguzi huo ili kupata viongozi bora wa Serikali za Mitaa kwa maendeleo ya Nchi, na Kanisa kwa ujumla.
Aliongeza kuwa ni vizuri pia kuwapatia elimu vijana kuhusu uchaguzi wa serikali za mitaa kwa kuzingatia uzalendo, na wasitumiwe na mamluki kuuza haki yao ya kuchagua au kuchaguliwa katika ngazi zote za uongozi serikalini.
Alisema pia kuwa vijana ni hazina ya Taifa, hivyo wasipoelimishwa vizuri, watapotea na kupoteza haki yao ya kuchagua au kuchaguliwa.
Askofu Libena alisisitiza waamini kujiandikisha sasa wakati tangazo la serikali limeshatolewa, ili wasipate shida wakati wa kupiga kura, lakini pia kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura ili kuonyesha ukomavu wa kisiasa badala ya kujiandikisha na kuwaachia wengine kupiga kura.
Kwa mujibu wa Askofu Libena, ni muhimu kwa Mkristo kujitokeza na kushiriki uchaguzi huo na ujao, kwani utampatia nafasi ya uwakilishi katika kuiongoza Jamii na Kanisa kwa ujumla.
Inavyoeleza Katiba kuhusu Uchaguzi:
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, Ibara 145 na 146 inaelezea uwepo wa Serikali za Mitaa pamoja na madhumuni yake. Mojawapo ya madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi.
Aidha, Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288, zinaelekeza kufanyika kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Lengo ni kuzifanya Serikali za Mitaa ziongozwe kidemokrasia.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 201A cha Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na Kifungu cha 87A cha Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa ana mamlaka ya kutunga Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, ambazo hutumika kuongoza uchaguzi huo.
Viongozi wanaochaguliwa katika ngazi hizi ni Wenyeviti wa Vijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji, Wenyeviti wa Mitaa, Wajumbe wa Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa vitongoji.
Uchaguzi wa mwisho wa Serikali za Mitaa ulifanyika mwezi Novemba mwaka 2019, hivyo, uchaguzi mwingine unatakiwa kufanyika Novemba, 2024.
Uchaguzi huu unaongozwa na Kanuni za Uchaguzi wa Viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ngazi ya Vijiji, Vitongoji na Mitaa katika Mamlaka za Wilaya na Mamlaka za Miji, kwa mujibu wa Matangazo ya Serikali Na. 571, 572 573 na 574 ya Mwaka 2024.
Kwa mujibu wa Kanuni hizi, Waziri wa TAMISEMI anapaswa kutoa Tangazo la Uchaguzi likiainisha ratiba, shughuli za uchaguzi zinazohusika na masharti muhimu ya uchaguzi.
Masharti muhimu ya kuzingatia katika Uchaguzi huo ni kama ifuatavyo:- (a) Nafasi zitakazogombewa katika uchaguzi huu ni Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi mchanganyiko la wanaume na wanawake), Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi la wanawake) na Wenyeviti wa Vitongoji katika Mamlaka za Wilaya.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Wilaya za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 571 la Mwaka 2024), (ii) Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo.
Kwa nafasi hiyo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 572 la Mwaka 2024) (iii) Mwenyekiti wa kijiji, wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi mchanganyiko la wanaume na wanawake), wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi la wanawake) na wenyeviti wa vitongoji katika Mamlaka za Miji.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na.573 la Mwaka 2024) (iv) Mwenyekiti wa mtaa na wajumbe wa kamati ya mtaa (Kundi Mchanganyiko la Wanaume na Wanawake) na wajumbe wa kamati ya mtaa (Kundi la Wanawake) katika Mamlaka za Miji.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mtaa na Wajumbe wa Kamati ya Mtaa katika Mamlaka za Miji za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 574 la Mwaka 2024).
RUVUMA
Na Mwandishi wetu
Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga amesema kwa Serikali imetenga takribani Shilingi bilioni 4.6/- kupeleka umeme kwenye maeneo ya migodi mkoani Ruvuma.
Kapinga (pichani) aliyasema hayo wakati akizindua Kituo cha Mauzo ya Makaa ya Mawe ya kampuni ya Market Insight Limited (MILCOAL), inayojihusisha na uchimbaji, uuzaji na usambazaji wa makaa ya mawe, Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.