Dekano wa Dekania ya Mtakatifu Gaspar na Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Dominick Somola, akisalimiana na Waamini wa Chama cha Moyo Mtakatifu wa Yesu wa Parokia ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu, Makongo Juu, baada ya kushiriki Adhimisho la Misa Takatifu iliyofanyika katika Parokia ya Bunju, hivi karibuni.
Paroko mpya wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Mungu, Mbopo-Madale, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, (wa tatu kutoka kushoto), akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kamati Tendaji ya Parokia hiyo, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Kumsimika Paroko huyo, iliyofanyika hivi karibuni parokiani hapo. (Picha zote na Yohana Kasosi)
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, akiwa na Mapadri katika picha ya pamoja na vijana 153 waliopata Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Augustino, Salasala jimboni humo, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Kipaimara. Kulia kwa Kardinali ni Paroko wa Parokia hiyo, Padri Peter Assenga.
DAR ES SALAAM
Na Mathayo Kijazi
Imeelezwa kuwa hakuna kitu kinachoweza kufanywa na Waamini katika Parokia, bila kumshirikisha Askofu Mkuu, kwani vitu vyote ni mali ya Jimbo.
Kauli hiyo ilitolewa hivi karibuni na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba wakati wa homilia yake katika Adhmisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 80 wa Parokia ya Mtakatifu Teresa wa Benedicta wa Msalaba – Msumi, jimboni Dar es Salaam.
“Maeneo yote hayo mliyoyanunua, mjue kwamba ni mali ya Jimbo, sawa jamani. Kwa hiyo, msije mkaanzisha kitu chochote kile, bila kumhusisha Askofu Mkuu, kwa sababu nilisikia tetesi tetesi kwamba mnataka kununua sijui shamba la kuzikia, mkienda kienyeji bila baraka ya Askofu Mkuu, ni kosa,” alisema Askofu Musomba.
Awali, katika homilia yake Askofu huyo aliwataka wazazi kuongeza usimamizi kwa watoto wao waliopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, kwani hiyo itawasaidia watoto hao kutambua wajibu wao walioitiwa.
“Kwa hiyo wazazi na walezi, ni jukumu lenu kuongeza usimamizi kwa watoto hawa kwa sababu hiyo ndiyo njia itakayowafanya watambue wajibu wao. Hakikisheni watoto hawa wasiyumbishwe wala wasichanganywe katika imani,” alisema Askofu Musomba.
Vile vile, alisema kuwa mtoto anapopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, anatakiwa kushuhudia kile anachokiishi, kwani kwa Sakramenti hiyo, tayari ameimarika.
Aliongeza kuwa Sakramenti hiyo Takatifu ina umuhimu mkubwa kwa kila anayeipokea, kwa sababu inamkamilisha katika Neema ya Ubatizo, na kumkamilisha pia katika imani Katoliki.
Sambamba na hayo, Askofu huyo Msaidizi aliwakumbusha Wakristo kutambua kwamba zawadi ya Kristo mfufuka kwa Waamini wake, ni amani.
Wakati huo huo, Askofu huyo, aliwasihi Waamini wa Parokia ya Msumi kumshukuru Mungu, kwani kupitia Adhimisho hilo la Misa Takatifu, wamepata Wakristo wengine 80 waliokomaa ambao ni Waimarishwa.
Aliwashukuru Waamini wa Parokia hiyo kwa kuwachangia Skauti Shilingi laki 3 kwa ajili ya Kongamano lao linalotarajia kufanyika jimboni humo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Frank Werema, katika risala yake, alisema kuwa miongoni mwa mambo wanayoendelea kuyafanya kiroho, ni pamoja na kuwahamasisha Waamini ambao bado hawajafunga ndoa, wafunge, kwani kaya zaidi ya 482, wakazi wake hawajafunga ndoa.
Akizungumzia changamoto zinazowakabili hadi sasa parokiani hapo, Mwenyekiti huyo alisema kwamba kubwa ni ubovu wa miundombinu ya barabara katika maeneo ya Parokia hiyo.
Naye Mwandishi Laura Chrispin, anaripoti kuwa, Watoto wanaopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara wametakiwa kufahamu kuwa wanampokea Roho Mtakatifu kwa mara ya pili atakayewaongoza siku zote za maisha yao.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Martha -Mikocheni, alisema kuwa hata kipindi cha Mitume kabla ya kumpokea Roho Mtakatifu, Mitume mara zote walikuwa ni watu wa kuuliza maswali lakini baada ya kumpokea Roho Mtakatifu, walikuwa ni watu wa ushuhuda zaidi.
Hiyo ikiwa ni kama funzo kwenu kuwa inawapasa kuwa ni watu wa kumshuhudia Kristu kwa matendo yenu wenyewe, pamoja na kueleza makuu ya kristu kwa watu wengine.
Alisema hata katika Sinodi ya Maaskofu, inatuelekeza kutembea pamoja na kuwataka wengine wasibaki nyuma bali kutembea pamoja, ndiyo maana ukisema Kanisa la Kisinodi unaseama Ushirika na Ushiriki wa Kimisionari.
Katika Ushirika hawa ni Wanajumuiya, Wanafamilia ambayo kuna huduma wana hudumiana na kufanya kazi zote kwa pamoja na ni washiriki, ndo mana wanakuwa Wamisionari.
Mhashamu Musomba alisema “Roho Mtakatifu anavyokuja kwetu, anatufanya tuzungumze Lugha moja, hiyo ambayo ni katika upendo zaidi”.
Askofu Musomba aliwataka Waamini kuwa na amani katika familia zao na kumwomba zaidi Mungu awaepushe na dhambi kwani dhambi ni mojawapo ya sababu inayopelekea kupotea kwa amani.
Aidha, aliwataka Waamini kutosahau baadhi ya dhambi, hasa dhambi ya jamii ambayo ni kwa mtu yeyote anaweza kufanya mfano kwa wafanya biashara kutengeneza chakula kwa uchafu na kusababisha magonjwa kwa jamii, hiyo ni dhambi na inakupasa kuiungama mara moja.
Askofu Musomba alitoa wito kwa wazazi na walezi kwa kuwataka wasaidie kuwasindikiza katika imani moja ya Kanisa Katoliki, na siyo kuwachanganya watoto katika imani zingine.
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, amewataka Waamini wamtangulize Mungu, wanapofanya jambo lolote, ili wapate neema kamili.
Kardinali Pengo alisema hayo katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 150, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Augustino – Salasala, jimboni Dar es Salaam.
“Watu wengi huwa wanapenda kujifanyia mambo wanayoyajua wao, na kuamua kumuacha Mungu. Ukijifanyia kitu bila kumtanguliza Mungu huwezi kufanikiwa,” alisema Kadrinali Pengo na kuongeza, “Hata kama unatamani na wewe uje kuwa Rais wa Taifa hili la Tanzania, au unataka uje kuwa mfanyabiashara mkubwa katika nchi hii, lazima umtangulize Muumba wako ambaye ni Mungu Baba iliyekubariki ili uweze kufaulu vizuli.”
Aliwasihi vijana waliopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kufahamu kwamba, sasa wamekuwa Wakristo kamili, akiwasisitiza kuyazingatia mafundisho ya Kanisa ili waendelee kudumu katika imani.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Peter Assenga aliwaomba wazazi na walezi wa vijana hao wasihame imani yao Katoliki, kwani ndiyo imani ya kweli.
Alimshukuru Kardinali Pengo kwa kuwapatia vijana hao Sakramenti Takatifu ya Kipaimara.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei wa parokia hiyo, Boniface Ngowi alisema kuwa kwa sasa Parokia hiyo imepata mafanikio makubwa, kwani wamejenga kanisa jipya kubwa ambalo lilitabarukiwa na Kardinali Pengo, alisema kuwa wao kama Parokia, wamejenga nyumba kubwa ya kisasa ambayo ilibarikiwa na kuzinduliwa na Askufu Mkuu wa Jimbo hilo, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi.
KIGOMA
Na Mwandishi wetu
Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amewahakikishia Watanzania kuwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuleta mapinduzi kwenye Sekta ya Umwagiliaji, hivyo miradi yote aliyoahidi itatekelezwa.
Waziri Bashe alisema hayo wakati akizungumza na wadau wa umwagiliaji katika eneo la mradi wa Luiche, ambapo amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha utekelezaji wa mradi huo.
“Leo tumefanya uzinduzi wa Mradi Mkubwa wa Umwagiliaji katika Bonde la Luiche Wilayani Kigoma katika Mkoa wa Kigoma. Miradi hiyo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 60 itakwenda kunufaisha zaidi ya wakulima 9312 kupitia Kilimo cha Umwagiliaji,”alisema Bashe.
Waziri Bashe alisisitiza kwamba utekelezaji wa miradi hiyo unaofanywa na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, si hadithi, bali umelenga kuinua Sekta ya Kilimo cha Umwagiliaji, na kuchochea ukuaji wa uchumi nchini.
Aliitaka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kujipanga kuhakikisha wanatekeleza miradi hiyo, na wananchi wapuuze wanaowalaghai kuuza mashamba.
Aliongeza kuwa wizara inamshukuru Rais Dk. Samia kwani anafanya kwa vitendo na hataki utani katika kilimo cha umwagiliaji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, Raymond Mndolwa alimshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kufanikisha utekelezaji wa mradi wa Bonde la Luiche, ambao umekuwa ukizungumzwa tangu nchi ilipopata Uhuru, na kwamba uwekezaji huo mkubwa uliofanywa na serikali unakwenda kuleta mapinduzi makubwa kiuchumi kwa wananchi wa Kigoma.
Mndolwa pia ametumia fursa hiyo kupokea maagizo ya Waziri wa Kilimo.
“Mradi huu ni mkubwa na utazingatia uwekaji wa miundo mbinu muhimu kama barabara na itazingatia kulinda vyanzo vya maji na mazingira”, alisema Mndolwa.
Mndolwa pia aliongeza kuwa Tume ilipokea maelekezo ya Serikali kuwa mradi ujumuishe ujenzi wa ghala, nyumba ya watumishi, pamoja na Ofisi ya Umwagiliaji.
Akiwasilisha Taarifa ya Umwagiliaji kwa Mkoa wa Kigoma, Mhandisi Umwagiliaji Mkoa wa Kigoma, Katuta Mustang, alisema kwamba Mkoa wa Kigoma una eneo linalofaa kwa umwagiliaji lenye ukubwa wa hekta 147,000 ukiwa na skimu 59 za umwagiliaji skimu 6 pekee ndizo zilizoendelezwa.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Salum Kalli alisema serikali itahakikisha ulinzi wa mradi huo.
Akimkaribisha Waziri wa Kilimo, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto Thobias Andengenye, aliishukuru serikali kwa uwekezaji Mkubwa unaofanywa katika Mkoa wa Kigoma, kupitia kilimo cha umwagiliaji.
Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini, Ngenda Shabani Kirumbe,alimshukuru raid Dk. Samia Suluhu Haasan kwa kufanikisha utekelezaji wa Mradi wa Luiche.
Mradi wa Luiche upo katika wilaya ya kigoma, mkoa wa Kigoma. Mradi huu unajumuisha vijiji vya Kamara, Simbo, Kaseke, Nyamori, Msimba, Matiazo pamoja na Kagera. Mradi huu utakuwa na ya hekta 3000 zitakazomwagiliwa baada ya ujenzi kukamilika. Mradi huu wa Luiche umegawanyika katika mikataba miwili ambayo ni Mkataba wa ujenzi wa bwawa pamoja na mkataba wa ujenzi wa skimu ya umwagiliaji.
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, ameonya tabia ya unyanyasaji na ukatili unaofanyika dhidi ya watu wenye ualbino, kwani hali hiyo inaleta hofu kubwa katika jamii.
Kardinali Pengo alitoa onyo hilo katika Adhmisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 35, wa Parokia ya Utatu Mtakatifu – Changanyikeni, jimboni Dar es Salaam.
“Unaposikia kuna mtoto anauawa, eti kisa ni albino, na moja kati ya watu waliohusika, ni baba yake mzazi, unaanza kupata hofu ya ajabu. Mtoto bila kosa lake amezaliwa vile,” alisema Kardinali Pengo.
Alisema kuwa Waimarishwa hao, moja ya mambo wanayotakiwa kuyafanya, ni kuleta utofauti, ikiwemo kuhakikisha kwamba kila wanapokwenda, wanapeleka mwanga wa Injili.
Aidha, aliongeza kuwa wasiruhusu popote walipo pakose mwanga wa Injili, badala yake watekeleze wajibu huo kwa matendo, na si kwa maneno pekee.
Katika homilia yake, Kardinali Pengo aliwataka Waimarishwa hao kutambua ukuu wa jukumu walilopewa kwa mfano wa maisha, na si vinginevyo.
Aliwashauri Wanachanganyikeni kwamba kama wataweza, wajenge shule ya Chekechea itakayohudumiwa na Watawa katika eneo la Parokia yao.
Kwa upande wake, Rita Mzava, mmoja wa Waimarishwa, akisoma risala yao kwa niaba ya vijana wenzake, aliuomba Uongozi wa Jimbo hilo kuwawekea utaratibu wa kuendelea kupatiwa Mafundisho ya Imani, ili waendelee kuiishi imani yao.
Kwa mujibu wa risala iliyosomwa, Parokia ya Utatu Mtakatifu – Changanyikeni, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, ina jumla ya Waamini wapatao 1,500.
DAR ES SALAAM
Viongozi wa Halmashauri ya Walei wa Parokia za Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wametakiwa kuacha kuingia kwenye mizozo na malumbano na Maparoko, ili kazi ya Mungu isonge mbele.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 34, katika Parokia ya Bikira Maria Mama wa Mungu – Mbopo Madale, jimboni Dar es Salaam.
“Viongozi mhakikishe mnadumisha mshikamano na Maparoko wenu, kwani kwa kufanya hivyo, kazi ya Mungu itasonga mbele,”alisema Askofu Mchamungu.
Akitoa nasaha kwa Wasimamizi, Askofu Mchamungu alisema kuwa: “Wasimamizi nawaomba sana mshikamane na wazazi au walezi wa vijana hawa kuwalea kiimani, maana wewe umepewa jukumu hili umsaidie mlezi au mzazi kumsimamia huyu kijana…
“Sasa jukumu ni lako, umuongoze ili aweze kuiishi vizuri imani yake ya Ukristo, maana wasimamizi wengi wakimsimamia kijana wakafurahi siku hiyo, basi hana muda naye tena, hamfuatilii wala kuwajulia hali, inakuwa imetoka,” alisema Askofu Mchamungu.
Aliwasisitiza Waimarishwa kutoacha kwenda kusali, kujifuza, pamoja na kushiriki shughuli mbalimbali za Kanisa, kwani wakifanya hivyo, watakuwa vijana wema na wenye nguvu ya Roho Mtakatifu waliyempokea.
Aidha, aliwaasa vijana hao kutodanganywa na manabii wa uongo katika maeneo wanayoishi.
Padri Luwena asimikwa rasmi:
Katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu, Askofu Mchamungu alimsimika rasmi Paroko wa Parokia hiyo, Padri Joseph Luwena akiwaomba Waamini kushirikiana naye vizuri katika kazi zake za Kitume.
Aidha, aliwasihi Waamini wa Parokia hiyo kuongeza jitihada juu ya ujezi wa nyumba ya Mapadri, ili ujenzi huo ukamilike kwa wakati, na Paroko aweze kuishi sehemu bora.
“Hakikisheni Paroko wenu anakaa mahali pazuri, kwa sababu anawahudumia kiroho. Mmpende, mmjali, mthamini, kwa kuwa Paroko huyu mmekabidhiwa na Askofu Mkuu wa Jimbo, kwa hiyo msipomjali, sio vizuri…
Kwa upande wake, Padri Joseph Luwena aliwaomba Waamini wa Parokia hiyo kumpa ushirikiano, ili aweze kufanya kazi kwa amani, akimshukuru Askofu Mchamungu kwa kuwapatia sakramenti vijana hao.
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
Diwani wa Kata ya Makurumla Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo Mkoani Dar es Salaam, Bakari Kimwanga, amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanakuwa na utulivu hasa kutokana na taharuki ya utekaji watoto kwenye shule.
Pamoja na hali hiyo, amesema kuwa mpaka sasa ndani ya Kata ya Makurumla, hakuna tukio la kutekwa kwa mtoto, huku akiweka wazi kuwa ni lazima kila mwana jamii ahakikishe anatoa ulinzi kwa mtoto, hasa wanapokuwa mitaani.
Kauli hiyo aliitoa hivi karibuni alipokuwa akizungumza na wazazi, walezi na waalimu katika shule za Msingi za Mianzini, Karume na Dk. Omari, ambapo juzi ilizuka taharuki ya kutekwa watoto kwenye shule hizo, na kuibua sintofamu kwa wazazi kulazimika kuvamia shule ili kuona usalama wa watoto wao.
“Tangu zilipoibuka taarifa hizi za taharuki Julai 22, 2024 (Jumatatu), tumefuatilia taarifa kwenye shule zetu, vyombo vya ulinzi na usalama, kwa maana ya Jeshi la Polisi, hali iko shwari wazazi wenzangu.
Aidha, aliwataka wazazi kutambua kuwa ni lazima kuweka mkazo kwenye suala la lishe kwa watoto kwa kuhakikisha wanachangia Shilingi 500 ya chakula kama walivyokubaliana kwenye mikutano ya wazazi, jambo ambalo litamsaidia mtoto kupata chakula shuleni badala ya kwenda mitaani wakati wa kipindi cha mapumziko.
Kwa upande wake Afisa Elimu Msingi, Manispaa ya Ubungo, Denis Nyoni aliwataka wazazi kuwa na utulivu kwani hadi kufikia jana hakuna taarifa za watoto kutekwa katika shule kwenye manispaa hiyo.
“Naomba waalimu msisahau wajibu wa kuandika mahudhurio ya watoto kila siku wawapo darasani, na hata wakati wanapomaliza masomo kwa siku, majina yaitwe. Hatua hii ndiyo njia ya kuendelea kudhibiti usalama wa watoto wetu,” amesema Nyoni
Naye Polisi Kata ya Makurumla, Insp Emmanuel Humba, alisema kuwa katika Kata ya Makurumla hali ni shwari, hakuna tukio la utekaji kwa watoto, huku akiwaomba wazazi wawe na utulivu wanapopata taarifa za taharuki.
Morogoro
Na Modest Msangi
Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu Augustino – Mzumbe, Jimbo Katoliki la Morogoro, Padri Dk. Romanus Dimoso amewataka Waamini kutafakari maisha yao na kutambua kwamba wao ni Viongozi bora.
Padri Dimoso alisema hayo wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika ya 16 ya Mwaka ‘B’ wa Kanisa iliyoadhimishwa parokiani hapo.
Padri Dimoso ambaye pia ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, alisema kuwa katika familia, kaya, na jamii, Viongozi wameweka kipaumbele kutafuna mali za familia, na kuwaacha watu wakiteseka kwa kukosa huduma za kijamii.
“Ukiona maendeleo katika familia au jamii fulani, ujue kiongozi wao anawajibika vyema, lakini baadhi yao wamekuwa panya wa maendeleo ya watu, baba au mama katika familia anakuwa panya, huwezi kuona maendeleo katika familia au kaya yao,”alisema Padri Dimoso.
Padri Dimoso alisema kuwa Yesu Kristo ni mfano bora wa kuigwa alipowatuma Wafuasi wake waliporudi kutoa ripoti ya kazi waliyotumwa, aliwapongeza na kuwaambia waende mahali pasipo na watu, wakapumzike.
Azungumzia uchaguzi Mkuu
Aliongeza kusema kwamba huu ni mwaka wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, na mwakani ni Uchaguzi Mkuu, hivyo Waamini kama sehemu ya wananchi, wanapaswa kutafakari kwanza kabla ya kuamua wamchague nani.
Alisema kwamba kwa Miaka 60 ya Uhuru, maendeleo yamekuwa ni ya kupapasa, kwani baadhi yao wamekuwa na tabia zisizofaa katika jamii yao.
Padri Dimoso alibainisha kwamba ili kupata viongozi ambao hawatakuwa kama panya, kabla ya kuwachagua, wananchi wanapaswa kutafakari kwanza hali ya changamoto zilizopo katika jamii, na kuona kama anayechaguliwa, anaweza kuzitatua.
KIEV,Ukraine
Watu wa Mungu nchini Ukraine, bado wanaendelea kukabiliwa na kiu ya haki na amani kutokana na mapigano ya vita yanayoendelea nchini humo, kati ya majeshi ya Serikali dhidi ya majeshi vamizi ya Urusi.
Katika mahubiri yake kwenye Adhimisho la Misa Takatifu, Mwadhama Pietro Kardinali Parolin kwa niaba yake na Askofu Msaidizi Edward Kawa wa Jimbo la Lviv la Kanisa Katoliki nchini Ukraine, alikazia muujiza unaotamaniwa ni amani nchini humo.
Kardinali huyo (pichani) alisema kuwa watu wa Mungu nchini Ukraine kama ilivyokuwa kwa Nabii Eliya, wanaitwa na kutumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu, inayosimikwa katika fadhila ya amani, kwani hakuna jambo ambalo haliwezekani kwa Mungu, akiwasihi Waamini kuendelea kusali ili kuombea amani Taifa lao.
“Madhabahu ni mahali ambapo panapaswa kukuza na kudumisha ari na moyo wa Sala ya Kanisa, maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa kama sehemu ya kazi ya ukombozi.. ni mahali pa shuhuda za imani, matumaini na mapendo, kielelezo cha Kanisa linalokesha na kusali daima,”alisema Kardinali Parolin.
Alisema kuwa ni matumaini ya Baba Mtakatifu Fransisko kwamba katika madhabahu, kamwe hawatakosekana Wamisionari wa huruma, mashuhuda wa upendo wa Mungu unaookoa na kuponya! Madhabahu yawe ni mahali pa kumwilisha upendo, kielelezo cha utekelezaji wa Amri ya Upendo kwa Mungu na jirani.
Kardinali Parolin katika Ibada hiyo alifuatana na Padri Ruslan Mykhalkiv, Gombera wa Seminari ya Jimbo Katoliki la Kyiv-Zhytomir; pamoja na Padri Andriy Lehovich, Katibu Muhtasi wa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la lviv, nchini Ukraine.
Hii inaonesha kwamba hakuna jambo lisilowezekana mbele ya Mungu. Somo la pili linakazia kuhusu toba na wongofu wa ndani. Watu wa Mungu nchini Ukraine wanaitwa na kutumwa kutekeleza unabii wa kusali bila ya kuchoka, ili Mwenyezi Mungu aweze kuwaongoa wenye kiburi, wanaopandikiza mbegu ya chuki na uhasama, vita na kifo, ili waweze kusitisha vitendo hivi vinavyosigina utu, heshima na haki msingi za binadamu.
Amani na Salama! Tumekuwa tukisoma na kutafakari Injili ya Marko, leo Liturjia inatualika kugeukia Injili ya Yohane na hasa sura ile maarufu ya sita, juu ya Yesu kama chakula cha uzima. Mwaka B wa Kiliturjia wa Kanisa kwa kawaida tunasoma Injili ya Marko, lakini Liturjia ya Mama Kanisa ameingiza pia Injili ya Yohane sura ile ya sita kwa Dominika tano mfululizo. Injili ya Marko inatupa masimulizi mawili juu ya muujiza wa Yesu kulisha makutano mikate. Na ndipo tunaona kwa jinsi anavyotoa mkazo na msisitizo huo, hapo Mama Kanisa ameona ili kupata mafundisho ya kina hatuna budi kugeukia sura ya sita ya Injili ya Yohane. Leo tunasikia juu ya muujiza ule wa kugawa mikate kwa watu wengi, na baadaye zaidi katika dominika zijazo tutasikia juu ya mafundisho ya Yesu mkate wa uzima, aliyoyatoa akiwa katika sinagogi la Kapernaumu.
Ni vema ili kupata ujumbe kusudiwa wa Mwinjili Yohane, badala ya kuwahi kuhitimisha juu ya fundisho la Yesu la Ekaristi Takatifu, ambalo kwa kweli linagusiwa sio mwanzoni mwa sura ile ya sita bali mwishoni kabisa, hivyo niwaalike kusoma na kubaki na kile ambacho kipo mbele yetu ili kukwepa kupotoka au kupata maana inayokuwa siyo ile inayokusudiwa na Mwinjili.
Kati ya miujiza iliyofanywa na Bwana wetu Yesu Kristo, ni muujiza huu wa kugawa mikate unaosimuliwa mara nyingi zaidi na Wainjili wote wanne. Wainjili wote haidhuru mara moja wanatupa masimulizi ya muujiza huu, na Wainjili Matayo na Marko wanasimulia mara mbili juu ya muujiza huu, hivyo kufanya masimulizi juu ya kugawa mikate kuwa sita.
Na ndio hapo tunaweza kujiuliza, kwa nini Kanisa lile la mwanzo linatoa msisitizo mkubwa kabisa juu ya muujiza huu? Yesu alitenda miujiza mingine mingi tena mikubwa zaidi, lakini kwa nini Wainjili wote wanne wanatoa mkazo na msisitizo mkubwa kwa muujiza huu? Na kama ndivyo, kwa nini basi miujiza mingine inasimuliwa mara moja peke yake tofauti na muujiza huu wa leo?
Muujiza wa mikate kama unavyosimuliwa na Mwinjili Yohane ni tofauti na jinsi inavyosimuliwa na Wainjili wengine. Na ndio mwaliko wangu leo kujaribu kuingia ndani ya Injili hii ili tuweze kwa pamoja kuchota ujumbe unaokusudiwa kwetu. Na ndio tunaona pia Mama Kanisa ameingiza sura ile ya sita ya Injili ya Yohane kwa Dominika tano mfululizo, ili tuweze kuchota mafundisho ya kina kabisa juu ya utambulisho wa Yesu kama mkate wa uzima.
Tafakari hizi zitusaidie na kutusindikiza tunapoelekea kwenye kilele cha Kongamano la Ekaristi Takatifu Kitaifa hapo Septemba katika Jimbo Kuu la Dar es Salaam. Yesu wa Ekaristi Takatifu ni nani haswa katika maisha yako na yangu, katika maisha ya kila mwamini na kwa Kanisa kiujumla. Mababa wa Mtaguso wa II wa Vatikano wanatualika kuona Ekaristi Takatifu kama chemuchemu na kilele cha maisha ya Kanisa. Ni Ekaristi Takatifu inayolifanya Kanisa liwepo, na Kanisa linadumu hata ukamilifu wa dahari kwa kuadhimisha Ekaristi Takatifu.
Kwanza yafaa kutambua kuwa Mwinjili Yohane hauiti kama muujiza bali kama ishara, na pia hatusikii moja kwa moja kuwa Yesu aliifanya mikate na samaki kuwa mingi na wengi ili kuwatosha watu wote, na badala yake ni mikate ile ile na samaki wale wale kidogo waliwekwa kwa ajili ya wote mpaka kila mmoja akapata kadri ya haja na mahitaji yake na hata kusaza.
Na bado wakaweza kukusanya mabaki vikapu kumi na viwili vya mikate, ndio kusema waliweza kupata kila mmoja na bado hawakuweza kumaliza chote kilichowekwa mbele yao. Hivyo tunaona mara moja msisitizo wa somo la Injili ya leo haupo katika ongezeko la mikate wala samaki, na badala yake moyo na roho ile ya kushirikiana kidogo kinachokuwepo kwa wote kadri ya uhitaji wa kila mmoja wetu.
Falsafa ya ulimwengu wa leo ni kuwa na kila kitu kwa wingi katika maisha, iwe ni pesa, afya, elimu, miaka ya kuishi, marafiki, mafanikio, na kadhalika na kadhalika. Na huu ndio ugonjwa wa wengi wetu, wa kujikusanyia, wa kujilimbikizia, wa kujijali na wenye kutaka na kusaka zaidi na zaidi. Ugonjwa huu wa kujilimbikia unaakisi hasa utamaduni wa kifo, unaotokana na maisha yenye kujaa hofu ya kifo, na ndio dalili ya wazi ya kukosa imani, kwani tunakuwa watumwa wa vitu na mali na badala ya kuwekeza katika upendo kwa Mungu na kwa jirani.
Somo la Injili ya leo, Yesu anatufundisha juu ya ugonjwa huu wa kujilimbikizia na kujikusanyia kila kitu, ugonjwa wa kutaka zaidi na zaidi katika maisha, ni njaa ya vitu na mali.Yesu leo anatupa dawa ya ugonjwa wetu huu, dawa ambayo ni kinyume kabisa na mantiki na utamaduni na falsafa ya ulimwengu wetu, Yesu leo anatuonesha njia salama na sahihi ya ugonjwa wa ubinafsi na umimi ni ile ya kushirikiana sote kwa pamoja bila ubaguzi kidogo kinachokuwepo mbele yetu.
Pasaka, ndiyo sikukuu ya Wayahudi ilikuwa karibu. Mwinjili Yohane anatuonesha ni wakati gani Yesu alitenda ishara ile. Ndio kusema mazingira yalikuwa ni pale walipokumbuka kukombolewa kwao kutoka utumwani Misri.
Ndiyo kusema Mwinjili anajaribu kuoanisha na kuhusianisha tukio la ishara ya mikate, pamoja na tukio la kihistoria la kutoka utumwani Misri. Yesu leo anavuka kama vile Musa alivyowavusha Wanawaisraeli katika bahari ile ya Shamu, na ndipo tunaona leo hakuna chombo kinachotajwa kumvusha Yesu.
Kama vile Musa alivyowaongoza watu wengi, ndivyo na Yesu leo wanamkusanyikia watu wengi na hapo anatenda ishara kama vile Musa nyakati za kuwakomboa Wanawaisraeli. Mara mbili Yesu anapanda juu mlimani, ni kama Musa alivyokuwa akipanda juu mlimani na huko kupokea maagizo ya jinsi ya kuliongoza taifa lile teule.
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
”Zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni muhimu sana katika kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuendeshwa kwa misingi ya kidemokrasia”.
Kauli hii ilitolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika hotuba yake ya uzinduzi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Mpiga Kura Mkoani Kigoma uliofanyika kwenye uwanja wa Kawawa katikaka Manispaa ya Kigoma - Ujiji, Julai 20, 2024.
Uboreshaji huo utafanyika katika mizunguko 13, na mzunguko wa kwanza unahusisha Mikoa mitatu ya Kigoma, Tabora na Katavi, kisha Geita na Kagera, ikifuatiwa na Mwanza, Shinyanga na baadae Mara, Simiyu na sehemu ya Mkoa wa Manyara.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa zoezi hilo lina lengo la kuhakikisha wananchi wote wenye sifa wanapata na kutumia haki yao ya kikatiba ya kupiga kura kama ilivyobainishwa kwenye Ibara ya 5 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
”Vile vile, umuhimu wa zoezi hili unatokana na ukweli kwamba hii ni hatua muhimu ya maandalizi ya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika mwaka 2025 hapa nchini. Pia kutokana na uwepo wa kundi kubwa la wananchi waliopata sifa ya kiumri tangu uchaguzi uliopita, zoezi hili ni muhimu kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya”.
Akieleza kuhusu umuhimu zoezi hilo Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa maboresho ya daftari la mpiga kura, mbali ya kuandikisha wapiga kura wapya, pia yanalenga kutoa fursa muhimu kwa wapiga kura ambao kwa sababu moja au nyingine, kadi zao za mpiga kura zimepotea au kuharibika, au wamehama kutoka eneo moja la uchaguzi kwenda jingine waboreshewe taarifa zao ili wawe na sifa za kuwawezesha kupiga kura katika uchagu ujao wa Rais, Wabunge na Madiwani.
Aliwataka wote waliohama kutoka kwenye vituo vyao vya kupigia kura au kupoteza kadi zao, kufika kwenye vituo vya kuandikisha wapiga kura ili kuboresha taarifa zao na kupatiwa kadi mpya zitakazowawezesha kupiga kura.
Alisisitiza kuwa kwa mujibu wa Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022; inakadiriwa kuwa jumla ya wapiga kura wapya 5,586,433 wataandikishwa, wakiwemo waliotimiza umri wa miaka 18 katika kipindi cha kuanzia mwaka 2020 baada ya uchaguzi mkuu uliopita, na ambao watatimiza umri huo ifikapo tarehe ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. ”Kwa mujibu wa taarifa za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, inakadiriwa kuwa wapiga kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao”.
Idadi hii siyo ndogo kwenye zoezi la kupiga kura. Hivyo, nitoe rai kwa kila mpiga kura aliyeandikishwa mwenye uhitaji wa kuboresha taarifa, iwe kwa kurekebisha taarifa au kuhama kutoka eneo moja la uchaguzi kwenda lingine, asisite kufika katika kituo cha kuandikisha, kwani Tume imeshajipanga ili kuhakikisha wananchi wote wanafikiwa.
Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa ili kufanikisha zoezi hili, kila Mtanzania, Asasi za Kiraia, Vyama vya Siasa, Jeshi la Magereza na Vyuo vya Mafunzo, Vyombo vya Habari, Mawakala Vyama vya Siasa na Watendaji wa walioteuliwa na Tume, wanapswa kutimiza wajibu wao ili zoezi hili liweze kufanikiwa.
Wajibu wa kila Mtanzania:
Mheshimiwa Majaliwa alisema kuwa kila Mtanzania ashiriki katika usimamizi wa suala hilo, kwani wanaotakiwa kuandikishwa ni raia wa Tanzania tu wenye sifa zilizobainishwa kwa mujibu wa sheria. ”Wananchi ni watambuzi wa kwanza, niwasihi sana tuwe wazalendo, huu ni wajibu wa raia wa Tanzania kuhakikisha wanaoandikishwa ni Watanzania tu”.
Jeshi la Magereza, vyuo vya Mafunzo na Uhamiaji:
Hapa Waziiri Mkuu anasema kuwa, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa pamoja na Uchaguzi Mkuu, umeongeza kundi jingine ambalo ni wafungwa wanaotumikia vifungo vya chini ya miezi sita gerezani, au kwenye vyuo vya Mafunzo na mahabusu hawa wote watapata nafasi ya kupiga kura. Hivyo Jeshi la Magereza na upande wa Zanzibar Vyuo vya Mafunzo wanawajibika kuweka miundombinu wezeshi ili Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi iweze kutekeleza wajibu huo kwa ufanisi.
Aidha, Jeshi la Uhamiaji liwajibike kutoa elimu kwa wananchi kuhusu kuwatambua na kutoa taarifa za uwepo wa mtu au watu ambao sio raia wa Tanzania, walioandikishwa tayari, au wanaopanga kwenda kuandikishwa, ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa mapema dhidi yao.
Wajibu wa Vyama vya Siasa Majaliwa anatoa rai kwa viongozi wa Vyama vya Siasa kuhakikisha mawakala wao wanatoka kwenye mitaa, Kijiji na shehia husika ili waweze kutimiza wajibu wao wa kisheria wa kuwatambua watu wenye sifa za kuandikishwa kuwa wapiga kura.
Mawakala wa Vyama vya Siasa:
Anasema kuwa kwa upande wa mawakala watakaoteuliwa na Vyama vya Siasa, wanao wajibu wa kutambua watu wenye sifa za kuandikishwa wanaofika kwenye vituo kwa ajili ya kuandikishwa kuwa wapigakura.
Watendaji walioteuliwa na Tume:
”Ninawasihi sana watendaji walioteuliwa na kuanzia ngazi ya Mkoa, Jimbo, Kata na Kituo cha kuandikisha wapiga kura kuwa waadilifu, na watangulize uzalendo kwa kutotoa fursa kwa watu ambao hawana sifa za kushiriki katika uboreshaji. Kila mmoja ajitume, afanye kazi kwa weledi na kutumia lugha nzuri kwa wananchi wanaokuja kujiandikisha”.
Taasisi na Asasi za Kiraia
Anasema kuwa eneo jingine muhimu ni suala la utoaji wa elimu ya mpiga kura, ambapo alizitaka taasisi na asasi zote zilizopewa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura kutekeleza zoezi kwa weledi, na wasiingize vitu ambavyo havitakiwi, na ambavyo havipo kwenye makubaliano.
”Wakati wa zoezi hili la uboreshaji daftari la mpiga kura, , hakikisheni mnatekeleza kazi zenu kwa kuzingatia masharti ya vibali na miongozo iliyotolewa na itakayotolewa na Tume. Ni vema wakati wote taasisi ziepuke kufanya masuala ambayo hayamo kwenye miongozo waliyopewa kwa mujibu wa vibali vyao”.
Vyombo vya Habari: Alisema kuwa Vyombo vya Habari vinao wajibu wa kutumia kalamu zao, kuwakumbusha wadau wa uboreshaji kutumia taratibu zilizoainishwa kwenye sheria, kanuni na miongozo, kutatua au kuwasilisha malalamiko iwapo kutajitokeza changamoto ya aina yoyote wakati wa uendeshaji wa zoezi hili.
Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa aliwahakikishia Watanzania kuwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amedhamiria kuhakikisha kuwa Uchaguzi unakuwa wa huru na haki.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) Ummy Nderiandanga, alisema kuwa uzinduzi wa uandikishaji na uboreshaji, mchakato huo umeshirikisha wadau mbalimbali wa uchaguzi, ikiwa ni utekelezaji wa falsafa ya 4R za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Tume imekutana na wadau wa makundi mbalimbali kama vile Vyama vya Siasa, Asasi za Kiraia,Viongozi wa Dini, Makundi Maalum kama vile Vijana, Wanawake na Watu wenye Ulemavu. Lengo ni kuhakikisha kuwa mchakato huu unakuwa shirikishi kwa Watanzania wote bila kujali itikadi za Vyama vya Siasa au Dini”
Naye Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Jacobs Mwambegele alisema kuwa jumla ya vituo 40,126 vitatumika katika Zoezi la Uboreshaji wa Daftari, ambapo kati ya hivyo, vituo 39,709 vipo Tanzania Bara, na vituo 417 vipo Tanzania Zanzibar.
UNGUJA
Na Paul Mabuga
Unaweza kusema kuwa kijiji cha Paje kule Unguja ni mahali ambapo tamaduni zinapambana ili kuleta moja inayowakilisha mchanganyiko wa watu wanaoishi hapo wakiwa ni wageni wa muda kama watalii, wengine walioamua kuhamia, na pia wenyeji.
Wakati maeneo mengine ya Unguja, kama Tumbatu na Makunduchi yakipambana na kuhifadhi tamaduni na hasa mila, desturi na historia, Paje inazidi kukaribisha na kukumbatia mchanganyiko wa amali hizo za maisha na kupata kile kinachoitwa ‘cultural amalgamation’.
Ni rahisi kutambua hili, kwani unapokuwa pale Unguja, utashuhudia mji ukijitambulisha kwa mavazi, ambayo kwa akina mama, kama siyo baibui, basi ni nguo ndefu inayofunika mwili na kichwa, huku wanaume wakiwa katika kanzu, ama hata kama ni shati na suruali, kibagarashia na makubasi, basi ni katika mtindo unaoashiria ustaarabu wa Kizanzibari.
Lakini ukipanda zile daladala za mbao na kusafiri kwa saa nzima hadi Paje, utakaribishwa mji unaonekana mkiwa umepoa kwa mchana lakini wenye mambo makubwa kinapoingia kiza. Pamoja na kuwa ni kama kijiji, lakini kuna hoteli zaidi ya 35, hizi zote pamoja na malazi na chakula, lakini pia zinatoa burudani mbali mbali kwa watalii, wahamiaji na wenyeji pia.
Paje inapendelewa na wageni wengi wakiwemo watalii, kutokana na fukwe yake kuwa mahali salama kwa kuogelea, na hata kutiara kwenye maji [kiteboating] na kuwepo kwa maji ‘meupe’. Wingi wa migahawa na hoteli pia unawafanya wageni kuvutiwa ma machaguo kulingana na uwezi wao kifedha. Wapo wanaoona heri wafanye huko makazi na kwenda kutembelea vuvutio vya Unguja, na kurudi huko kwa malazi.
Kutokana na mazingira haya, kuna wahamiaji wengi wameingia Paje kwa ajili ya ajira katika sekta ya huduma na biashara, wao ukichanganya na watalii na wenyeji, unapata mchanganyiko wa tamaduni ambazo ni dhahiri kupitia mavazi, lugha na mitindo ya maisha. Mavazi unayoyaona Paje ni nadra kuyaona katika miji kama Unguja, Makunduchi ama Wete.
Katikati ya kuchangamka huko akina mama wameanzisha kikundi cha ujasiriamali ili kufaidika na fursa katika kijiji cha Paje. Walikianzisha mwaka 2011, na wanakiita ‘Furahia Mwanamke’, na wanajishughulisha na kuzalisha na kuuza zao la baharini la mwani.
“Nimefanya kazi kwa miaka 40, lakini tangu tumejiunga na kikundi, niseme tu, mazingira ya biashara ni mazuri, na karibu sisi hivi siyo tegemezi tena, maana mwani una soko kutokana na thamani yake ya virutubisho muhimu,” anasema Hifadhi Ally, mmoja wa wanachama wa kikundi.
Akina mama hawa wameweka hata duka lao hapo Paje, wakiuza bidhaa mbali mbali zinazotokana na mwani, ikiwa ni pamoja na unga, ambao thamani yake inafika hadi shilingi elfu arobaini kwa kilo moja, mafuta ya kupaka, sabuni, pamoja na dawa za mafua.
“Kuna changamoto kadhaa katika biashara zetu, ikiwa ni pamoja na magonjwa kwa mmea wenyewe, na wakati mwingine bei kupungua. Ilifika hadi shilingi 50,000 kwa kilo, lakini sasa hivi bei imeteremka. Ila tunashukuru tunasomesha watoto, na hata tuna mashine ya kusaga mwani,” anasema mwanachama mwingine wa kikundi hicho,Tano Hassan.
Artifisha Abdul Harim, yeye amepata ajira ya kuuza duka la bidhaa za mwani la umoja wa akina mama hawa ambao anasema kwa idadi wapo 34. Katika duka hilo kuna bidhaa nyingi za mwani na kinachovutia kuna mwani wenye rangi nyekundu, mwingine kijani na ipo ya rangi nyeupe pia. Na hizi rangi ni za mimea yenyewe.
Mwani wanaupanda baharini na hutegemea kupwa na kujaa kwake, na kwamba wakati mwingine katika jua kali, kilimo chao huathiriwa. Wanasema kwamba kwa sasa kilimo hicho kimekuwa na faida kidogo kutokana na gharama yake ya uzalishaji kuwa kubwa.
Licha ya malalamiko haya kutokana na akina mama hawa, lakini bado Zanzibat ni nchi ya nane duniani kwa uzalishaji wa zao hilo, na katika hali ya ubora. Na wanakikundi wana msemo wao kwamba “mwani ni pesa, mwani ni chakula, mwani ni zawadi kutoka kwa Mungu.”
“Mwani una sifa nyingi. Sabuni ya mwani ni nzuri kwa watoto na hata kupaka kabla ya kunyoa nywele ama ndevu kwa kuwa inafanya mwili kuwa laini. Pia karajina [unga wake] Unaweza kuchanganywa kwenye sharubati [juisi], tambi, chachandu, kachumbari na kuleta ladha ya kuvutia,” anasema Artifisha.
Paje inajiweka mahala pema, kwani wakati akina mama hawa wanachangamka na mwani, huku utalii nao ukichagiza biashara, lakini pia una nafasi katika maendeleo ya uchumi wa bluu, ambao serikali ya Zanzibar imeiweka kama ajenda yake ya kipaumbele.
Kilimo cha mwani ambacho kwa sehemu kubwa kinaendeshwa na akina mama, kinatajwa katika na ripoti ya umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara kuwa kimechangia pakubwa katika kuifanya Zanzibar kuelekea kuyafikia Malengo ya Milenia ambayo, pamoja na mambo mengine, yanalenga kupambana na umaskini, na hivyo kuboresha hali za wanawake na watoto.
Mafanikio haya yanapatikana ingawa ripoti hiyo inaonesha kuwa kuna kushuka katika rekodi kwa uzalishaji wa mwani kutoka tani 178,000 mwaka 2016 hadi 81,000 ilipofika mwaka 2021. Lakini hata hivyo, bado zao hilo limeendelea kuwa na mchango mkubwa, huku likitoa ajira kwa akina mama zaidi ya 400 visiwani humo.
Ukiacha Paje, kuna kijiji kinaitwa Makunduchi, huko utamkuta Bibi Nali Kombo! Yeye anakuonesha kuwa unahitaji kujifunza Kiswahili, kwani akikusemesha anakutaka uitikie ‘enhee’, na wala siyo kuitikia kwa kichwa ama kuguna, huko ni kukosa nidhamu.
“Hano pa, swalaa swalaa hiyo” anakuambia, pengine akimaanisha, ‘ameamka alfajiri’, na zaidi anakujibu kwa swali lako la kutaka kujua jinsi huduma bora za afya zilivyomsaidia kupambana na shinikizo kubwa la damu, “dawa maungoni zinaingia, upo!” Anakuona kama unazubaa kidogo, kisha anakuambia, “ useme enhee!”