Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

MVOMERO

Na Mwandishi wetu

Club ya mpira ya wahitimu Chuo Kikuu Mzumbe wameahidi kuchangia ujenzi wa vyoo na sehemu ya kubadilisha mavazi kwa Wasichana wa Shule ya Msingi Mzumbe, iliyopo wilayani Mvomero, mkoani Morogoro.
Hayo yalisemwa na Dk. Lucy Massoi, Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Kimataifa, Baraza la Wahitimu Chuo Kikuu Mzumbe, na kusema kwamba mkakati wa Chuo hicho ni kuendeleza mashirikiano na wahitimu wawe mabalozi wazuri  kikitangaza Chuo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, itaendelea kushirikiana na Jumuiya ya Wasioona Zanzibar (ZANAB), na Jumuiya nyingine za watu wenye ulemavu, ili kuweka mazingira wezeshi yatakayowasaidia watu wenye ulemavu kufaidika na fursa mbalimbali nchini.
Rais Mwinyi aliyasema hayo katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla wakati wa kuahirisha Maadhimisho ya Kuongeza Uwelewa kwa Jamii Juu ya Watu Wenye Ulemavu katika viwanja vya mpira wa Mto wa Pwani Wilaya ya Kaskazini ‘A’ Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Alisema kwamba kwa kutambua kuwa watu wenye ulemavu wamekuwa wakikumbana na chamgamoto mbali mbali katika jamii, kumeanzishwa Baraza la Taifa la Watu Wenye Ulemavu na Mabaraza ya Wilaya ya watu wenye Ulemavu yenye dhamana ya kusimamia, kutekeleza, kutetea na kulinda haki na fursa za watu wenye Ulemavu.
Rais Dk. Mwinyi alisema Serikali imetoa nafasi za Uongozi kwa watu wenye ulemavu katika Wizara mbalimbali, ambapo wamekuwa wakitekeleza majukumu kwa ufanisi mkubwa, jambo linalotoa hamasa kwa Serikali kuendelea kuweka mazingira mazuri kwa wenye ulemavu.
Dkt. Mwinyi alisema Serikali itahakikisha Sheria ya Watu Wenye Ulemavu inafanyiwa kazi na kupelekwa Baraza la Wawakilishi kwa ajili ya kujadiliwa, na hatimaye kupitishwa kuwa Sheria kamili, ikitoa miongozo kwa Taasisi na Jumuiya za watu wenye ulemavu ili kuwawezesha kufanikisha malengo yao waliyojipangia.
Alibainisha kuwa kupitia Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020-2025, Serikali imekuwa ikichukua hatua za kuweka mazingira bora kwa watu wenye ulemavu, ikiwemo kutunga Sheria ya watu wenye Ulemavu Namba (8) ya Mwaka 2022 kwa lengo la kulinda na kutetea haki na fursa za watu wenye ulemavu.
Aidha, Rais Mwinyi alisema Serikali kupitia Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, itaandaa programu maalum itakayowajengea uwelewa wananchi juu ya kutambua haki na wajibu wa watu wenye ulemavu katika Mikoa yote ya Zanzibar.
Sanjari na hilo, Rais Dk. Mwinyi alitoa wito kwa Jumuiya za Watu Wenye Ulemavu kuongeza nguvu zaid ya uwajibikaji, na kuwahamasisha watu wenye ulemavu kuchangamkia fursa mbali mbali zinazojitokeza katika Taifa.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Dk. Khalid Salum Muhammed alisema, Serikali zote mbili zimefanya mapitio ya Sera na Sheria kuhakikisha watu wote wanapata haki sawa, ikiwa ni pamoja na makundi maalum katika nyanja zote za kiuchumi na kijamii.
Dk. Khalid alifahamisha kuwa Serikali kupitia Mfuko wa Uwezeshaji, imejipanga kumaliza kilio cha muda mrefu cha watu wenye ulemavu kwa kuwapatia mikopo itakayowasaidia kujiendeleza kiuchumi katika miradi yao, pamoja na kujikimu kimaisha.

UZINDUZI MWEZI MOYO MTAKATIFU WA YESU

Maasi yaibua mjadala

  •  Askofu: Dunia ingekuwa basi, abiria wote wangeshuka

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Imeelezwa kuwa Dunia ingekuwa ni basi ama daladala, abiria wote wangeshuka na kuondoka zao, hasa kutokana na maasi yaliyokithiri, ikiwemo vitendo vya ushoga na usagaji vinavyozidi kushamiri nchini na dunia kwa ujumla.
Aidha waamini wamatakiwa kuchangia na kuitegemeza Tumaini Media, kwani kufanya hivyo ni sawa na kuwekeza mbinguni, kwani kazi kubwa ya chombo hicho ni uinjilishaji.
Hayo yalisemwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Uzinduzi wa Kampeni ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kwa mwaka 2024, iliyoadhimishwa katika Parokia ya Kristo Mfalme – Tabata, jimbioni humo.
“Kwa maasi haya ya sasa, dunia ingekuwa ni basi, abiria wote wangeshuka na kuondoka zao,”alisema Askofu Mchamungu.
Aidha, Askofu Mchamungu, aliwakumbusha Wanamoyo Mtakatifu wa Yesu kuiga mfano wa Yesu Kristo juu ya kuwapenda na kuwasaidia wengine, kwani Kristo alikubali kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu.
“Alitupenda mpaka kufa msalabani. Na sisi tunajua waziwazi kwamba moyo unaashiria upendo, lakini pia moyo unaashiria huruma. Kristo alitupenda upendo usiokuwa na mwisho. Kwa hiyo, na sisi Wanamoyo Mtakatifu wa Yesu tunapaswa kumuiga Kristo ambaye alitupenda mpaka kumwaga damu yake.
“Pengine si rahisi kufikia kile kiwango chake kwamba tuko tayari kutoa uhai wetu kwa ajili ya wengine. Mbona hata katika familia wakati mwingine mwanandoa mmoja anaweza akamuacha mwenzake, kisa ‘ame-paralyse’, kwa sababu ameshaona kwamba mwenzake hajiwezi tena, hivyo anaona atapata shida sana. Kwa hiyo pamoja na hayo, tutambue kwamba tunapaswa kupendana,” alisema Askofu Mchamungu.
Wakati huo huo, Askofu huyo aliwataka Wanamoyo kuongeza nguvu katika kusal ili maovu yapungue, kwani baadhi ya mambo yanayoendelea ulimwunguni, si ya kuridhisha.
Aliwapongeza pia kwa jinsi wanavyojitahidi katika masuala ya imani, huku akiwasihi kuongeza jitihada hizo ili zionekane katika matendo juu ya kuichukia dhambi.
Askofu alibainisha kuwa miongoni mwa mambo makubwa wanayotakiwa kuyazingatia Wanamoyo Mtakatifu wa Yesu, ni pamoja na kuichukia dhambi, kwani haipendezi kumuona mwanachama huyo kushabikia dhambi katika maisha yake.
Aliwaonya pia kuepuka kufanya vitendo vya mauaji, wala kuhusika katika tukio lolote la kuangamiza uhai wa mtu mwingine, kama vile kibaka, kwani lengo la chama hicho ni kuiga upendo na huruma ya Mungu katika maisha yao.
“Ikitokea, kwa mfano, kuna kibaka huko ameiba akakamatwa, watu wakaanza kumzunguka wanataka kumuadhibu kwa kumchoma moto, itakuwa ni kitu cha kushangaza sana kuona kwamba kati ya hao wanaotaka kufanya kitendo hicho, yupo mtu wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, kitakuwa kitu cha ajabu sana, yaani haiingii akilini…
“Katika tukio hilo, unamkuta mtu wa Moyo Mtakatifu wa Yesu ndiye anaenda kutafuta kibiriti au mafuta ya taa kwa ajili ya kumchoma kibaka, hiyo haiji kabisa, haviendani na vile Kristo alivyotutaka, na kwamba mtu anajiunga kwenye Shirika la Moyo Mtakatifu wa Yesu, ili kuiga ule upendo na huruma ya Mungu,” alisema Askofu Mchamungu.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Padri Chesco Msaga, ambaye pia ni Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi Tumaini Media, aliwaomba Waamini kuendelea kuvichangia vyombo hivyo, kwani kwa kufanya hivyo, watakuwa wameshiriki katika kazi ya uinjilishaji.
Naye Mkurugenzi wa Tumaini Media, Padri Joseph Massenge alimshukuru Askofu Mkuu wa Jimbo hilo, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi kwa kukubali mwezi Juni uwe ni maalumu kwa ajili ya kukichangia chombo hicho, ili kiendelee vyema katika kazi yake ya uinjilishaji.
Padri Massenge aliwashukuru Maaskofu Wasaidizi wa Jimbo hilo, Mhashamu Henry Mchamungu na Mhashamu Stephano Musomba kwa kuendelea kuhamasisha pamoja na kuvilea vyombo hivyo vya Tumaini Media, vinavyohusisha televishen, radio, pamoja na gazeti.
Sambamba na hayo, Mkurugenzi huyo alimshukuru Askofu Mchamungu kwa kuadhimisha Misa hiyo Takatifu, huku akiwashukuru pia Mapadri wenzake wote walioungana naye kwa ajili ya Adhimisho hilo.
Padri Cornelius Mashare, Paroko wa Parokia ya Kristo Mfalme - Tabata, alikipongeza chombo hicho kwa kazi yake kubwa ya uijilishaji, huku akiwaomba Waamini kuendelea kukiwezesha, kukitangaza, pamoja na kukisaidia chombo hicho.
Kwa upande wake, Mkuu wa Masoko wa Tumaini Media, Arnord Kimanganu Mtui aliwashukuru Waamini kwa majitoleo yao, huku akisema kuwa kutokana na mwitikio mkubwa ambao ulionekana mwaka jana 2023, mwaka huu wameanza vyema kwa kujiwekea malengo ya kukusanya kiasi cha Shilingi milioni 550, wakiwa na imani kwamba kama zitafanyika juhudi kama za mwaka jana, watafikia malengo hayo.
Kimanganu  aliongeza kuwa mpaka sasa tayari gharama za upanuzi wa masafa kwenda Mahenge Shilingi milioni 30 zimeshafanyika, hivyo kinachosubiriwa kwa sasa ni kwenda tu kuwasha mitambo hiyo, na kuongeza kuwa sababu iliyochelewesha ni kutokana na ubovu wa miundombini ya barabara ya kwenda Mahenge.
Naye Mhandisi John Ndazi, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam alisema kuwa Tumaini Media ni chombo cha wote, hivyo ni wajibu wao kujitolea kukichangia chombo hicho.
Akizungumza katika Adhimisho hilo, Mwenyekiti wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, Godon Rwenyagira, alimwahidi Mkurugenzi pamoja na wafanyakazi wa Tumaini Media kuwa wao kama Wanamoyo, wamejipanga kuhakikisha kwamba bahasha zote zilizotolewa kwa ajili ya michango hiyo, zitarudishwa kama ilivyokusudiwa, kwani wamelibeba jukumu hilo kwa upendo mkubwa.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Vijana wameonywa kuacha kuiga tamaduni zisizofaa, ikiwemo wanaume kuvaa hereni na kusuka nywele zao.
Aidha, wametakiwa kudumu katika imani, wakitambua kwamba tamaduni hizo zinaweza kuwaingiza  kwenye dhambi.
Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 98 katika Parokia ya Mtakatifu Fransisko Ksaveri – Chang’ombe, jimboni humo.
“Mnapopokea Sakramenti hii ya Kipaimara na mnatakiwa muendelee kudumu katika imani yenu, hivyo mnatakiwa kuepuka kuiga tamaduni zisizofaa, mfano, unamkuta mwanaume anavaa suruali anaweka mlegezo, anavaa hereni, anasuka nywele kichwani kama mwanamke. Epukeni kuiga tamaduni za namna hiyo,” alisema Askofu Mchamungu.
Pia, aliwasisitiza kujiepusha na tabia za udokozi pamoja na kutumia mali zisizokuwa za kwao, bali wahakikishe kwamba pale wanapookota vitu, wavirudishe kwa wenyewe.
Aliwasisitiza pia kuwajibika katika usafi pamoja na kutunza mazingira, akisema kuwa suala la usafi wa mazingira wao kama vijana, linatakiwa kuwa kipaumbele kwao.
Wakati huo huo Askofu Mchamungu aliwakumbusha Wasimamizi wa Waimarishwa hao kwamba miongoni mwa majukumu yao, ni pamoja na kusaidiana na Wazazi katika malezi, ili kujenga maadili ya vijana hao.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Novatus Mbaula alimshukuru Askofu Mchamungu kwa kufika parokiani hapo pamoja na kuwaimarisha vijana 98 wa Parokia hiyo.
Aidha, Padri Mbaula aliwasihi vijana hao kuendelea kuyazingatia yale yote waliyoambiwa na Askofu wakati wa homilia yake, kwani mafundisho hayo yatawasaidia kukua katika misingi iliyo bora.
Naye Katibu wa Parokia hiyo, Simon Sangawe alivishukuru vyombo vya habari vya Kanisa vilivyoshiriki katika Adhimisho hilo, ikiwemo Tumaini Media, akisema kuwa vyombo hivyo vinafanya kazi kubwa katika suala la uinjilishaji.

Dar es Salaam

Na Mwandishi wetu

Paroko Msaidizi wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Kalmeri, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Paul Mallewa, amesema kuwa Yesu akijitoa sadaka kwa ajili ya ukombozi, akiwasihi waamini kujisadaka na wao ili kuitangaza Injili yake Mwokozi.
Padri Mallewa alisema hayo wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Ekaristi Takatifu, iliyofanyika hivi karibuni parokiani hapo.
“Yesu amejitoa sadaka, nasi tunapaswa kujitoa sadaka kwa ajili ya changamoto katika maisha,”alisema Padri Mallewa.
Alisema kuwa Yesu aliulizwa na wanafunzi wake, ni wapi angependa wamuandalie ale Pasaka, lakini aliwatuma wanafunzi wawili akawambia waende wakakutana na kitu si cha kawaida, hasa kwa wanaume kubeba maji, enzi hizo ilikuwa jambo la kushangaza, kwani kazi hiyo ilikuwa ya wanawake.
“Katika maisha ya kawaida tunakuwa tumebeba mizigo mikubwa, isiyo ya kawaida…Waamini wa Bunju tunapaswa kujitoa kwa dhati, ili tuweze kula Pasaka na Yesu katika majitoleo yetu tunayotoa katika familia zetu,”alisema Padri Mallewa.
Alisema pia kuwa moja ya pasaka ya kula ya Yesu ni kujitoa kwa dhati kuchangia shughuli za Kanisa, kusudi Kristo mwenyewe abadilishe matoleo hayo na kuwa kama sadaka, kama ambavyo yeye alijitoa sadaka ili kuwakomboa wanadamu.
“Yeye ataibadilisha sadaka yetu na kuiweka katika mazingira yasiyo ya kawaida, na kuiweka katika sadaka ya mwili wake, ndipo na sisi tutabarikiwa,”aliongeza kusema Padri Mallewa.
Alibainisha pia kuwa Yesu, pia alitoa damu yake, yenye harufu nzuri ya upatanisho, na utakaso, ambayo inawaimarisha wanadamu wote, hasa wenye changamoto dhidi ya jirani zao na hata kuwa mbali na Kristo mwenyewe.
“Damu ya Kristo Yesu ina harufu nzuri ya upatanisho, harufu nzuri ya msamaha na kuoshwa dhambi zetu na kurudishwa katka hali ya kawaida, damu ambayo tuliipoteza kwa dhambi zetu,” alisema Padri Mallewa.
Naye Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Kalmeri, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Dominic Somola, alisema kuwa Pentekoste ni Utatu Mtakatifu, Mwili na Damu ya Bwana Yesu Kristo ambayo ni chimbuko la Kanisa.
Mkakati wa kukuza Watoto Kiimani
Padri Somola alisema kuwa kwa sasa Parokia hiyo ina mikakati mbalimbali ya kuendelea kutoa mafundisho, kwa watoto wadogo, hasa baada ya kupokea Sakranenti, kwani wengi hawafiki kwenda kusali, hasa baada ya kumalizia Masakramenti yao ya awali.
“Wazazi wapo wajitahidi kusimamia imani, kwani ni eneo mtambuka la malezi ya watoto. Sisi kama Parokia, tunajipanga kuhakikisha watoto wanaendelea na mafundisho baada ya kupata Masakramenti yao ya awali,”alisema Padri Somola.
Aidha, Padri Somola alitumia nafasi hiyo kuvishukuru Vyama vya Kitume, Kamati za Liturujia ngazi ya Parokia, kwa kufanikisha siku hiyo ya Ekaristi Takatifu.
Aliwapongeza watoto wote kwa kufanya vizuri mitihani yao ya mafundisho ya Kanisa, na hata wale ambao walifanya vibaya, aliwapa nafasi ikiwemo ya kuendelea kujifunza zaidi, Neno la Mungu.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu akiwa katika picha ya pamoja na Mapadri, Viongozi wa Kamati Tendaji pamoja na Waamini wengine baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 98 katika Parokia ya Mtakatifu Fransisko Ksaveri – Chang’ombe, jimboni humo. Kulia kwa Askofu, ni Paroko wa Parokia hiyo, Padri Novatus Mbaula. (Picha na Mathayo Kijazi)

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi (katikati mwenye Fimbo ya Kichungaji) na Mapadri, wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kamati Tendaji ya Parokia ya Mtakatifu Maria De Mathias, Mivumoni, jimboni humo.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu (nyuma mwenye Fimbo ya Kichungaji) akiwa katika maandamano na Mapadri kutoka Parokia mbalimbali za Jimbo hilo wakiingia kanisani kwa Adhimisho la Misa Takatifu ya Uzinduzi wa Mwezi wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, Somo wa Tumaini Media, iliyoadhimishwa katika Parokia ya Kristo Mfalme, Tabata.

Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Dominick Somola ambaye pia ni Dekano wa Dekania ya Mtakatifu Gaspar, (wa sita kulia), na Paroko Msaidizi wa Parokia hiyo, Padri Paul Mallewa (mwenye kanzu nyeupe), wakiwa katika picha ya pamoja na Wanakamati wa Zaka wa Parokia hiyo, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa hivi karibuni parokiani hapo. (Picha zote na Yohana Kasosi)

DODOMA

Na Bartholomew Wandi

Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 hauko mbali sana kuanzia sasa, kwani ukipiga hesabu umebaki takribani muda wa mwaka mmoja (1) na miezi kadhaa hivi. Wananchi wengi ambao watafikisha miaka kumi na minane wakati wa jukumu hili, waliofikisha miaka kumi na minane (18) tayari na zaidi, na wale ambao waliokuwa na sifa zote za kuandikishwa mwaka 2020, lakini kutokana na sababu zisizoweza kuzuilika walikosa nafasi ya kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, wataandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Awamu ya Kwanza na ya pili  ya uboreshaji.
Mpaka sasa mikoa yote 25 Tanzania Bara tayari ina watu ambao wanahitaji kuandikishwa kuwa wapiga kura wenye sifa nilizozielezea hapo juu.Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni hitaji la kisheria na Kikatiba pia. Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria kuandikisha wapiga kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na pia Madiwani Tanzania Bara.
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utakuwa mahsusi kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao zilizokosewa awali, waliopoteza kadi za kupigia kura, wenye kadi zilizoharibika ili waweze kupata kadi nyingine,  na wale ambao wanataka kuhama Jimbo au Kata kwenda Jimbo au Kata nyingine ili waweze kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kifungu cha 12 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inaeleza, “Mkurugenzi wa Uchaguzi ataweka, atatunza na kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililoanzishwa chini ya kifungu cha (1)”.
Kulingana na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, Kifungu cha 9 (2) inasema, “Bila kujali Masharti ya kifungu kidogo cha (1), na kwa kuzingatia uthibitisho wa umri , Mtanzania yeyote ambaye hajapoteza sifa chini ya Sheria hii au Sheria nyingine yoyote ya Bunge, na ambaye wakati au kabla ya tarehe ya Uchaguzi atatimiza umri wa miaka kumi na minane (18) atastahili kuandikishwa kuwa Mpiga Kura chini ya
Kifungu cha 13 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, pia inaeleza kwamba, “Tume itamwandikisha mtu yeyote Tanzania Zanzibar ambaye anastahili kuandikishwa kuwa mpiga kura katika Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano”.
Zaidi ya hayo, Ibara ya 5(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inafafanua, “Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane (18) anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti mengine ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi”.
Pamoja na hayo, pia Ibara ya 5(3)(a-d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inaeleza kuwa Bunge  litatunga sheria ya uchaguzi na kuweka masharti kuhusu kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika Daftari hilo, kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga kura na kupiga kura, utaratibu wa kumwezesha mpiga kura aliyejiandikishwa sehemu moja kupiga kura sehemu nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa utaratibu huo, na kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.
Marekebisho ambayo yanapaswa  kuingizwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni kuondoa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja, waliojiandikisha na huku wako chini ya umri wa miaka kumi na minane (18), waliofariki dunia  au kupoteza sifa ya kuwa wapiga kura kwa namna nyingine, kuwapa kadi za mpiga kura mpya waliopoteza kadi zao, kurekebisha taarifa za wapiga kura zilizokosewa awali,  na kuwaingiza waliofikisha umri wa miaka kumi na minane (18) na kuendelea.
Kifungu cha  16(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inasema, “Tume itakuwa na jukumu la kupanga muda na kupitia upya uandikishaji wa wapiga kura katika kila eneo la uchaguzi ndani ya jimbo”
Kwa mujibu wa kifungu cha 16 (5) cha  Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, inaeleza kwamba Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika mara mbili kwa miaka mitano (5), yaani baada ya Uchaguzi Mkuu kupita, na kabla ya siku ya uteuzi.
Uchaguzi Mkuu wa Mwisho ulifanyika Oktoba 28 mwaka, 2020, na sasa Tume ipo kwenye maandalizi ya kuboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Mchakato wa Uboreshaji huo wa Daftari umeanza kwa kukagua vituo vilivyotumika kuandikishia Wapiga Kura mwaka 2019/2020.
Uhakiki huo wa vituo hivyo vya kuandikishia wapiga kura, unalenga kuona kama kuna haja ya kuongeza vituo, kuona kama vilivyopo bado vinakidhi matakwa ya kisheria, na kufanya marekebisho mengine kama vile kubadilisha au kurekebisha majina ya vituo vilivyokosewa.
Matokeo ya uhakiki huo kwa Tanzania Bara yanaonesha kuwa, vituo vya kuandikisha wapiga kura vimeongezeka kutoka 37,814 hadi 40,126 ambapo kati ya vituo hivyo, 39,709 ni vya Tanzania Bara na vituo 417 ni vya Zanzibar.
Baada ya kazi ya kukagua vituo hivyo, Tume imefanya Uboreshaji wa majaribio (pilot) unaofanyika katika baadhi ya vituo vilivyoko kwenye halmashauri za Wilaya na Halmashauri za miji kwa  lengo la kujaribu kuona namna na jinsi vifaa vya uboreshaji vinavyofanya kazi katika mazingira tofauti, na kupata namna bora ya kufanikisha zoezi hili la uboreshaji.
Tume tayari imeshafanya uboreshaji wa majaribio katika kata ya Ikoma iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mkoani Mara na Kata ya Ng’ambo iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mkoani Tabora. Kata hizi zilichaguliwa ili kupata mazingira tofauti ya kijiografia, pamoja na idadi ya watu.
Uboreshaji huu wa majaribio umefanyika kwa mafanikio kutokana na kuboreshwa kwa vipuri na mfumo wa uandikishaji wa wapiga kura. Aidha, ilibainika kuwa betri mpya za BVR Kits zinao uwezo wa kuhifadhi chaji kwa muda mrefu, na hivyo zitaweza kukabiliana na changamoto ya nishati ya umeme katika baadhi ya maeneo ambayo hayana miundo mbinu hiyo.
Pamoja na mafanikio hayo kulikuwa na changamoto ndogo ya baadhi ya  wapiga kura kutokuwa na uhakika ama kukumbuka majina yao wanapokuja kurekebisha taarifa zao na hivyo kuchukua muda mrefu kituoni kutokana na kazi ya kutafuta majina yao kwa usahihi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi  itaendelea kuwaelekeza Wapiga Kura kuhakikisha wanakumbuka taarifa zao kwa usahihi ili waweze kuhudumiwa kwa haraka vituoni.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele wakati akiongea na Waandishi wa Habari Mjini unguja, Zanzibar, amesema kuwa uzinduzi rasmi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika Mkoa wa Kigoma tarehe 01 Julai, 2024.
Uboreshaji huo wa Daftari kwa Teknolojia ya BVR kwa mwaka huu 2024, hautakuwa tofauti na wa mwaka 2019/2020, ambao ulihusisha wananchi wote wapya wenye sifa za kuwa wapiga kura, waliohama jimbo au Kata, na ambao kadi zao zilipotea au kuharibika.
Wapiga kura ambao waliandikishwa mwaka 2015 na  2020 na wanazo kadi zao za kupigia kura na hazina matatizo yoyote, au hawajahama Jimbo/Kata kwenda Jimbo/Kata nyingine au hakuna mabadiliko yoyote ya mipaka ya kiutawala,  wanatakiwa pia kwenda katika vituo vya kuandikisha Wapiga Kura ili kuhakiki taarifa zao kwenye Daftari.
Kwa upande wa idadi ya Wapiga Kura watakaoandikishwa awamu hii, Tume imeshafanya makadirio kulingana na uandikishaji uliopita pamoja na matokeo ya Sensa ya watu na makazi uliofanyika mwezi wa Agosti mwaka huu, 2022.
Mhe. Jaji Mwambegele aliwaambia Waandishi wa Habari kuwa, makadirio ya Tume kwa kutumia ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ya Sensa ya Watu na Makazi, inatarajiwa idadi ya Wapiga Kura kuongezeka kufikia 34,746,638 kutoka 29,754,699 ya Wapiga Kura katika mwaka 2020, idadi hii itajumuisha wapiga kura wapya 5,586,433, sawa na asilimia 18.7 wanaotarajiwa kuandikishwa.
Pamoja na hayo, Mwnyekiti wa Tume anasema kuwa inakadiriwa Wapiga Kura 594,494 wataondolewa katika Daftari kwa kupoteza sifa na jumla ya Wapiga Kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao. Hawa watakaoboresha ni wale ambao taarifa zao zilikosewa au wamehama kutoka Kata au Jimbo moja kwenda eneo lingine la Uchaguzi, na wengine ni wale ambao kadi zao zimeharibika au zimepotea.
Hata hivyo, Uboreshaji wa safari hii hautofautiana sana na ule wa mwaka 2015 na 2020, kwani Teknolojia itakayotumika ni ile ile ya kuchukua alama za kibaiolojia yaani Biometric Voters Registration (BVR), pamoja na Android.
Aidha, mabadililiko yanayotazamiwa ni kwa upande wa kupunguza ukubwa na uzito wa BVR Kits ambapo awali wakati wa uboreshaji wa Dafrari wa mwaka 2014/2015 na 2019/2020 BVR zilikuwa na uzito wa kilo 35 lakini kwa uboreshwaji wa mwaka huu kwa 2024/2025, uzito umepunguzwa  hadi kufikia kilo 18 ambapo yapo masanduku mawili, moja ni kwa kuhifadhia mashine ya BVR Kits, na lingine ni kuhifadhia vifaa vingine vya kuunganishia BVR Kit hiyo ikiwemo kishikwambi kwa ajili ya kupigia picha ya Mpiga Kura na kuchukulia alama za vidole, ila vifaa hivi vitatoa huduma ile ile ya kuandikisha wapiga kura na kutoa kadi hapo hapo kituoni.
Mabadiliko mengine katika Uboreshaji wa Daftari ni Tume kuanzisha mchakato wa uboreshaji kwa njia ya mtandao (Online) ambapo mpiga kura anaweza kuanzisha mchakato huu wa awali kwa njia ya mtandao ili kurekebisha, au kubadilisha taarifa zake, kuhamisha taarifa zake kutoka kituo cha awali kwenda kingine, au anayetaka kufanya vyote kwa pamoja.
ITAENDELEA WIKI IJAYO.
Wapiga kura wanaotaka kuboresha taarifa binafsi na wanaohama vituo au vyote viwili kwa wakati mmoja, wanaweza kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zao kwa njia ya mfumo wa mtandao ‘online’ kuingia kwenye Tovuti ya Tume www.inec.go.tz kwa kutumia kompyuta au simu janja, kisha atabonyeza kiunganishi (link) iliyoandikwa Boresha Taarifa za Mpiga Kura, au atatumia anuani ya ovrs.nec.go.tz itakayompeleka moja kwa moja kuanzisha mchakato huo.
Katika mfumo huu, wapiga kura wanatakiwa kuingiza namba ya kitambulisho cha taifa (National Identity Number: NIN), namba ya kadi ya mpiga kura, namba ya simu anayotumia kwa sasa, na jina la Kata, kisha watapata ujumbe wenye namba za utambulisho (token namber) ambazo wataenda nazo kituoni ili kukamilisha taratibu za kupata kadi za mpiga kura.
Mwombaji ambaye ni mpya anatakiwa kwenda kituoni bila kuwa na kitambulisho cha aina yoyote kiinachomtambulisha ili aweze kupatiwa kadi ya mpiga kura. Mwaombaji huyu atakapofika kituoni atamwona Mwandishi Msidizi wa Kituo cha kuandikisha Wapiga Kura na  kuajaza fomu Na. 1,
Baada ya kujaza Fomu Na. 1, Mwombaji huyo Mpya atampatia Afisha Mwendesha Mashine ya Bayometriki (BVR Kits Operetor) ambaye ataingiza taarifa zake kwenye BVR Kit, atapigwa picha, atachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili  na kuweka saini na kupewa Kadi ya Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Kwa wapiga kura ambao walipoteza, kuharibika au kukosewa Kadi zao na ambao hawatajaza Online, watakapofika Kituoni, watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo , kisha Afisa Mwendesha Mashine ya Bayometriki ataingiza taarifa zao kwenye BVR Kit, akisha watapigwa picha, watachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili, na kuweka saini na mwishowe watapewa Kadi zao za Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Vile vile,, Wapiga Kura ambao wanataka kuhamisha taarifa zao, pia watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo ili kuomba kuhamishiwa taarifa zao kwenda Jimbo au Kata na Kituo kingine cha Kupigia Kura wakati wa Uchaguzi Mkuu, na Chaguzi nyingine Ndogo zitakazofuata baada ya Uchaguzi Mkuu kupita.
Aidha, Mtu anatakiwa aende mwenyewe kituoni na anatakiwa kujiandikisha mara moja tu. Ni kosa la jinai kwa mwananchi yeyote kwa makusudi kwenda kituoni na kujiandikisha zaidi ya mara moja. Mwaka 2015, Kwa Mkoa mmoja tu wa Njombe, Kanzi Data hiyo imeweza kung’amua wapiga kura zaidi ya 600 waliojiandikisha zaidi ya mara moja, na walichukuliwa hatua za kisheria.
Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024,  kifungu cha 114(1)(b) inaeleza kuwa “kwa kujua au ana sababu ya kuamini kuwa ameandikishwa katika eneo la Uchaguzi anaomba kuandikishwa kinyume na kifungu cha 25, na bila kufichua kwa Msimamizi wa Uchaguzi kujiandikisha kwake kwa awali katika eneo jingine la Uchaguzi atenda kosa na akitiwa hatiani atapaswa kulipa faini isiyopungua shilingi laki moja na isiyozidi shilingi laki tatu au kifungo cha muda usiozidi Miaka miwili au vyote kwa pamoja”.
Baada ya zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaandaa Daftari la Awali la Wapiga Kura na kupelekwa mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) kwa ajili ya wapiga kura kuangalia kama majina yao yamo kwenye Daftari.
Kama baadhi ya majina hayaonekani, Wapiga Kura watamweleza Mwandishi Msaidizi kutoonekana kwa majina hayo na Mwandishi Msaidizi ataandika majina ya Wapiga kura hao waliokosekana kwenye Daftari la Awali na kisha ataleta orodha hiyo ya Majina Tume kwa ajili ya kuingizwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Pamoja na hayo, dhumuni lingine la Tume kupeleka Daftari la Awali la Wapiga Kura mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) ni kuwapa fursa Wapiga Kura kuangalia kama kuna majina ya Wapiga Kura walioandikishwa na hawana sifa kisha watawawekea pingamizi kwa kujaza fomu Na. 3B na kumkabidhi Mwandishi Msaidizi fomu hiyo ambaye ataileta Tume kwa ajili ya Wapiga Kura hao ili wafutwe kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kama kweli hawana sifa.
Hata hivyo, Majina hayo yaliyowekewa pingamizi hayafutwi moja kwa moja kwenye Kanzi Data ya Tume badala yake yanahifadhiwa sehemu nyingine kwenye Kanzi Data ili kama mtu huyo ana ushahidi wa kutosha kuwa ana sifa za kutosha kuandikishwa na kubaki kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura anarudishwa mara moja, Machapisho mbalimbali ya Elimu ya Mpiga Kura ya uhamasishaji ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yatasambazwa nchi nzima  ili kuwaelimisha Wapiga Kura kuwa na uelewa na mwamko wa kujiandikisha kwa wingi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga kura.
Mchapisho hayo pia yanasistiza Wapiga Kura kutunza Kadi zao za kupigia kura na hatimaye kujitokeza kwa wingi kupiga Kura kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2025 utakapowadia na Chaguzi Ndogo zitakazofuata  na kila mmoja anatakiwa awe na Kadi yake ya kupigia kura.
Tume pia katika uhamasishaji wake wa Uboreshaji wa Daftari itatumia vyombo mbalimbali vya habari kama Magazeti, Radio kubwa na Radio za Kijamii, TV, INEC TV ONLINE, Tovuti ya Tume na Mitandao ya Kijamii, machapisho yakiwemo mabango, vijitabu na vipepeperushi, gari la Elimu ya Mpiga Kura na kushirikisha wadau kwa kutoa vibali kwa taasisi na asasi za kiraia.
Mwandishi wa Makala haya ni Afisa Habari Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) Simu  0754203015.