DAR ES SALAAM
Na Arone Mpanduka
Katika Makala haya tunaangazia baadhi ya takwimu muhimu zilizojitokeza kwenye msimu wa Ligi Kuu soka Tanzania Bara wa 2023/24 uliomalizika Mei 28 mwaka huu, huku Yanga ikiibuka na ubingwa wa 30 kihistoria.
MABEKI NA PASI ZA MABAO
Beki wa pembeni wa Yanga, Yao Kwasi na wa Azam FC Lusajo Mwaikenda ndio vinara wa kupiga pasi nyingi za mabao kuliko mabeki wote walioshiriki Ligi Kuu kwa msimu huo wa 2023/24 uliomalizika.
Kila mmoja amepiga pasi saba za mabao (assist). Beki wa kushoto wa Simba Mohammed Hussein amepiga pasi sita, Pascal Msindo (Azam FC), Nickson Kibabage (Yanga) na Rahim Shomari (KMC) kila mmoja amepiga pasi 5 za mabao kwa msimu mzima.
MABAO MENGI NDANI YA BOKSI
Kiungo mshambuliaji wa Azam FC, Feisal Salum ndiye kinara wa kufunga mabao mengi zaidi akiwa ndani ya boksi la mpinzani. Ikumbukwe kuwa wapo wachezaji ambao wanaweza kufunga nje ya boksi kwa kupiga mashuti makali. Feisal amefunga jumla ya mabao 17 akifuatiwa na Aziz Ki ambaye amefunga 15 ndani ya boksi huku Waziri Junior wa KMC akifunga 11.
MABAO MENGI NJE YA BOKSI
Aziz Ki ndiye kinara kwenye hilo, baada ya kufunga mabao 6 nje ya boksi, huku akifuatiwa na Nicolaus Gyan wa Singida Fountain Gate aliyefunga mabao matatu.
AZIZI KI NA MABAO YAKE
Mabao 21 yaliyofungwa na kiungo mshambuliaji wa timu ya Yanga, Stephane Aziz Ki yamepiku mabao ya jumla ya timu tatu zilizoshiriki Ligi hiyo. Timu alizozipiku Aziz Ki ni Geita Gold (18), Dodoma Jiji (19), na Tabora United (20), ambazo zimemaliza msimu zikiwa hazijafikisha mabao 21 ya kufunga, huku akilingana idadi ya mabao ya kufunga na timu ya JKT Tanzania (21).
KIWANGO CHA UFANISI
Yanga imemaliza msimu ikiwa na kiwango bora cha ufanisi cha asilimia 88.88 ambacho ni kikubwa zaidi kuwahi kutokea tangu Ligi Kuu Tanzania Bara ianzishwe mwaka 1965. Asilimia hizo hupatikana kwa kuchukua namba 30(idadi ya mechi), kisha unazidisha mara 3(pointi za ushindi) ambapo jibu linakuja 90, na kisha unatoa 10(pointi ilizokosa Yanga msimu mzima) na kupata 80.
Baada ya hapo unachukua 80 unaweka juu ya 90(pointi za jumla za msimu) na kuzidisha mara 100 ili kupata asilimia za ufanisi.
TIMU YENYE ‘CLEAN SHEET’NYINGI
Achana na hati safi (clean sheet) ya golikipa mmoja mmoja, hapa tunazungumzia timu nzima ya mpira katika msimu uliopita ambayo kwa ujumla wake ubora wa safu ya ulinzi unakuwa na mchango wa kuifanya isiruhusu bao lolote kwenye mechi nyingi.
Yanga ndiyo inayoongoza kuwa na clean sheet nyingi zaidi(20) ikifuatiwa na Coastal Union ya Tanga(16). Ikumbukwe pia kuwa timu hizo zilichezesha makipa tofauti tofauti kwenye msimu mzima ambapo Yanga iliwatumia Djigui Diarra, Aboutwalib Mshery na Metacha Mnata ingawa Diarra alitumika kwenye mechi nyingi kuliko wenzake, na Coastal ikimtumia zaidi Ley Matampi.
TIMU YENYE PASI NYINGI
Yanga inaongoza kwa kupiga jumla ya pasi 10,830 kwenye mechi zote 30 za msimu, ikifuatiwa na Azam FC iliyopiga pasi 10,084 huku Simba ikiwa nafasi ya tatu kwa kupiga pasi 9890.Yanga pia imepiga kona nyingi (200) ikifuatiwa Simba ambayo ilipiga kona 165 msimu mzima.
TIMU ILIYOPOTEZA MECHI NYIGI
Mtibwa Sugar ya Morogoro ndiyo kinara kwa kupoteza mechi nyingi msimu uliopita baada ya kupoteza mechi 19 na kusababisha washuke Daraja.
LONDON, Uingereza
Meneja wa Middlesbrough, Michael Carrick ametia saini mkataba mpya wa miaka mitatu na klabu hiyo ya Championship.
Klabu hiyo ilimaliza katika nafasi ya nane katika Ligi Daraja la Pili na kufika nusu fainali ya Kombe la Ligi msimu huu uliopita.
Carrick alisema kuwa kwake ni furaha sana kuhusu hilo, na siku zote amekuwa mtulivu kuhusu hilo na uhusiano huo, uaminifu huo na imani hiyo ndani ya klabu ni muhimu sana.
Alisema kuwa hakika wameipata hiyo ndiyo bado inampa hisia nzuri aliyokuwa nayo alipopitia mlango mara ya kwanza.
“Inahisi kama hatua kubwa kama kichwa cha habari, kama taarifa, lakini kwa kweli haibadilishi chochote ninachofanya au jinsi ninavyoishughulikia, inaendelea tu kile tunachojaribu kufikia.”
DAR ES SALAAM
Na Mwandishi wetu
Beki wa zamani wa timu ya soka ya Simba, Boniface Pawasa ameushauri uongozi wa klabu ya Simba kuhakikisha unafanya maboresho ya kikosi ili iweze kurejesha ufalme wake katika msimu ujao wa 2024/25.
Simba imemaliza msimu uliopita ikiwa haina mafanikio kwenye malengo iliyojiwekea baada ya kuambulia Ngao ya Jamii pekee, huku ikikosa taji la Ligi Kuu na la Shirikisho la soka nchini TFF.
Akizungumza kuhusiana na kitu ambacho timu hiyo inapaswa kufanya, Pawasa ambaye aliwahi kuichezea Simba kwanzia mwaka 2001 hadi 2005 alisema kuwa wanapaswa kusajili wachezaji wapya wa kitaifa na kimataifa ili kusalia kwenye soko la ushindani.
Alisema kuwa msimu uliopita Simba ilisajili kwa kubahatisha, kitu ambacho kwenye soka la sasa hakifanywi na timu nyingi ambazo zina malengo makubwa ya kufika mbali.
“Mimi ukiniuliza kwa wachezaji wa kimataifa nani anapaswa kubaki nitakwambia wabaki watu watatu tu, beki Che Malone, Babacar Sarr na mshambuliaji Freddy Michael Kouablan. Hao wengine ni wa kawaida sana, hawanishawishi kuendelea kuvaa jezi ya Simba” alisema Pawasa.
Aliongeza kuwa wachezaji hao wanapaswa kuongezewa wengine wenye viwango bora zaidi ili waweze kuwasaidia kwenye mashindano ya kitaifa na kimataifa.
Pia, alibainisha kwamba kilichoigharimu Simba msimu uliopita ni kuwa na wachezaji wengi wasiojituma na wenye nidhamu mbovu, huku kila mmoja akijiona mkubwa kuliko klabu.
Pawasa ambaye kwa sasa ni Kocha Mkuu wa timu ya taifa ya Soka la Ufukweni, alienda mbali zaidi kwa kuiangalia timu ya Taifa Stars akisema kwamba wekundu hao wanapaswa kufanya usajili kwa maslahi ya timu ya taifa.
“Zamani timu hizi zilikuwa zinasajili wachezaji wazuri wazawa ambao ninaamini wapo, na faida kubwa inakuja kupatikana kwenye uteuzi wa kikosi cha timu ya taifa. Siku hizi tunajaza wachezaji wengi wa kimataifa, linapokuja suala la timu ya taifa tunanza kuhangaika, hasa jinsi gani ya kupata washambuliaji na mabeki,” alisema.
Alisema kuwa klabu za Tanzania zimekuwa zikifanya vizuri katika misimu ya sasa kwa msaada mkubwa wa wachezaji wa kigeni, kitu ambacho kinampa hofu kubwa.
ARUSHA
Na Mwandishi wetu
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda amesema kuwa ajira za ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu ambao unatarajiwa kutumika katika mashindano ya Mataifa ya Afrika (African Cup of Nations: AFCON) mwaka 2027, zinapaswa kuwalenga zaidi Watanzania, badala ya wageni.
Akizungumzia kuhusu umuhimu wa mradi huo, Makonda alisema kuwa ujenzi wa uwanja huo umeleta nafuu ya maisha kwa wakaazi wa Mkoa huo ambao kwa kiasi kikubwa watapata kipato kutokana na kazi ya ujenzi.
Makonda (pichani) pia aliagiza kuwa shughuli zote zinazoendelea katika ujenzi wa uwanja huo, wahusika wakuu wawe ni Watanzania, huku akisistiza ununuzi wa malighafi zozote za ujenzi uzingatiwe ndani ya Mkoa wa Arusha.
Alisema kuwa kutokana na kusaini kwa Mkataba wa ujenzi huo kati ya Serikali na wahandisi wa ujenzi wa ujanja kumeongeza thamani katika maisha ya watu mbalimbali wa Arusha, huku akitamani kuona watu wa maeneo hayo wanakuwa wa kwanza katika kuangaliwa kwenye kupata ajira.
Kwa upande mwingine alisisitiza umakini uzingatiwe katika kujenga uwanja huo, kwani utafanyiwa uchunguzi na wataalamu mbalimbali lakini pia kujengwa katika viwango kutasaidia kuitangaza Serikali ya Awamu ya Sita kuwa makini katika miradi yake.
DAR ES SALAAM
Na Celina Matuja
Utume wa Kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA), Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wametajwa kuwa ndiyo wamekuwa wakikoleza Uinjilishaji kupitia tungo na nyimbo zao za Injili.
Kutokana na kuifanya kazi hiyo kwa bidii na kwa sifa na utukufu kwa Mungu, Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stefano Musomba amewapongeza Wanakwaya hao, alisema kuwa wanafanya kazi kubwa licha ya dosari chache zinazojitokeza ambazo zikirekebishwa mambo yatakuwa mazuri zaidi.
Askofu Musomba alisema hayo katika sherehe ya UKWAKATA Jimbo, iliyofanyika Parokia ya Mtakatifu Bonaventura, Kinyerezi wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Jumatatu ya Pasaka, ambayo mwaka huu ilikuwa na kauli mbiu “ Tumwimbie Bwana, katika Roho na kweli.”
Alisema kuwa kuimba na kumtangaza Kristo Mfufuka ni jambo muhimu ambako linatakiwa kwenda sambamba na matendo namna ya kuishi kwao, unyenyekevu, utii, moyo wa ibada na
uchaji kwa kufanya hivyo ili kila anayewaona aseme kweli hilo ni tanganzo la Kristo mfufuka.
Aidha Askofu Msomba aliwataka Wakatoliki kuiga mfano wa wanawake waliokwenda kulitazama Kaburi, alimozikwa Yesu Kristo na kupewa Habari kuwa amefufuka, aliendea mbio kuwapasha habari wanafunzi wake ila walipo kutana na Yesu walianguka chini na kumsujudia na kumwabudu.
Alisema sio vema kuishi kwa mazoea kwa kuwa wakati mwingine mazoea yanapotosha na kupelekea watu kutozingati misingi ya Imani na kupokea EkaristiTakatifu kwa mazoea.
Aliwasihi waamini hao kuhakikisha kutojiongelesha mezani pwa Bwana na kuonyesha hali ya kuabudu na kwa unyenyekevu katika kuonyesha heshima kwa Mungu.
“Ni suala la kujiuliza kila mmoja wetu, hasa anapokwenda kushiriki Ekaristi Takatifu …utaona kuhani anamwambia mtu mwili wa Kristo anakutazama tu, ni kama hajawahi kusikia na kuhani akirudia mwili wa kristo, basi hapo atadhani anasalimiwa na kujibu milele amina hajui nafanye nini,’’ alisema Askofu Msomba.
Akiwageukia waimbaji ambao ndio ilikuwa siku yao, Askofu Musomba, alisema wote wanatakiwa kuonyesha ushirikiano kati ya walimu na wanafunzi wao, ili kuondoa majivuno, kwani wapo baadhi hawaimbi kama Utume, bali hupenda kujionyesha kuwa bila yeye hakuna mwingine anayeweza.
Kwa mujibu wa Askofu Musomba, ingawa wapo wanaotumikia vema utume wao, wapo baadhi wanaimba kwa kiburi na kuwakwaza hata wenzano, wengine wameshindwa kabisa kuimba na kucha kazi hiyo, akiwataka kutambua kwamba kipaji cha uimbaji kimetoka kwa Mungu.
Alisema si vema mwanakwaya kujigamba kwa namna yoyete ile, kwani wakati mwingine baadhi ya wanakwaya huleta fujo kwa kutofautiana na Makuhani hasa wanaporekebishwa ana kukosolewa.
‘Niwaombe msimruhusu adui shetani kutawala bali wamtangulize Mungu daima, ili maisha ya utume wa uimbaji yawe mazuri na kuwafikisha katika uzima wa milele, tumeumbwa ili tumjue Mungu na tuchochee karama zetu na za wengine ili kauli mbiu yenu iendane na kile mnachofanya,’’ alisema Askofu Musomba.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utume wa Walei Jimbo, Padri Vitalis James Kassembo aliwapongeza WanaUKWAKATA na kuwataka wajibidiishe katika elimu ya mambo ya Uchumi yaani elimu endelevu, ambayo itawasaidia kujikwamua kiuchumi.
Aliwaomba Viongozi wa Halimashari za Walei ngazi zote kuhakikisha wanasaidia baadhi ya wanakwaya, ambao hawana elimu juu ya Uchumi ili waipate kama kikundi.
Naye Dekano wa Dekania ya Segerea Padri Cornelius Mashale ambaye pia Paroko wa Parokia ya Kristo Mfalme Tabata, alikazia kuhusu wale Wanakwaya wanaoishi kama mume na mke kwa muda mrefu kuhakikisha wanarekebisha maisha yao, wka kutoka kuishi giza na kuukaribisha mwanga kwa kufunga ndoa Takatifu.
Padri Mashale alisema maisha hayo hayatafsiri vizuri maisha ya mkristo anayejua nini maana ya kuishi Sakramenti ya ndoa na uimbaji wao ama uinjilishaji wanaoufanya.
Alibainisha kwua haina maana pale wanakwaya wanapoomba barua au kibali cha kwenda kuinjilisha parokia Fulani, halafu nusu ya kikundi chote cha kwaya unapofika muda wa komunio wao ndio wa kwanza kutoshiriki.
Naye Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Bonaventura, Kinyerezi Padri Francis Hiza, aliwapongeza wanaUKWAKATA Jimbo, kwa kuadhimisha siku yao hiyo.
Akisoma risala mbele ya Askofu Katibu wa UKWAKATA, Jimbo, Paulina Abias alitaja mafanikio katika utume wao kuendelea kuimarika, kutokana na semina za kiroho na kwamba wanayo mipango mingi ya kufanya ikiwemo kuwa na studio yao ya kurekodi nyimbo jimboni.
Sherehe hizo zilikwenda sanjari na utoaji vyeti vya kuhitimu muziki Mtakatifu kwa wahitimu 24 katika madaraja manne na walitakiwa kujitokeza kujifunza muziki mtakatifu ili kutekeleza zoezi la kuutunza muziki huo.
MVOMERO
Na Faustine Gimu
Mkuu wa Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro, Judith Nguli ametoa wito kwa wananchi wa Wilaya hiyo kutumia fursa ya Siku ya Afya Duniani kuchunguza Afya zao bure.
Aidha amewataka wananchi hao kushiriki kikamilifu kaatika mazoezi ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.
Judith alisema hayo ofisini kwake wilayani Mvomero mkoani Morogoro, baada ya kufanya Kikao na Timu kutoka Wizara ya Afya, Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa na Halmashauri ya Mvomero, kuelekea maadhimisho hayo yanayofanyika April 7, kila mwaka.
Alibainisha kuwa katika kuelekea Siku ya Afya Duniani April 7, wananchi wanatakiwa kuchangamkia fursa kuchunguza Afya zao na kushiriki Michezo mbalimbali.
“Wananchi wa Mvomero tuchangamkie kuchunguza Afya zetu katika kuelekea Siku ya Afya Duniani, maana kutakuwa na uchunguzi wa Saratani ya mlango wa kizazi, shinikizo la juu la damu, lishe hivyo nawakaribisha sana,”alisema Judith.
Aidha, Judith alisema kupitia maonesho hayo itakuwa ni fursa kubwa kwa Wananchi kufanya mazoezi kupitia mashindano ya michezo yatakayosaidia kuimarisha Afya ya mwili, na akiipongeza Wizara ya Afya kwa kuchagua Wilaya ya Mvomero kufanyiwa maadhimisho hayo.
Maadhimisho ya Afya Duniani yatafanyika yakienda sambamba na kaulimbiu isemayo”Afya Yangu, Haki Yangu”
KILIMANJARO
Na Muhina Semwenda
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa Watanzania kuepuka matumizi ya dawa za kulevya kwani yanaharibu nguvukazi ya Taifa, hasa kwa vijana ambao wanategemewa kuongoza kufanya shughuli za uzailishaji na kuharakisha maendeleo.
Alitoa wito huo katika sherehe za uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru zilizofanyika kitaifa katika Viwanja vya Chuo cha Ushirika Moshi, Mkoani Kilimanjaro.
“Idadi kubwa ya waathirika wa matumizi ya dawa za kulevya ni watoto na vijana wenye umri kati ya miaka 13 hadi 24. Kundi hili ni nguvukazi ya Taifa letu, Serikali, haiwezi kunyamaza itaendelea kufanya msako mkali ili wahusika wote wa biashara hiyo haramu wachukuliwa hatua kali,”alisema Waziri Mkuu Majaliwa.
Alisema kuwa Serikali kwa kutambua umuhimu wa udhibiti wa biashara ya dawa za kulevya imeendelea kuongeza kasi ya mapambano ili kukomesha biashara, kilimo na matumizi ya dawa za kulevya. “Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya wote wanaojihusisha na kilimo hicho haramu pamoja na biashara ya dawa za kulevya”
Alisema mbio za Mwenge wa Uhuru za mwaka 2024 zitaendelea kutoa hamasa kwa jamii kusitisha kilimo haramu cha bangi, biashara na matumizi ya dawa za kulevya. Aidha, utajiekeleza kwenye kuhamasisha jamii kulima kilimo cha mazao halali ya biashara na chakula, pamoja na kuhamasisha jamii kushiriki katika shughuli nyingine halali na zenye staha.
Alibainisha, “Hivi karibuni, kumeibuka aina nyingine ya bangi yenye kiasi kikubwa cha kilevi, ikifahamika kama “skanka”. Aina hii ya bangi yenye sumu nyingi huchanganywa kwenye sigara, na vijana wamekuwa wakitumia skanka ambayo imekuwa ikipelekea kuchanganyikiwa,.”
Alisema kuwa vijana wamekuwa wakitumia bidhaa hizo wakifahamu uwepo wa skanka na wengine bila kufahamu na hivyo hujikuta wanakuwa waraibu wa bangi.
Kwa mujibu wa Waziri Majaliwa, idadi kubwa ya waathirika wa matumizi ya dawa za kulevya ni watoto na vijana wenye umri kati ya miaka 13 hadi 24.
Alisema kuwa Serikali itaendelea kufanya msako mkali ili wahusika wote wa biashara hiyo haramu wachukuliwe hatua kali, na kuongeza kasi ya mapambano ili kukomesha biashara, kilimo na matumizi ya dawa za kulevya.
Katika hatua nyingine Waziri Mkuu Majaliwa alisema kwamba mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu utaendelea kuhimiza mapambano dhidi ya rushwa, huku akitoa wito kwa Watanzania kupambana na vitendo vya rushwa.
“Tafiti za taasisi za kitaifa na kimataifa zinaonesha kuwa Tanzania imeendelea kufanya vizuri katika mapambano dhidi ya rushwa. Kwa mujibu wa taarifa ya utafiti wa REPOA iliyotolewa Machi 9, mwaka 2022, Tanzania inafanya vizuri katika mapambano dhidi ya rushwa, ambapo zaidi ya asilima 77 ya Watanzania waliohojiwa walikiri kuwa rushwa imepungua nchini.”
Kadhalika, amesema kwamba Serikali kupitia mbio za mwenge, itaendelea kuwashurikisha wananchi na wadau wengine katika mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI.
Naye Waziri wa Habari, Vijana Utanaduni na Michezo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Tabia Mwita Maulid, alisema kuwa mbio za mwenge wa Uhuru zimeendelea kudumisha Uhuru, amani mshikamano uzalendo na umoja wa kitaifa pia zimekuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kijamii.
Awali, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi Vijana Ajira na Wenye Ulemavu, Mheshimiwa Patrobas Katambi, amesema kwamba falsafa ya Mwenge wa Uhuru imekuwa ni kuwaunganisha Watanzania, kuleta matumaini pamoja na kukagua miradi inayotoa huduma kwa wananchi ili kusogeza huduma kwa wananchi.
GEITA
Na Mwandishi wetu
Mbunge wa Jimbo la Busanda Tumaini Magesa ameahidi mwezi mmoja na nusu kukamilisha ujenzi wa bweni katika shule ya sekondari Lutozo iliyopo katika mamlaka ya mji mdogo wa Katoro mkoani Geita.
Ameyasema hayo aliposhiriki kuchimba msingi wa bweni hilo ambalo linatakiwa kutumika katika msimu mpya wa masoma ya Kidato cha Tano mwaka huu.
Dodoma
Na Julieth Sasili
Serikali imeanza kufanya marekebisho ya kubadili muundo wa Baraza la Taifa na Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (National Environment Management Council:NEMC,) na kuwa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (National Environment Management Authority:NEMA).
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Khamis Hamza Khamis alisema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Maryam Azan Mwinyi aliyetaka kujua ni lini Serikali itawasilisha Marekebisho ya Sheria ya Mazingira ili kuipa NEMC uwezo wa hadhi ya Mamlaka.
Alisema kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais inatarajia kuwa hadi kufikia Juni mwaka 2024, Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira, Sura 191, uwasilishwe katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua zaidi.
Naibu Waziri Khamis (pichani) alisema kuwa marekebisho hayo ya kubadili muundo huo ni moja ya masuala yanayopendekezwa kufanyiwa marekebisho, ili NEMC iwe Mamlaka.
Akijibu maswali ya nyongeza ya mbunge huyo, Waziri Khamis alisema kuwa miongoni mwa majukumu ya mameneja wa kanda wa NEMC ni kusimamia sheria, pamoja na kutoa elimu kwa jamii.
Alitumia nafasi hiyo kuwapongeza kwa utendaji kazi mzuri, na kusema kuwa majukumu hayo yanaweza kufanyiwa marekebisho kulingana na sheria itakavyopendekeza.
Hivyo, Naibu Waziri Khamis alibainisha kuwa NEMC itakayofahamika kama NEMA, itaendelea kushirikiana kwa ukaribu na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira ya Zanzibar (ZEMA), katika utekelezaji wa majukumu, ili usimamizi wa mazingira nchini uwe endelevu na wenye mafanikio.
Dar es Salaam
Na Mwandishi wetu
Dekano wa Dekani ya Mtakatifu Thomas More, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Romwald Mukandala, amewataka waamini kuwa na upendo kwa majirani zao.
Padri Mukandala ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Kizito, Kilongawima, jimboni Dar es Salaam, alisema hayo hivi karibuni wakati wa Misa Takatifu ya Alhamisi Kuu iliyofanyika parokiani hapo.
Alisema kuwa waamini inabidi muoneshane upendo, hasa kwa majirani zetu…mkitambua kwamba sisi sote ni Watoto wa Baba Mmoja, ambaye ni Mungu Mwenyezi,” alisema Padri Mukandala.
Alisema kuwa jambo lingine ambalo waamini hao wanatakiwa kulisimamia ni kuwa na Imani na Mapadri wao wanaowaongoza katika Imani.
Padri Mukandala alisema kuwa Mapadri ni watumishi wa Mungu, ambao hawapaswi kutetwa na kusemwa kama inavyofanyika kwa baadhi ya waamini, akiwasihi waendelee kuwaombea Mapadri ili waweze kutekeleza vyema utume wao.
Akizungumzia Alhamisi Kuu, Padri Mukandala alisema kuwa hiyo ni Siku ya Mapadri, kwani ndiyo siku ambayo Bwana Yesu Kristo alisimika rasmi Misa Takatifu kwa njia ya karamu ya mwisho, alipokula pamoja na wanafunzi wake.
“Sisi ni wafuasi wa Kristo. Je tunapomfuata yeye, tunayaishi hayo? Mungu atusaidie tuache tabia ya ubinafsi, uchoyo, tujitoe kwa wenzetu,”alisema Padri Mukandala.
Ahimiza utunzaji wa mazingira
Kwa mujibu wa Padri Mukandala, waamini wote wanatakiwa kuhakikisha wanatunza mazingira katika maeneo yao kwa kupanda miti katika kutekeleza Waraka wa Baba Mtakatifu Fransisko wa ‘Laudato Si’ unaohitimiza utunzaji wa mazingira.
Alisema kuwa kuna kila sababu kwa waamini kila mmoja kwa nafasi yake, kuhakikisha anatimiza wajibu wa kupanda miti kwa wingi katika maeneo yake, na hata katika Maparokia ili kutunza mazingira ili yawe katika hali bora.
Naye Mlezi wa Seminari Kuu ya Segerea, Padri Siegried Ntare aliwataka Wakristo kuishi Ukristo wao kwa kumpenda Mungu kwa kusali na kuyashika Maandiko Matakatifu.
Dar es Salaam
Na Mwandishi wetu
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu, amewaonya watu wenye tabia ya kusengenya, kuponda na kuwachafua wengine kwa maneno mabaya ya kashfa.
Askofu Mchamungu alisema hayo wakati akitoa homilia yake katika Ibada ya Ijumaa Kuu, iliyofanyika katika Parokia ya Bikira Maria Msaada wa Daima, Kimara Korogwe.
“Katika jamii pia watu wengine kazi yao ni kuponda wengine na kusengenya watu wengine. Wanatumia midomo yao vibaya kusema mabaya juu ya wengine, hawa hawana tofauti na wale waliomtemea mate Yesu Kristo,”alisema Askofu Mchamungu.
Askofu Mchamungu alisema kuwa katika jamii ya sasa pia wapo watu wengine ambao kazi yao ni kuchafua sifa za watu kwa kuwashuhudia maneo ya uongo, jambo alilosema ni baya katika maisha.
Ataka wenye mamlaka kutoa haki
Aliwataka waamini kuhakikisha wanatetea haki za wengine, na kutoogopa maneno ya watu kama alivyofanya Pilato, hasa wanapokuwa katika nafasi za kutetea haki za wengine.
“Kila mmoja kwa nafasi yake ajitahidi kutetea haki za jamii, hasa wanapoona kitu kimekuwa siyo sahihi,”alisema Askofu Mchamungu.
Kwa upande wake Ibrahimu Meresho, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei Parokia ya Kimara Korogwe, alisema kuwa wapo katika mkakati wa ujenzi wa Kanisa kubwa jipya na la kisasa, kwani kila kitu kimefanyika.
“Kwa sasa vibali vyote vya ujenzi vimeshapatikana. Tunatafuta mtu wa kurekebisha tu ramani yetu, na baada ya hapo tutaipelekea kwa Baba Askofu ili naye aiangalie na kutoa baraka zake ili ujenzi uanze kufanyika,”alisema Meresho.
Parokia ya Kimara Korogwe haina Kigango hata kimoja, na ina mwaka mmoja tu tangu itangazwe kuwa Parokia kamili, ikiwa na Kanda tano na Jumuiya 20, ikiongozwa na Mapadri wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam.
Dar es Salaam
Na Israel Mapunda
Paroko wa Parokia ya Familia Takatifu, Mburahati, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Vitalis Kassembo, amesema kwamba kila muamini anatakiwa kuwa shuhuda wa Imani.
Padri Kassembo alisema hayo hivi karibuni wakati akizungumza na gazeti Tumaini Letu katika mahojiano maalumu yaliyofanyika baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Pasaka, iliyofanyika parokiani hapo.
Alisema kuwa waamini wanapaswa kuendelea kusherehekea Pasaka kwa amani na upendo kwa kumtafuta Bwana Yesu Kristo.
“Tunapaswa tuendelee kuumbwa upya, kwa njia ya Sala, kutenda matendo mema, na kupokea masakramenti,”alisema Padri Kassembo na kuongeza,
“Neema hizi za Pasaka zisikae kwetu tu bali tuwashirikishe na wenzetu kile ambacho Mungu ametujalia, furahini na wengine,”alisema Padri Kassembo.
Naye Katibu Msaidizi wa Parokia ya Mburahati, Edward Alex, alisema kuwa mwaka huu Parokia hiyo inatarajia kuadhimisha Jubilei ya Miaka 50 ya Parokia, hivyo wapo katika harakati za maandalizi kuelekea kwenye jubilei hiyo.
Alisema pia kuwa kila muamini anatakiwa kushirikiana na wenzake katika kutenda matendo mema kwa kusaidia wahitaji kile ambacho wamejaal;iwa na Mwenyezi Mungu.
Naye Katibu Msaidizi wa Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) wa Parokia hiyo, Magreth Charles, alisema kuwa wanawake wanatakiwa kutulia na kuendelea kulea familia zao.
Alisema kuwa waamini pia nao wanatakiwa kuendelea kushikamana katika kuiishi Imani yao Katoliki, hasa katika kipindi hiki cha Oktava ya Pasaka.
Dar es Salaam
Na Mwandishi wetu
Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Bonaventura, Kinyerezi, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Francis Hiza, amewasihi wanaume kuhakikisha wanajitoa kwa dhati katika kuhudhuria Jumuiya na kanisani, kwani uwepo wao ni mihimu kwa kuwa wao ni nguzo ya Kanisa.
Padri Hiza alitoa wito huo hivi karibuni wakati akizungumza katika hafla fupi ya Wanaume Wakatoliki Parokia ya Kinyerezi (UWAKA DAY), iliyofanyika Jumatatu ya Pasaka parokiani hapo, ikiwa ni utaratibu wa Parokia kuadhimisha UWAKA Day.
“Katika kuwatia moyo kwa mara ya kwanza nimeaandaa sherehe kwa pesa ya Parokia kwa mwaka huu ili kila kitu wafanye wenyewe. Kwa hiyo hii inanipa mwanga kwamba tunasonga mbele kama wanaume,”alisema Padri Hiza.
Padri Hiza alisema pia kuwa malengo makuu ya kuwakutanisha Wanaume Wakatoliki kukaa pamoja na kujadiliana maisha ya kiimani, ni kuwajenga ili washiriki kikamilifu shughuli za Kanisa, kwani wao ni nguzo ya Kanisa.
Alisema kuwa kila Mwanaume Mkatoliki anatakiwa kuhakikisha anauishi uamaume wake, hasa kwa kutambua kwamba wao ni kichwa cha famiilia, hivyo uhalisia huo lazima udhihirishwe kwa vitendo.
“Mwanaume ni kichwa cha familia, hivyo ni wajibu kwetu lazima tujipange ili tusije kuzidiwa na wanawake na hata katika Kanisa,”alisema Padri Hiza.
Kwa mujibu wa Padri Hiza, wanaume wasikubali kuuza haki zao za kuzaliwa wa kwanza, na kuliacha Kanisa likaangamia, kwani kufanya hivyo wataiangamiza pia jamii.
Kwa upande wake Paroko Msaidizi wa Parokia hiyo, Padri Benson Mapunda, aliwataka Wanaume hao waamke katika maisha ya sala na maisha ya ibada kila mara.
Alisema kuwa UWAKA wanatakiwa kujitahidi walau kila mwezi kusali katika Jumuiya na Misa za Dominika walau mara moja na kufanya maungamo, kwani ni jambo muhimu katika maisha yao.
Padri Mapunda alisema kwamba kila Baba anatakiwa kuhakikisha anazungumza na mwenza wake katika maisha yao ya kila siku, hasa katika mambo ya kiroho, na kuhimizana kufanya maungamo ili kuzirudishia roho zao uhai.
Alibainisha pia kuwa maungamo ya pamoja yanasaidia kwa kiasi kikubwa katika kudumisha mahusiano yao ya ndoa.
Naye Didas Ndyemela-Mwenyekiti wa UWAKA Parokia ya Mtakatifu Bonaventura, Kinyerezi, alisema kuwa huo ni utaratibu wa kawaida unaofanyika kila mwaka katika Siku ya Jumatatu ya Pasaka, ili kutafakari nguvu ya upendo kwa Wanaume Wakatoliki.
“Tunabadilishana mawazo ili tuweze kuona namna gani ya kuendeleza Parokia yetu sisi kama UWAKA,”alisema Ndyemela.
Hata hivyo alisema kuwa UWAKA imefanya kazi kubwa katika kufanikisha ujenzi wa kanisa, nyumba za Mapadri na vituo vya njia ya Msalaba, kwani Kituo cha Tano kimejengwa na UWAKA.
KASESE, Uganda
Askofu wa Jimbo Katoliki la Kasese, Mhashamu Francis Aquirinus Kibira Kambale amewataka Wakristo kuiga mfano wa marehemu Bi. Augustino Muhindo, “anayejulikana kama Kithabutsunde” aliyemtaja kama nguzo ya ukuhani, elimu, na mabadiliko ya kijamii na kiuchumi katika wilaya ya Kasese.
Askofu Kambale alisema hayo wakati wa Misa Takatifu ya kumbukizi ya miaka 10 ya Marehemu Bi. Muhindo aliyemtaja kuwa ni watu wa kwanza wa Mukonzo kutawazwa kuwa Kasisi katika Kanisa Katoliki la Roma, Desemba 14, mwaka 1958.