Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

DAR ES SALAAM

Na Arone Mpanduka

Jumamosi ya Februari 10 mwaka huu majira ya mchana, zilitoka taarifa za kwamba aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Imani Madega, amefariki dunia.
Hakika zilikuwa ni taarifa za ghafla zilizotokana na kifo cha ghafla, kwani inaelezwa kwamba asubuhi ya siku hiyo akiwa nyumbani kwake Chalinze mkoani Pwani, alimuomba mtoto wake ampeleke hospitali kwa madai kwamba anajisikia vibaya, ingawa alikuwa na nguvu zake akitembea mwenyewe, lakini wakati akifanyiwa vipimo na matibabu hospitalini, hali ilibadilika na alifariki kwa tatizo la shinikizo la damu.
Katika kolamu hii, nitakusimulia baadhi ya matukio ambayo Madega aliwahi kuyafanya akiwa na Yanga ambayo aliiongoza kuanzia Mei mwaka 2007 hadi 2010.
APINGA YANGA KAMPUNI
Hiyo ilikuwa ni mwaka 2007 ikiwa ni siku chache baada ya kushinda nafasi ya uenyekiti wa Yanga, ambapo yeye na Viongozi wenzake, waliitwa ofisini kwa Yusuph Manji ambaye wakati huo alikuwa mfadhili.
Katika wito huo, Manji alimtaka atie saini mkataba wa makubaliano ya kuifanya Yanga iwe Kampuni na baada ya hapo Francis Kifukwe angepewa urais ndani ya mfumo huo, kitu ambacho Madega alikataa.
Sababu ya kukataa ni Katiba kutoruhusu kwa wakati huo, huku pia akiwa na wasiwasi kwamba huenda likawa changa la macho la kutaka klabu hiyo kubinafsishwa kihuni.
Madega aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema kwamba hawezi kufanya kitu kama hicho na kwamba Manji hana nia nzuri na klabu, hivyo ni vyema awaachie timu yao na wao wapo tayari kupambana nayo ili kuiendesha. Hapo ndipo uhasama kati yake na Manji ulipoanza.
KAULI YA KIBABE BAADA YA YANGA KUTEKWA
Ilikuwa Oktoba mwaka 2007, ambapo wakati huo uhasama kati yake na Manji ulizidi kupamba moto na kuibua makundi mbalimbali ambayo mengine yaikuwa yanampinga yakitaka aondoke madarakani.
Siku moja Yanga ikiwa chini ya kocha Mmalawi, Jack Chamangwana (sasa marehemu), ilitekwa na kundi la makomandoo ambao inasemekana walikuwa upande wa Madega na kwenda kufichwa Morogoro.
Katika mahojiano yake na kipindi cha Spoti Leo cha Redio One, Madega alikaririwa akisema, “Sitakuwa tayari kuiona Yanga ikiuzwa na kutawaliwa na mtu mmoja kwa nguvu ya pesa, masikini na mwanawe, tajiri na mali zake, Manji baki na mali zako au heshimu Katiba. Vinginevyo baki na mali zako au fadhili timu nyingine.” Baada ya sekeseke hilo, baadaye hali ya hewa ilikaa sawa.
AMSHUTUMU MANJI KUHUJUMU TIMU
Mwezi huo huo mwaka 2007, Yanga ilicheza dhidi ya Simba kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro, na Yanga kufungwa bao 1-0. Baada ya mchezo Madega aliibuka na kumshutumu Manji kwamba alitoa pesa kwa wachezaji ili wajifungishe kwa lengo la kumfanya aonekane hafai kuiongoza klabu hiyo na aondolewe kirahisi.
Ikumbukwe kuwa kabla ya mchezo, Manji alitoa Shilingi milioni 40 za maandalizi, huku akitoa na milioni 10 kwa wazee ili wafanye mambo ya kishirikina kwa ajili ya mchezo.
AOMBA RADHI WAZEE/MANJI
Ilikuwa mwishoni mwa mwaka huo huo wa 2007, ambapo siku moja waandishi tuliitwa kwenda kuchukua habari kwenye ukumbi wa hoteli ya Travertine, Magomeni jijini Dar es Salaam ambapo Madega aliingia ukumbini, na wanahabari wote tulitakiwa kusubiri nje kwanza. Baada ya dakika kadhaa tukaitwa na kutaarifiwa kwamba mzozo kati ya Madega, Manji, na wazee umekwisha baada ya Mwenyekiti huyo kuomba radhi.
AONGOZA MKUTANO KWA DAKIKA TATU
Ilikuwa mwaka 2008 ambapo Madega aliitisha mkutano wa wanachama kwenye ukumbi wa Police Officers Mess, na waandishi wa habari tulikwenda kushuhudia kile kilichofanyika. Miongoni mwa yaliyokwenda kufanyika, ni kupitisha baadhi ya marekebisho ya vipengele kwenye katiba.
Kabla ya mkutano kuanza, wanachama walipewa rasimu ya katiba ili kuweza kupitia na kufanya maamuzi. Ilipofika majira kama ya saa 3 na nusu asubuhi, Madega aliingia mkutanoni kuhakiki akidi na moja kwa moja kuhoji wanachama wote kama wanakubali rasimu ipite ama la.
Wanachama wengi walinyoosha mikono juu kuonyesha wameridhia, na hapo hapo Madega alitangaza kuwa rasimu imepita na kufunga mkutano huo, huku akisindikizwa na wimbo wa Pepe Kalle (hayati) wa Young Africans. Mkutano huo ulitumia dakika 3 tu na kuwashangaza wengi.
ATUKANWA NA NICOLAUS MUSONYE
Hilo lilijiri baada ya Yanga kukataa kuingiza timu uwanjani julai mwaka 2008, ambapo ilitakiwa kucheza na Simba kuwania mshindi wa tatu katika michuano ya Kagame. Siku hiyo uwanja ulifurika kuzisubiri timu ziingie uwanjani, lakini walionekana wachezaji wa Simba pekee.
Madega alipoulizwa, alisema kuwa walikubaliana pande zote (Simba na Yanga), kuwa wasipeleke timu uwanja mpya wa Taifa (sasa Benjamin Mkapa) kama matakwa yao yasingetekelezwa na CECAFA (ya mgawo wa mapato ya milangoni), lakini cha kushangaza wenzao wamewasaliti kwa kupeleka timu uwanjani.
Siku moja baada ya tukio hilo, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CECAFA Nicolaus Musonye, alituita wanahabari kwenye ukumbi wa jengo la Millenium Tower, Mwenge, na ‘kuwaponda’ viongozi wa Yanga akidai kwamba wote wakiongozwa na Madega, ni dhaifu, na hawajitambui pamoja na kauli zingine nyingi zisizoandikika, huku wakiifungia Yanga kutoshiriki kwa miaka mitatu.
AIWEKEA NGUMU TBL
Ilikuwa mwaka 2008 ambapo Madega alikataa agizo la wadhamini wao TBL la kutaka waajiri watendaji kama mkataba wao ulivyokuwa unaelekeza.
Madega alisema kuwa hayo hayakuwa makubaliano, bali walikubaliana kuajiri Mweka Hazina kwa sababu hawakuwa na uwezo wa kuwalipa watendaji, kama vile Katibu.
Mvutano huo ulitokea kabla ya Shirikisho la Soka Duniani FIFA kutaka wanachama wake wote kuwa na watendaji wa kuajiriwa, ambapo mwaka 2010 Simba na Yanga zilianza kuajiri Maafisa Habari na Makatibu.
AMSHUSHUA NGASSA
Ilikuwa mwaka 2009 ambapo ilidaiwa kwamba mchezaji Mrisho Ngassa aliuomba uongozi umuongezee mshahara kwa sababu kipindi hicho alikuwa na uwezo mkubwa uwanjani kushinda hata baadhi ya wachezaji wa Kimataifa waliokuwa wanasajiliwa klabuni hapo.
Siku moja Madega alifanya mkutano na waandishi wa habari na kuchomekewa swali hilo, na katika majibu yake, alisema kwamba haiwezekani mchezaji anakwenda Yanga akiwa mnyenyekevu halafu baadaye anatanua mabega akitaka kuongezewa mshahara.
Aliongeza kwa kusema kwamba Ngassa kuna kipindi alikuwa akipewa Shilingi elfu tano tu anatetemeka, hivyo asijifanye ana thamani sana, na badala yake akumbuke alipotoka.
AWEKA MSIMAMO USAJILI WA NGASSA ULAYA
Kuna mwaka ziliibuka taarifa kwamba klabu ya Lov-ham ya Norway ilikuwa inamtaka Ngassa, lakini uongozi ulimzuia.
Madega alitoa ufafanuzi kwa kusema kwamba haiwezekani wakala akawa anazungumza na vyombo vya habari tu bila wao kujua, hivyo suala hilo ni uzushi kwa sababu taarifa rasmi hazijawafikia mezani.
AACHA MILIONI 200 KWENYE AKAUNTI
Mwaka 2010 baada ya muda wake kuisha ndani ya Yanga, Madega hakutaka kutetea tena kiti chake na kuwaachia wengine wagombee. Katika taarifa yake kwenye Mkutano Mkuu wa Uchaguzi, Madega alitangaza rasmi kwamba anaondoka, huku kwenye akaunti ya klabu akiwa ameacha zaidi ya shilingi milioni 200.
Hali hiyo ilimfanya awe Mwenyekiti pekee wa timu za Tanzania kuondoka madarakani na kuacha akaunti zikiwa zimenona.
Huyo ndiyo marehemu Imani Madega na harakati zake ndani ya Yanga. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.

LOS ANGELES, Marekani
Bingwa mara tano wa National Basketball Association (NBA), Kobe Bryant, alifariki dunia akiwa na umri wa miaka 41 katika ajali ya helikopta, pamoja na bintiye Gianna mwenye umri wa miaka 13, na watu wengine saba, mwaka 2020.
Sanamu yake ya shaba, iliyo na futi 19 na uzani wa lb 4,000, iko nje ya nyumba ya Lakers, Crypto.com Arena. Inaonyesha Bryant ambaye aliichezea Lakers maisha yake yote, katika jezi yake namba nane maarufu.
Gwiji wa Los Angeles Lakers Kobe Bryant ametunukiwa sanamu hiyo na timu ya NBA kufuatia kifo chake mwaka 2020. Mjane wake Vanessa na nguli wa zamani wa Lakers, Kareem Abdul-Jabbar walikuwa miongoni mwa watu waliotoa heshima zao, wakimuelezea Bryant kama “jinsi ubora unavyoonekana”.

LEVERKUSEN, Ujerumani
Mkurugenzi wa Michezo wa klabu ya Bayer Leverkusen ya Ujerumani, Simon Rolfes anasema kuwa ana uhakika kwamba kocha wa klabu hiyo, Xabi Alonso atasalia katika klabu hiyo baada ya majira ya joto, huku kukiwa na uvumi unaomhusisha kocha huyo kwenda katika klabu ya Liverpool ya Uingereza.
Alonso, ambaye alishinda Ligi ya Mabingwa na Kombe la FA katika kipindi cha miaka mitano kama mchezaji Anfield, ametajwa kama mbadala wa Jurgen Klopp, ambaye ataondoka katika klabu hiyo mwishoni mwa msimu huu.
Mhispania huyo ameibadilisha Leverkusen tangu kuteuliwa kwake BayArena Oktoba mwaka 2022, na amekuwa akiwahangaisha vigogo wengi katika mechi zake ambazo amekutana nao.
Leverkusen walikuwa kwenye eneo la kushushwa daraja wakati Alonso alipochukua usukani, lakini sasa wanajikuta wakiwa kileleni mwa msimamo baada ya kuichapa Bayern Munich 3-0 kwenye mchezo wa Ligi hiyo ya Bundesliga uliochezwa hivi karibuni.
“Ndiyo, nina uhakika na hilo moja ya sababu ni mkataba, nyingine ni jinsi anavyojisikia vizuri, familia, yeye mwenyewe”.

DAR ES SALAAM

Na Nicolaus Kilowoko

Baada ya kukaa miezi saba bila kuwa na pambano lolote, bondia Suleiman Kidunda anatarajiwa kupanda ulingoni mwezi Machi mwaka huu dhidi ya bondia kutoka nchini Afrika Kusini.
Selemani Kidunda anatarajiwa kuzipiga dhidi ya bondia Asemahle Wellem kutoka Afrika Kusini katika pambano ambalo litapigwa Machi 1 mwaka huu katika ukumbi wa Warehouse, Masaki, jijini Dar es Salaam.
Kidunda alisema kuwa kimya kingi, kishindo huvuma, hivyo kwa sasa ameshaingia vitani kupambana na kukaa kwake pembeni kumemfanya aendelee kujifua dhidi ya mapambano yake huko mbele.
Bondia Asemahle Wellem kutoka Afrika Kusini ni sawa na mfupa uliowashinda wengi, kwani amekuwa na mapambano mengi na kuwashinda wengi katika mapambano yake.
“Mashabiki wangu naomba msiwe na hofu, dogo katangaza vita na mimi nishaingia vitani, yaani nimeshaingia chaka, nipo tayari kupambana, tuombe Mungu tukutane hiyo siku,” alisema Kidunda.

DAR ES SALAAM

Na Nicolaus Kilowoko

Aliyekuwa kocha wa makipa wa zamani wa timu ya soka ya Yanga, Juma Pondamali ameelezea kukerwa na ufalme wanaopewa makipa wa kigeni ndani ya Ligi ya Tanzania.
Pondamali alisema kuwa haikubaliki kwa makipa wa kigeni kutawala soka la Tanzania wakati kuna makipa wengi wenyeji wenye uwezo mkubwa ambao bado hawajapewa nafasi ya kuonyesha vipaji vyao.
Alisema kuwa nchi kama Misri wamefanikiwa kuweka utaratibu ambao unawasaidia hata sasa kuwa na wachezaji wengi wazawa kuliko wale wakigeni, na hiyo imewasaidia sana kufanya vyema katika soka lao.
“Never never’, haikubaliki wachezaji wa kigeni kuja kutawala soka la Kitanzania wakati sisi tuna vijana wengi sana ambao wana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri katika vipaji vyao”, alisema Pondamali.
Alisema kuwa yeye anashauri hata Tanzania kuweka utaratibu wa kutokuwapa sana nafasi wachezaji wa kigeni ambao kwa wakati mwingine, ni sawa tu na wachezaji wenyeji.
Pondamali ambaye alidumu ndani ya klabu ya soka ya Yanga kwa miaka minne kama kocha wa makipa, alikuwa na wakati mzuri tangu alipokuwa akicheza, mpaka kuwa kocha.
Mbali na kuishauri mamlaka husika kuweka utaratibu wa wachezaji wa kigeni, lakini aliwashauri wachezaji vijana wazawa kuhakikisha kwamba wanajitahidi kufanya mazoezi na kutafuta mafunzo kwenye vituo mbalimbali ili kujinoa zaidi.
Pondamali alisema kuwa wao wamekuwa wakiwasaidia wachezaji wengi katika kituo chao kilichopo Mkwajuni wakati ligi inaposimama kwa muda, na wamekuwa wakifanya vyema kwenye timu zao, hivyo akaendelea kuwaomba wachezaji vijana kutafuta uzoefu kwenye kazi zao.
Ikumbukwe pia kuwa Pondamali aliwahi kuwa kipa wa Taifa Stars miaka ya zamani, ambapo mwaka 1980 alishiriki fainali za AFCON zilizofanyika nchini Nigeria, ambazo ndizo fainali za kwanza Tanzania kushiriki.
Mbali na hilo, aliidakia timu ya Yanga akiwa pamoja na wachezaji kama Fred Minziro (sasa kocha), Leodgar Tenga (Rais wa zamani wa TFF), na wengineo wengi.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, akiwabariki Watawa wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Watawa iliyoadhimishwa katika Parokia ya Kristo Mfalme – Tabata, jimboni humo. (Picha na Yohana Kasosi)

DAR ES SALAAM

NA MATHAYO KIJAZI

Watawa nchini Tanzania wametakiwa kutokengeuka, wakidhani mahali walipo wamepotea njia, bali watambue kuwa wanapaswa kuyaishi yale waliyoyapokea kwa furaha, kwa sababu wao ni zawadi kutoka kwa Mungu kwa ajili ya Kanisa.
Hayo yalisemwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, wakati akitoa homilia katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Watawa iliyoadhimishwa katika Parokia ya Kristo Mfalme – Tabata, jimboni humo.
“Nasema hivyo nikijua kwamba hapa na pale, wapo Watawa wanaokengeuka, wako wanaodhani wamepotea njia, na katika mahangaiko, wanabadili mwelekeo….
“Naomba yale ambayo mmeyapokea kwa unyofu, mmeyapokea kwa furaha, na mmetamka kwa hiari yenu kwamba mtayaishi, basi muyaishi,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Aidha, Askofu Ruwa’ichi aliwashukuru wote kadri ya karama zao mbalimbali, akiwaomba kuziendeleza karama hizo katika maisha yao.
Wakati huo huo, Askofu Mkuu Ruwa’ichi aliwataka Watawa hao kuwa watii kwa Mungu na mpango wake, kwa ajili yao na Kanisa, pia Ulimwengu.
“Tumejitosa kwa nadhiri zetu kumfuata Kristo, Nuru ya Ulimwengu, ambaye ni Mtii, ambaye ni Fukara, ambaye ni mwenye Usafi Kamili wa Moyo.
“Na kama ndivyo, basi tunao wito wa kuwa watii, watii kwa Mungu na mpango wake kwa ajili yetu, kwa ajili ya Kanisa, na kwa ajili ya Ulimwengu,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Alisema kuwa watawa hao wanatakiwa kuwa wasafi wa moyo, wakiishi kitakatifu, wakiishi kwa upendo, na kushuhudia na kuutangazia Ulimwengu upendo wa Mungu.
Kwa mujibu wa Askofu Mkuu Ruwa’ichi katika Ulimwengu wa sasa, wapo wanaowashangaa Watawa kwa kukubali kuishi maisha ya ufukara, usafi wa moyo na utii, wakidhani kwamba wamepotea njia, bali watambue kuwa mbele ya Mungu, maisha ya Wakfu, ni Matakatifu.
Aliwataka Watawa kuuishi utakatifu wa maisha yao pamoja na ushuhuda unaowapasa, ili kwa njia yao, Kristo atambulike, aungamwe, na aaminiwe na wengi.
Askofu Mkuu aliwasisitiza Watawa hao kuwa na shauku ya kumuona, kumpokea, kumuungama, pamoja na kumtukuza Kristo kwa maisha matakatifu na ya kumpendeza Mungu.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Wakristo wametakiwa kufuata nyayo za Mtakatifu Theresa wa Kalkuta za kuwasaidia watu wenye uhitaji, hasa wanaoteseka kiroho, ili wawapatie faraja katika maisha yao ya kila siku.
Hayo yalisemwa na Sista Carmela anayefanya utume wake katika Kituo cha Furaha na Amani kilichopo Parokia ya Familia Takatifu – Mburahati, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, baada ya Tumaini Media kufanya matendo ya huruma Kituoni hapo.
“Karibuni katika Kituo hiki cha Furaha na Amani, kama mnavyoona hapa kuna watoto, wazee pamoja na walemavu... Kituo hiki siyo kipya sana, kwani kilianzishwa mwaka 1976, na kimetoa huduma kwa miaka hiyo yote, na bado kinaendelea kutoa huduma.
“Tunafuata nyayo za Mama Theresa wa Kalkuta, kile alichokifanya, na anatamani na sisi tuendelee kukifanya, kuwatembelea na kuwajua wenye shida au wahitaji, siyo tu kwa ajili ya mavazi au chakula, wapo watu wengine ambao wanateseka kiroho, kwa hiyo tunatakiwa kuwagusa waliokata tamaa ili warudi kwa Mungu,” alisema Sista Carmela.
Aliongeza kuwa ni vyema kila mmoja akajitahidi kuwa mwanga kwa wengine, ili wanapomwona yeye, wamwone Mungu kutokena na jinsi yeye anavyoishi.
Sista Carmela aliwashukuru wafanyakazi wa Tumaini Media pamoja na wadau mbalimbali kwa majitoleo yao katika kituo hicho, akiwaomba kuendelea na moyo huo, kwani Mungu anawaita wote ili wawe Watakatifu.
Kwa upande wake, Paroko wa Parokia ya Familia Takatifu- Mburahati, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Vitalis Kassembo aliwashukuru Wanatumaini Media waliokwenda kufanya matendo ya huruma.
“Lakini kwa namna ya pekee tunaishukuru sana familia ya Tumaini Media kwa majitoleo yenu mazuri. Hapa tunajifunza jambo moja - ‘furaha katika kutoa’. Tunapomtolea Mungu, tunabarikiwa zaidi;
“Kwa hiyo Mungu azidi kuwabariki, na hasa Wanatumaini Media tunapomshukuru Mungu kwa miaka 30 ya Utume wetu katika Kanisa, ni miaka mingi sana hiyo. Katika miaka yote hiyo, kuna watu wengi wamefaidika, kuna watu wengi wamepata uponyaji,” alisema Padri Kassembo na kuongeza,
“Tunaendelea kuwashukuru na kuwaombea kwa Mungu ili kazi hiyo iendelee zaidi kwa msaada wa Mungu, na kwa msaada wa Waamini ambao wanaendelea kujitolea kwa hali na mali ili kuhakikisha Injili inamfikia kila mmoja wetu,” alisema Padri Kassembo.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Tumaini Media, Arnold Kimanganu alisema kuwa kama Wakristo Wakatoliki, jukumu lao ni kushirikiana, akiongeza kuwa amefarijika kuona namna huduma inavyotolewa katika Kituo hicho.
Kimanganu alimshukuru Padri Kassembo kwa kuwa kiunganishi kizuri kwa Tumaini Media na Kituo cha Furaha na Amani.

NA MATHAYO KIJAZI

Wakati Redio Tumaini ikiadhimisha Jubilei ya Miaka 30 tangu kuanzishwa kwake maadhimisho ambayo yameonekana kufana, imeelezwa kuwa mtu anayetunza afya ya akili, ataweza kuamua na kutenda mambo mema maishani  mwake.
Paroko wa Parokia ya Familia Takatifu- Mburahati, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Vitalis Kassembo, alisema hayo wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Shukrani kwa Mungu kwa Redio Tumaini kutimiza miaka 30, tangu kuanzishwa kwake Februai 3, mwaka 1994.
Aliwasisitiza Waamini kuitunza afya ya akili na roho, wakiitunza miili yao ili waendelee kuunda utakatifu katika maisha yao.
“Katika maisha, wengi wetu mara nyingi tunajikuta tunaumwa afya ya akili. Afya ya akili imetusababishia miili yetu isiwe na afya njema. Hata hivyo, magonjwa hayo yametufanya tuteseke mno, kwa sababu wakati mwingine unaweza kupewa habari ya msiba wa kifo cha mtu wako wa karibu, unjikuta unashikwa na ‘presha’ kwa kuwa akili yako haikuwa tayari kupokea habari hiyo,” alisema Padri Kassembo.
Padri Kassembo aliwaasa Waamini kuwa na utayari wa kumtumikia Mungu, kwani anayefanya mambo ya Mungu, na Mungu naye hufanya mambo ya mtu huyo.
“Tunakumbushana kufanya Tafakari ndugu zangu. Tuwe na utayari wa kumtumikia Mungu…kumbuka kwamba unapoamua kufanya mambo ya Mungu, na Mungu naye anafanya mambo yako,” alisema Padri Kassembo.
Ka mujibu wa Padri Kassembo Waamini wanatakiwa kujenga utamaduni wa kusameheana, wanapokoseana, kwani hiyo itawafanya wazidi kupokea baraka za Mungu katika maisha yao.
Aidha, Padri huyo aliipongeza      Tumaini Media, hasa Redio Tumaini kwa kutimiza miaka 30 tangu ilipoanzishwa, akisema chombo hicho cha habari kina mchango mkubwa katika kuinjilisha na kuhabarisha.
Alibainisha kwamba wapo wagonjwa ambao hawawezi kwenda popote, ila wanafarijika wanaposikiliza Redio Tumaini, kutazama Tumaini Tv, na kusoma taarifa mbalimbali zinazoandikwa katika gazeti la Tumaini Letu.
Kwa upande wake Mratibu wa Matukio ya Kanisa Tumaini Media, Gaudence Hyera, alimshukuru Padri Kassembo kwa kukubali Sherehe za Miaka 30 ya Redio Tumaini zifanyike parokiani hapo.
Hyera alisema kuwa Familia Takatifu ndiyo chanzo cha yote yanayoendelea kutendwa na Kanisa, hivyo Misa hiyo kuadhimishwa katika Parokia ya Familia Takatifu, ni kumshukuru Mungu aliyeamua Familia hiyo iwepo.

NA MWANDISHI WETU

Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Dominiko - Mbezi Juu, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Daniel Kilala amesema kuwa kila Mbatizwa anatumwa kupokea wajibu wa kutangaza Injili kwa maneno na matendo yake.
Padri Kilala aliyasema hayo wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Domonika ya Tano ya Mwaka ‘B’ wa Kanisa, iliyoadhimishwa parokiani hapo.
“Paulo anatukumbusha wajibu wetu wa kuhubiri Injili. Sisi sote katika Ubatizo, tulipobatizwa, tumeshirikishwa Ukuhani, Ufalme, na Unabii wa Kristo. Kumbe kila Mbatizwa anapokea wajibu wa kutangaza Injili kwa maneno na matendo yake,” alisema Padri Kilala.
Padri huyo aliwaasa Waamini kuacha kukata tamaa, akiwasihi kuwa na matumaini kila wakati, kwani Mungu yuko pamoja nao kila wakati.
Aliwasisitiza kutokupenda tu mambo yao binafsi, bali wapende pia mambo yanayomhusu Mungu, akisema, “Watu wanapenda sherehe tu, hata ndoa nyingi zinavunjika kwa sababu ya kutokuwaombea wanandoa, badala yake watu wanaangalia tu sherehe wakati wa harusi,” alisema Padri Kilala.
Padri Kilala aliwaonya Wakristo kuepuka kutawaliwa na mambo ya anasa na choyo katika maisha yao, akisema kuwa jambo hilo linasababisha baadhi ya mambo yao kuwa magumu.
Aliwataka kuitumia Dominika ya Tano ya Mwaka ‘B’ wa Kanisa kutafakari kuhusu mateso na mahangaiko mbalimbali wanayoyapata, huku wakizidi kumtumainia Kristo katika maisha yao.
Aliongeza kuwa hata wanapokumbana na changamoto mbalimbali za kimaisha, hakuna yeyote wa kumkimbilia, zaidi ya Kristo pekee, kwani yeye ndiye muweza wa mambo yote.
Alibainisha pia kuwa Waamini wanapaswa kutumia muda wao kuwasiliana na Mungu, huku wakitambua umuhimu wa sala, pamoja na kutenga muda maalum kwa ajili ya kusali.
Katika hatua nyingine, Padri Kilala aliwataka waamini kuitegemeza Tumaini Media kwa kuendelea kukiunga mkono chombo hicho, ili Injili iendelee kutangazwa Tanzania na duniani kote.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei wa Parokia hiyo, Neo Pascal, aliishukuru Tumaini Media kwa namna inavyoendeleza uinjilishaji, akiwasihi Waamini kuendelea kukitegemeza chombo hicho.
Naye Katekista Joseph Francis alisema kuwa wao kama Wakristo, hawana budi kuendelea kujikita katika sala, kwani hiyo itawasaidia kupata neema ya Mungu katika maisha yao.