Na Angela Kibwana
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametoa mchango wa Sh milioni 100 kwa ajili ya ukarabati wa Kanisa Kuu la Mt. Patrick jimboni Morogoro.
Mchango wa Rais Samia umewezesha kuezeka upya Kanisa hilo kongwe ambao ukarabati wa Kanisa hilo umefikia asilimia 98.
Askofu wa Jimbo Katoliki Morogoro Mhashamu Lazarus Msimbe (SDS) ametoa shukrani kwa Serikali na wadau mbalimbali kwa ushirikiano walioonesha tangu kuanza kwa shughuli za ukarabati wa Kanisa kuu la Mtakatifu Patris jimboni humo.
Mhashamu Askofu Msimbe ametoa pongezi hizo kwa mahojiano maalum na Tumaini Letu ofisini kwake akisema kuwa anawashukuru pia waamini wa Kanisa hilo walioshiriki kuchangia ukarabati wa Kanisa hilo huku akiwapongeza uongozi wa Halmashauri Walei kwa umoja na mshikamano wao.
Aidha Mhashamu Askofu Msimbe alisema kuwa baada ya hatua zote muhimu kukamilika kukarabati Kanisa hilo ikiwa ni pamoja hatua itakayofuata ni kutabaruku kutokana na kugusa sehemu mbalimbali za Kanisa hilo nje na ndani, maeneo matakatifu ya Kanisa hilo kuguswa wakati wa ukarabati huo.
“Napenda kutoa shukurani kwa Mwenyezi Mungu ambaye ametupa nguvu na kutuwezesha kimawazo, ni Mungu mwenyewe amefanya hii kazi kwa ajili ya nyumba yake. Nipende kutoa shukurani nyingi kwa ushirikiano tuliokuwa nao kwa Serikali katika suala zima la ukarabati wa Kanisa, niwashukuru viongozi na waamini wote walioshiriki kuchangia ukarabati huu,” alisema Askofu Msimbe.
Na Waandishi Wetu
Waamini wameaswa kutopokea Ekaristi Takatifu kimazoea huku wakia hawana maandalizi mazuri kiroho.
Ujumbe huo umetolewa na maaskofu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Askofu Mkuu wa Jimbo hilo Mhashamu Sana Jude Thaddeus Ruwa’ichi na Askofu Msaidizi Mhashamu Henry Mchamungu kwa nyakati tofauti wakati wa maadhimisho ya Misa Takatifu ya Sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana Wetu Yesu Kristo
Akiwa katika Kanisa Kuu la Mt. Yosefu, Mhashamu Sana Jude Thaddeus Ruwa’ichi alisema waamini wanapaswa kukumbuka kuwa Ekaristi Takatifu si kitu cha kupokelwa kimazoea bali kinahitaji tafakari na maandalizi ya kiroho.
“Mnatakiwa kutambua kuwa Ekaristi siyo kitu cha mazoea wala cha kubahatisha bali ni adhimisho Takatifu sana na kuu la wokovu wetu,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Aidha alisema kuwa kila mtu anatakiwa kufahamu ni nini anafanya pale kwenye adhimisho la Misa Takatifu kwa sababu ndipo kwenye kiini cha imani.
Mbali na hayo aliwasisitiza waamini kuziishi Sakramenti kwa imani, upendo na ibada kwa ajili ya kupata uzima wa kimungu.
Alisema kwamba wana wa Israeli walipokuwa jangwani walimlalamikia Musa kwa kuwa na njaa na kusema ni bora angewaacha utumwani kuliko kuwapeleka jangwani jambo ambalo alisema lilionesha jinsi binadamu walivyo vigeugeu.
Askofu Ruwa’ichi aliwataka waamini wafahamu kwamba utumwa ni mateso japo kuwa wanadamu wengi ni vigeugeu wanaoweza kutakani kurudi utumwani wanapopata shida katika safari ya ukombozi.
Askofu Ruwa’ichi aliwataka waamini watambue kuwa wao ni Taifa jipya la Mungu na wako hivyo kwa sababu ya sadaka ya Yesu Kristu ya kukubali kujishusha na kutwaa ubinadamu na kufa kifo cha aibu.
Sambamba na hayo alisema kuwa Yesu Kristu alikubali kuteswa na kufa msalabani kwa ajili ya kutaka kukomboa ulimwengu kutoka katika dhambi na kabla ya kufa kwake aliweka Ekaristi Takatifu ikiwa alama ya upendo wake mkuu kwa wanadamu.
Pia alisema kuwa Ekaristi ni ukumbusho wa mateso,kifo na ufufuko wa Yesu Kristu kwani katika Ekaristi kila mtu amepewa sadaka ya ukombozi yenye kuwapatanisha watu na Mungu.
Askofu Ruwa’ichi aliendelea kusema kuwa Ekaristi ni Sakramenti Kuu ya wokovu ambayo Yesu Kristu aliitoa kama zawadi kwa mitume wake kwa ajili ya kuiadhimisha na kupokea mwili na damu ya Yesu Kristu.
Na Mwandishi Wetu
Serikali imeendelea kuimarisha hatua za kudhibiti, na kutokomeza tatizo la mbegu feki nchini, kupitia mifumo ya kisasa ya uthibitishaji wa ubora, ukaguzi wa mara kwa mara, pamoja na utoaji wa elimu kwa wakulima.
Akijibu swali la Mbunge wa Mbozi, Onesmo Merdson Mnkondya, kuhusu mpango wa Serikali wa kukomesha mbegu feki nchini, Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde amesema kwamba, kwa mujibu wa Kifungu cha 15 cha Sheria ya Mbegu (Sura ya 308, Toleo la Urekebu la mwaka 2023), mbegu zote zinazouzwa nchini, zinapaswa kuthibitishwa ubora wake, na Taasisi ya Uthibitishaji wa Mbegu Tanzania (TOSCI).
Silinde amesema kuwa, TOSCI imeanzisha matumizi ya lebo za kielektroniki, zinazotolewa kwa kampuni za mbegu, ili kuwasaidia wakulima, kuhakiki uhalisia wa mbegu wanazonunua. Kupitia mfumo huo, mkulima anaweza kukwangua lebo maalumu, iliyowekwa kwenye kifungashio cha mbegu, na kuingiza namba husika kwenye simu yake ya mkononi, ili kupata taarifa za uthibitisho wa mbegu hizo.
Matumizi ya teknolojia hiyo, yameleta mafanikio makubwa katika mapambano dhidi ya mbegu feki, ambapo matukio yaliyoripotiwa yamepungua kutoka 325 mwaka 2014/2015, hadi kufikia matukio 10 pekee mwaka 2023/2024.
Mbali na matumizi ya teknolojia, Serikali kupitia TOSCI, inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara, katika maduka yanayouza mbegu nchini. Katika ukaguzi uliofanyika kati ya Julai 2025 na Januari 2026, wafanyabiashara 13 walibainika kujihusisha na uuzaji wa mbegu feki, au mbegu zisizokidhi viwango vya ubora.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri Silinde, kesi moja tayari ipo mahakamani, huku uchunguzi dhidi ya watuhumiwa wengine 12 ukiendelea, ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.
Aidha, Serikali imeendelea kutoa elimu kwa wakulima, kuhusu umuhimu wa kutumia mbegu bora, na namna ya kutambua mbegu feki. Kupitia Kampeni ya Mali Shambani, wakulima 5,822 walipatiwa elimu hiyo, huku wakulima wengine 6,763, wakipata huduma na ushauri kupitia Kituo cha Huduma kwa Wateja (Call Center), katika kipindi cha Novemba 2025 hadi Januari 18, 2026.
Silinde amesisitiza kwamba, Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi wa sekta ya mbegu, ili kuhakikisha wakulima wanapata mbegu bora na salama, sambamba na kuwalinda dhidi ya wafanyabiashara, wanaojihusisha na uuzaji wa mbegu feki.
Na Mwandishi Wetu
Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Watumishi wa Umma kote nchini, watambue na wathamini nafasi za kazi walizonazo, kwamba ni huduma wanazotakiwa kuzitoa kwa wananchi.
“Ninapokuwa kwenye hizi ziara, nimekuwa ninawaambia watumishi wenzangu walioko maofisini kwamba, kuwa kwenye hizi nafasi ni huduma, ni utumishi, na kuwazungusha watu wanapotaka hizo huduma ni ushamba,” alisema.
Waziri Mkuu alitoa wito huo Ijumaa, Juni 05, 2026, wakati akizungumza na wakazi wa Jimbo la Isimani, katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Kijiji cha Isimani, Kata ya Kihorogota, Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.
“Tutahakikisha hoja zote zinazotolewa na wananchi zinafanyiwa kazi, kwa sababu huo ndio wajibu wa Serikali, kuwatimizia wananchi yale yaliyo mahitaji yao ya kila siku, ili waweze kufanya kazi wakiwa na utulivu. Nitoe rai kwa ofisi zote za umma, tuyazingatie hayo,” alisisitiza.
Na Mathayo Kijazi
Imeelezwa kuwa vijana wakishapokea Sakramenti ya Kipaimara, hawawi watoto tena, bali wanakuwa Wakristo wakomavu, na wenye kuwajibika katika kuishuhudia Injili ya Yesu Kristo.
Hayo yalisemwa hivi karibuni, na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Sana Jude Thaddaeus Ruwa’ichi - OFMCap, wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara, katika Parokia ya Mtakatifu Nicholaus wa Tolentino - Msingwa, jimboni humo.
“Kama kwenye Ubatizo walizaliwa, kwenye Kipaimara wanakamilishwa, wanafanywa kuwa Manabii, wanakabidhiwa Utume, wanapewa jukumu la kuishuhudia Injili ya Bwana wetu Yesu Kristo;
“Kwa hiyo vijana wapendwa, wanangu wapendwa, leo mnaanza ngwe mpya, ngwe mpya ya safari yenu ya imani. Kuanzia leo mkiwa mnarudi nyumbani, mkiwa mmepata Kipaimara, jitambueni kuwa ninyi sio watoto tena, utoto mtaucha pale kwenye mlango wa Kanisa. Na Paroko naomba kuanzia leo usiwaite tena watoto, waite Waimarishwa, waite watu wakomavu, waite watu wenye kuwajibika,” alisema Askofu huyo.
Aidha, Askofu Mkuu aliwasihi vijana hao kutokumhadaa Kristo, na kwamba wamshuhudie kwa maneno, matendo na kwa maisha yao yote.
Sambamba na hayo, aliwasisitiza kutoona aibu kusema mbele za watu kwamba, wanamuungama Kristo katika maisha yao, kwani kazi kubwa wanayotumwa kuifanya, ni kuitetea imani yao.
“Nanyi vijana wapendwa, hakikisheni kwamba hamumhadai Kristo, bali mnamshuhudia kwa maneno, kwa matendo, na maisha yenu yote. Na msione haya kujibainisha kuwa Wakristo, msione haya kusema kwamba, ‘Mimi namuungama Kristo Mwokozi wangu aliyeteswa, aliyekufa na aliyefufuka’. Simameni imara, simameni kidete kuujenga Ufalme wa Kristo,” alisema Askofu huyo.
Wakati huo huo, Askofu Mkuu Ruwa’ichi alitoa wito kwa wazazi, kushirikiana na watoto wao, katika kuuendeleza utume huo unaowapasa.
Pia, aliwasihi Mapadri, Makatekista pamoja na Viongozi wa Kamati Tendaji, kuhakikisha kuwa wanashikamana na kusindikizana na vijana hao, katika safari ya kuujenga Ufalme wa Mungu.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo ya Msingwa, Padri Geofrey Mtitu - OSA, alimshukuru Askofu Mkuu Ruwa’ichi, kwa kufika parokiani hapo, na kuadhimisha Misa hiyo Takatifu.
Na Mathayo Kijazi
Chama cha Kitume cha Vijana Wakatoliki Wafanyakazi (VIWAWA) ngazi ya Taifa, kimefanya Uchaguzi Mkuu, na hivyo kuwapata viongozi wapya, watakaoongoza chama hicho hadi mwaka 2029.
Akizungumza hivi karibuni, katika Mkutano wa makabidhiano, uliofanyika katika Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Kurasini, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwenyekiti mpya wa VIWAWA Taifa, Elia Mshana, alisema kwamba Dira Kuu waliyonayo ni kumjenga kijana mwenye nafasi katika jamii na katika Kanisa.
Aidha, Mwenyekiti huyo alitoa wito kwa walezi, wanaowalea vijana hao kuanzia ngazi za Parokia pamoja na Majimbo, kuwapa nafasi vijana katika Halmashauri za Walei, kwani wanaweza kufanya kazi katika maeneo hayo.
“Wito wangu kwa walezi wanaowalea vijana, kuanzia ngazi za Parokia mpaka Majimbo, Wakurugenzi wote wawape nafasi vijana. Lakini pia katika Halmashauri za Walei kwenye Parokia zao, vijana wapewe nafasi kubwa zaidi, kwa sababu wakiaminiwa wanaweza,” alisema Mwenyekiti, Elia Mshana.
Aliongeza kwamba, imekuwa ni desturi ya Viongozi wa VIWAWA Taifa, kukutana Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), kufanya makabidhiano kati ya Viongozi Wastaafu na Viongozi wapya, kwa ajili ya kuanza rasmi majukumu yao ya kiuongozi.
Mwenyekiti huyo aliwashukuru viongozi waliomaliza muda wao, kwani wamefanya kazi kubwa, katika kipindi chote cha uongozi wao, wakiahidi kwenye kuendeleza yale yaliyoanzishwa na uongozi uliopita.
Kwa upande wake Mwenyekiti Mstaafu VIWAWA Taifa, Mwalimu Leonard Mapolu, alimshukuru Mungu kwa kuwawezesha kufanya shughuli zao za kitume, katika Chama hicho tangu walipoanza mwaka 2023 mpaka 2026.
Mwalimu Leonard Mapolu kutoka Jimbo Katoliki la Shinyanga, ambaye pia ni Mratibu wa VIWAWA Afrika, alisema kwamba katika utume wanashirikishwa, hivyo wana wajibu wa kutii na kufuata miongozo ya Kanisa, lengo likiwa ni kumpeleka Kristo kwa wengine.
Pia, alitoa wito kwa vijana kuendelea kushiriki Makongamano mbalimbali ya Kanisa, pamoja na Semina pale wanapopata nafasi, kwani kupitia matukio hayo, wanapata utatuzi wa changamoto zao.
Mwalimu Mapolu alitoa wito kwa Viongozi wapya wa VIWAWA, kuendeleza mradi wao wa kitenge cha VIWAWA, hasa katika kukizalisha kwa ubora mzuri, kwani kwa kufanya hivyo, watakiendeleza vema Chama hicho.
Naye Katibu Mstaafu wa VIWAWA Taifa, Benedict Agustino, alimshukuru Mungu kwa kutumikia katika mihula miwili, ambapo alianza mwaka 2020–2023, kisha 2023-2026, akisema kuwa katika vipindi hivyo, walijitahidi kutekeleza majukumu yao kama ilivyokusudiwa.
Kwa mujibu wa Benedict, miongoni mwa miradi waliyofanikiwa kuitekeleza, katika kipindi cha uongozi wao, ni pamoja na kununua shamba la VIWAWA, lenye ukubwa wa ekari 50, lililopo katika Jimbo Katoliki la Singida, pamoja na shamba jingine lililopo Kibiti, ndani ya Jimbo Kuu la Dar es Salaam.
Na Mwandishi wetu
Wakurugenzi na wawakilishi wa vyombo vya habari vya Kanisa nchini Tanzania wamekutana na wawakilishi wa Kurugenzi ya Mawasilano ya Vatican na kujadili kuhusu ushirikiano wa pamoja kwa lengo la kukuza na kuimarisha mawasiliano kati ya Kanisa Katoliki ulimwenguni na jamii.
Kikao hicho kimefanyika hivi karibuni katika Ubalozi wa Vatican nchini uliopo Jijini Dar es Salaam.
Akifungua kikao hicho Mkurugenzi wa Mawasilano wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini (TEC) Padri Faustine Furaha ameeleza namna vyombo vya habari vya kanisa vinavyofanyakazi hapa nchini.
Alisema kupitia vyombo hivyo Kanisa limefanikiwa kuwafikia zaidi ya waamini Mmilioni 30 na kuwapatia ujumbe wa Injili.
Kupitia kikao hicho wawakilishi hao kutoka Vatican walieleza miradi ya kuboresha ushirikiano na mawasiliano baina ya Kanisa Katoliki na jamii ikihusisha vijana wenye umri usiozidi miaka 35.
Walieleza kuwa wahusika katika mradi huo mradi huo watatakiwa kuwa Shahada ya Mawasiliano, wafanyakazi wa taasisi ya Kanisa Katoliki na wenye uwezo wa kuzungumza lugha ya Kiingereza.
Wameutaja mradi wa pili kuwa ni Mafunzo ya Muda wa miezi mitatu kwa Masista wa Kanisa Katoliki ulimwenguni ambao wana taaluma ya Mawasilano, wenye uzoefu wa kazi kwenye radio, Televisheni, gazeti na mitandao ya kijamii.
Vyombo vya mawasiliano vilivyoshiriki katika kikao hicho ni pamoja na Kurugenzi ya mMawasilino TEC, Tumaini Media, Jugo media, Radio Maria, Radio Habari Njema Mbulu, na gazeti la Kiongozi.
Dar es Salaam
Na Mathayo Kijazi
Mkurugenzi wa Utume wa Walei Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Padri Vitalis James Kassembo amezindua kitenge cha Chama cha Kitume cha Wajane na Wagane, akiwataka kuutumia vema mradi huo katika kuendeleza utume kupitia chama chao.
Uzinduzi huo umefanyika hivi karibuni katika ofisi ya Halmashauri ya Walei iliyopo katika viunga vya Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu, jimboni humo.
Padri Kassembo aliwaasa wote watakaonunua kitenge hicho kuwa waaminifu, akisema kwamba anayechukua vitenge vya idadi fulani, arudishe fedha inayolingana na idadi ya vitenge hivyo.
“Mradi huu utusaidie pia kuendeleza utume. Lakini pia kama wanautume kuweza kujitawala vizuri sisi kama wanachama wa chama hiki. Maana yake tunaongea kuhusu uaminifu katika yale ambayo tutakuwa tumekabidhiwa, kama umekabidhiwa vitenge kumi, basi urudishe fedha ya vitenge kumi, usilete kona kona, kwa sababu ukileta kona kona, tunakwama wote,” alisema Padri Kassembo.
Aliwasisitiza kuutumia mradi huo kuwaunganisha na kuwafanya wawe wamoja zaidi, akiwaasa kutotengana kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo za kutokuwa waaminifu.
LILONGWE, Malawi
Chansela wa Chuo Kikuu cha Katoliki cha Malawi, Askofu Martin Anwel Mtumbuka, ametoa mwito wa kuanzishwa kwa wahitimu, wanaozingatia uadilifu na maadili thabiti, pamoja na ubora wa kitaaluma.
Akizungumza wakati wa Mkutano wa 25 wa Chuo Kikuu, kwa ajili ya utoaji wa Astashahada, Stashahada na Shahada, uliofanyika Ijumaa iliyopita, Askofu Mtumbuka alieleza wasiwasi wake, kuhusu idadi inayoongezeka ya watu walioelimika, ambao hawana uadilifu katika majukumu yao ya kitaaluma na utumishi wa umma.
“Tayari tuna watu wa kutosha walioelimika, lakini kwa kusikitisha, tuna watu wengi sana waliopotoka. Tunachohitaji sasa ni wanaume na wanawake walioelimika, ambao watahudumu kwa uaminifu, uadilifu na huruma,” alisema Askofu Mtumbuka.
Msemaji wa kuanza kwa Sherehe hiyo, Mheshimiwa Jaji Annabel Mtalimanja, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Malawi (MEC), pia aliwasihi wanafunzi waliohitimu hivi karibuni, kukataa ufisadi na rushwa, akielezea kuwa ni vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya taifa.
VATICAN CITY
Mkuu wa Baraza la Kipapa la Makanisa ya Mashariki ya Vatican, Mwadhama Claudio Kardinali Gugerotti, amewasili nchini Ethiopia kwa ziara ya kichungaji na kitume, akiambatana na Padri Dmytro Sabadokh, Katibu Maalumu wa Rais, na Padri Jarozlav Lajciak, anayehusika na Makanisa ya Mashariki ya Ethiopia na Eritrea.
Baada ya kuwasili hivi karibuni, katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Bole wa Addis Ababa, Kardinali Gugerotti alipokelewa na wawakilishi wa Maaskofu, Mapadri, Watawa, na Waamini Walei, wafanyakazi wa uwanja wa ndege, na baadaye katika Ubalozi wa Vatican.
Kardinali huyo baadaye alikaribishwa na Askofu Mkuu wa Metropolitan ya Addis Ababa, Mwadhama Abune Kardinali Berhaneyesus Demerew Souraphiel, na Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki la Ethiopia (CBCE), pamoja na Mapadri wa Jimbo katika Kanisa Kuu la Kikatoliki la Kuzaliwa kwa Bikira Maria, huku ikifanyika sherehe rasmi ya ufunguzi, kuashiria mwanzo wa ziara hiyo.
Kama sehemu ya mpango wake, Kardinali Gugerotti alitembelea Sekretarieti Kuu ya Mkutano wa Maaskofu Wakatoliki wa Ethiopia, ambapo alikutana na maafisa wakuu na wafanyakazi. Wakati wa ziara hiyo, alielezwa kuhusu huduma za Sekretarieti, na jukumu lake katika kusaidia shughuli za dayosisi kote nchini.
Katika ushirikiano muhimu wa kiekumene, Kardinali Gugerotti alikutana na Mtakatifu Abune Mathias I, Patriaki wa Kanisa la Orthodox la Ethiopia la Tewahdo, ambapo aliwasilisha ujumbe kutoka kwa Papa Leo XIV, na kuelezea furaha yake ya kuwa Ethiopia.
Naye Patriaki aliwakaribisha ujumbe huo, akawatakia kila la kheri kwa kukaa kwao, na kuwapa baraka zake, ambapo wakati wa majadiliano yao, viongozi wote wawili walitafakari kuhusu masuala ya amani duniani, na changamoto zinazowakabili Wakristo leo.
Walisisitiza umuhimu wa umoja katika sala, na hatua za ushirikiano, ili kushughulikia changamoto na mateso, yanayowapata Wakristo nchini Ethiopia na duniani kote.
Ziara ya Kardinali Gugerotti itaendelea nchini humo, na kwamba amepangwa kutembelea makanisa yote ya Eastern Rite nchini Ethiopia, ikiwa ni pamoja na Utawa wa Adigrat, Utawa wa Bahir Dar-Dessie, Utawa wa Emdeber, na Utawa wa Metropolitan wa Addis Ababa.
VATICAN CITY
Wakristo wameitwa kuleta chachu ya ukarimu kwa ulimwengu, hasa katika ulimwengu unaoathiriwa kila mara na mantiki ya ubinafsi, huku wakifikiria na kuishi kulingana na mantiki ya kweli zaidi, ile ya ukuaji fungamani wa mwanadamu.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Leo XIV, huku akiwaelekea Waamini katika kituo cha IFEMA, Madrid, ikiwa ni hotuba yake ya mwisho, kabla ya kuanza sehemu ya Pili ya ziara yake ya kitume nchini Hispania.
Hitaji la kufikiria na kuishi, kulingana na mantiki ya maendeleo fungamani ya binadamu, limesikika katika hotuba ya Baba Mtakatifu Leo XIV, akihitimisha hija yake mjini Madrid, kwa kukutana na watu wa kujitolea 17,000, katika Ukumbi wa 3 wa IFEMA, kabla ya kupanda Ndege kuelekea kwenye Mji wa Barcelona, ikiwa ni sehemu yake ya Pili ya ziara ya 4 ya Kitume nchini Hispania, iliyoanza tangu Juni 6 na kuhitimishwa Juni 12, kwa kutembelea pia Visiwa vya Kanari na Tenerife.
Banda hilo la 3 ni moja ya taasisi tano muhimu zaidi, za maonyesho ya biashara barani Ulaya, moja kuu nchini Hispania, ambapo alifika kwa gari katikati ya watu wa kujitolea, waliotambulika kwa rangi ya machungwa.
Katika hotuba yake Askofu huyo wa Roma, alianza na shukrani kwa Mwadhama José Kardinali Cobo Cano, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Madrid, kwa kaka na dada wapendwa katika Jimbo hilo.
Hapa wote walisikika wakitoa ukelele wa kusikitika, na Papa akaendelea. “Kila mmoja wenu na wengine wengi, ambao hawakuweza kuwa hapa asubuhi ya leo, wanastahili “shukrani” maalumu sana, kwa sababu mmetoa uwepo wenu na huduma yenu, na mmefanya hivyo kwa upendo kwa Bwana, Kanisa na Papa.”
VATICAN CITY
Kiongozi wa Kanisa Katoliki Ulimwenguni, Baba Mtakatifu Leo XIV, amewataka Wahispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana katika utamaduni, ili kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini, huku wakisimama kidete, kudumisha na kulinda tunu msingi za ndoa na familia.
Aliyasema hayo katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, akiwa katika ziara yake ya kitume nchini humo, huku akikazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi, kwa kuongozwa na kaulimbiu ya Umoja wa Ulaya, umoja katika utofauti, mambo yanayounda amana na utajiri wa watu wa Mungu.
Ikumbukwe kuwa Baba Mtakatifu Leo XIV, kuanzia Juni 6 hadi 12, 2026, anafanya Hija ya 4 ya Kitume nchini Hispania, kwa kunogeshwa na kaulimbiu: “Alzad la mirada” Yaani “Inueni macho yenu.”
Sambamba na hayo, Papa alikutana na Waziri Mkuu wa Hispania, Pedro Sánchez Pérez-Castejón, ambaye amekuwa madarakani tangu Juni 2, 2018, na ndiye Kiongozi Mkuu wa Serikali ya Hispania, ambapo alitumia nafasi hiyo pia, kukutana na kuzungumza na Bunge la Hispania, na baadaye kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania (Conferencia Episcopal Española: CEE)”.
Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Leo XIV, alikutana pia na kuzungumza na Jumuiya ya Jimbo Kuu la Madrid, nchini Hispania, ambapo Mama Kanisa anatembea bega kwa bega na binadamu, anashiriki matumaini na madonda yake, anaendelea kusikiliza na kujibu maswali msingi ya binadamu wa kila nyakati, na kwamba kuna tofauti ya utendaji kati ya Kanisa na Serikali.
Aliongeza kwamba utu, heshima na haki msingi za binadamu, ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuzingatia kuwa uhuru, ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu.
Alibainisha kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya sheria, kanuni maadili na utu wema, na kuongeza kuwa uongozi unabeba dhamana kubwa ya haki na uwajibikaji.
Alisisitiza kuwa vijana wa kizazi kipya, wanapaswa kufundishwa kutafuta na kupenda ukweli, na kwamba watu waondokane na tabia ya ubaguzi na maamuzi mbele, bali wajitahidi kujenga haki jamii.
Sera na mikakati ya Kanisa Katoliki kwa ajili ya wakimbizi na wahamiaji inajikita katika misingi mikuu minne: Kuwapokea, kuwalinda, kuwaendeleza na kuwahusisha, ambapo mwongozo huo unalenga kutetea utu, kuzuia nyanyaso na kuleta mshikamano kupitia huduma za kiroho na kijamii.
Papa alisema kuwa wakimbizi na wahamiaji ni watu wanaokosa haki, amani na usalama; ni watu wanaosiginwa na umaskini, njaa, maradhi sanjari na athari za mabadiliko ya tabianchi, akitoa wito kujenga utamaduni wa mshikamano wa dhati.
Ili kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani na maridhiano, Papa Leo XIV alisema kwamba, kuna haja ya kuheshimiana na kuthaminiana, kwani ulimwengu umekumbwa na mgogoro wa maisha ya kiroho na kitamaduni.
Na Pd. Gaston George Mkude
Amani na Salama!
Injili ya leo, tunakutana na Yesu mbele ya makutano, waliokuwa wamechoka na kutawanyika. Makutano si tu wanawakilisha watu wa nyakati zile za Yesu, bali hata katika siku zetu leo hii.
Ni watu wangapi leo wanapitia magumu na mahangaiko, pamoja na mateso ya kila namna, labda hata baadhi yetu tumechoka, na kutawanyika kama kondoo tusio na mchungaji.
Wangapi leo wanaishi maisha yenye kila majeraha na maumivu! Wangapi leo wamechoka kimwili, kiakili na hata kiroho, kiasi cha kutawanyika na hata kutangatanga kiimani.
Wapo wanaokwenda kila siku, kwa wanaojiita mitume na manabii, na wengine kwa waganga wa kienyeji na wapiga ramli! Yesu anamuona kila mmoja wetu, na moja tu kutoka kwake, anatuhurumia!
Labda mara nyingi tunajiuliza, kwanini Mungu aliye upendo na huruma, anaruhusu wana na watoto wake tupitie magumu kiasi hicho?
Je, Mungu hawezi kutukinga na mateso na magumu? Au je, Mungu hatupendi hata anatuacha tukipitia kikombe hicho cha mateso na mahangaiko?
Ni maswali msingi na ya haki kabisa, kutuingiza katika tafakari ya fumbo la mateso, katika maisha ya ufuasi wetu.
Ni katika Injili ya leo, tunaona Yesu anapokutana na makutano wale, hata anapokutana nasi katika hali ngumu na taabu, anajawa na moyo wa huruma.
Yesu alipowaona, aliwahurumia! Huruma kama alivyokuwa anatukumbusha daima, hayati Baba Mtakatifu Fransisko, ndio haswa sura na utambulisho halisi wa Mungu wetu.
Mungu ni upendo na huruma! Papa Fransisko daima alipenda kurudiarudia na kusema ni sisi tunaochoka kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu, kwani Mungu kamwe hachoki kutuhurumia na kutukumbatia tena na tena!
Shime katika kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu! Jina na utambulisho wa Mungu ni Huruma!
Nabii Isaya anapotambulisha wema na huruma ya Mungu, anajaribu kutuonesha Mungu anatupenda zaidi ya mama anavyopenda watoto wake.
Sisi ni watoto wa Mungu kwa nafasi ya kwanza, na hivyo Mungu kwetu anajifunua kama upendo na huruma. (Isaya 49:14-16).
Na Mwandishi Maalumu
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Katika hotuba yake hiyo, Papa alikazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya umoja katika utofauti, mambo yanayounda amana na utajiri wa watu wa Mungu.
Hija hiyo ya 4 ya Kitume nchini Hispania imebebwa na kauli mbiu: “Alzad la mirada” Yaani “Inueni macho yenu.” Yn 4:35.
Baba Mtakatifu Leo XIV, alikutana na Waziri mkuu wa Hispania Pedro Sánchez Pérez-Castejón, ambaye amekuwa madarakani tangu Juni 2, 2018 na ndiye kiongozi mkuu wa Serikali ya Hispania.
Papa pia amekutana na kuzungumza na Bunge la Hispania na baadaye amepata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania na baadaye jioni wakakutana kwa sala na Ibada kwa Bikira Maria Mama wa Almudena “Santa María de la Almudena” ambaye ni Mlinzi na Mwombezi wa Jimbo kuu la Madrid, Hispania na kila mwaka ifikapo Novemba, 9, mwaka huu, anakumbukwa na Mama Kanisa nchini Hispania. Baadaye usiku, Baba Mtakatifu Leo XIV amekutana na kuzungumza na Jumuiya ya Jimbo kuu la Madrid, Hispania, Waswahili wanasema, siku hii ilikuwa “full shangwe.”
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Amekazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya “In varietate concordia” yaani “Umoja katika Utofauti” kwa kusimikwa katika tofauti za tamaduni, mapokeo na vipaumbele tofauti; mambo ambayo kwa pamoja yanaunda amana na utajiri mkubwa wa watu wa Mungu nchini Hispania.
Mama Kanisa anatembea bega kwa bega na binadamu, anashiriki matumaini na madonda yake, anaendelea kusikiliza na kujibu maswali msingi ya binadamu wa kila nyakati na kwamba, kuna tofauti ya utendaji kati ya Kanisa na Serikali; na kwamba, utu, heshima na haki msingi za binadamu ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuzingatia kwamba, uhuru ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu.