VATICAN CITY
Kiongozi wa Kanisa Katoliki Ulimwenguni, Baba Mtakatifu Leo XIV, amewataka Wahispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana katika utamaduni, ili kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini, huku wakisimama kidete, kudumisha na kulinda tunu msingi za ndoa na familia.
Aliyasema hayo katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, akiwa katika ziara yake ya kitume nchini humo, huku akikazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi, kwa kuongozwa na kaulimbiu ya Umoja wa Ulaya, umoja katika utofauti, mambo yanayounda amana na utajiri wa watu wa Mungu.
Ikumbukwe kuwa Baba Mtakatifu Leo XIV, kuanzia Juni 6 hadi 12, 2026, anafanya Hija ya 4 ya Kitume nchini Hispania, kwa kunogeshwa na kaulimbiu: “Alzad la mirada” Yaani “Inueni macho yenu.”
Sambamba na hayo, Papa alikutana na Waziri Mkuu wa Hispania, Pedro Sánchez Pérez-Castejón, ambaye amekuwa madarakani tangu Juni 2, 2018, na ndiye Kiongozi Mkuu wa Serikali ya Hispania, ambapo alitumia nafasi hiyo pia, kukutana na kuzungumza na Bunge la Hispania, na baadaye kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania (Conferencia Episcopal Española: CEE)”.
Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Leo XIV, alikutana pia na kuzungumza na Jumuiya ya Jimbo Kuu la Madrid, nchini Hispania, ambapo Mama Kanisa anatembea bega kwa bega na binadamu, anashiriki matumaini na madonda yake, anaendelea kusikiliza na kujibu maswali msingi ya binadamu wa kila nyakati, na kwamba kuna tofauti ya utendaji kati ya Kanisa na Serikali.
Aliongeza kwamba utu, heshima na haki msingi za binadamu, ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuzingatia kuwa uhuru, ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu.
Alibainisha kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya sheria, kanuni maadili na utu wema, na kuongeza kuwa uongozi unabeba dhamana kubwa ya haki na uwajibikaji.
Alisisitiza kuwa vijana wa kizazi kipya, wanapaswa kufundishwa kutafuta na kupenda ukweli, na kwamba watu waondokane na tabia ya ubaguzi na maamuzi mbele, bali wajitahidi kujenga haki jamii.
Sera na mikakati ya Kanisa Katoliki kwa ajili ya wakimbizi na wahamiaji inajikita katika misingi mikuu minne: Kuwapokea, kuwalinda, kuwaendeleza na kuwahusisha, ambapo mwongozo huo unalenga kutetea utu, kuzuia nyanyaso na kuleta mshikamano kupitia huduma za kiroho na kijamii.
Papa alisema kuwa wakimbizi na wahamiaji ni watu wanaokosa haki, amani na usalama; ni watu wanaosiginwa na umaskini, njaa, maradhi sanjari na athari za mabadiliko ya tabianchi, akitoa wito kujenga utamaduni wa mshikamano wa dhati.
Ili kukuza na kudumisha misingi ya haki, amani na maridhiano, Papa Leo XIV alisema kwamba, kuna haja ya kuheshimiana na kuthaminiana, kwani ulimwengu umekumbwa na mgogoro wa maisha ya kiroho na kitamaduni.
Na Pd. Gaston George Mkude
Amani na Salama!
Injili ya leo, tunakutana na Yesu mbele ya makutano, waliokuwa wamechoka na kutawanyika. Makutano si tu wanawakilisha watu wa nyakati zile za Yesu, bali hata katika siku zetu leo hii.
Ni watu wangapi leo wanapitia magumu na mahangaiko, pamoja na mateso ya kila namna, labda hata baadhi yetu tumechoka, na kutawanyika kama kondoo tusio na mchungaji.
Wangapi leo wanaishi maisha yenye kila majeraha na maumivu! Wangapi leo wamechoka kimwili, kiakili na hata kiroho, kiasi cha kutawanyika na hata kutangatanga kiimani.
Wapo wanaokwenda kila siku, kwa wanaojiita mitume na manabii, na wengine kwa waganga wa kienyeji na wapiga ramli! Yesu anamuona kila mmoja wetu, na moja tu kutoka kwake, anatuhurumia!
Labda mara nyingi tunajiuliza, kwanini Mungu aliye upendo na huruma, anaruhusu wana na watoto wake tupitie magumu kiasi hicho?
Je, Mungu hawezi kutukinga na mateso na magumu? Au je, Mungu hatupendi hata anatuacha tukipitia kikombe hicho cha mateso na mahangaiko?
Ni maswali msingi na ya haki kabisa, kutuingiza katika tafakari ya fumbo la mateso, katika maisha ya ufuasi wetu.
Ni katika Injili ya leo, tunaona Yesu anapokutana na makutano wale, hata anapokutana nasi katika hali ngumu na taabu, anajawa na moyo wa huruma.
Yesu alipowaona, aliwahurumia! Huruma kama alivyokuwa anatukumbusha daima, hayati Baba Mtakatifu Fransisko, ndio haswa sura na utambulisho halisi wa Mungu wetu.
Mungu ni upendo na huruma! Papa Fransisko daima alipenda kurudiarudia na kusema ni sisi tunaochoka kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu, kwani Mungu kamwe hachoki kutuhurumia na kutukumbatia tena na tena!
Shime katika kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu! Jina na utambulisho wa Mungu ni Huruma!
Nabii Isaya anapotambulisha wema na huruma ya Mungu, anajaribu kutuonesha Mungu anatupenda zaidi ya mama anavyopenda watoto wake.
Sisi ni watoto wa Mungu kwa nafasi ya kwanza, na hivyo Mungu kwetu anajifunua kama upendo na huruma. (Isaya 49:14-16).
Na Mwandishi Maalumu
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Katika hotuba yake hiyo, Papa alikazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya umoja katika utofauti, mambo yanayounda amana na utajiri wa watu wa Mungu.
Hija hiyo ya 4 ya Kitume nchini Hispania imebebwa na kauli mbiu: “Alzad la mirada” Yaani “Inueni macho yenu.” Yn 4:35.
Baba Mtakatifu Leo XIV, alikutana na Waziri mkuu wa Hispania Pedro Sánchez Pérez-Castejón, ambaye amekuwa madarakani tangu Juni 2, 2018 na ndiye kiongozi mkuu wa Serikali ya Hispania.
Papa pia amekutana na kuzungumza na Bunge la Hispania na baadaye amepata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania na baadaye jioni wakakutana kwa sala na Ibada kwa Bikira Maria Mama wa Almudena “Santa María de la Almudena” ambaye ni Mlinzi na Mwombezi wa Jimbo kuu la Madrid, Hispania na kila mwaka ifikapo Novemba, 9, mwaka huu, anakumbukwa na Mama Kanisa nchini Hispania. Baadaye usiku, Baba Mtakatifu Leo XIV amekutana na kuzungumza na Jumuiya ya Jimbo kuu la Madrid, Hispania, Waswahili wanasema, siku hii ilikuwa “full shangwe.”
Baba Mtakatifu Leo XIV katika hotuba yake kwa Bunge la Hispania, ameitaka Hispania kuendelea kuwa ni mahali pa watu kukutana, katika utamaduni ili hatimaye, kujenga mshikamano wa udugu wa kibinadamu, chemchemi ya Injili ya matumaini.
Amekazia utu, heshima, haki msingi za binadamu, ustawi, maendeleo na mafao ya wengi kwa kuongozwa na kauli mbiu ya Umoja wa Ulaya “In varietate concordia” yaani “Umoja katika Utofauti” kwa kusimikwa katika tofauti za tamaduni, mapokeo na vipaumbele tofauti; mambo ambayo kwa pamoja yanaunda amana na utajiri mkubwa wa watu wa Mungu nchini Hispania.
Mama Kanisa anatembea bega kwa bega na binadamu, anashiriki matumaini na madonda yake, anaendelea kusikiliza na kujibu maswali msingi ya binadamu wa kila nyakati na kwamba, kuna tofauti ya utendaji kati ya Kanisa na Serikali; na kwamba, utu, heshima na haki msingi za binadamu ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuzingatia kwamba, uhuru ni zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu.
Baadhi ya Waamini wa Parokia ya Mtakatifu Peter Clavery-Mbezi Louis Jimbo Kuu la Dar es Salaam wakiwa katika maandamano ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu yaliyofanyika Parokiani hapo.
Katibu wa Halmashauri ya Walei Parokia ya Bikira Maria Mama wa Huruma - Mbezi Beach, Jimbo Kuu la Dar es Salam, Juliana Urio akiongoza maandamano wakati wa sherehe za Sikukuu ya Ekaristi Takatifu baada ya adhimisho la Misa Takatifu ya Sherehe ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa Dominika iliyopita parokiani hapo.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mhashamu Henry Mchamungu (wa tatu kushoto) akiwa katika maandamano na Waamini wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Huruma - Mbezi Beach, Jimboni humo wakati wa sherehe za Sikukuu ya Ekaristi Takatifu baada ya adhimisho la Misa Takatifu ya Sherehe ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa Dominika iliyopita parokiani hapo. Aliyebeba Monstranti yenye Ekaristi Takatifu ni Padri Rogatian Msafiri Paroko wa Parokia hiyo.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mhashamu Henry Mchamungu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mapadri, WAWATA na Viongozi mbalimbali wa Walei baada ya Askofu kuwaapisha Viongozi wapya wa WAWATA Jimbo sanjari na adhimisho la Misa Takatifu iliyofanyika katika Parokia ya Bikira Maria Mama wa Fatima. Kulia kwa Askofu ni Mlezi wa WAWATA Padri Joseph Mosha na kushoto ni Mkurugenzi wa Walei Jimbo, Padri Vitalis Kassembo.
Na Dk. Philip Komba
inaadhimishwa ifikapo Juni 3, kila mwaka nchini Uganda, na inakumbusha sadaka ya watu kadhaa, kutoka mahakama ya Mfalme Mwanga II, waliouawa kati ya mwaka 1885 na 1887, kwa kubadili dini na kuwa Wakristo.
Dini hiyo, Mfalme aliiona kama tishio kwa mila za kikabila, na kikwazo cha maisha yake.
Hivyo, kutokana na hilo, Papa Paulo VI mwaka 1969, huko Kampala nchini Uganda, akihutubia Bunge alisema kwamba: “Ninyi Waafrika mnajua maana kubwa ya jumuiya, ni mojawapo ya sifa zenu nzuri na za kibinadamu.”
Kundi la watumishi 22 Wakatoliki (karibu wote ni Waganda), wa mahakama ya Mfalme (Kabaka) Mwanga II wa Buganda, ambao Mama Kanisa aliwatangaza kuwa Watakatifu, waliteswa sana na baadaye kuuawa kishahidi kati ya 1885 na 1887, kwa kutetea imani yao ya kidini.
Watu wengine 150 walikufa katika mapigano kati ya vikundi tofauti, vilivyohusishwa na ushawishi wa wamisionari Wakatoliki au Waprotestanti, na wafanyabiashara wa Kiswahili au Wamisri.
Kifo cha kwanza cha shahidi mnamo Januari 1885, kilifuatiwa mnamo Oktoba, na kile cha Askofu wa Kiingereza J. Hannington na Joseph Mukasa Balikuddembe. Kundi la Waislamu lilimshawishi Mwanga, kuhusu kuhusika kwa Wakristo katika kuchomwa moto, kwa eneo la kifalme (1886), na kwa hiyo ukatili wa mfululizo mpya wa mauaji, uliwashtua sana viongozi wasio Wakristo, kiasi kwamba walizuia mauaji zaidi na hata kusababisha ongezeko la ubatizo. Mashahidi 22 Wakatoliki, walitangazwa kuwa Watakatifu mnamo 1964 na Papa Paulo XIV, ambaye pia alifanya ziara ya Kitume nchini Uganda.
Mtakatifu Paulo VI, alitimiza ziara hiyo kuanzia tarehe 13 Julai hadi tarehe 2 Agosti 1969. Ziara hiyo ya Uganda mara nyingi, imekumbukwa kwa kutia moyo Kanisa changa la Afrika, kukua katika ukomavu, kwa ajili ya kukuza ubinadamu na kwa ajili ya kutafuta amani.
Papa Mtakatifu akikutana na baadhi ya Waamini wa Kiislamu, katika Ubalozi wa Vatican mjini Kampala alieleza kuwa:
“Tuna uhakika wa kuwa katika ushirika nanyi, tunapomwomba Mwenyezi Mungu, aamshe mioyoni mwa Waamini wote barani Afrika, hamu ya upatanisho na msamaha, ambayo mara nyingi hupendekezwa katika Injili na Kurani.
Na tunawezaje kushindwa kuhusisha na ushuhuda wa uchamungu, na uaminifu wa mashahidi Wakatoliki na Waprotestanti, kumbukumbu ya wale wanaoungama imani ya Kiislamu, ambao historia yao inatukumbusha kwamba, walikuwa wa kwanza mnamo 1848, kulipa kwa maisha yao kwa kukataa kukiuka maagizo ya dini yao?”
Hotuba ya Papa Paulo XIV kwa Uganda
Ndugu msikilizaji na msomaji, vilevile Mtakatifu Paulo VI akikutana na Rais, Mamlaka za kiraia na kikosi cha Kidiplomasia cha Uganda, katika Ukumbi wa Bunge huko Kampala tarehe 1 Agosti 1969, wakati wa hija yake ya kitume alitoa hotuba yake.
Katika muktadha huu wa maadhimisho ya Mashahidi, tunapenda kukumbusha hotuba hii ya Kinabii, katika ziara yake ya kwanza barani Afrika. Maono yake na utabiri wake, ulikuwa kama wa watangulizi wake, na wale ambao walifuata hadi leo hii. Mapapa wote kilio ni kimoja. Katika ulimwengu uliogawanyika vipande vipande na vita, unahitaji amani, haki na usawa.
Katika safu hii ya Chimba Chimba Historia ya Kanisa wiki iliyopita, tuliendelea kuwaletea historia ya Uasi wa Martin Luther na historia ya maisha yake ya uasi.
Leo tunaendelea kuwaletea historia ya uasi wa Luteri hata kwa Shirika lake, na mafundisho yake ya dini. Sasa endelea…
Februari 3, mwaka 1518, Luteri aliitwa na Mkutano Mkuu wa Shirika lake, lakini kwa kulindwa na Frederick, hakuudhiwa na hata ndugu zake wengine shirikani walimshangilia.
Tarehe 16/05/1518, Luteri akiogopa kutengwa na Kanisa, alihubiri akipinga uwezo wa Papa kumtenga Mkristo.
Hapo Papa alimwita afike Roma kwa hukumu, lakini Frederick wa Saxony, aliweza kumfanya Papa akubali, asikilizwe huko huko Ujerumani na Kardinali Kajetani.
Luteri alikataa kuacha uzushi, na baadaye akakimbilia kwa Frederick asikamatwe. Bahati mbaya Papa hakufanya lolote, akihofia kupoteza urafiki wa Frederick.
Mambo yalifikia kilele mwaka 1519, Luteri alipobishana na Mdominikani makini sana John Eck, aliyemzidi akili na utundu.
Kabla ya hapo, Luteri alikuwa akijificha katika maneno magumu ya teolojia, lakini sasa ilibidi aseme wazi, kujibu maswali makali ya John Eck.
Pale alikiri, mawazo yake na kusema kwamba, siyo tu Papa lakini hata Mtaguso Mkuu, unaweza kufanya makosa na mtu binafsi akaupinga.
Sasa ikawa wazi kwamba, ni mzushi na vyuo vikuu vikubwa vikamkana kama mzushi. Ni tokea wakati huo, sasa Luteri akahesabika rasmi kama mzushi katika Kanisa.
Tarehe 15/06/1520, Papa Leo X, alituma hukumu ya kumtenga na Kanisa kwa Luteri, akimpa siku 60 akane uzushi.
Luteri badala ya kukana uzushi, akaichoma ile hukumu hadharani, kama dharau kwa Papa. Mwaka 1521, aliitwa na Mfalme Mkuu Karoli V, kukana uzushi na alipokataa alihukumiwa, lakini akakimbizwa na Frederick na kufichwa.
Wakati huo, ambapo Mfalme Mkuu Karoli angefuatilia kwa matendo, ilimbidi aondoke haraka kurudi Hispania kwa shida maalumu.
Hispania ilikuwa ikigombana na Ufaransa, na wakati huo huo Waturuki walitaka kuiteka Ulaya. Mfalme Mkuu Karoli, hakuweza kurudi Ujerumani mpaka baada ya miaka 9, yaani mwaka 1530.
Katika muda huo, Luteri aliachwa kueneza mafundisho yake, kwa sababu hakuna mwingine ambaye angelimsema au kumshika, kwa sababu alilindwa na Frederick wa Saxony.
Waamini wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Huruma - Mbezi Beach, Jimbo Kuu la Dar es Salam, wakiwa katika maandamano wakati wa sherehe za Sikukuu ya Ekaristi Takatifu baada ya adhimisho la Misa Takatifu ya Sherehe ya hiyo iliyoadhimishwa Dominika iliyopita parokiani hapo.
Kikosi cha Police Band Dar es Salaam kikiwa katika picha ya pamoja na Mapadri ndani ya kanisa baada ya kuongoza maandamano ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu yaliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Peter Clavery-Mbezi Louis Jimbo Kuu la Dar es Salaam.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mhashamu Henry Mchamungu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali wa Walei baada ya Askofu kuwaapisha Viongozi wapya wa Wazee na Wastaafu. Kulia kwa Askofu ni Padri Joseph Mosha na kushoto ni Padri Vitalis Kassembo.
Vijana Waimarishwa wa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara wa Parokia ya Mtakatifu Nicholaus wa Tolentino - Msingwa, Jimbo Kuu la Dar es Salaam wakiwa kanisani wakati wa adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti hiyo.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam Mhashamu Henry Mchamungu (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mapadri wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Huruma - Mbezi Beach, Jimboni humo baada ya adhimisho la Misa Takatifu ya Sherehe ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa Dominika iliyopita parokiani hapo. Wengine ni Viongzi wa Kamati Tendaji ya Parokia hiyo.