Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba-OSA, amesema kuwa vijana wanapopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, wanapokea ili watambue wajibu wao.
Askofu Musomba alisema hayo wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 60 katika Parokia ya Mtakatifu Paulo VI-Mikwambe, jijini Dar es Salaam.
Alitoa wito kwa Waamini wa Mikwembe kuepuka kiburi na majivuno, kwani tabia hizo zimetajwa kuwa ni vyanzo vinavyosababisha watu washindwe kumwelekea Mungu katika maisha yao.
Vile vile, alitoa msisitizo kwa Waamini kuepuka kuusaliti Ukatoliki wao kutokana na kudanganywa na waganga wa kienyeji wanaodai kwamba wanasafisha nyota.
Aliwasihi Wakristu kutenga muda maalum wa kuombea familia zao, kwani familia nyingi hukosa utulivu kutokana na kutokuwa karibu na Mungu katika maisha yao.
Askofu Musomba aliwakumbusha Waamini kutokufanya shughuli binafsi siku ya Jumapili zitakazowafanya washindwe kwenda kanisani, akiwataka kutambua kwamba Mungu ndiye anayewapa nguvu kila wakati.
Vile vile, aliwataka kuondoa vikwazo vinavyowafanya wawe mbali na Mungu, bali wajitahidi kuwa karibu naye ili waweze kuishi maisha yaliyo mema.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Gregory Kijanga alisema kuwa ni furaha kwao kutembelewa na Askofu Musomba, ambaye ni mara yake ya kwanza kufika parokiani hapo.
Padri huyo aliwasihi vijana walioimarishwa katika Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, kuyaishi yale waliyofundishwa, kwani hiyo itawasaidia kuiishi vyema imani yao.
Naye Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Stefano Shirima alimshukuru Askofu Msaidizi Musomba, akiwasisitiza wazazi na walezi kuwa karibu na vijana hao katika ukuaji wao, kwani wasipowasimamia vyema, wataharibika.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Viongozi wa Dini na Wanasiasa nchini, wanatakiwa kuzingatia hekima ili waweze kutenda vyema, kwani wasipokuwa na hekima, watasababisha vurugu na taharuki katika jamii kwa kuongea mambo mabaya dhidi ya watu wengine, hata kama mambo hayo hayapo.
Hayo yalisemwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu, wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Maria Salome, Kimara, jimboni Dar es Salaam, iliyokwenda sanjari na kumsimika Parokoa mpya wa parokia hiyo, Padri Boniphace Omondi.
“Wazingatie hekima, kwani watatenda kama vile Mungu anavyotaka, asiye na hekima anaweza kuingia katika mambo ya ulevi, hana cha maana sana sana ataongelea ya wengine na tena ya ajabu ajabu,”alisema Askofu Mchamungu, baada ya kumsimika Parokia mpya, Padri Omondi.
Viongozi wasiokuwa na hekima fujo:
Akiwazungumzia Viongozi wa Kanisa na Serikali ama Wanasiasa, Askofu Mchamungu alisema,
“Katika Nchi Rais aliyemaliza muda wake anapoondoka anakuja  mwingine yule aliyestaafu hatakiwi kuingilia mambo ya Rais aliyopo madarakani, anapaswa kuendelea na shughuli zake bila kumwingila mwingine, hiyo ndiyo itakuwa hekima,”alisema Askofu Mchamungu.
Askofu Mchamungu alibainisha kuwa hata katika Kanisa, Viongozi wakiwemo Maaskofu na Maparoko wanapomaliza muda wao na kustaafu, wanapaswa kutulia na kuendelea na shughjuli zao bila ya kuwaingilia wengine ambao wapo madarakani, kwani kwao kufanya hivyo, hiyo ndiyo hekima, lakini kinyume chake ni vurugu katika jamii.
“Hata katika Kanisa, Askofu anapomaliza muda wake na kustaafu, kwa mwenye hekima, anapaswa kutulia na kuendelea na shughuli zake huko aliko, bila kumuingilia mwingie ambaye yupo madarakani, endapo atamwingi maana yake atakuwa amekosa hekima, na hiii italeta vurugu, kwani atakuwa anafanya uchochezi kwa kusema wengine vibaya, hata kama mambo husika hayapo,”alisema Askofu Mchamungu na kuongeza,
“Katika Parokia, hata Paroko aliyemaliza muda wake, naye ni hivyo hivyo, anapaswa kukumbatia hekima na kuendelea na kazi zake, bila ya kumuingilia mwingine ambaye anayeendelea na kazi zake katika Parokia,”alisema.
Kwa mujibu wa Askofu Mchamungu, Kiongozi wa namna hiyo asiyeingilia wenzake kwenye majukumu madarakani, ndiye anayoonekana kuwa mwenye hekima...popote pale, lakini endapo atakwenda kinyume, atakuwa mchochezi dhidi ya mwenzake.
“Kiongozi mjinga ni yule mwenye kupita chini chini na kuchochea watu kwa kusema maneno mengi ya uongo dhidi ya viongozi waliopo madarakani... hiyo ni mbaya, kwani hata Mtume Paulo mwenyewe anataka tuache kufanya hivyo, na kutekeleza mapenzi ya Mungu.”
Aidha, Askofu Mchamungu aliwataka Waamini kuhakikisha katika nafasi zao, wanakumbatia hekima ya Mungu, na kuendelea na kazi zao bila ya kuwaingilia wenzao waliopo madarakani na kuwafanyia vurugu za chini kwa chini katika nafasi zao za Uongozi, kwani kufanya hivyo, ni kusababisha vurugu katika uongozi.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba-OSA katika Kigango cha Mtakatifu Antoni wa Padua – Nyeburu, Parokia ya Mtakatifu Yohane Paulo II – Buyuni, Adhimisho la Misa Takatifu ya Somo wa Kigango hicho. (Picha na Michael Ally)

DAR ES SALAAM

Na Israel Mapunda

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekta Binafsi kwa kuweka mazingira wezeshi, ili kuhakikisha Sekta ya anga inakua na kuchangia ukuaji wa Pato la Taifa.
Waziri Kihenzile (pichani), alisema hayo jijini Dar es Salaam baada ya kutembelea anga ya kampuni ya Ndege ya Precision, kukutana na kuzungumza na Wakurugenzi watendaji wa Coastal Aviation na Flightlink.
Katika ziara yake hiyo, Naibu Waziri Kihenzile alisema kwamba uwekezaji unaofanywa na Serikali kwenye eneo la kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege, utakuwa na matokeo makubwa pale ambapo sekta binafsi pia itawekeza katika ununuzi wa ndege.
Kihenzile aliongeza kuwa Serikali ipo katika hatua mbalimbali ya kufanya maboresho kwenye sera ya Uchukuzi na Sheria ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, kwa lengo la kuimarisha sekta ya usafiri wa anga.
Naye Mkurugenzi wa Precision, Patrick Mwanri alisema kwamba katika mpango kazi wake, imepanga kuongeza ndege ambazo zitakwenda sambamba na ongezeko la vituo ambavyo kampuni itakuwa ikitoa Huduma nchini.
Mkurugenzi Mwanri aliiomba Serikali kupitia Naibu Waziri Kihenzile, kuzisaidia kampuni binafsi za ndege kuweza kupata mikopo kupitia benki za ndani, ili kuziimarisha kwenye uendeshaji.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Flightlink, Kapteni Munawer Dhirani aliishukuru Serikali kwa kutekeleza dhamira yake ya kuweka mazingira mazuri ya sekta ya anga, na kuhakikisha makampuni binafsi yanaendelea kuwekeza kwa kununua ndege nchini.
Kapteni Munawer aliongoza kuwa  mazingira yaliyowekwa yameiwezesha Kampuni ya Flightlink kuweka mipango ya  kuongeza mtandao wa safari, ambapo mapema mwisho wa mwaka, Kampuni hiyo itaongeza kituo cha Mwanza.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwai’chi amewataka waimarishwa kuwa Manabii wa kweli na kusikiliza sauti ya kichungaji wanapoitwa na Mungu.
Askofu Mkuu Ruwa’ichi alisema hayo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyoadhimishwa katika Parokia ya Mwenyeheri Antonio Rosmini - Mpigi Magoe, jimboni humo.
“Muimarishwa unaitwa kuhubiri Habari Njema za Kristu, pamoja na kufanya mambo yaliyo mema na yenye kumpendeza Mungu, na si kuwa nabii wa uwongo,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Aliongeza kuwa zama za sasa zimekuwa na manabii wengi wa uongo, ambao lengo lao ni kudanganya, na si kutangaza Neno la Mungu.
Aidha, Askofu Mkuu Ruwai’chi alisema kuwa Mkatoliki aliyebatizwa, hapaswi kuwaamini manabii wa uongo, bali anatakiwa kuishi katika imani yake.
Aliwakumbusha Waamini kwamba manabii wa uwongo wamekuja kwa kazi ya kutafuta fedha tu, na si kwa ajili ya kuhubiri Neno la Mungu, akiwasisitiza kusimama imara katika imani yao.
“Nabii wa kweli hutokana na kusema ukweli, na siku zote maisha yao si rahisi, kwa sababu ndani yao mara zote kumejaa manyanyaso ya kusakamwa, ya kusutwa, pamoja na kudhulumiwa,” alisema Askofu Mkuu, na kuongeza,
“Hata katika Somo la Kwanza anazungumziwa Nabii Yeremia ambaye ni kati ya manabii mahiri zaidi katika Agano la Kale, ambaye mara zote alikuwa anawaambia watu wamrudie Mungu kutokana na mambo yao waliyokuwa wakitenda.
“Lakini, kwa sababu alikuwa ni nabii aliyesimama katika ukweli zaidi, watu hao walimkamata na kumuhukumu kifo, lakini ni kwa sababu Yeremia aliwataka watu wabadilike kwa kutubu ili yasije kujitokeza tena yale ya Sodoma na Gomora. Hiyo inaonesha fika ni kwa jinsi gani Manabii wa ukweli wanavyoteseka.”
Aidha, Askofu Ruwa’ichi aliwakumbusha Waamini kutubu na kuamini Injili, ikiwa kama ujumbe wa Yesu aliowaachia wanafunzi wake, akiwataka kutokufanya maamuzi ya haraka, bali wafikiri zaidi na kutenda ili baadaye wasije kujuta.
Aliwakumbusha Waimarishwa kuwa siku ya Ubatizo walizaliwa mara ya pili kama hekalu la Roho Mtakatifu, akiwataka watambue na wajiheshimu kwa kuuishi vyema wito wao.
Aliwasisitiza kushuhudia matendo makuu ya Mungu, akiwaasa kuwa kipaumbele ni kuzungumza habari njema kwa watu, na kuwakumbusha kutokuwa manabii waliokufa, wala manabii wasiokuwa na uthubutu.
Hata hivyo, Askofu Mkuu aliwataka wazazi na wasimamizi kuwa mfano bora wa kuigwa na watoto, kwa kuwasaidia kuishi vyema wito wao siku zote za maisha yao.

DODOMA

Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amewaasa wataalamu wa sekta za mifugo na uvuvi kupeleka na kufundisha teknolojia za sekta hizo vijijini, ili kuwapa elimu wafugaji kuhusu ufugaji wa kisasa, na hivyo kuleta tija.
Alisema hayo alipotembelea kwenye Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa (Nane Nane) yaliyofanyika Kitaifa mkoani humo.

MOROGORO

Na Winfrida Kobelo-SJMC

Wakazi wanaoishi karibu na Hifadhi ya Hululu iliyopo Kata ya Bunduki, mkoani Morogoro wametakiwa  kuitunza hifadhi hiyo.
Kauli hiyo imekuja wakati huu Taifa linapoendelea na harakati za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, ambayo yamezidi kuwa tishio duniani kote.
Wakizungumza na gazeti  Tumaini Letu hivi karibuni, baadhi ya viongozi wa mazingira wa kata hiyo walisema kuwa kwa sasa wanatumia njia mbalimbali kudhibiti uharibifu wa hifadhi hiyo, ikiwemo kufanya doria za mara kwa mara.
Afisa Misitu wa Kata hiyo, Protches Elias alisema kwamba wamekuwa wakitoa elimu kwa wanakijiji, ili wahakikishe mazingira yanatunzwa, ikiwemo kutokuchoma moto katika misitu iliyomo ndani ya vijiji hivyo.
“Tumekuwa tukitoa elimu kwa vijiji na vitongoji kuhusiana na majanga ya moto pamoja na uanzishwaji wa vitalu vya miti, na upandaji miti. Pia tunafanya doria za mara kwa mara ili kukabiliana na vitendo vya uharibifu kama vile ukataji miti, kilimo na upitishwaji wa mifugo ndani ya hifadhi,” alisema Afisa Misitu huyo, na kuongeza,
“Suala lingine ni ulinzi na uimarishaji wa mipaka ya hifadhi kwa kufyeka na kusafisha mipaka ili miti iliyopo mpakani ikue vizuri na hivyo kuzuia majanga ya moto ambayo yanaweza kusababishwa na mashamba ya wenyeji yaliyo jirani.”
Akizungumzia changamoto wanazokumbana nazo katika kuitunza hifadhi hiyo, Afisa Misitu huyo alisema kuwa changamoto hizo ni pamoja na uhaba wa watumishi, na baadhi ya wananchi kufanya shughuli za kilimo katika maeneo ya pembezoni mwa hifadhi hiyo.
Naye Mwenyekiti wa Mazingira katika Kijiji cha Vinile kilichopo karibu na hifadhi hiyo ya Hululu, Paulo Joseph alisema kuwa wananchi ndio watunzaji namba moja wa hifadhi kutokana na kamati mbalimbali za mazingira ambazo zimeundwa kwa ajili ya kusimamia misitu na kupanda miti, kwani misitu ndiyo chanzo cha upatikanaji wa maji.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo aliwaasa wananchi kuendelea kutunza na kuyathamini mazingira kwa kuachana na tabia za kukata miti, kuchoma moto misitu, pamoja na kuharibu vyanzo vya maji, ili kuepuka madhara yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi.
Kwa upande wake Veronica Mwenda, mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Mazingira katika Kata ya Bunduki, alieleza kuwa bado wanakumbana na changamoto za matukio ya uharibifu wa misitu, kama vile ukataji hovyo miti.
Naye mkazi wa Kijiji cha Maguruwe kilichopo Kata ya Bunduki, Josephina Christopher, alisema kuwa wameunda baadhi ya vikundi vya upandaji miti katika vitalu kwa ajili ya kutokomeza uhaba wa miti katika misitu hiyo.
“Kwa mfano, pale kijijini kwetu tumekuwa na baadhi ya vikundi mbalimbali mahsusi kwa kupanda miti, na hii ni kwa sababu tunaipenda hifadhi ya Hululu, maana ile ni hazina ya asili tunayojivunia,” alisema Josephina.
Aidha, hifadhi ya Hululu kwa jina lingine hujulikana kama Maporomoko ya Maji ya Hululu, na yana urefu wa sentimita 80 kutoka yanapotoka hadi yanapotiririka, yaliyopo ndani ya msitu wa hifadhi ya mazingira asilia ya Uluguru.

RUKWA

Na Lusungu Helela

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deus Sangu, amesema kuwa Serikali imepanga kutangaza jumla ya  ajira mpya  37, 616, huku ajira za kada ya Ualimu, Afya   na kada nyinginezo, ikiwemo kada ya Uhasibu  na Ugavi, zikiwa tayari zinaendelea kutangazwa, lengo likiwa ni kupunguza tatizo la upungufu wa watumishi nchini.
Sangu alisema hayo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza  katika mikutano ya hadhara iliyofanyika katika vijiji vya Kitete, Laela, Kamsamba na Kavifuti vilivyopo katika  Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, mkoani Rukwa, ikiwa ni ziara yake ya  kwanza tangu alipouteliwa kushika  wadhifa huo.
Akizungumzia nafasi za ajira ya Ualimu ambazo tayari zimeshatangazwa na Sekretarieti ya Ajira kwenye ngazi ya mikoa kulingana na mahitaji ya mkoa husika,. Sangu alisema kuwa utaratibu wa kuwapata waalimu kwa mwaka huu umeanza kuwa wa tofauti ukilinganisha na ilivyokuwa katika miaka ya nyuma.
Alifafanua kuwa usaili huo umeanza kufanyika kwa kada ya Ualimu kwa sababu nafasi  za ajira za Ualimu  ni chache, ukilinganisha na idadi ya walimu wa shule ya msingi na sekondari waliohitimu vyuo mbalimbali hapa nchini, ambapo zaidi ya waalimu 100,000 wapo mitaani wakiwa hawana ajira.
Alisema kuwa Serikali imekuja na uamuzi huo ili kuchagiza dhana ya ushindani kwa lengo la kuhakikisha kila mwenye sifa stahiki, anapata ajira katika mazingira aliyopo pasipo kulazimika kusafiri kwenda Dodoma au Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya usaili.
Kufuatia hatua hiyo. Sangu alitoa wito kwa vijana waliohitimu vyuo mbalimbali hapa nchini kuchangamkia nafasi hizo za ajira, huku akiwataka wajiandae ipasavyo kwa ajili ya usaili huo, ikiwa ni mara ya kwanza kwa kada hiyo ya Ualimu kufanya usaili
Alitumia fursa hiyo kuwatoa wasiwasi wote walioomba nafasi hizo za Ualimu, huku akiwahakikishia kuwa Ofisi yake yenye dhamana ya kusimamia masuala ya ajira nchini, imejizatiti kuhakikisha mchakato huo wa kuwapata waalimu wenye sifa stahiki utakuwa huru na wa haki.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo kijazi

Imeelezwa kuwa kila mmoja anatakiwa kujiwekea utaratibu wa kuwasaidia wahitaji, badala ya kujilimbikizia mali, ikiwemo fedha, kwani hakuna aliyefilisika kwa kutoa msaada kwa wenye shida.
Wito huo ulitolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 53 katika Parokia ya Mtakatifu Rita wa Kashia – Temboni, jimboni Dar es Salaam.
“Elisha alivyopewa ile mikate, angeamua kubaki nayo peke yake, lakini aliona kubaki nayo siyo sawa, akaamua kuwagawia wengine. Kwa hiyo ndugu zangu Waamini, nawaomba sana tujiwekee utaratibu huo wa kuwashirikisha wengine, kwa sababu hiyo itasaidia kutuwekea hazina mbinguni,” alisema Askofu Mchamungu.
Aliongeza kuwa fedha haziwezi kumkumbuka mtu aliyezimiliki kwa muda mrefu, bali atakapoamua kuwasaidia wengine, watamkumbuka na kumwombea hata akiwa hayupo duniani.
Alisema pia kuwa hata kama watu wanajitahidi kufanya kazi kwa bidii ili kujipatia kipato, watambue kwamba hawatakiwi kuwa wabinafsi na mali wanazozipata, kwani uhai walio nao na nguvu za kufanya hivyo, wamepewa na Mungu.
Aliongeza kuwa wapo watu ambao Mungu amewajalia kuwa na fedha ili zitumike kwa ajili ya kuwasaidia wengine, hivyo ni vyema kutekeleza wajibu huo wa kusaidiana.
Aliwasisitiza vijana kutowaacha wazee wahangaike kwa kutokuwasaidia, akiongeza kuwa kupitia Adhimisho hilo la Misa Takatifu ambayo pia ni Siku ya Kuwakumbuka Wazee, wajitahidi kuwasaidia.
Wakati huo huo alitoa wito kwa Waamini kwa pamoja kutokuwasahau wazazi wao waliopo vijijini, kwani wakiwakumbuka, kuwajulia hali, na kuwasaidia, wazee wao watafarijika.
Vile vile, alisema kuwa yeyote anayewasaidia wazazi wake, hubarikiwa, bali anayewaacha wakihangaika na kuteseka, hawezi kufanikiwa katika kila analolifanya.
Alitoa wito kwa Waimarishwa wa Sakramenti Takatifu ya Kipamiara, kuishi maisha ya kumpendeza Mungu na wanadamu, akiwataka kufahamu kwamba, ‘Kipaimara, siyo kwa heri Kanisa’.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Festo Ngonyani alimshukuru Askofu Msaidizi Mchamungu kwa Adhimisho hilo la Misa Takatifu ya kuwaimarisha vijana 53 wa parokia hiyo.
Padri Ngonyani aliongeza kwamba siyo tu kwa ajili ya Kipaimara, bali hata kwenda kuwasalimia kwa mara nyingine, watafarijika kumuona.
Naye Katibu wa Halmashauri ya Walei wa Parokia hiyo, George Kashushura aliwakumbusha wasimamizi kuwafanya vijana hao kuwa ni sehemu ya familia zao.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Imeelezwa kuwa moja kati ya dhambi kubwa zinazowasakama wanadamu, ni kigeugeu, wakiaswa kuishi maisha yaliyo mema, huku wakijihami dhidi ya ugeugeu.
Hayo yalisemwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 78 katika Parokia ya Bikira Maria wa Rozari Takatifu – Makongo Juu, jimboni humo.
“Moja kati ya dhambi kubwa zinazowasakama wanadamu, ni kigeugeu. Kwa hiyo ndugu zangu, nawaomba sana mjiepushe dhidi ya ugeugeu,” alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Aliwataka waamini hao kuacha tabia ya kwenda kwa waganga wa kienyeji kuaguliwa ili wafanikiwe, akiwasihi kuendelea kumtegemea Yesu Kristo kila wakati, kwani Kristo hapendi njia za mkato katika kufanikiwa.
Aidha, aliwasihi kujifunza kuundwa kwa njia za kuwajibika, akisema kuwa hiyo ndiyo njia pekee itakayowaepusha na njia za mkato.
Katika homilia yake Askofu Mkuu Ruwa’ichi, aliwataka Waamini kuacha uzembe, akiwasisitiza kuwa watu wa kupokea Neno la Mungu na mwili wa Kristu katika maisha yao.
“Tuache uzembe, tuwe watu wa kulishwa Neno la Mungu, na tuwe watu wa kupokea mwili wa Kristu, yaani Ekaristi Takatifu. Hayo mawili, tuyapokee katika hali ya kuwa na Roho safi. Tusipokee Neno la Mungu na mwili wa Kristu katika hali ya Roho zenye masizi, Roho zilizosakamwa na dhambi;
Alisema pia kuwa Mkristo hatakiwi kuona aibu kutokana na kujaa neema, bali aone aibu kutokana na kusakamwa na dhambi katika maisha yake.
Aidha, Askofu Mkuu Ruwa’ichi aliwasihi Waamini kutohangaikia chakula chenye kupita, bali wajitahidi kuhangaikia chakula chenye kudumu, ambacho ni Mapenzi ya Mungu, kwani yeyote anayekula chakula hicho, amekula chakula cha uzima.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Joseph Massenge, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Tumaini Media alimshukuru Askofu Mkuu kwa kuadhimisha Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara.
Padri Massenge aliwakumbusha wasimamizi kuwasaidia watoto hao kupokea Sakramenti ya Kitubio, kwani asiyepokea Sakramenti hiyo, ni sawa na mtu asiyeoga.
“Wasimamizi nawaomba sana, wasaidieni watoto hawa kupokea Sakramenti ya Kitubio, kwa sababu asiyepokea Sakramenti ya Kitubio, ni sawa na mtu asiyeoga. Na kama mnavyojua, mtu asiyeoga ananuka, si ndiyo jamani,” alisema Padri Massenge.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei wa Parokia hiyo, Deogratius Mwarabu alimshukuru Askofu Mkuu, huku akimkabidhi kiasi cha fedha Shilingi milioni moja iliyoandaliwa na Parokia hiyo, ikiwa ni kumpongeza kwa Jubilei ya Miaka 25 ya Uaskofu wa Askofu huyo.