Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Vijana wanapopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, wametakiwa kusimama imara, kujitambua na kuelewa wajibu wao wa kuishi maisha bora ya Imani Katoliki kama walivyofundishwa.
Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba OSA, wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 166 katika Parokia ya Mtakatifu Agustino – Ukonga, jimboni humo.
Askofu huyo alisema kuwa dhambi ni kikwazo katika ubinadamu, ambacho kinawafanya watu wawe vipofu na kushindwa kumwona Mungu katika maisha yao.
“Kwa hiyo ndugu zangu tutambue kwamba dhambi ni kikwazo katika ubinadamu, ambacho kinawafanya watu wawe vipofu na washindwe kumwona Mungu. Tuishi maisha ya kumpendeza Mungu,” alisema Askofu Musomba.
Vile vile, aliwasihi vijana waliopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kuepuka kuyumbishwa, huku akiwasisitiza kubaki katika imani yao Katoliki kwani wao wamekuwa ni Askari hodari wa Kristu.
Aliwaagiza Wazazi, Walezi na Waamini wote kwa pamoja, kushirikiana katika kusimamia malezi ya vijana hao, kwani kwa kufanya hivyo, Kanisa litapata watendaji walio bora.
Katika homilia hiyo Askofu Musomba pia aliwasihi Waamini kutokuisaliti imani yao na kutokuionea haya, akisema kwamba kufanya hivyo, ni kupotea katika imani.
Pia, alisisitiza kuepuka kiburi na majivuno katika mazingira wanayoishi, akiwasisitiza kuguswa na Roho Mtakatifu pamoja na kusikiliza kila wanachoelezwa.
“Epukeni kiburi na majivuno, kwamba bila mimi, hiki hakiwezi kufanyika. Jitahidini kuishi maisha ya kuguswa na Roho Mtakatifu huku mkisikiliza kila mnachoelezwa,” alisema Askofu Musomba.
Aliwataka Waamini kutambua kwamba ni wajibu wao kuiishi pamoja na kuishuhudia imani siku zote za maisha yao, kwani wao ni sura na mfano wa Mungu.
Katika hatua nyingine Askofu Musomba aliwashukuru Waamini wa Parokia ya Ukonga kwa ukarimu waliouonyesha kwake, kwani hiyo imemfanya ajihisi kuwa yuko nyumbani.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri James Mweyunge alisema kuwa alipo Askofu, ndipo Kanisa lilipo, hivyo ni furaha kwao kusali pamoja na Askofu katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu.
Padri Mweyunge aliwashukuru walimu (Makatekista) waliowafundisha vyema vijana hao hadi wameweza kufahamu mambo mengi yanayohusu Imani Katoliki.

IFAKARA

Na Celina Matuja

Wakati Serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa, Mbunge wa Jimbo la Rufiji, kutangaza rasmi kuanza kwa mbio za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27 mwaka huu, Askofu wa Jimbo Katoliki la Ifakara, Mhashamu Salutaris Libena, ametoa ya moyoni.
Uchaguzi huo ni muhimu kwani utatoa fursa kwa wananchi kuwachagua Viongozi wa mitaa na vijiji, na ni maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani wa mwakani.
Askofu Libena alisema hayo hivi karibuni katika Mahojiano Maalumu na gazeti Tumaini Letu ofisini kwake Jimboni Ifakara, kuhusu uchaguzi huo.
Alisema kwamba ni muhimu kwa Waamini wote kujitokeza kushiriki katika masuala ya kitaifa kwa kuwa ni haki ya kila raia Mtanzania, bila kujali dini, ili kupata viongozi wazuri na wanaowataka kwa maendeleo yao.
Askofu Libena aliwataka Waamini wa Jimbo hilo kujitokeza kwa wingi kujiandikisha, kugombea kupiga kura, kugombea na kushiriki katika Uchaguzi huo ili kupata viongozi bora wa Serikali za Mitaa kwa maendeleo ya Nchi, na Kanisa kwa ujumla.
Aliongeza kuwa ni  vizuri pia kuwapatia elimu vijana kuhusu uchaguzi wa serikali za mitaa kwa kuzingatia uzalendo, na wasitumiwe na mamluki kuuza haki yao ya kuchagua au kuchaguliwa katika ngazi zote za uongozi serikalini.
Alisema pia kuwa vijana ni hazina ya Taifa, hivyo wasipoelimishwa vizuri, watapotea  na kupoteza haki yao ya kuchagua au kuchaguliwa.
Askofu Libena alisisitiza waamini kujiandikisha sasa wakati tangazo la serikali limeshatolewa, ili wasipate shida wakati wa kupiga kura, lakini pia kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura ili kuonyesha ukomavu wa kisiasa badala ya kujiandikisha na kuwaachia wengine kupiga kura.
Kwa mujibu wa Askofu Libena, ni muhimu kwa Mkristo kujitokeza na kushiriki uchaguzi huo na ujao, kwani utampatia nafasi ya uwakilishi katika kuiongoza Jamii na Kanisa kwa ujumla.
Inavyoeleza Katiba kuhusu Uchaguzi:
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, Ibara 145 na 146 inaelezea uwepo wa Serikali za Mitaa pamoja na madhumuni yake. Mojawapo ya madhumuni ya kuwepo kwa Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi.
Aidha, Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288, zinaelekeza kufanyika kwa uchaguzi wa Serikali za Mitaa.
Lengo ni kuzifanya Serikali za Mitaa ziongozwe kidemokrasia.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 201A cha Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura 287 na Kifungu cha 87A cha Sheria za Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa ana mamlaka ya kutunga Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, ambazo hutumika kuongoza uchaguzi huo.
Viongozi wanaochaguliwa katika ngazi hizi ni Wenyeviti wa Vijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji, Wenyeviti wa Mitaa, Wajumbe wa Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa vitongoji.
Uchaguzi wa mwisho wa Serikali za Mitaa ulifanyika mwezi Novemba mwaka 2019, hivyo, uchaguzi mwingine unatakiwa kufanyika Novemba, 2024.
Uchaguzi huu unaongozwa na Kanuni za Uchaguzi wa Viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ngazi ya Vijiji, Vitongoji na Mitaa katika Mamlaka za Wilaya na Mamlaka za Miji, kwa mujibu wa Matangazo ya Serikali Na. 571, 572 573 na 574 ya Mwaka 2024.
Kwa mujibu wa Kanuni hizi, Waziri wa TAMISEMI anapaswa kutoa Tangazo la Uchaguzi likiainisha ratiba, shughuli za uchaguzi zinazohusika na masharti muhimu ya uchaguzi.
Masharti muhimu ya kuzingatia katika Uchaguzi huo ni kama ifuatavyo:- (a) Nafasi zitakazogombewa katika uchaguzi huu ni Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi mchanganyiko la wanaume na wanawake), Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi la wanawake) na Wenyeviti wa Vitongoji katika Mamlaka za Wilaya.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Wilaya za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 571 la Mwaka 2024), (ii) Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo.
Kwa nafasi hiyo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji Midogo za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 572 la Mwaka 2024) (iii) Mwenyekiti wa kijiji, wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi mchanganyiko la wanaume na wanawake), wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji (kundi la wanawake) na wenyeviti wa vitongoji katika Mamlaka za Miji.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Kijiji, Wajumbe wa Halmashauri ya Kijiji na Mwenyekiti wa Kitongoji katika Mamlaka za Miji za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na.573 la Mwaka 2024) (iv) Mwenyekiti wa mtaa na wajumbe wa kamati ya mtaa (Kundi Mchanganyiko la Wanaume na Wanawake) na wajumbe wa kamati ya mtaa (Kundi la Wanawake) katika Mamlaka za Miji.
Kwa nafasi hizo, uchaguzi utaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mtaa na Wajumbe wa Kamati ya Mtaa katika Mamlaka za Miji za Mwaka 2024 (Tangazo la Serikali Na. 574 la Mwaka 2024).

RUVUMA

Na Mwandishi wetu

Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga amesema kwa Serikali imetenga takribani Shilingi bilioni 4.6/- kupeleka umeme kwenye maeneo ya migodi mkoani Ruvuma.
Kapinga (pichani) aliyasema hayo wakati akizindua Kituo cha Mauzo ya Makaa ya Mawe ya kampuni ya Market Insight Limited (MILCOAL), inayojihusisha na uchimbaji, uuzaji na usambazaji wa makaa ya mawe, Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.

SIMANJIRO

Na Mwandishi wetu

Wachimbaji wa madini ya Green Garnet eneo la Lemshuku, Kata ya Komolo Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamelalamikia kwa Waziri wa Madini, Anthony Mavunde juu ya changamoto ya ukosefu wa maji, nishati ya umeme na kuwa na ubovu wa barabara.
Mmoja wa wachimbaji madini ya Green Garnet, Mkurugenzi wa Kampuni ya Chusa Mining Ltd, Joseph Mwakipesile alisema hayo wakati akizungumza na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde baada ya kutembelea machimbo ya Lemshuku.
Mwakipesile alisema kuwa huduma ya maji ni changamoto kubwa kwenye machimbo ya Lemshuku, na hakuna nishati ya umeme, hivyo kushindwa kufanya uchimbaji kwa uhakika.
“Maji yanafuatwa umbali wa kilomita 17 kutoka kijiji cha Komolo hadi hapa machimboni, na tulikuwa na kisima cha maji, ila hivi sasa tuna maji tunafuata mbali, na pia barabara ni mbovu,” alisema Mwakipesile.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini (MAREMA), Tawi la Lemshuku, Swalehe Abdalah aliiomba Serikali kufanikisha utatuzi wa changamoto hizo ili waweze kufanya shughuli za uchimbaji kwa uhakika.
“Tunakushukuru Waziri Mavunde kwa kufika Lemshuku na kuona mazingira ya hapa Lemshuku, tunaomba serikali imalize vikwazo tulivyonavyo ili tufanye kazi vyema,” alisema Swalehe.
Akijibu malalamiko hayo, Waziri Mavunde alisema atakutana na Mawaziri husika ili kuhakikisha changamoto hizo zinafanyiwa kazi kuwawezesha wachimbaji hao waweze kufanya kazi zao ipasavyo, na Serikali iongeze mapato.
Waziri Mavunde alisema miundombinu ikiboreshwa na changamoto zikipatiwa ufumbuzi, Watanzania hao watatajirika kwa kupata fedha nyingi, na serikali itaongeza mapato kupitia kodi.
Hata hivyo, ili kumaliza changamoto ya ukosefu wa huduma ya afya, ameendesha harambee ya ghafla ya ujenzi wa zahanati na kupatikana Sh23 milioni matofali 3,000 na mifuko 185 ya saruji
Aliuagiza uongozi wa mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) Wilaya ya Simanjiro, kuhakikisha pampu iliyozama kisima cha maji Lembole inatolewa ili wachimbaji wapate huduma wakati wakisubiri mradi mkubwa wa maji.
Akizungumza kuhusu mawasiliano alisema kwamba atazungumza na waziri husika ili mnara wa simu ufungwe kwenye machimbo hayo na hivyo mawasiliano yapatikane.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Fakii Lulandala alisema kuwa hii ni mara ya kwanza Waziri wa madini kufika kwenye machimbo ya Lemshuku, hivyo Waziri Mavunde anapaswa kupongezwa.
Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Madini nchini, Femata John Bina alisema Waziri Mavunde ni kiongozi wa pori kwa pori asiyekaa ofisini ndiyo sababu amefika Lemshuku huku Mwenyekiti wa chama cha mabroka Tanzania (Chamata) Jeremiah Kituyo amewaasa wanunuzi wa madini kukata leseni ili waweze kuwa huru na biashara yao.
Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole Sendeka naye alisema wachimbaji hao wa Lemshuku wakitatuliwa changamoto zao watanufaika ikiwemo wachekechaji.

LINDI

Na Mwandishi wetu

Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, (NEEC) limewataka viongozi wa Mkoa wa Lindi, kutengeneza mkakati kabambe utakaozuia mimba za utotoni kwa wasichana kuwakatiza masomo na kuzima ndoto zao.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Beng’i Issa wakati baraza hilo lilipozindua programu ya Imarisha Uchumi na Mama Samia (IMASA)mkoani humo.
“Mkoa huu una matatizo ya wasichana kuacha masomo, hata wakiwa wamefaulu kujiunga na shule za sekondari hawaendi na inakadiriwa asilimia 30 yao hukatisha masomo kutokana na mimba za utotoni…mimba za utotoni zinakatisha ndoto za kiuchumi za wasichana,”alisema Beng’i.
Alisema programu ya IMASA imekuja kuwezesha Makundi ya kinamama, vijana, na makundi maalum. Hivyo makundi ya vijana yakipata elimu, ni nyenzo kubwa ya kufikia malengo yao ya kiuchumi na ukizingatia mkoa huo una fursa nyingi za kiuchumi.
Beng’i alisema kwamba mkoa huo wananchi wanajishughulisha na kilimo cha korosho,alizeti,uvuvi, mazao ya mwani, hivyo programa hiyo itashirikiana na mkoa huo kuweka vipaumbele ili kuandaa programu kwa ajili ya uwezeshaji wake.
Alisema pia kuwa program ilipokelewa vizuri mkoani humo na wananchi walitamani sana programu ianze haraka, na washiriki wengi walikuwa ni wafanya biashara, wakulima, wakulima wa kuongeza thamani mazao, na madalali wa kilimo.
Aidha, aliutaka uongozi wa Mkoa huo kuendelea na programu zao za kawaida katika kilimo cha korosho, ubanguaji korosho kuongeza thamani mazao na uvuvi, na zile za uwezeshaji za asilimia kumi na kuendelea, kufuata maelekezo ya serikali.
Naye Katibu wa Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu Manispaa ya Lindi, Zuhura Meza alisema anamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha programu hiyo ambayo imekuja kuwainua kiuchumi wanawake kupitia mafunzo ya ujasiriamali na uwezeshaji watakaopewa.
“Nikirirudi nyummbani naenda kuwaelimisha watu wenye ulemavu, wale ambao hawajajisajili na programu ili nao waende kujisajili ili kupata fursa ya mafunzo na uwezeshaji,” alisema.
Naye Mkulima wa Mwani kutoka Kata ya Lindi Mjini ya Kitumbi, Kwela, Manispaa ya Lindi, Rukia Selemen alisema yeye ni mkulima na mchakataji wa bidhaa za mwani. Anashukuru ujio wa program hiyo kufika katika manispa yao kutoa elimu ya ujasiriamali na itamwezesha kufanya vizuri zaidi.
Mjasiriamali toka Kilwa Masoko Fatuma Juma alisema anajishughulisha na usindikaji wa mazao mbalimbali, yakiwemo ya maziwa (yogati), juice ya mwani na anatengeneza bidhaa za urembo kama nguo, na alidai kwa kusema kuwa programu hiyo imewaingiza katika mfumo na hivyo kufanya kazi kwa ubora.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewaasa Waamini kutambua kwamba ufukara na umaskini isiwe ni sababu ya wao kuikana imani.
Kardinali Pengo (pichani), alitoa wito huo hivi karibuni wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, iliyoadhimishwa Parokia ya Bikira Maria wa Fatima-Msimbazi, jimboni Dar es Salaam.
“Kuna baadhi ya watu kutokana na umaskini na ufukara wao, wamediriki kuikana imani yao ili mradi wapate baadhi ya vitu walivyokuwa wakihitaji,”alisema Kardinali Pengo.
Aliendelea kusema, “Nanyi Waamini na watoto mnaopokea Sakramenti ya Kipaimara, inawapasa kufahamu, hata Yesu alikuwa ni mtu fukara zaidi, lakini bado aliishi katika imani…hivyo basi nanyi inawapasa  kuishi katika imani hiyo hiyo aliyokuwa nayo Yesu Kristo mwenyewe, ikiwa kama kielelezo na mfano bora wa maisha ya Mkatoliki.”
Kardinali Pengo alisema wanatakiwa kutambua kuwa Mwenyezi Mungu hana shida na fedha za mtu yeyote, bali anahitaji watu waongoke na kuiamini Injili.
Inawapasa kufahamu “maskini anayeongelewa na Muinjili Mathayo, si maskini wa mavazi, malazi au makazi, bali ni maskini yule asiyelifahamu Neno la Mungu”
Kardinali Pengo alisema kwamba Yesu Kristo alikuja duniani kwa kazi moja ya kuwahubiria Injili watu maskini na kuwakomboa wanadamu.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba-OSA, amesema kuwa vijana wanapopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, wanapokea ili watambue wajibu wao.
Askofu Musomba alisema hayo wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 60 katika Parokia ya Mtakatifu Paulo VI-Mikwambe, jijini Dar es Salaam.
Alitoa wito kwa Waamini wa Mikwembe kuepuka kiburi na majivuno, kwani tabia hizo zimetajwa kuwa ni vyanzo vinavyosababisha watu washindwe kumwelekea Mungu katika maisha yao.
Vile vile, alitoa msisitizo kwa Waamini kuepuka kuusaliti Ukatoliki wao kutokana na kudanganywa na waganga wa kienyeji wanaodai kwamba wanasafisha nyota.
Aliwasihi Wakristu kutenga muda maalum wa kuombea familia zao, kwani familia nyingi hukosa utulivu kutokana na kutokuwa karibu na Mungu katika maisha yao.
Askofu Musomba aliwakumbusha Waamini kutokufanya shughuli binafsi siku ya Jumapili zitakazowafanya washindwe kwenda kanisani, akiwataka kutambua kwamba Mungu ndiye anayewapa nguvu kila wakati.
Vile vile, aliwataka kuondoa vikwazo vinavyowafanya wawe mbali na Mungu, bali wajitahidi kuwa karibu naye ili waweze kuishi maisha yaliyo mema.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Gregory Kijanga alisema kuwa ni furaha kwao kutembelewa na Askofu Musomba, ambaye ni mara yake ya kwanza kufika parokiani hapo.
Padri huyo aliwasihi vijana walioimarishwa katika Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, kuyaishi yale waliyofundishwa, kwani hiyo itawasaidia kuiishi vyema imani yao.
Naye Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Stefano Shirima alimshukuru Askofu Msaidizi Musomba, akiwasisitiza wazazi na walezi kuwa karibu na vijana hao katika ukuaji wao, kwani wasipowasimamia vyema, wataharibika.

DAR ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Viongozi wa Dini na Wanasiasa nchini, wanatakiwa kuzingatia hekima ili waweze kutenda vyema, kwani wasipokuwa na hekima, watasababisha vurugu na taharuki katika jamii kwa kuongea mambo mabaya dhidi ya watu wengine, hata kama mambo hayo hayapo.
Hayo yalisemwa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu, wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Maria Salome, Kimara, jimboni Dar es Salaam, iliyokwenda sanjari na kumsimika Parokoa mpya wa parokia hiyo, Padri Boniphace Omondi.
“Wazingatie hekima, kwani watatenda kama vile Mungu anavyotaka, asiye na hekima anaweza kuingia katika mambo ya ulevi, hana cha maana sana sana ataongelea ya wengine na tena ya ajabu ajabu,”alisema Askofu Mchamungu, baada ya kumsimika Parokia mpya, Padri Omondi.
Viongozi wasiokuwa na hekima fujo:
Akiwazungumzia Viongozi wa Kanisa na Serikali ama Wanasiasa, Askofu Mchamungu alisema,
“Katika Nchi Rais aliyemaliza muda wake anapoondoka anakuja  mwingine yule aliyestaafu hatakiwi kuingilia mambo ya Rais aliyopo madarakani, anapaswa kuendelea na shughuli zake bila kumwingila mwingine, hiyo ndiyo itakuwa hekima,”alisema Askofu Mchamungu.
Askofu Mchamungu alibainisha kuwa hata katika Kanisa, Viongozi wakiwemo Maaskofu na Maparoko wanapomaliza muda wao na kustaafu, wanapaswa kutulia na kuendelea na shughjuli zao bila ya kuwaingilia wengine ambao wapo madarakani, kwani kwao kufanya hivyo, hiyo ndiyo hekima, lakini kinyume chake ni vurugu katika jamii.
“Hata katika Kanisa, Askofu anapomaliza muda wake na kustaafu, kwa mwenye hekima, anapaswa kutulia na kuendelea na shughuli zake huko aliko, bila kumuingilia mwingie ambaye yupo madarakani, endapo atamwingi maana yake atakuwa amekosa hekima, na hiii italeta vurugu, kwani atakuwa anafanya uchochezi kwa kusema wengine vibaya, hata kama mambo husika hayapo,”alisema Askofu Mchamungu na kuongeza,
“Katika Parokia, hata Paroko aliyemaliza muda wake, naye ni hivyo hivyo, anapaswa kukumbatia hekima na kuendelea na kazi zake, bila ya kumuingilia mwingine ambaye anayeendelea na kazi zake katika Parokia,”alisema.
Kwa mujibu wa Askofu Mchamungu, Kiongozi wa namna hiyo asiyeingilia wenzake kwenye majukumu madarakani, ndiye anayoonekana kuwa mwenye hekima...popote pale, lakini endapo atakwenda kinyume, atakuwa mchochezi dhidi ya mwenzake.
“Kiongozi mjinga ni yule mwenye kupita chini chini na kuchochea watu kwa kusema maneno mengi ya uongo dhidi ya viongozi waliopo madarakani... hiyo ni mbaya, kwani hata Mtume Paulo mwenyewe anataka tuache kufanya hivyo, na kutekeleza mapenzi ya Mungu.”
Aidha, Askofu Mchamungu aliwataka Waamini kuhakikisha katika nafasi zao, wanakumbatia hekima ya Mungu, na kuendelea na kazi zao bila ya kuwaingilia wenzao waliopo madarakani na kuwafanyia vurugu za chini kwa chini katika nafasi zao za Uongozi, kwani kufanya hivyo, ni kusababisha vurugu katika uongozi.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba-OSA katika Kigango cha Mtakatifu Antoni wa Padua – Nyeburu, Parokia ya Mtakatifu Yohane Paulo II – Buyuni, Adhimisho la Misa Takatifu ya Somo wa Kigango hicho. (Picha na Michael Ally)

DAR ES SALAAM

Na Israel Mapunda

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekta Binafsi kwa kuweka mazingira wezeshi, ili kuhakikisha Sekta ya anga inakua na kuchangia ukuaji wa Pato la Taifa.
Waziri Kihenzile (pichani), alisema hayo jijini Dar es Salaam baada ya kutembelea anga ya kampuni ya Ndege ya Precision, kukutana na kuzungumza na Wakurugenzi watendaji wa Coastal Aviation na Flightlink.
Katika ziara yake hiyo, Naibu Waziri Kihenzile alisema kwamba uwekezaji unaofanywa na Serikali kwenye eneo la kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege, utakuwa na matokeo makubwa pale ambapo sekta binafsi pia itawekeza katika ununuzi wa ndege.
Kihenzile aliongeza kuwa Serikali ipo katika hatua mbalimbali ya kufanya maboresho kwenye sera ya Uchukuzi na Sheria ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, kwa lengo la kuimarisha sekta ya usafiri wa anga.
Naye Mkurugenzi wa Precision, Patrick Mwanri alisema kwamba katika mpango kazi wake, imepanga kuongeza ndege ambazo zitakwenda sambamba na ongezeko la vituo ambavyo kampuni itakuwa ikitoa Huduma nchini.
Mkurugenzi Mwanri aliiomba Serikali kupitia Naibu Waziri Kihenzile, kuzisaidia kampuni binafsi za ndege kuweza kupata mikopo kupitia benki za ndani, ili kuziimarisha kwenye uendeshaji.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Flightlink, Kapteni Munawer Dhirani aliishukuru Serikali kwa kutekeleza dhamira yake ya kuweka mazingira mazuri ya sekta ya anga, na kuhakikisha makampuni binafsi yanaendelea kuwekeza kwa kununua ndege nchini.
Kapteni Munawer aliongoza kuwa  mazingira yaliyowekwa yameiwezesha Kampuni ya Flightlink kuweka mipango ya  kuongeza mtandao wa safari, ambapo mapema mwisho wa mwaka, Kampuni hiyo itaongeza kituo cha Mwanza.