Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

MTWARA

Na Mwandishi wetu

Serikali imesema kuwa itajenga Kongani ya Viwanda vya kuchakata mazao ya Mikoa ya Kusini kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 300.
Akizungumza katika mwendelezo wa ziara yake mkoani Mtwara, Waziri wa Kilimo Hussein Bashe, kuwa alisema iwe jua ama mvua itajenga Kongani ya Viwanda vya kuchakata mazao ya Mikoa ya Kusini eneo la Maranje Mkoani Mtwara yenye gharama ya zaidi ya sh. Bilioni 300.
Kongani ya Viwanda (Industrial Park) inajengwa katika kijiji cha Maranje na Tulia, Kata ya Mtiniko, Nanyamba Mji, Mkoani Mtwara
Alisema eneo la mradi lina jumla ya ekari 1,572, ambapo eneo linaloendelezwa kwa sasa ni ekari 354, na ekari 1,218 zilizobaki zitasafishwa na kuwekewa uzio mwezi ujao.
Waziri Bashe alieleza kuwa, Kongani hiyo ya Viwanda ndilo suluhisho la changamoto walizonazo wakulima wa mikoa hiyo.
“Wapo watu walisema ni ndoto, haitawezekana leo, nawaambia Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ni msikivu na mtendaji, ameamua iwe jua iwe mvua, Kongani itajengwa hapa na itahusisha viwanda mbali mbali vya kuchakata korosho, ufuta, mbaazi na mengine,”alisema Waziri Bashe.
Alisema, Serikali imeanza hatua za awali za ujenzi wa Kongani hiyo, na zaidi ya sh. Bilioni 7 zimewekezwa.
“Mradi huu mkubwa unaoitwa Dkt Samia Suluhu Hassan, unalenga kujenga viwanda vya kubangua korosho visivyopungua 30 kwa awamu, na tayari zaidi ya shilingi bilioni saba zimetumika kujenga maghala mawili na kisima kimoja,”allisema Bashe.
Aliongeza pia kuwa maghala hayo mawili ya awali, yenye uwezo wa kuhifadhi tani 20,000 za korosho, yanatarajiwa kukamilika ifikapo Desemba mwaka huu, ili msimu wa korosho wa mwaka kesho uanze kwa ufanisi.
alisema huo pia utatoa fursa za ajira kati ya watu 33,000 mpaka 35,000 ambapo ajira za kwanza zitanufaisha wananchi wenyeji .
“Mradi huu unatarajiwa kuajiri kati ya watu 33,000 mpaka watu 35,000 na utakuwa suluhisho la changamoto ya muda mrefu juu ya bei ya korosho kwa mikoa yote inayolima korosho, ikiwemo Mtwara, Ruvuma, na Lindi. Serikali yenu ni sikivu haitarudi nyuma, hiki kiwanda kitajengwa kwa maslahi ya wananchi wa kusini,”alisisitiza Bashe.
Aidha, Waziri Bashe alimshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kurejeshwa kwa agenda ya ushuru wa mauzo ya nje, lengo ni kuwezesha upatikanaji wa ruzuku na pembejeo, ili kumuinua mkulima.
Bashe alisema kuwa fedha hizo za ushuru huo zikikusanywa, zinarudi Bodi ya Korosho ili kusimamia mahitaji ya korosho.
“Faida zake ni kubwa kwa kuwa ushuru huu sasa unarudi bodi ya Korosho ili kuwezesha wakulima wa zao hilo. Sasa tumetoka kuzalisha tani 180,000 hadi tani 310,000 na tunatarajia kufikia tani 500,000”, alisema.
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Nanyamba Abdallah Chikota alimpongeza Waziri Bashe kwa mapambano ya kutetea maslahi ya wakulima wadogo nchini.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es salaam amewaasa Vijana 129 waliopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kuishi katika viapo walivyoweka kwa Mungu kwa ajili ya kazi ya kuhubiri Injili kwa mataifa.
Alitoa wosia huo hivi karibuni wakati wa homilia yake katika adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Mtakatifu Maria Faustina, Lulanzi-Kibaha, Jimboni humo.
“Inawapasa mtambue kuwa mkiishi vyema, ahadi zenu mlizo weka kwa Mungu, basi tambueni mtapewa uwezo wa kujua na kutambua lile analolitaka Mwenyezi Mungu kwa wakati na kwenye mazingira ya wakati huo”Alisema Kardinali Pengo
Aliwataka Waamini watambue Pentekoste ya kwanza ya Mitume, ambao walipewa uwezo wa kuhubiri injili kwa mataifa bila ya uwoga na wasiwasi, hata Mwinjili Yohane anasimulia kuwa Mitume walikuwa wakijificha ndani kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi, lakini waliposhukiwa na Roho Mtakatifu, uwoga uliondoka, kwani Roho huyo aliwafanya kuwa na ujasiri.
Kardinali Pengo alisema kuwa viongozi wa Kiyahudi hawakupenda na hawakutaka kusikia habari za Yesu na yeyote aliyekuwa akitangaza imani ya Kristo, alikuwa ni adui kwa viongozi hao.
Sambamba na hayo alisema jambo ambalo kwa sasa linatia hofu, ni kuhusu watu wanaopotea katika mazingira ya kutatanisha, na kesho yake kukutwa wameshauawa, na kwamba hali hiyo inawasukuma watu kujiuliza matendo kama hayo yanafanywa na nani.
Kardinali Pengo alisema kuwa hayo yanayotendeka ya watu kuuawa na mtu akijitokeza kusema ukweli naye anauawa ndiyo sababu ya watu wengine kuogopa kusema ukweli, na kuwataka Waimarishwa wazidi kumwomba Roho Mtakatifu awatoe hofu katika kufanya kazi zao, na kuwataka wamtumie vyema Roho wa Mungu.
Pia, aliwataka Waamini wote watambue kuwa chimbuko la maafa yote ni dhambi, na wakati mwingine dhambi hizo ni katika kutafuta utajiri, au ukosefu wa imani, wazazi kwa watoto wao kwa kutambua kuwa watoto wao ni chimbuko la Utajiri.
Kardinali Pengo aliwataka Waamini wajitahidi kuishi bila dhambi na kushuhudia imani huku wazazi na walezi wakiwaombea vijana wanaopokea Sakramenti Takatifu ya Kipaimara ili waweze kuishi imani yao na kutangaza habari njema ya wokovu bila uwoga.
Vilevile aliwataka waamini kuwakumbusha vijana hao mambo yote watakayo yaahidi na kuwasaidia kwa kukaa nao siku zote za maisha yao ili wasisahau kumuomba Mungu awasimamie katika vita yao ya kupambana na dhambi.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Paroko Msaidizi wa Parokia Mtakatifu Maximiliam Kolbe, Mwenge, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam,  Padri Daniel Mapunda amewataka Waamini kuachana na wivu, kwani huo ni ushamba wa kutojitambua.
Alisema hayo katika homilia yake wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu iliyoadhimishwa  parokiani hapo.
“Wivu ni ile hali ya mtu kutokupenda mafanikio ya mwenzako, lakini inawapasa kutambua kuwa wivu kwa maana nyingine ni ushamba wa mtu kumtolea mwenzako kijicho kwa yale mafanikio aliyopewa na Mungu,”alisema Padri Mapunda.
Padri Mapunda aliwaasa Waamini wazidi kumwomba Mungu ili wajitambue kuwa wao ni nani, na kufahamu uwezo wao waliopewa na Mungu.
Aidha, aliwataka Waamini wafahamu, vizuri jinsi ya kuzitumia karama zao walizojaliwa na Mungu na kuzifahamu kwani hata kama ndugu wamezaliwa tumbo moja hawawezi kufanana karama zao.
Kwa mujibu wa Padri Mapunda, Waamini wanapaswa kufahamu kuwa utajiri wa Mungu hauna mipaka, na kuwataka watambue kuwa Mungu aliwapa Manabii utajiri wa kuhubiri Injili kwa watu wake.
Aliwataka Waamini hao kila mmoja kwa nafasi yake kuonesha utu kila mahali, na kuziheshimu kazi  zao.
Padri Mapunda alisema hata katika somo la Injili inaonyesha namna Mungu alivyotoa, talanta na kuwataka Waamini wasizitumie vibaya.
Hata hivyo, aliwaomba Waamini hao kuachana na tabia za kuwakwaza wenzao kwa kuwafabyia matendo ambayo kwa upande wao hawayapendi.

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Yohane wa Mungu – Vituka, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Patrick Bwakila amewataka watoto kutokuufananisha mkate uletao uzima (yaani Mwili wa Kristu) na mikate mingine, kwani wanapokula Mkate huo, wanamla Kristu mwenyewe.
Aliyasema hayo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika, iliyokwenda sanjari na kuwapatia watoto hao Sakramenti ya Ekaristi Takatifu katika Parokia ya Yohane wa Mungu – Yombo Vituka, jimboni humo.
“Ndugu zangu wanangu wapendwa, Mama Kanisa alitufundisha kwamba Sakramenti ya Ekaristi Takatifu ni Sakramenti ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristu, Mungu kweli na Mtu katika maumbo ya mkate na divai…
“Kumbe, mkate tunaokula leo, siyo ule wa mama mpika chapati, hapana, ni Kristu mwenyewe ndiye mnayemla leo. Na Kristu mwenyewe anatuambia, aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu, huyo hukaa ndani yangu, na mimi hukaa ndani yake. Huu ni mkate wa uzima, mkate uletao uponyaji, afya ya roho, mkate unaotustahilisha sisi huurithi na kupata uzima wa milele,” alisema Padri Bwakila.
Padri Bwakila aliwaonya watoto hao kuepuka kumuasi Kristu mara baada ya kupokea Sakramenti hiyo Takatifu, na kuongeza kwamba atakayefanya hivyo, atatakiwa kuacha kushiriki sakramenti, kwani amemkana na kumkimbia Kristu.
Pia, aliwataka kukumbuka kwamba kwa Sakramenti hiyo ya Ekaristi Takatifu waliyoshiriki katika adhimisho hilo la Misa Takatifu, wametengeneza mahusiano ya kudumu na Yesu Kristu, ambaye ndiye waliyemla.
Mmisionari huyo wa Shirika la Watumishi wa Wagonjwa(Wakamiliani), aliwasihi watoto hao kujitahidi kujibidiisha siku zote, ili watamani na waendelee kupokea chakula hicho ambacho ni kitakatifu.
Aliongeza kwamba haipendezi kwa mtoto ambaye amepokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, na baada ya hapo, haonekani kanisani kushiriki katika Adhimisho la Misa Takatifu.
“Leo umepokea Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, baada ya hapo unasema sasa Kanisa ‘bye bye’. Ukifanya hivyo, na Yesu naye atakwambia ‘bye bye’. Utatoroka kanisani, utaliacha kanisa, utaenda kuhangaika, baadaye likikupata tatizo, utaanza kusema ‘Mungu wangu mbona umeniacha,” alisema Padri huyo.
Aliwasisitiza kutokumwacha Mungu ambaye tayari wameshatengeza mahusiano mazuri naye, kwani faida ya kuwa karibu na Mungu wataiona mbinguni.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi akiadhimisha Misa Takatifu ya Shukrani ya Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) kwenye viwanja vya Seminari ya Mtakatifu Maria, Visiga-Kibaha jimboni humo. (Picha na Michael Ally)

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi akiadhimisha Misa Takatifu ya Shukrani ya Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) kwenye viwanja vya Seminari ya Mtakatifu Maria, Visiga-Kibaha jimboni humo. (Picha na Michael Ally)

Askofu wa Jimbo Katoliki la Bunda, Mhashamu Simon Masondole, Mapadri, mgeni rasmi, Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Jenerali Venance Mabeyo (kushoto kwa Askofu), wakiwa katika picha ya pamoja na WAWATA, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Dominika ya 21 Mwaka B, sanjari na Harambee ya kuchangia ujenzi wa kanisa la Kigango cha Mtakatifu Theresia wa Mtoto Yesu – Kilimahewa Juu, Parokia ya Mtakatifu Agostino – Salasala, Jimbo Kuu la Dar es Salaam. (Picha na Mathayo Kijazi)

Viongozi wapya wa Dekania ya Mtakatifu Thomas More wakiweka kiapo mbele ya Dekano wa Dekania hiyo, Padri Romwald Mukandala wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu katika Parokia ya Mtakatifu Kizito, Kilongawima, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam. (Picha na Simon Peter)

Viongozi wa Utume wa Wanaume Katoliki (Uwaka), Parokia ya Mtakatifu Dominico, Mbezi Juu, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, wakiwa katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Uwaka Day, parokiani hapo hivi karibuni. (Picha na Yohana Kasosi)

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu na Mapadri wakiwa katika picha ya pamoja na Wasimamizi wa Waimarishwa wa Sakramenti ya Kipaimara, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu katika Parokia ya Mtakatifu Andrea Mtume Bahari Beach, jijini Dar es Salaam. (Picha na Yohana Kasosi)