Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

‘Zilizala’ la Boda; Limezaa vifo, vilema vya kusikitisha

MWANZA

Na Paul Mabuga

Biashara ya huduma ya usafiri wa pikipiki maarufu hapa Afrika Mashariki na hata katika miji na vijiji vyetu kama bodaboda, ni ajira ya uhai na kifo!
Ni kazi ya raha kwa kuwa inaiingiza  kipato, lakini pia ni ya karaha kutokana na wakati mwingine jamii inavyowatazama wanaoiendesha.
Pia, kazi hii imejaa mzuka wa kilele cha tijira kwa vijana wa fasheni, wanaopenda muziki ‘mnene’ na bomba la moshi linalobalaruka kwa sauti kubwa.
Kwao, hawa hii ni ruya ya kupaa hadi anga la saba na kujisikia katika ndoto ya kilele cha furaha, na hili ni zilizala katika ajira hii, ikisimuliwa kwa Tumaini Letu na waendesha bodaboda watatu kutoka katika Jiji la Mwanza.
Wa kwanza ni Emmanuel Kalima mwenye umri wa miaka 32 hivi sasa na mkazi wa Ilemela katika jiiji la Mwanza. Leo  analazimika kuendesha bajaji katika  kituo cha Sabasaba jijini humo baada ya kupata ulenavu uliotokana na kukatwa mguu wa kulia  kufuatia ajali aliyoipata miaka tisa iliyopita  wakati akiwa na kazi ya kuendesha bodaboda.
Kalima yupo katika kituo chake cha kazi akisubiri abiria, akiwa na Rozari yake shingoni, bila shaka ana matumaini kibao kwamba  maombi yake yatasikika, pengine leo kama jana atapata fedha ya kutosha kununua chakula kwa  familia yake ya  watoto wawili na mke, pia kumudu mahitaji ya shule kwa wanae wawili  wakubwa wanaosoma darasa la kwanza na la pili mtawalia. Lakini pia ana jukumu la kupeleka hesabu kwa mmiliki wa chombo hicho cha usafiri.
“Nipo naishi na mke wangu na watoto, na maisha ni ya furaha, hakuna unyanyapaa ndani ya familia yangu, na kuna mapenzi makubwa. Tunafurahia maisha kwa wakati huu,” anasema Kalima ambaye mara baada ya kumaliza elimu yake ya Kidato cha Nne  mwaka 2007, aliingia katika mapambano ya kutafuta naisha.
Wa pili ni Nhumba Mihaye ambaye pia aliacha kazi ya udereva wa bodada aliyokuwa akiifanya katika jiji la Mwanza na  kuamua kuedesha bajaji katika kituo cha Buswelu jijini humo.
Kwa sasa ana umri kama wa miaka 55 hivi na alikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuanza biashara hiyo ya huduma katika jiji hilo. Kama ilivyo kwa Kalima, Mihaye naye anatakiwa kukamilisha hesabu ya ‘bosi’ na nyingine ya kujikimu kwa familia yake.
“Boda hapa ziliingia mwaka 2008, na mie wakati huo niliingia kufanya kazi hiyo. Ili kumudu maisha na mipango yangu, nilikuwa nakesha na  kipindi hicho kupata hesabu ya shilingi 70,000/- hadi 80,000/- kwa siku, ilikuwa ni kawaida.
 Ingawa abiria walikuwa wachache, lakini na sisi watoa huduma tulikuwa wachache, na  kazi ilikuwa nzuri kwa kweli kulinganisha na sasa  hivi ambapo ushindani ni mkubwa, na watu wamepigika, hawana fedha hadi wengine wanatembea kwa miguu” anasema Mihaye.
Anashukur u kwa kazi hiyo kwa kuwa ameweza kujenga nyumba, na ana watoto ambao angalau wamesoma hadi chuo kikuu. Lakini changamoto alizokutana nazo wakati huo ndizo zilizomfanya aachane na udereva wa  bodaboda, hasa baada ya kuona kuwa anaweza kupoteza maisha.
Wa tatu ni Bahati Yohane, mkazi wa Kiseke Jijini humo, na  yeye anashukuru kwa kazi ya bodaboda kwa kuwa  ilimfanya akapata mke ambaye anaye hadi sasa. Anasema wakati huo anaendesha boda boda, mambo yalikuwa mazuri na hata alimudu kila mahitaji katika familia yake.
“Kutokana na kuwa na fedha nyingi, nilijikuta naongoza matumizi ambapo kila baada ya kazi kabla ya kurudi nyumbani, nilikuwa napita baa na kupata  [nakunywa bia] kidogo.  Ilifikia mahali, mke wangu alikuwa anagomba sana kuendesha piki piki nikiwa nimelewa, lakini sikukoma, hadi nilipokomeshwa, na ndiyo maana unaniona hivi, nachechemea,” anasema Yohane ambaye ana umri wa miaka 46, ambaye kwa sasa amehamia kwenye bajaji.
Yohane anasema kuwa nyakati hizo wandesha bodaboda walikuwa wakituhumiwa  kuwapa ujauzito mabinti wanafunzi, na anadai kwamba kwa siku hizi hilo limepungua  kwa kuwa wasichana wengi wamejitambua na hawadanganyiki na vitu vidogo vidogo kama ilivyokuwa zamani. Na pia wazazi wametambua majukumu yao ya kuwatimizia mahitaji mabinti zao.
Anasema pia ni kweli wapo waendesha boda boda  ambao hata wanafikia hatua ya  kufukuzwa kwenye vituo kutokana na tuhuma za unyanyasaji wa kingono kwa abiria wao, wakiwemo watoto na wanawake. Anaongeza kuwa licha ya tabia hizi mbaya  kupungua, lakini zimekuwa zikijenga taswira mbaya ya kazi hiyo machoni pa jamii.
“Ila kisa cha kuacha kazi ya bodaboda, ilikuwa ni siku moja pale Kiseke, nilikuwa nimekunywa pombe na naendesha, nikajikuta naingia  barabara kubwa bila tahadhari. Ilitoka huko, bodaboda kwenye barabara kuu ikiwa kasi na kunichota kama  mwewe anavyonyakua ikifaranga. Kutoka hapo sikujitambua hadi nilipojikuta  hospitalini natibiwa na hicho ndicho kisa cha huu ulemavu nilionao,” anasimulia Yohane.
Kwa upande wake Mihaye anasema kuwa kuna mtindo wa vijana, kupanua mabomba ya moshi ya pikipiki zao ili zitoe mlio mkubwa wakiendesha, wengine wanaweka muziki sauti ya juu kujifirahisha na hata kuzing’oa sight mirror  [vioo vye pembeni; na kuweka urembo mwingine kama fasheni.
“Ila wengi wanaong’oa vioo vya pembeni, huwa ni wahalifu, nia yao huwa ni kwamba wakimkwapua abiria wa pikipiki ya mbele yao au mtembea kwa miguu, wakimbie bila kikwazo cha kuona kuna mtu anawafuata, wanaamini kwamba, wakiwa wanaona wanafuatwa wataghafirika na kupunguza mwendo,” anasema Mihaye na kuongeza,
“Kuna siku nilikuwa na abiria mwanamke napita barabara ya hospitali ya mkoa  wa Mwanza, Sekou Toure. Vijana wanamna walikuwa nyuma yangu na pikipiki yao, wakakwapua mkoba wa abiria huyo. Niliamua kumshusha na kuanza kuwafukuza.
Walikuwa  wakikata mitaa ninao, huku ninapiga kelele  za mwizi, na walipoona ninawakaribia wakautupa chini mkoba, nikauchukua na kumrejeshea abiria kule  nilikomuacha baada ya kuachana na wezi hao.”
Na kuhusu kisa cha kuachana na udereva bodaboda, anasema kuwa, siku moja saa nane za usiku, alimpakia abiria mwanamke na hakujua kuwa yule alikuwa ni sehemu  ya majambazi, “ilikuwa ni ile njia ya kutoka Ilemela Mahakamani kuja njia  ya lami, tulipokaribia sehemu yenye miti isiyo na watu wengi, yule abiria alianza kujichezesha nyuma ili  nipunguze mwendo ama kuanguka, na kwa mbele nikaona kundi la vijana wakiwa na nondo na mapanga.
“Nilipoona hivyo, nikaendesha pikipiki kuwafuata waliko ili niwagonge, wakatawanyika na kujiweka mbali  walipoona hivyo, nikashuka na kumg’amg’amia yule mwanamke kwenye pikipiki,huku nikimpiga na kumgeuza kinga endapo wangenishambulia;
“Waligundua manbo ni magumu, wakakimbia na nikabaki na yule abiria feki, nikamwambia alete hela yangu, akabisha, nikamsachi na kumkuta ana shilingi 15,000/= nikamnyang’anya, nikamwambia ondoka naye akatimka kama hana akili sawa sawa.  Na huo ndio mwisho wangu na bodaboda,” anasimulia Mihaye.
Kalima yeye anasema kwamba kwa siku hizi mambo mengi yamebadilika, uhasama wa wenye magari au madereva wa daladala na waendesha bodaboda kitu ambacho kilikuwa chanzo cha ajali nyingi, umepungua baada ya kila upande kuuheshimu mwingine.  Pia uelewa wa sheria miongoni mwa madereva wa bodboda kumeondoa pia ile tabia ya wao kufukuzana na askari wa usalama barabarani.
“Nimeshuhudia vifo vya madereva boda boda sita ama saba hivi kutokana na ajali zilizo katika mazingira haya tangu nianze kuendesha bodaboda mwaka 2010,” anasimulia Kalima ambaye kabla ya kujinunulia pikipiki yake alifanya kazi ya ajira Halmashauri ya Jiji la Mwanza kama mhudumu, na baadaye hotelini, na hivyo kujipatia fedha kwa ajili hiyo.
“Hata hivyo siku moja mwaka 2015,  nikiwa naendesha pikipiki kuelekea mjini kutoka Airport na abiria wangu akiwa dereva bodaboda mwenzagu, na wakati trafiki wameyazuia magari ya  upande mmoja wa barabara, [wakati huo barabara ya Aiport haijawa na njia mbili] ili kuruhusu basi la timu ya Mbao iliyokuwa ikifanya mazoeazi katika viwanja vya DIT hapa Mwanza, kuingia barabara kuu ili waelekee upande wa kulia kwetu,  lilikuja gari moja likiwa na mwendo mkali.
Gari hilo ni kama lilikataa amri ya trafiki na kuingia upande wetu ulioruhusiwa,  na hivyo kukutana uso kwa uso na sisi  na kutugonga. Ilikuwa ajali mbaya sana. Tulipakiwa katika magari mawili tofauti, mwenzangu akapelekwa Sekou Toure na mimi nikapelekwa Bugando [hospuali] na huko, baada ya kulazwa kama mwezi mzima wakanikata mguu,” anasimulia Kalima, na kuongeza kuwa, “ Baada ya kukatwa mguu, nilikaa siku tatu bila fahamu, baadaye nilijitambua na kujiona mwenye afya na nikawa nakula chakula kama kawaida.
Nilishtuka  baada ya kuona kama kuna wepesi usio wa kawaida kwenye mguu wa kulia, na ndipo nilpotambua kuwa umekatwa. Nilisikitika sana, wakanipa moyo kuwa, utaota na kurejea hali ya kawaida, na nikayaamini haya maneno.”
Anasema aliielewa hali hiyo baadaye na kuendelea kuisha nayo.  Ila kwa sasa anawaomba wasamaria wema kama wanaweza kusaidia  fedha za kupata mguu bandia ili maisha yake yaendee kawaaida. Anapatikana kwa namba  0786858676, mwenye kuwiwa kumsaidia anaweza kuwasiliana nae. Kwa naelezo ya awali anadai mguu bandia  unaweza kugharimu kati ya shilingi milioni mbili hadi tatu.

Rate this item
(0 votes)

Leave a comment

Make sure you enter all the required information, indicated by an asterisk (*). HTML code is not allowed.