Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

WAWATA watikisa Visiga

September 02, 2022

KIBAHA

Na Mathayo Kijazi

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi amewataka Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA), na waamini wote kutambua kwamba wanapomsifu Mtakatifu Agustino, wanapaswa pia kumshukuru Mama yake mzazi Mtakatifu Monica.
Askofu Ruwa’ichi aliyasema hayo wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Kilele cha Jubilei ya Miaka 50 ya Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA) Kijimbo, katika Kumbukumbu ya Mtakatifu Monica, iliyofanyika katika Seminari Ndogo ya Mtakatifu Maria, Visiga, jimboni humo.
“Tunaadhimisha mambo kadhaa, kwanza kabisa tunawamkumbuka WAWATA, na hususan Mtakatifu Monica, mama yake Mtakatifu Agustino. Huyu ni mama wa mfano, mama aliyetukuka, mama wa kuigwa. Mama huyu alizaliwa mwaka 331 katika Bara la Afrika, huko Afrika ya Kaskazini,” alisema Askofu Mkuu, na kuongeza,
“Alizaliwa na kulelewa vizuri katika familia ya Kikristo, akajenga na kustawisha fadhila zilizo njema; fadhila ya Imani; fadhila ya mapendo; fadhila ya huruma na fadhila za kimama. Tumtukuze Mungu kwa zawadi ya Mama huyu kutoka Bara la Afrika,” alisema Askofu Mkuu Ruwa’ichi.
Askofu Ruwa’ichi aliwapongeza WAWATA kwa kuendelea kusimama imara na kwa kujitolea kwao katika shughuli mbalimbali za Kanisa, huku akiwasihi kufahamu kwamba wao ni zawadi ya Mungu kwa Kanisa na Ulimwengu.
Askofu Mkuu Ruwa’ichi alimshukuru Mungu kwa utume unaofanywa na akinamama hao, hasa kuwalea Vijana wa Seminari ya Visiga, akimwomba Mungu awazidishie neema na baraka zake, ili utume wao uendelee kustawi, na kuutukuza ukuu wa Mungu.
Askofu Ruwa’ichi aliwasihi WAWATA kutafakari kwamba wao ni baraka kutoka kwa Mungu, kwa uwepo wao wa Miaka 50 sasa, kwani Utume wa Wanaume Wakatoliki (UWAKA), hata miaka 30 bado hawajafikisha, huku akiwasihi akinamama hao kumshukuru Mungu kwa mema yote anayowajalia.
Aidha, aliwaasa WAWATA kuendelea kubaki kuwa Wakristo Wakatoliki wazuri, hata katika Kanisa la nyumbani, kwa kusimama imara na kuwa mama bora, hata katika familia zao.
Kwa upande wao, Maaskofu Wasaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu na Mhashamu Stephano Musomba, waliwapongeza WAWATA kwa kuadhimisha Jubilei yao ya Miaka 50, na kwa kazi nzuri ya utume wanaoendelea nao kuufanya jimboni humo.
Naye, Mwenyekiti wa Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA), Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Stella Rwegasira aliwashukuru waamini wote walioshiriki Adhimisho hilo.
Aidha, Catherine Mwingira, Katibu wa WAWATA Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam alisema kuwa wanamshukuru Mungu kwa kufikisha Miaka 50 tangu chama hicho cha Kitume kuanzishwe na waasisi wao, huku akisema kuwa yamefanyika mengi mazuri tangu kuanzishwa kwa chama hicho hadi sasa.
Chama cha Kitume cha Wanawake Wakatoliki Tanzania (WAWATA), kilianzishwa rasmi mwaka 1972.

DAR ES SALAAM

Na John Kimweri
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddeus Ruwa’ichi, amewataka waamini kutoa kipaumbele na kuwakumbuka wanyonge na watu wasiojiweza katika karamu mbalimbali wanazoziandaa.
Wito huo aliutoa hivi karibuni wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa ya kutoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, iliyokwenda sanjari na uchangiaji wa ujenzi wa nyumba ya Mapadri, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Dominiko Savio, Mikoroshini Tandika, jimboni humo.
Alisema Wakristo hawawezi kumlipa Kristo kwa kazi kubwa ya ukombozi aliyoifanya, lakini kwa njia ya kuwasaidia wengine, wanaweza kufanya utume na kazi ya kumpendeza Mungu.
“Yesu anatuambia kwamba tunapofanya karamu, tuwakumbuke wanyonge kama maskini, viwete, na wale wasio na cha kutulipa, wale ambao hutegemei nao waandae sherehe wakualike,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Askofu Ruwa’ichi alieleza kuwa katika Pentekoste, Roho Mtakatifu aliwashukia mitume na kuwapa nguvu, uthubutu na msukumo wa kwenda kuitangaza Injili, bila kuogopa.
Alisema kijana anayeimarishwa akimpokea Roho Mtakatifu, anakamilishwa katika neema ya ubatizo, kwa kuwa katika ubatizo huzaliwa mara ya pili, na kufanywa kuwa mtoto wa Mungu na ndugu wa Kristo.
“Katika Pentekoste, Roho Mtakatifu aliwashukia Mitume na kuwapa nguvu na uthubutu na msukumo wa kwenda kuitangaza Injili. Hawa watoto leo kwao ni Pentekoste, na watampokea tena Roho Mtakatifu, kwasababu tayari walishampokea” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Katika hatua nyingine, Padri Canisius Hali, wa Parokia hiyo amewaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushirikiana nao katika kazi hiyo ya ujenzi wa nyumba ya mapadri.
Kwa mujibu wa Padri Hali, alibainisha kuwa kwa sasa ujenzi huo upo katika hatua za mwisho, na kumshukuru Baba Askofu kwa ushauri na kuwa pamoja nao katika shughuli hiyo.
“Tunajenga nyumba ya mapadri ambayo ipo katika hatua za mwisho, na Baba Askofu amekuwa karibu nasi katika hatu zote, ninawaalika waamini kutoka maeneo mbalimbali ili kushirikiana nasi katika kazi hii” alisema Padri Hali.
Katibu wa Halmashauri ya Walei Parokia hiyo, Pankrasia Heri, alifafanua kuwa kwa sasa Paroko wa Parokia hiyo anaishi nje ya nyumba hiyo, na hivyo kumshukuru mmoja wa waamini ambaye ndiye aliyejitolea nyumba hiyo.
Alisema pia kuwa kukosekana kwa nyumba hiyo, na wasaidizi wengine ndani ya Parokia kama Mafrateri na mashemasi, kumesababisha utendaji kazi wa Paroko uwe mgumu.

 

GULU, Uganda
Maandalizi ya kutangazwa Padri Joseph Ambrozoli kuwa Mwenyeheri yanaendelea vizuri, tukio litakalofanyika wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu itakayofanyika Jimbo Kuu Katoliki la Gulu, Uganda Novemba 20, mwaka huu.
Mchungaji John Baptist Odama wa Jimbo Kuu Katoliki la Gulu alisema kuwa Kamati Kuu ya Maandalizi (COC) yenye kamati ndogo 16 imeundwa, na wote wanafanya kazi ya kuona jinsi ya kuwapokea watu watakaokuja kuhudhuria ibada hiyo.

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, akimpatia Sakramenti Takatifu ya Kipaimara mmoja wa vijana waliopokea Sakramenti hiyo, katika Adhimisho la Misa Takatifu iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Imakulata, Upanga, Jimboni humo, (kulia kwa Kardinali) ni Paroko wa Parokia hiyo Padri Casmir Kavishe. (Picha na Mathayo Kijazi)

Na Mathayo Kijazi

Mwadhama Polycarp Kardnali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, amewasihi Waimarishwa wa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kutambua kwamba kwa sakramenti hiyo wanatumwa kuitangaza habari njema kwa Mataifa.
Kardinali Pengo aliyasema hayo hivi karibuni wakati akihubiri katika Adhimisho la Misa ya kutoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara kwa vijana 37, iliyofanyika katika Parokia ya Mtakatifu Imakulata, Upanga, Jimboni humo.
“Ndugu zangu mnaoimarishwa leo katika Sakramenti hii Takatifu, tambueni kwamba mnapopakwa mafuta, mnatumwa kwenda kuifanya kazi ya Mungu ya kuitangaza habari njema kwa Mataifa, yaani mnatumwa kuwatangazia masikini habari njema,” alisema Kardinali Pengo, na kuongeza,
“Masikini hao wanaotangaziwa habari njema, siyo umasikini wa kukosa fedha, kwa sababu kama ni umasikini wa fedha, hata Yesu Kristu mwenyewe alikuwa ni masikini.”
Aidha, Kardinali Pengo aliwasihi vijana hao kufahamu kwamba hata kama ni masikini na wenye kujiona kuwa hawana thamani maishani mwao, lakini Mungu hajawaacha, hajawatupa na wala hajawalaani.
Kardinali Pengo aliongeza pia kuwa heri watu walio masikini ambao wanamtegemea Mungu, kuliko matajiri ambao wanadhani kwamba wana kila kitu, na hivyo hawahitaji uwezo wa Mungu katika maisha yao.
Alisema pia kuwa kuitangaza habari njema ni pamoja na kuyaishi Maandiko Matakatifu, kwani mtu hawezi kuitangaza habari njema kwa kutenda kinyume na mafundisho ya Mungu.
Kardinali Pengo aliwasihi wazazi na walezi kuwasindikiza watoto wao katika kumsifu na kumtukuza Mungu, ili waendelee kudumu kuwa Askari hodari wa Kristo.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Casmir Kavishe alimshukuru Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo kwa kufika Parokiani hapo na kuwapatia Sakramenti hiyo Takatifu vijana 37 katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu.
Padri Kavishe aliwashukuru Makatekista na waalimu wote walioshiriki katika kuwafundisha vijana hadi kuwa imara na kuweza kupokea Sakramenti Takatifu, huku akiwasihi vijana hao kuendelea kudumu katika yale yote waliyofundishwa.

Padri Germine Laizer akiwavisha rozari baadhi ya wanachama wapya wa Chama cha Wajane na Wagane

Dar es Salaam

Na Benedikto Agostino

Wajane na Wagane nchini wametakiwa kuendelea kuishi fadhila za Mtakatifu Monica bila kukata tamaa, na kumshukuru Mungu kwa maisha ya wenzi wao waliotangulia mbele ya haki, bila kusahau kuwaombea hao na watoto waliochwa na wazazi wao kila mara.
Hayo yalisemwa na Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Kamili, Yombo Kiwalani, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaaam, Padri Germine Laizer, wakati akihubiri katika Adhimisho la MIsa Takatifu ya Somo wa Wajane na Wagane, Mtakatifu Monica, iliyofanyika kwa ngazi ya Jimbo katika Parokia hiyo.
Katika homilia yake, Padri Laizer aliwakumbusha wajane na wagane kutambua maisha ya Mtakatifu Somo wao, Monica, kama mjane aliyeishi katika mateso na maisha mabaya ya mwanae Augustino, lakini licha ya kupitia changamoto hizo, hakukata tamaa hadi mtoto wake alipoongoka, na sasa ni Mtakatifu.
Alisema kwamba pamoja na ujane na ugane wao, ni muhimu kuishi fadhila ya unyenyekevu, kwani ni ishara ya itii mbele ya Mungu na watu, na hasa kila mmoja anapojishusha na kuwa kama mtoto mdogo.
“Maisha yetu yana maana kubwa kila tunapojinyenyekeza na kujikabidhi mbele ya Mwenyezi Mungu, kwani kila mmoja wetu anadaiwa kadri anavyokuwa mkuu kunyenyekea,” alisema Padri Laizer.
Aliongeza kusema kwamba watu wengi walioishii fadhila hiyo ya unyenyekevu wamepata kibali mbele za Mungu, na kujibiwa sala na maombi yao na kumbukumbu lao linaishi hata hivi leo.
“Tabia ya kiburi na majivuno ni kinyume cha unyenyekevu, na mara baada  ya mtu kuwa na maisha hayo, hali ya mtu hubadilika na kuharibika kabisa,” alisema Padri Laizer.
Alisema kuwa tukiongozwa na unyenyekevu ni lazima tufike mbali, kwani fadhila hiyo inalipa, na hakuna aliyeishi hali hiyo ambaye hakufanikiwa kamwe.
“Ni wazi unyenyekevu unapokosekana popote, yanatawala mafarakano, uogomvi na majigambo, hali inayotawanya kundi na kupoteza amani na mshikamano miongoni mwa familia ya Mungu,” alisema padri huyo.
Aliwataka waamini kuiga mfano mzuri wa mtu pekee aliyeishi fadhila ya unyenyekevu, ambaye ni Bikira Maria ambapo pamoja na magumu aliyoyapitia, aliyaweka mengi moyoni mwake.
Naye Mwenyekiti wa Wajane na Wagane Jimbo, Sweetbeter Mzungu alimshukuru Paroko wa Parokia hiyo, kwa utayari wake wa kupokea ujio wa sherehe hizo, na kuwapongeza wanachama wote waliojitokeza kufanikisha shughuli hiyo muhimu ambayo hufanyika mara moja kila mwaka.
Sweetbeter alisema kwamba moja ya mafanikio makubwa kwa sasa ni hatua waliopiga kutoka kutambuliwa kama kikundi na kuwa chama cha kitume ingawa bado changamoto kubwa ni mwitikio, hasa wa kupokelewa katika Parokia zote.
Alibainsha kuwa mara nyingi watu wengi hawapendi kujitambulisha kama wajane au wagane, na hali hiyo hutokana na kutokujikubali au kuipokea baada ya kuondokewa na wapendwa wao, na hasa wagane.