Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

Madega na harakati zake Yanga

DAR ES SALAAM

Na Arone Mpanduka

Jumamosi ya Februari 10 mwaka huu majira ya mchana, zilitoka taarifa za kwamba aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Imani Madega, amefariki dunia.
Hakika zilikuwa ni taarifa za ghafla zilizotokana na kifo cha ghafla, kwani inaelezwa kwamba asubuhi ya siku hiyo akiwa nyumbani kwake Chalinze mkoani Pwani, alimuomba mtoto wake ampeleke hospitali kwa madai kwamba anajisikia vibaya, ingawa alikuwa na nguvu zake akitembea mwenyewe, lakini wakati akifanyiwa vipimo na matibabu hospitalini, hali ilibadilika na alifariki kwa tatizo la shinikizo la damu.
Katika kolamu hii, nitakusimulia baadhi ya matukio ambayo Madega aliwahi kuyafanya akiwa na Yanga ambayo aliiongoza kuanzia Mei mwaka 2007 hadi 2010.
APINGA YANGA KAMPUNI
Hiyo ilikuwa ni mwaka 2007 ikiwa ni siku chache baada ya kushinda nafasi ya uenyekiti wa Yanga, ambapo yeye na Viongozi wenzake, waliitwa ofisini kwa Yusuph Manji ambaye wakati huo alikuwa mfadhili.
Katika wito huo, Manji alimtaka atie saini mkataba wa makubaliano ya kuifanya Yanga iwe Kampuni na baada ya hapo Francis Kifukwe angepewa urais ndani ya mfumo huo, kitu ambacho Madega alikataa.
Sababu ya kukataa ni Katiba kutoruhusu kwa wakati huo, huku pia akiwa na wasiwasi kwamba huenda likawa changa la macho la kutaka klabu hiyo kubinafsishwa kihuni.
Madega aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema kwamba hawezi kufanya kitu kama hicho na kwamba Manji hana nia nzuri na klabu, hivyo ni vyema awaachie timu yao na wao wapo tayari kupambana nayo ili kuiendesha. Hapo ndipo uhasama kati yake na Manji ulipoanza.
KAULI YA KIBABE BAADA YA YANGA KUTEKWA
Ilikuwa Oktoba mwaka 2007, ambapo wakati huo uhasama kati yake na Manji ulizidi kupamba moto na kuibua makundi mbalimbali ambayo mengine yaikuwa yanampinga yakitaka aondoke madarakani.
Siku moja Yanga ikiwa chini ya kocha Mmalawi, Jack Chamangwana (sasa marehemu), ilitekwa na kundi la makomandoo ambao inasemekana walikuwa upande wa Madega na kwenda kufichwa Morogoro.
Katika mahojiano yake na kipindi cha Spoti Leo cha Redio One, Madega alikaririwa akisema, “Sitakuwa tayari kuiona Yanga ikiuzwa na kutawaliwa na mtu mmoja kwa nguvu ya pesa, masikini na mwanawe, tajiri na mali zake, Manji baki na mali zako au heshimu Katiba. Vinginevyo baki na mali zako au fadhili timu nyingine.” Baada ya sekeseke hilo, baadaye hali ya hewa ilikaa sawa.
AMSHUTUMU MANJI KUHUJUMU TIMU
Mwezi huo huo mwaka 2007, Yanga ilicheza dhidi ya Simba kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro, na Yanga kufungwa bao 1-0. Baada ya mchezo Madega aliibuka na kumshutumu Manji kwamba alitoa pesa kwa wachezaji ili wajifungishe kwa lengo la kumfanya aonekane hafai kuiongoza klabu hiyo na aondolewe kirahisi.
Ikumbukwe kuwa kabla ya mchezo, Manji alitoa Shilingi milioni 40 za maandalizi, huku akitoa na milioni 10 kwa wazee ili wafanye mambo ya kishirikina kwa ajili ya mchezo.
AOMBA RADHI WAZEE/MANJI
Ilikuwa mwishoni mwa mwaka huo huo wa 2007, ambapo siku moja waandishi tuliitwa kwenda kuchukua habari kwenye ukumbi wa hoteli ya Travertine, Magomeni jijini Dar es Salaam ambapo Madega aliingia ukumbini, na wanahabari wote tulitakiwa kusubiri nje kwanza. Baada ya dakika kadhaa tukaitwa na kutaarifiwa kwamba mzozo kati ya Madega, Manji, na wazee umekwisha baada ya Mwenyekiti huyo kuomba radhi.
AONGOZA MKUTANO KWA DAKIKA TATU
Ilikuwa mwaka 2008 ambapo Madega aliitisha mkutano wa wanachama kwenye ukumbi wa Police Officers Mess, na waandishi wa habari tulikwenda kushuhudia kile kilichofanyika. Miongoni mwa yaliyokwenda kufanyika, ni kupitisha baadhi ya marekebisho ya vipengele kwenye katiba.
Kabla ya mkutano kuanza, wanachama walipewa rasimu ya katiba ili kuweza kupitia na kufanya maamuzi. Ilipofika majira kama ya saa 3 na nusu asubuhi, Madega aliingia mkutanoni kuhakiki akidi na moja kwa moja kuhoji wanachama wote kama wanakubali rasimu ipite ama la.
Wanachama wengi walinyoosha mikono juu kuonyesha wameridhia, na hapo hapo Madega alitangaza kuwa rasimu imepita na kufunga mkutano huo, huku akisindikizwa na wimbo wa Pepe Kalle (hayati) wa Young Africans. Mkutano huo ulitumia dakika 3 tu na kuwashangaza wengi.
ATUKANWA NA NICOLAUS MUSONYE
Hilo lilijiri baada ya Yanga kukataa kuingiza timu uwanjani julai mwaka 2008, ambapo ilitakiwa kucheza na Simba kuwania mshindi wa tatu katika michuano ya Kagame. Siku hiyo uwanja ulifurika kuzisubiri timu ziingie uwanjani, lakini walionekana wachezaji wa Simba pekee.
Madega alipoulizwa, alisema kuwa walikubaliana pande zote (Simba na Yanga), kuwa wasipeleke timu uwanja mpya wa Taifa (sasa Benjamin Mkapa) kama matakwa yao yasingetekelezwa na CECAFA (ya mgawo wa mapato ya milangoni), lakini cha kushangaza wenzao wamewasaliti kwa kupeleka timu uwanjani.
Siku moja baada ya tukio hilo, aliyekuwa Katibu Mkuu wa CECAFA Nicolaus Musonye, alituita wanahabari kwenye ukumbi wa jengo la Millenium Tower, Mwenge, na ‘kuwaponda’ viongozi wa Yanga akidai kwamba wote wakiongozwa na Madega, ni dhaifu, na hawajitambui pamoja na kauli zingine nyingi zisizoandikika, huku wakiifungia Yanga kutoshiriki kwa miaka mitatu.
AIWEKEA NGUMU TBL
Ilikuwa mwaka 2008 ambapo Madega alikataa agizo la wadhamini wao TBL la kutaka waajiri watendaji kama mkataba wao ulivyokuwa unaelekeza.
Madega alisema kuwa hayo hayakuwa makubaliano, bali walikubaliana kuajiri Mweka Hazina kwa sababu hawakuwa na uwezo wa kuwalipa watendaji, kama vile Katibu.
Mvutano huo ulitokea kabla ya Shirikisho la Soka Duniani FIFA kutaka wanachama wake wote kuwa na watendaji wa kuajiriwa, ambapo mwaka 2010 Simba na Yanga zilianza kuajiri Maafisa Habari na Makatibu.
AMSHUSHUA NGASSA
Ilikuwa mwaka 2009 ambapo ilidaiwa kwamba mchezaji Mrisho Ngassa aliuomba uongozi umuongezee mshahara kwa sababu kipindi hicho alikuwa na uwezo mkubwa uwanjani kushinda hata baadhi ya wachezaji wa Kimataifa waliokuwa wanasajiliwa klabuni hapo.
Siku moja Madega alifanya mkutano na waandishi wa habari na kuchomekewa swali hilo, na katika majibu yake, alisema kwamba haiwezekani mchezaji anakwenda Yanga akiwa mnyenyekevu halafu baadaye anatanua mabega akitaka kuongezewa mshahara.
Aliongeza kwa kusema kwamba Ngassa kuna kipindi alikuwa akipewa Shilingi elfu tano tu anatetemeka, hivyo asijifanye ana thamani sana, na badala yake akumbuke alipotoka.
AWEKA MSIMAMO USAJILI WA NGASSA ULAYA
Kuna mwaka ziliibuka taarifa kwamba klabu ya Lov-ham ya Norway ilikuwa inamtaka Ngassa, lakini uongozi ulimzuia.
Madega alitoa ufafanuzi kwa kusema kwamba haiwezekani wakala akawa anazungumza na vyombo vya habari tu bila wao kujua, hivyo suala hilo ni uzushi kwa sababu taarifa rasmi hazijawafikia mezani.
AACHA MILIONI 200 KWENYE AKAUNTI
Mwaka 2010 baada ya muda wake kuisha ndani ya Yanga, Madega hakutaka kutetea tena kiti chake na kuwaachia wengine wagombee. Katika taarifa yake kwenye Mkutano Mkuu wa Uchaguzi, Madega alitangaza rasmi kwamba anaondoka, huku kwenye akaunti ya klabu akiwa ameacha zaidi ya shilingi milioni 200.
Hali hiyo ilimfanya awe Mwenyekiti pekee wa timu za Tanzania kuondoka madarakani na kuacha akaunti zikiwa zimenona.
Huyo ndiyo marehemu Imani Madega na harakati zake ndani ya Yanga. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.

Rate this item
(0 votes)
Last modified on Monday, 19 February 2024 07:08

Leave a comment

Make sure you enter all the required information, indicated by an asterisk (*). HTML code is not allowed.