Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

Historia ya Kanisa Barani Afrika

Na Askofu Method Kilaini

Katika safu hii wiki iliyopita, tuliendelea kuwaletea jinsi himaya za kipagani zilivyokuwa kigingi kwa wakristo na pingamizi toka kwa watawala wa enzi hizo. Leo tunaanza sehemu nyingine ya Historia ya Kanisa Afrika. Sasa Endelea…

UTANGULIZI
Afrika iliinjilishwa katika vipindi vitatu katika historia yake. Kipindi cha kwanza ni kuanzia siku ya Pentekoste hadi karne ya nane. Katika kipindi hiki nchi ya kwanza kuinjilishwa  ilikuwa ni Misri kufuatana na uhusiano wake wa karibu na Palestina. Kutoka Misri dini ilienea hadi Nubia ambayo sasa ni Sudan na Ethiopia au Abyssinia. Sehemu ya  pili kuinjilishwa ilikuwa Afrika ya Kaskazini ambayo ilikuwa inatawaliwa na Warumi.
Isipokuwa Ethiopia katika sehemu nyingine Ukristo ulitoweka au kudhoofika shauri ya Uislamu. Kipindi hiki kwa sehemu kubwa kilisimuliwa katika historia ya jumla ya kanisa.
Hapa tutaongelea kwa ufipi ili kuiunganisha na historia nyingine ya Afrika. Katika historia ya jumla tuliongelea sana juu ya dhuluma na mateso dhidi ya Wakristo kati ya mwaka 64 BK hadi mwaka 313 BK. Katika dhuluma hiyo Wakristo Waafrika wengi walikufa kwa ajili ya imani yao.
Vile vile katika historia jumla tuliongelea juu ya uzushi na mitaguso mbali mbali iliyojaribu kusuluhisha na kuleta umoja na amani ndani ya kanisa.
Kipindi cha pili kilikuwa katika karne ya 15 hadi 17. Wareno katika uvumbuzi wao na ukoloni waliambatana na wamisionari kuanzia Afrika ya Magharibi, ya kati, ya kusini na ya mashariki. Uinjilishaji wa kipindi hiki haukudumu isipokuwa katika sehemu chache sana kwa sababu ulitegemea sana nguvu za Wareno wakoloni. Ukoloni uliposhindwa na dini ilitoweka.
Kipindi cha tatu ni kuanzia karene ya 18 hadi sasa. Wamisionari Wakatoliki na Waprotestanti walijitosa bila kungojea wakoloni na kuwainjilisha Waafrika moja kwa moja hasa chini ya Sahara kwa mafanikio makubwa. Hadi leo Ukristo Afrika unakua kwa kasi kuliko bara lingine lo lote lile. Kipindi hiki ndicho cha uinjilishaji halisi wa Afrika.
KANISA LA MISRI
Misri ilikuwa na usataarabu miaka mingi sana kabla ya Kristo. Watu wemgi waliishi kwenye mwambao wa bahari ya Mediteranea na ukingo wa mto Nile. Nje ya hapo lilikuwa ni jangwa bila watu. Miaka 300 kabla ya Kristo Misri ilitekwa na Aleksanda Mkuu, mfalme huyu  Mgriki alijenga mji wa Aleksandria na kuingiza utamaduni wa Kigriki. Miaka 30 KK Misri ilitekwa na Warumi kisiasa lakini kiutamaduni ilibakia ya Kigriki kama sehemu nyingine za mashariki ya kati. Aleksandria ulikuwa mji wa pili kwa ukubwa na umaarufu katika dola ya Kirumi baada ya Roma. Hata hivyo huko Misri utamaduni wa Kigriki ulikuwa kwa ajili ya wasomi wachache, wengi hasa mashambani na nje ya miji walikuwa Wakopti, wengi wao wakiwa maskini.
Kwa zaidi ya miaka 2000 KK, Misri ilikuwa na uhusiano wa karibu na Palestina na Syria. Tunasoma katika biblia hata Ibrahimu na Yakobo walikwenda Misri. Wakati wa Kristo ikiwa chini ya Waruni ilikuwa na zaidi ya Wayahudi milioni moja na mji wa Aleksandira ulikuwa na Wayahudi zaidi ya 200,000 au 2/5 ya wakazi wa mji huo.
UINJILISHAJI WA MISRI
Katika Agano Jipya, Misri inatajwa mara kadhaa, kwa mfano Maria na Yoseph walimkimbiza mtoto Yesu Misri asiuawe na Herode, (Mt. 2:13); Simoni wa Kirene alitoka Misri (sehemu hiyo siku hizi iko Libya), (Lk. 23:26); na Apolo alikuwa mzaliwa wa Aleksandria (Mat. 18:24). Katika mapokeo ya mitume inaaminika kwamba Mtakatifu Tomaso akielekea India alipitia Misri na kuinjilisha na baadaye alikuwa mwinjilisti Marko aliyeinjilisha Misri na kufia huko kama shahidi.
Wamisri wa kwanza kuongoka walikuwa wale walioongea Kigriki hasa watu wa mataifa waliokuwa wamekubali desturi za Kiyahudi. Hawa tayari waliijua biblia ya Kigriki ‘Septuagint’. Kwa ajili yao biblia ilikuwa imetafriwa kutoka katika Kiebrania. Hawa Wamisri-Wagriki walianza kuelezea Ukristo katika lugha na falsafa ya Kigriki.
Aleksandria palifunguliwa shule maarufu ya dini chini ya Panteanus na baadaye ikawa na waalimu mashuhuri kama Clementi wa Alexandria na Origen. Katika kanisa la mwanzo kanisa la Aleksandria lilikuwa la pili kwa umaarufu baada ya Roma. Mwishowe askofu wa Aleksandria alitambuliwa kama patriarka akiwa na mamlaka karibu yote katika kanisa la Misri.
Mwishoni mwa karne ya pili Ukristo ulienea mashambani kati ya Wakopti. Mwaka 202 wakati wa mateso ya mfalme Kaizari Septimus Severus wanatajwa Wakristo Wakopti wengi waliouawa mashahidi kwa ajili ya imani yao. Katika dhuluma hiyo dhidi ya Ukristo, viongozi wa dini walipopelekwa uhamishoni mashambani kama adhabu, lilikuwa kosa lenye heri kwa sababu liliwapa fursa nzuri ya kuanzisha makanisa imara huko mashambani. Hata biblia ilitafsiriwa katika lugha ya Kikopti katika kilugha (dialect) cha Bohairic ambayo baadaye ilikuwa lugha rasmi ya kanisa la Kikopti na kanisa zima la Misri. Wakati Misri ilikuwa imetawaliwa na Warumi toka Roma au Konstantinopole, dini ndiyo iliwaunganisha katika utaifa wao.
 Wakati Wakristo wa Misri wa lugha ya Kigriki walichangia sana katika kuunda teologia ya kanisa zima la ulimwengu, Wakristo Wamisri - Wakopti walichangia katika kuanzisha umonaki wa wakaa pweke kama Paulo wa Thabes na Antoni wa Jangwani na umonaki wa monasteri kubwa ulioanzishwa na Pakomius. Mwishowe pole pole Wakristo wa Misri  walitengeneza utamaduni mmoja wa Kikopti na kuacha lugha ya Kigriki.
Ingawa kanisa la Misri lilijulikana kwa mafundisho yao sahihi likiongozwa na mapatriarka shupavu kama Aleksanda na Atanasio waliotetea Utatu Mtakatifu, bahati mbaya mwishowe alikuja patriarka Dioscorus aliyekosea na kufundisha kwamba Kristo ni Mungu tu ambaye  utu wake uliliwa na umungu wake. Huu ulikuwa ni uzushi wa monofisiti  uliopingwa na Mtaguso Mkuu wa Kalcedoni mwaka 451 BK.
Bahati mbaya kanisa la Misri wakati zamani lilifurahia ushindi katika mitaguso mbali mbali huko nyuma halikutaka kushindwa na kukubali uamuzi wa mtaguso nkuu huo bali lilijitenga. Kujitenga kwao kuliwagonganisha na kanisa la Konstantinopoli na wafalme wao na kuleta uhathama kati yake na kanisa la ulimwengu. Ingawa utengano ulisaidia kujenga kanisa imara la kitaifa, kanisa la Misri lilijifungia peke yake na kuwa kisiwa likiacha kuchangia katika mawazo ya ulimwengu yaliyolikuza hadi hapo.
Vile vile wamonaki ambao walikuwa ngome kubwa ya kanisa la Misiri bahati mbaya kufikia karne ya tano na kuendelea watu wengi mno wenye uwezo walikimbilia milimani na jangwani kuwa wamonaki wakaa pweke na miji ikabaki na watoto na wazee ambao hawakuweza kuendeleza nchi au kuilinda dhidi ya maadui.  Vile ile wamonaki hao mara nyingi walipokuja mjini wakati wa migongano na mafarakano, walitetea upande mmoja kisiasa na kufanya fujo na hili lilidhoofisha kanisa la Misri.
 Uislamu ulipokuja katika karne ya sita ulikuta kanisa limedhoofika na kutengana na kanisa la ulimwengu la Roma na Konstantinopoli. Siyo tu Kanisa la Kikopti la Misri halikuwa na nguvu ya kugigana na majeshi wa Waislaamu lakini mara nyingine liliungana nao kupigana na Wakristu wengine wa Konstantinopoli.
KANISA LA AFRIKA YA KASKAZINI
Afrika ya kaskazini ilikuwa sehemu ya mwambao yenye upana wa kilometa 320 kuanzia Libya ya leo hadi Morroco.  Mji mkuu wa sehemu hiyo ulikuwa Kartago, ulioanzishwa na wapuniki kutoka Lebanoni karibu miaka 1,000 Kabla ya Kristo, (KK).
Dola ya kipuniki ilienea hadi Sierra Leone. Baada ya vita vya karibu miaka 100, gemadali Mpuniki Hannibal alishindwa na Warumi mwaka 146KK. Warumi walipoteza sehemu kubwa ya dola na kubakia tu na sehemu ya upana wa kilomita 320 kwa sababu wao walijali tu kutunza mipaka kwa usalama wa dola yao.
Wakati wa dola ya Kirumi kuanzia mwaka 146 ustaarabu wa Kirumi uliletwa hasa na maaskari pamoja na wahamiaji wachache na kuenea sehemu zilizotekwa. Wapuniki kwa kiasi fulani waliingia katika utamaduni wa Kirumi lakini wazawa, Waberba, ambao leo tunawaita wabeduini wengi wao walibaki katika utamaduni wao. Hivyo utamaduni wa Kirumi au Kilatini ulibakia wa waja.
Itaendelea wiki ijayo.
UINJILISHAJI WA AFRIKA YA KASKAZINI
Mapokeo yanasimulia kwamba mtume Filipo aliinjilisha Kartago katika safari zake za kimisionari. Maandishi ya kwanza ya kuthibitisha Ukristo ni ya mwaka 180 BK ambapo watu 12 (wanaume saba na wanawake watano) walihukumiwa kuuawa wakati wa mateso ya Marko Aurelio kwa kukataa kumkana Yesu. Tangia hapo Afrika ilikuwa na mashahidi wengi waliofia dini. Mwanateologia maarufu, Tertullian aliandika kwamba ‘damu ya mashahidi ndiyo mbegu ya Ukristo’.
Kartago ulikuwa ndiyo mji wa fasihi ya Kilatini katika dola ya kirumi, wasomi wake walijivunia namna ya kuongea Kilatini kuliko hata katika mji wa Roma wenyewe. Vile vile walifundisha wanasheria wengi na stadi mpaka mji huo ukaitwa kiota cha wanasheria. Kanisa la Afrika Kaskazini lilifuata nyayo likawa kanisa la Kilatini na sheria.
Kanisa la Afrika ndilo lilitafsiri kwa mara ya kwanza Biblia Takatifu katika Kilatini. Kanisa lilitoa wanateologia wakubwa kama Tertullian, Cyprian na Augustino walioweka misingi ya teologia ya kanisa lote la magharibi au kanisa la Roma. Tertulian anaitwa baba wa teologia ya Kilatini. Wanateologia hawa wenye misingi ya kisheria walielezea mafundisho katika maneno ya msamiati wa kisheria yasiyo na ncha mbili au maana zenye utata. Ni kwa sababu hiyo kanisa la magharibi halikuwa na uzishi ya kinadharia bali uzushi wa utendaji na hukumu kati ya dhambi na haki pamoja na adhabu zake.
UZUSHI KATIKA KANISA LA AFRIKA YA KASKAZINI MAGHARIBI
Kwa sababu kanisa la Afrika ya kaskazini magharibi lilitwama juu ya sheria, hivyo hata teologia yake ilikuwa ya mambo ya kimatendo na si kinadharia. Hasa walitaka Mkristu aishi maisha ya utauwa kiasi kwamba ionekane tofauti kati ya maisha yake na yale ya wapagani. Bahati mbaya hii ilielekea kwenye dini kuwa na msimamo mkali na hivyo uzushi wa msimamo mkali ulipata ardhi nzuri ya kusitawi.
Uzushi wa Montanus ilifundisha juu ya maono binafsi kama chanzo cha imani ya kanisa. Ulisisitiza juu ya ulazima wa kuwa mashahidi hivyo ilikuwa dhambi kujificha au kukimbia. Mbaya zaidi walisistiza kwamba dhambi kubwa tatu yaani kuua, kuzini na kuabudu miungu zisingeliweza kuondolewa au kusamehewa. Mtu akifanya hizo dhanbi hawezi kusamehewa na kanisa au kushiriki tena na wanakanisa wenzake. Hii siasa kali iliwateka wengi Afrika akiwamo hata mwanateologia mkuu Tertullian. Uzushi huu ulisumbua kanisa la Afrika hadi Karne ya sita.
Uzushi mbaya zaidi ulikuwa ule wa Donatus. Kwake yule aliyetenda dhambi kama kumkana Kristu kwa woga wa kuuawa alipoteza ukristo wake na inabidi abatizwe upya. Vile vile sakramenti inayotolewa na yule aliye na dhambi si halari lazima irudiwe. Kwa namna hiyo wote waliopewa upadre na uaskofu na maaskofu waliokuwa wametoa vitabu vitakatifu vichomwe hawakuwatambua. Hili lilileta mgawanyiko mkubwa sana. Hawa wafuasi wa Donatus walianza kanisa lao na walikuwa na nguvu hasa mashambani. Ilichukua nguvu za Mtakatifu Augustino kwa maandishi yake (393-411) na majeshi ya Mfalme Kaizari Honorius (398) kuwashinda. Ila vita hivyo vilidhoofisha sana kanisa la Afrika hasa mashambani na kulibakiza kanisa la Warumi tu.
Uzushi mwingine ulikuwa ule wa Pelagius ambaye ili kuwapinga wale waliofanya dhambi bila kujali, kwa kisingizio kwamba binadamu ni dhaifu sababu ya dhambi ya asili ya Adamu na Hawa, alifundisha kwamba binadamu anaweza kwa nguvu zake tu kufanya mema akitaka. Waafrika wengi walimfuata. Mtakatifu Augustino aliandika sana juu ya neema ya Mungu kumpinga mpaka akaitwa ‘Daktari wa neema ya Mungu’.  Alitetea kwamba binadamu hawezi kufanya lolote jema bila msaada wa neema ya Mungu, ila Mungu anatupa neema yake kila mara na tuna uhuru wa kuipokea.
Uzushi wa Afrika ya kaskazini magharibi kama unavyoonyeshwa unatafuta ukweli juu ya matendo ya binadamu, lipi ni sahihi na lipi ni dhambi, mtu afanye nini ili aokoke na ni nani mwenye uwezo wa kutoa huduma za kanisa. Siyo maswali ya kifalsafa kama kanisa la Kigriki la Mashariki ikiwemo Misri bali ya kisheria au kiutendaji.
UVAMIZI WA WAVANDALI
Katika karne ya tano dola ya kirumi ilidhoofika na washenzi mipakani mwake wakaanza kuivamia. Dola ya Kirumi ya magharibi, ambayo ndiyo hasa dola ya Kirumi mji wake mkuu ukiwa Roma, ilisambaratika kabisa mwaka 476. Tangia hapo hapakuwapo tena utawala wa kuunganisha dola nzima hapo Roma. Kaizari wa mashariki, Konstantinopole aliendelea kudai kutawala dola yote lakini hakuwa na maaskari au miundombinu ya kutosha kuithibiti, kila mara ilitegemea nguvu alizokuwa nazo.
Wakati sehemu nyingine za Ulaya zilivamiwa na washenzi wapagani kama Wafranki, Wavisigoti,  Wahuni, Wasaksoni, Waburgundi na wengine; Afrika ilikuwa na bahati mbaya kuvamiwa na wavandali. Hawa walikuwa wabaya kuliko wote kwa sababu waliharibu kila kitu walichoona. Kwa lugha za wazungu kusema vandali maanake mharibifu (vandalism). Baada ya kupitia Spain walitua Afrika na kuharibu ustaarabu wote chini ya kiongozi wao Genseriki. Wakiwa wazushi Waariani waliwanyanganya wakatoliki makanisa yao yote na wakawapeleka maaskofu uhamishoni. Walikataza ibada na mafundisho yote ya Kikatoliki na waliokataa kutii amri hiyo waliuawa mashahidi. Walichangia sana kudhoofisha kanisa la Afrika. Majeshi ya Kaizari Justiniani wa mashariki, Konstantinopole, yaliwashinda Wavandari mwaka 535 na kuwafukuza lakini kanisa la Afrika ya Kaskazini halikupata nguvu tena mpaka walipovamiwa na Waislamu katika karne ya nane.

Rate this item
(0 votes)

Leave a comment

Make sure you enter all the required information, indicated by an asterisk (*). HTML code is not allowed.