Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

DAR ES SALAAM

Na Mathayo Kijazi

Vijana wameonywa kuacha kuiga tamaduni zisizofaa, ikiwemo wanaume kuvaa hereni na kusuka nywele zao.
Aidha, wametakiwa kudumu katika imani, wakitambua kwamba tamaduni hizo zinaweza kuwaingiza  kwenye dhambi.
Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu wakati wa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 98 katika Parokia ya Mtakatifu Fransisko Ksaveri – Chang’ombe, jimboni humo.
“Mnapopokea Sakramenti hii ya Kipaimara na mnatakiwa muendelee kudumu katika imani yenu, hivyo mnatakiwa kuepuka kuiga tamaduni zisizofaa, mfano, unamkuta mwanaume anavaa suruali anaweka mlegezo, anavaa hereni, anasuka nywele kichwani kama mwanamke. Epukeni kuiga tamaduni za namna hiyo,” alisema Askofu Mchamungu.
Pia, aliwasisitiza kujiepusha na tabia za udokozi pamoja na kutumia mali zisizokuwa za kwao, bali wahakikishe kwamba pale wanapookota vitu, wavirudishe kwa wenyewe.
Aliwasisitiza pia kuwajibika katika usafi pamoja na kutunza mazingira, akisema kuwa suala la usafi wa mazingira wao kama vijana, linatakiwa kuwa kipaumbele kwao.
Wakati huo huo Askofu Mchamungu aliwakumbusha Wasimamizi wa Waimarishwa hao kwamba miongoni mwa majukumu yao, ni pamoja na kusaidiana na Wazazi katika malezi, ili kujenga maadili ya vijana hao.
Kwa upande wake Paroko wa Parokia hiyo, Padri Novatus Mbaula alimshukuru Askofu Mchamungu kwa kufika parokiani hapo pamoja na kuwaimarisha vijana 98 wa Parokia hiyo.
Aidha, Padri Mbaula aliwasihi vijana hao kuendelea kuyazingatia yale yote waliyoambiwa na Askofu wakati wa homilia yake, kwani mafundisho hayo yatawasaidia kukua katika misingi iliyo bora.
Naye Katibu wa Parokia hiyo, Simon Sangawe alivishukuru vyombo vya habari vya Kanisa vilivyoshiriki katika Adhimisho hilo, ikiwemo Tumaini Media, akisema kuwa vyombo hivyo vinafanya kazi kubwa katika suala la uinjilishaji.

Dar es Salaam

Na Mwandishi wetu

Paroko Msaidizi wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Kalmeri, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Paul Mallewa, amesema kuwa Yesu akijitoa sadaka kwa ajili ya ukombozi, akiwasihi waamini kujisadaka na wao ili kuitangaza Injili yake Mwokozi.
Padri Mallewa alisema hayo wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Ekaristi Takatifu, iliyofanyika hivi karibuni parokiani hapo.
“Yesu amejitoa sadaka, nasi tunapaswa kujitoa sadaka kwa ajili ya changamoto katika maisha,”alisema Padri Mallewa.
Alisema kuwa Yesu aliulizwa na wanafunzi wake, ni wapi angependa wamuandalie ale Pasaka, lakini aliwatuma wanafunzi wawili akawambia waende wakakutana na kitu si cha kawaida, hasa kwa wanaume kubeba maji, enzi hizo ilikuwa jambo la kushangaza, kwani kazi hiyo ilikuwa ya wanawake.
“Katika maisha ya kawaida tunakuwa tumebeba mizigo mikubwa, isiyo ya kawaida…Waamini wa Bunju tunapaswa kujitoa kwa dhati, ili tuweze kula Pasaka na Yesu katika majitoleo yetu tunayotoa katika familia zetu,”alisema Padri Mallewa.
Alisema pia kuwa moja ya pasaka ya kula ya Yesu ni kujitoa kwa dhati kuchangia shughuli za Kanisa, kusudi Kristo mwenyewe abadilishe matoleo hayo na kuwa kama sadaka, kama ambavyo yeye alijitoa sadaka ili kuwakomboa wanadamu.
“Yeye ataibadilisha sadaka yetu na kuiweka katika mazingira yasiyo ya kawaida, na kuiweka katika sadaka ya mwili wake, ndipo na sisi tutabarikiwa,”aliongeza kusema Padri Mallewa.
Alibainisha pia kuwa Yesu, pia alitoa damu yake, yenye harufu nzuri ya upatanisho, na utakaso, ambayo inawaimarisha wanadamu wote, hasa wenye changamoto dhidi ya jirani zao na hata kuwa mbali na Kristo mwenyewe.
“Damu ya Kristo Yesu ina harufu nzuri ya upatanisho, harufu nzuri ya msamaha na kuoshwa dhambi zetu na kurudishwa katka hali ya kawaida, damu ambayo tuliipoteza kwa dhambi zetu,” alisema Padri Mallewa.
Naye Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Kalmeri, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Dominic Somola, alisema kuwa Pentekoste ni Utatu Mtakatifu, Mwili na Damu ya Bwana Yesu Kristo ambayo ni chimbuko la Kanisa.
Mkakati wa kukuza Watoto Kiimani
Padri Somola alisema kuwa kwa sasa Parokia hiyo ina mikakati mbalimbali ya kuendelea kutoa mafundisho, kwa watoto wadogo, hasa baada ya kupokea Sakranenti, kwani wengi hawafiki kwenda kusali, hasa baada ya kumalizia Masakramenti yao ya awali.
“Wazazi wapo wajitahidi kusimamia imani, kwani ni eneo mtambuka la malezi ya watoto. Sisi kama Parokia, tunajipanga kuhakikisha watoto wanaendelea na mafundisho baada ya kupata Masakramenti yao ya awali,”alisema Padri Somola.
Aidha, Padri Somola alitumia nafasi hiyo kuvishukuru Vyama vya Kitume, Kamati za Liturujia ngazi ya Parokia, kwa kufanikisha siku hiyo ya Ekaristi Takatifu.
Aliwapongeza watoto wote kwa kufanya vizuri mitihani yao ya mafundisho ya Kanisa, na hata wale ambao walifanya vibaya, aliwapa nafasi ikiwemo ya kuendelea kujifunza zaidi, Neno la Mungu.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu akiwa katika picha ya pamoja na Mapadri, Viongozi wa Kamati Tendaji pamoja na Waamini wengine baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 98 katika Parokia ya Mtakatifu Fransisko Ksaveri – Chang’ombe, jimboni humo. Kulia kwa Askofu, ni Paroko wa Parokia hiyo, Padri Novatus Mbaula. (Picha na Mathayo Kijazi)

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi (katikati mwenye Fimbo ya Kichungaji) na Mapadri, wakiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Kamati Tendaji ya Parokia ya Mtakatifu Maria De Mathias, Mivumoni, jimboni humo.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu (nyuma mwenye Fimbo ya Kichungaji) akiwa katika maandamano na Mapadri kutoka Parokia mbalimbali za Jimbo hilo wakiingia kanisani kwa Adhimisho la Misa Takatifu ya Uzinduzi wa Mwezi wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, Somo wa Tumaini Media, iliyoadhimishwa katika Parokia ya Kristo Mfalme, Tabata.

Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Padri Dominick Somola ambaye pia ni Dekano wa Dekania ya Mtakatifu Gaspar, (wa sita kulia), na Paroko Msaidizi wa Parokia hiyo, Padri Paul Mallewa (mwenye kanzu nyeupe), wakiwa katika picha ya pamoja na Wanakamati wa Zaka wa Parokia hiyo, baada ya Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa hivi karibuni parokiani hapo. (Picha zote na Yohana Kasosi)

DODOMA

Na Bartholomew Wandi

Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 hauko mbali sana kuanzia sasa, kwani ukipiga hesabu umebaki takribani muda wa mwaka mmoja (1) na miezi kadhaa hivi. Wananchi wengi ambao watafikisha miaka kumi na minane wakati wa jukumu hili, waliofikisha miaka kumi na minane (18) tayari na zaidi, na wale ambao waliokuwa na sifa zote za kuandikishwa mwaka 2020, lakini kutokana na sababu zisizoweza kuzuilika walikosa nafasi ya kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, wataandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Awamu ya Kwanza na ya pili  ya uboreshaji.
Mpaka sasa mikoa yote 25 Tanzania Bara tayari ina watu ambao wanahitaji kuandikishwa kuwa wapiga kura wenye sifa nilizozielezea hapo juu.Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni hitaji la kisheria na Kikatiba pia. Tume ya Taifa ya Uchaguzi, imepewa jukumu la kisheria kuandikisha wapiga kura katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuliboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na pia Madiwani Tanzania Bara.
Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utakuwa mahsusi kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura wapya, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao zilizokosewa awali, waliopoteza kadi za kupigia kura, wenye kadi zilizoharibika ili waweze kupata kadi nyingine,  na wale ambao wanataka kuhama Jimbo au Kata kwenda Jimbo au Kata nyingine ili waweze kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Kifungu cha 12 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inaeleza, “Mkurugenzi wa Uchaguzi ataweka, atatunza na kuboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililoanzishwa chini ya kifungu cha (1)”.
Kulingana na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, Kifungu cha 9 (2) inasema, “Bila kujali Masharti ya kifungu kidogo cha (1), na kwa kuzingatia uthibitisho wa umri , Mtanzania yeyote ambaye hajapoteza sifa chini ya Sheria hii au Sheria nyingine yoyote ya Bunge, na ambaye wakati au kabla ya tarehe ya Uchaguzi atatimiza umri wa miaka kumi na minane (18) atastahili kuandikishwa kuwa Mpiga Kura chini ya
Kifungu cha 13 (2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, pia inaeleza kwamba, “Tume itamwandikisha mtu yeyote Tanzania Zanzibar ambaye anastahili kuandikishwa kuwa mpiga kura katika Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano”.
Zaidi ya hayo, Ibara ya 5(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inafafanua, “Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane (18) anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti mengine ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi”.
Pamoja na hayo, pia Ibara ya 5(3)(a-d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, inaeleza kuwa Bunge  litatunga sheria ya uchaguzi na kuweka masharti kuhusu kuanzisha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika Daftari hilo, kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga kura na kupiga kura, utaratibu wa kumwezesha mpiga kura aliyejiandikishwa sehemu moja kupiga kura sehemu nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa utaratibu huo, na kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.
Marekebisho ambayo yanapaswa  kuingizwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ni kuondoa wapiga kura waliojiandikisha zaidi ya mara moja, waliojiandikisha na huku wako chini ya umri wa miaka kumi na minane (18), waliofariki dunia  au kupoteza sifa ya kuwa wapiga kura kwa namna nyingine, kuwapa kadi za mpiga kura mpya waliopoteza kadi zao, kurekebisha taarifa za wapiga kura zilizokosewa awali,  na kuwaingiza waliofikisha umri wa miaka kumi na minane (18) na kuendelea.
Kifungu cha  16(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024 inasema, “Tume itakuwa na jukumu la kupanga muda na kupitia upya uandikishaji wa wapiga kura katika kila eneo la uchaguzi ndani ya jimbo”
Kwa mujibu wa kifungu cha 16 (5) cha  Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024, inaeleza kwamba Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika mara mbili kwa miaka mitano (5), yaani baada ya Uchaguzi Mkuu kupita, na kabla ya siku ya uteuzi.
Uchaguzi Mkuu wa Mwisho ulifanyika Oktoba 28 mwaka, 2020, na sasa Tume ipo kwenye maandalizi ya kuboresha Daftari hilo kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025. Mchakato wa Uboreshaji huo wa Daftari umeanza kwa kukagua vituo vilivyotumika kuandikishia Wapiga Kura mwaka 2019/2020.
Uhakiki huo wa vituo hivyo vya kuandikishia wapiga kura, unalenga kuona kama kuna haja ya kuongeza vituo, kuona kama vilivyopo bado vinakidhi matakwa ya kisheria, na kufanya marekebisho mengine kama vile kubadilisha au kurekebisha majina ya vituo vilivyokosewa.
Matokeo ya uhakiki huo kwa Tanzania Bara yanaonesha kuwa, vituo vya kuandikisha wapiga kura vimeongezeka kutoka 37,814 hadi 40,126 ambapo kati ya vituo hivyo, 39,709 ni vya Tanzania Bara na vituo 417 ni vya Zanzibar.
Baada ya kazi ya kukagua vituo hivyo, Tume imefanya Uboreshaji wa majaribio (pilot) unaofanyika katika baadhi ya vituo vilivyoko kwenye halmashauri za Wilaya na Halmashauri za miji kwa  lengo la kujaribu kuona namna na jinsi vifaa vya uboreshaji vinavyofanya kazi katika mazingira tofauti, na kupata namna bora ya kufanikisha zoezi hili la uboreshaji.
Tume tayari imeshafanya uboreshaji wa majaribio katika kata ya Ikoma iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Rorya Mkoani Mara na Kata ya Ng’ambo iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Mkoani Tabora. Kata hizi zilichaguliwa ili kupata mazingira tofauti ya kijiografia, pamoja na idadi ya watu.
Uboreshaji huu wa majaribio umefanyika kwa mafanikio kutokana na kuboreshwa kwa vipuri na mfumo wa uandikishaji wa wapiga kura. Aidha, ilibainika kuwa betri mpya za BVR Kits zinao uwezo wa kuhifadhi chaji kwa muda mrefu, na hivyo zitaweza kukabiliana na changamoto ya nishati ya umeme katika baadhi ya maeneo ambayo hayana miundo mbinu hiyo.
Pamoja na mafanikio hayo kulikuwa na changamoto ndogo ya baadhi ya  wapiga kura kutokuwa na uhakika ama kukumbuka majina yao wanapokuja kurekebisha taarifa zao na hivyo kuchukua muda mrefu kituoni kutokana na kazi ya kutafuta majina yao kwa usahihi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi  itaendelea kuwaelekeza Wapiga Kura kuhakikisha wanakumbuka taarifa zao kwa usahihi ili waweze kuhudumiwa kwa haraka vituoni.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Jacobs Mwambegele wakati akiongea na Waandishi wa Habari Mjini unguja, Zanzibar, amesema kuwa uzinduzi rasmi wa Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura utafanyika Mkoa wa Kigoma tarehe 01 Julai, 2024.
Uboreshaji huo wa Daftari kwa Teknolojia ya BVR kwa mwaka huu 2024, hautakuwa tofauti na wa mwaka 2019/2020, ambao ulihusisha wananchi wote wapya wenye sifa za kuwa wapiga kura, waliohama jimbo au Kata, na ambao kadi zao zilipotea au kuharibika.
Wapiga kura ambao waliandikishwa mwaka 2015 na  2020 na wanazo kadi zao za kupigia kura na hazina matatizo yoyote, au hawajahama Jimbo/Kata kwenda Jimbo/Kata nyingine au hakuna mabadiliko yoyote ya mipaka ya kiutawala,  wanatakiwa pia kwenda katika vituo vya kuandikisha Wapiga Kura ili kuhakiki taarifa zao kwenye Daftari.
Kwa upande wa idadi ya Wapiga Kura watakaoandikishwa awamu hii, Tume imeshafanya makadirio kulingana na uandikishaji uliopita pamoja na matokeo ya Sensa ya watu na makazi uliofanyika mwezi wa Agosti mwaka huu, 2022.
Mhe. Jaji Mwambegele aliwaambia Waandishi wa Habari kuwa, makadirio ya Tume kwa kutumia ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ya Sensa ya Watu na Makazi, inatarajiwa idadi ya Wapiga Kura kuongezeka kufikia 34,746,638 kutoka 29,754,699 ya Wapiga Kura katika mwaka 2020, idadi hii itajumuisha wapiga kura wapya 5,586,433, sawa na asilimia 18.7 wanaotarajiwa kuandikishwa.
Pamoja na hayo, Mwnyekiti wa Tume anasema kuwa inakadiriwa Wapiga Kura 594,494 wataondolewa katika Daftari kwa kupoteza sifa na jumla ya Wapiga Kura 4,369,531 wataboresha taarifa zao. Hawa watakaoboresha ni wale ambao taarifa zao zilikosewa au wamehama kutoka Kata au Jimbo moja kwenda eneo lingine la Uchaguzi, na wengine ni wale ambao kadi zao zimeharibika au zimepotea.
Hata hivyo, Uboreshaji wa safari hii hautofautiana sana na ule wa mwaka 2015 na 2020, kwani Teknolojia itakayotumika ni ile ile ya kuchukua alama za kibaiolojia yaani Biometric Voters Registration (BVR), pamoja na Android.
Aidha, mabadililiko yanayotazamiwa ni kwa upande wa kupunguza ukubwa na uzito wa BVR Kits ambapo awali wakati wa uboreshaji wa Dafrari wa mwaka 2014/2015 na 2019/2020 BVR zilikuwa na uzito wa kilo 35 lakini kwa uboreshwaji wa mwaka huu kwa 2024/2025, uzito umepunguzwa  hadi kufikia kilo 18 ambapo yapo masanduku mawili, moja ni kwa kuhifadhia mashine ya BVR Kits, na lingine ni kuhifadhia vifaa vingine vya kuunganishia BVR Kit hiyo ikiwemo kishikwambi kwa ajili ya kupigia picha ya Mpiga Kura na kuchukulia alama za vidole, ila vifaa hivi vitatoa huduma ile ile ya kuandikisha wapiga kura na kutoa kadi hapo hapo kituoni.
Mabadiliko mengine katika Uboreshaji wa Daftari ni Tume kuanzisha mchakato wa uboreshaji kwa njia ya mtandao (Online) ambapo mpiga kura anaweza kuanzisha mchakato huu wa awali kwa njia ya mtandao ili kurekebisha, au kubadilisha taarifa zake, kuhamisha taarifa zake kutoka kituo cha awali kwenda kingine, au anayetaka kufanya vyote kwa pamoja.
ITAENDELEA WIKI IJAYO.
Wapiga kura wanaotaka kuboresha taarifa binafsi na wanaohama vituo au vyote viwili kwa wakati mmoja, wanaweza kuanzisha mchakato wa kuboresha taarifa zao kwa njia ya mfumo wa mtandao ‘online’ kuingia kwenye Tovuti ya Tume www.inec.go.tz kwa kutumia kompyuta au simu janja, kisha atabonyeza kiunganishi (link) iliyoandikwa Boresha Taarifa za Mpiga Kura, au atatumia anuani ya ovrs.nec.go.tz itakayompeleka moja kwa moja kuanzisha mchakato huo.
Katika mfumo huu, wapiga kura wanatakiwa kuingiza namba ya kitambulisho cha taifa (National Identity Number: NIN), namba ya kadi ya mpiga kura, namba ya simu anayotumia kwa sasa, na jina la Kata, kisha watapata ujumbe wenye namba za utambulisho (token namber) ambazo wataenda nazo kituoni ili kukamilisha taratibu za kupata kadi za mpiga kura.
Mwombaji ambaye ni mpya anatakiwa kwenda kituoni bila kuwa na kitambulisho cha aina yoyote kiinachomtambulisha ili aweze kupatiwa kadi ya mpiga kura. Mwaombaji huyu atakapofika kituoni atamwona Mwandishi Msidizi wa Kituo cha kuandikisha Wapiga Kura na  kuajaza fomu Na. 1,
Baada ya kujaza Fomu Na. 1, Mwombaji huyo Mpya atampatia Afisha Mwendesha Mashine ya Bayometriki (BVR Kits Operetor) ambaye ataingiza taarifa zake kwenye BVR Kit, atapigwa picha, atachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili  na kuweka saini na kupewa Kadi ya Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Kwa wapiga kura ambao walipoteza, kuharibika au kukosewa Kadi zao na ambao hawatajaza Online, watakapofika Kituoni, watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo , kisha Afisa Mwendesha Mashine ya Bayometriki ataingiza taarifa zao kwenye BVR Kit, akisha watapigwa picha, watachukuliwa alama za vidole kumi vya mikono yote miwili, na kuweka saini na mwishowe watapewa Kadi zao za Mpiga Kura hapo hapo kituoni.
Vile vile,, Wapiga Kura ambao wanataka kuhamisha taarifa zao, pia watajaza fomu Na. 5A kwa Mwandishi Msaidizi wa Kituo ili kuomba kuhamishiwa taarifa zao kwenda Jimbo au Kata na Kituo kingine cha Kupigia Kura wakati wa Uchaguzi Mkuu, na Chaguzi nyingine Ndogo zitakazofuata baada ya Uchaguzi Mkuu kupita.
Aidha, Mtu anatakiwa aende mwenyewe kituoni na anatakiwa kujiandikisha mara moja tu. Ni kosa la jinai kwa mwananchi yeyote kwa makusudi kwenda kituoni na kujiandikisha zaidi ya mara moja. Mwaka 2015, Kwa Mkoa mmoja tu wa Njombe, Kanzi Data hiyo imeweza kung’amua wapiga kura zaidi ya 600 waliojiandikisha zaidi ya mara moja, na walichukuliwa hatua za kisheria.
Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya Mwaka 2024,  kifungu cha 114(1)(b) inaeleza kuwa “kwa kujua au ana sababu ya kuamini kuwa ameandikishwa katika eneo la Uchaguzi anaomba kuandikishwa kinyume na kifungu cha 25, na bila kufichua kwa Msimamizi wa Uchaguzi kujiandikisha kwake kwa awali katika eneo jingine la Uchaguzi atenda kosa na akitiwa hatiani atapaswa kulipa faini isiyopungua shilingi laki moja na isiyozidi shilingi laki tatu au kifungo cha muda usiozidi Miaka miwili au vyote kwa pamoja”.
Baada ya zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaandaa Daftari la Awali la Wapiga Kura na kupelekwa mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) kwa ajili ya wapiga kura kuangalia kama majina yao yamo kwenye Daftari.
Kama baadhi ya majina hayaonekani, Wapiga Kura watamweleza Mwandishi Msaidizi kutoonekana kwa majina hayo na Mwandishi Msaidizi ataandika majina ya Wapiga kura hao waliokosekana kwenye Daftari la Awali na kisha ataleta orodha hiyo ya Majina Tume kwa ajili ya kuingizwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.
Pamoja na hayo, dhumuni lingine la Tume kupeleka Daftari la Awali la Wapiga Kura mikoani kwa ajili ya kuwekwa wazi (Display) ni kuwapa fursa Wapiga Kura kuangalia kama kuna majina ya Wapiga Kura walioandikishwa na hawana sifa kisha watawawekea pingamizi kwa kujaza fomu Na. 3B na kumkabidhi Mwandishi Msaidizi fomu hiyo ambaye ataileta Tume kwa ajili ya Wapiga Kura hao ili wafutwe kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kama kweli hawana sifa.
Hata hivyo, Majina hayo yaliyowekewa pingamizi hayafutwi moja kwa moja kwenye Kanzi Data ya Tume badala yake yanahifadhiwa sehemu nyingine kwenye Kanzi Data ili kama mtu huyo ana ushahidi wa kutosha kuwa ana sifa za kutosha kuandikishwa na kubaki kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura anarudishwa mara moja, Machapisho mbalimbali ya Elimu ya Mpiga Kura ya uhamasishaji ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura yatasambazwa nchi nzima  ili kuwaelimisha Wapiga Kura kuwa na uelewa na mwamko wa kujiandikisha kwa wingi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga kura.
Mchapisho hayo pia yanasistiza Wapiga Kura kutunza Kadi zao za kupigia kura na hatimaye kujitokeza kwa wingi kupiga Kura kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2025 utakapowadia na Chaguzi Ndogo zitakazofuata  na kila mmoja anatakiwa awe na Kadi yake ya kupigia kura.
Tume pia katika uhamasishaji wake wa Uboreshaji wa Daftari itatumia vyombo mbalimbali vya habari kama Magazeti, Radio kubwa na Radio za Kijamii, TV, INEC TV ONLINE, Tovuti ya Tume na Mitandao ya Kijamii, machapisho yakiwemo mabango, vijitabu na vipepeperushi, gari la Elimu ya Mpiga Kura na kushirikisha wadau kwa kutoa vibali kwa taasisi na asasi za kiraia.
Mwandishi wa Makala haya ni Afisa Habari Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) Simu  0754203015.

DA ES SALAAM

Na Mwandishi wetu

Msemo wa ‘Mtoto umleavyo, ndivyo akuavyo,’ una maana kubwa katika familia na jamii kwa ujumla.
Licha ya kwamba wengi wanadhani kuwa hayo ni maneno ya wahenga tu hayana maana yoyote, lakini ukweli ni kwamba kuzingatia malezi kwa watoto, ni jambo la msingi sana.
Tukitazama katika Taifa la Tanzania na Mataifa mengine duniani, kila mtoto ana tabia yake, lakini kwa undani, utaona kwamba tabia hiyo imetokana na malezi aliyoyapata kutoka wazazi au walezi wake.
Hivi karibuni gazeti Tumaini Letu lilipiga hodi katika Parokia ya Mtakatifu Vincent wa Paulo – Kibamba, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, kufanya mahojiano maalum na uongozi wa Parokia kuhusu mwenendo wa Parokia hiyo.
Pamoja na mambo mengine, wazazi wanaendelea kukumbushwa kutimiza wajibu wao katika suala zima la malezi, ili kuwajenga kimaadili watoto wao.
Padri Prijo Joseph, Paroko wa Parokia hiyo anasema kuwa wazazi wamepewa tunu au malaika, hivyo ni jukumu lao kuhakikisha kwamba malaika hao huko mbeleni hawabadiliki.
Wazazi kutokupata muda wa kutosha kukaa na watoto wao ili kupima tabia zao, imetajwa pia kwamba ni moja ya mambo makubwa yanayosababisha watoto kupoteza mwelekeo katika suala la maadili.
“Ni kutokana na changamoto za wazazi za kutokupata muda wa kukaa na watoto wao na kupima tabia zao, ndipo wengi hawafuatilii maedeleo ya kiroho ya watoto wao, badala yake, wanafuatilia tu maendeleo ya masomo ya shuleni, lakini mambo ya Mafundisho ya Kipaimara au Komunio, hawafuatilii.
“Kwa hiyo, tunaona vijana wengi wanakuja kanisani, lakini ukiwaambia wabaki kidogo kwa ajili ya semina au tafakari, unawaona wachache tu, wengine wanakimbia. Kwa hiyo, kama wazazi wangekuwa makini kuwahimiza watoto wao washiriki, basi wangeshiriki kwa wingi, kwa sababu mtoto akipata mafundisho ya imani, hawezi kuharibikiwa katika maisha yake, kwani atakuwa na hofu ya Mungu, atakuwa na moyo wa kutubu dhambi, na atakuwa msaada mkubwa kwa Parokia na Kanisa baadaye,”anasema Padri Prijo.
Padri huyo anaendelea kuwahimiza wazazi kwamba pamoja na jitihada zao za kuwasomesha watoto katika shule na vyuo, lakini pia ipo haja ya kuyaangalia maendeleo yao ya kiroho, kwani hata walioko vyuoni, baadhi yao hawaendi kanisani.
Licha ya changamoto hiyo katika malezi, Padri Prijo anawapongeza Waamini wa Kibamba kwa kuwa na mwitikio mzuri, kwani kunapokuwa na vikao, watu wengi hushiriki.
“Mwatikio wa Waamini katika Parokia hii ya Kibamba ni mzuri kwa kila jambo, kwani kukiwa na kikao au semina, watu wanajitahidi kuja kwa wingi;
“Lakini pia hata katika mafungo mwitikio ni mzuri sana. Sijawahi kupata shida na Waamini wa hapa, hasa katika masuala ya imani, hata katika mwitikio wa ibada za Misa na hasa kipindi cha Sikukuu wanajitahidi kuja kanisani,” anasema Padri Prijo.
Padri Prijo anasema kwamba Waamini wanatakiwa  kuendelea kujikita katika imani kama wanavyojipanga katika maisha ya kimwili, kwani imani ya mtu ndiyo inayomfanya asonge mbele.
Mwenendo wa Vyama vya Kitume:
Padri Prijo anasema kwamba ni mzuri, na mara kwa mara hukutana kwa ajili ya kujadili mambo mbalimbali yanayohusu vyama vyao ikiwemo kuvifanya viendelee kuwa hai.
“Lakini Viongozi kwa upande wao wanajitahidi, na vile vile chama cha Vincent wa Paulo, VIWAWA, na Utoto Mtakatifu. Chama cha Vincent wa Paulo mara kwa mara hapa wana utaratibu wa kugawa misaada kwa wahitaji,” anasema Padri.
Kutokana na idadi ndogo ya wanaume wanaoshiriki katika mambo mbalimbali ya Kanisa, Padri huyo anawasisitiza wanaume hao kwamba pamoja jitihada za kutafuta riziki kwa familia zao, bali pia wajitahidi kutenga muda kwa ajili ya kumkumbuka Mungu katika maisha yao.
Mambo ya kuwainua watu kimwili:
Akizungumzia mambo waliyoyafanya ya kuwainua watu kimwili tangu Parokia kuanzishwa, Katibu wa Parokia hiyo, Victor Rweyongeza anasema kuwa wameanzisha Msaada wa Kisheria bure, huduma za afya bila malipo, Semina za Afya ya Akili, uokoaji katika majanga ya moto, ambapo yote yanaratibiwa na Christian Professionals of Tanzania (CPT), yaani Wanataaluma Wakristo Tanzania ambao ni Waamini wa Parokia hiyo.
Katibu huyo anasema kwamba wamefanikiwa pia kuanzisha misaada kwa wahitaji kupitia Shirika la Mtakatifu Vincent wa Paulo kila mwezi, Pasaka, Noel, pamoja na Sherehe ya Parokia.
Pia, Katibu anasema kuwa Parokia hiyo hufanya semina za ujasiriamali na kujitambua kupitia tafakari za vijana siku za Dominika.
Kuhusu mambo waliyoyafanya ya kuwainua watu kiroho tangu Parokia imeanzishwa, Katibu huyo anasema kuwa Misa siku za Dominika zimeongezeka kutoka moja hadi tatu, Kuabudu Ekaristi Takatifu kila siku ya Alhamisi, pamoja na kujenga moyo wa Ibada, Liturujia.
Pamoja na hayo, anasema kuwa ushiriki katika Mafungo, Semina na Makongamano, ni mzuri, hasa kwa vijana na watoto Kiparokia, Kidekania, Kijimbo, na hata Kitaifa.
Kwa mujibu wa Katibu, Parokia hiyo imepiga hatua katika mafundisho ya watoto, kuanzia chekechea hadi darasa la nne kupitia mpango wa MADIDO (yaani Mafundiho ya Dini Dominika), huku darasa la tano na la sita wakifanya mafundisho ya Komunyo na Kipaimara, na baada ya Kipamimara, watoto hao huingia katika mpango mwingine wa MADIBAKI (Mafundisho ya Dini Baada ya Kipaimara)
Katibu huyo alizungumzia pia kuhusu Logos, ambapo anabainisha kwamba Masomo ya Biblia kila mwaka yanachaguliwa, huku Waamini wakisoma, na kisha baadaye kufanya mitihani, na washindi katika mitihani hiyo hupewa zawadi siku ya Kipaimara.
Katika jitihada hizo za kuwainua watu kiroho, Parokia iliweka mikakati ya kupunguza uchumba sugu, huku ndoa zaidi ya 80 zikiwa zimefungwa ndani ya miaka miwili, yaani 2022 na 2023.
Aidha, Katibu Rweyongeza anasema kuwa Mapadre wanajitahidi kuzitembelea Jumuiya, ambapo kila wiki kuna Misa za Watakatifu Waombezi wa Jumuiya, huku Waamini katika Jumuiya hushiriki kwa pamoja.
Mipango ya kiuchumi, kijamii:
Akizungumzia mipango ya baadaye waliyo nayo kijamii na kiuchumi katika Parokia hiyo, Katibu Rweyongeza, anasema kuwa ni kuendeleza juhudi za kutoa huduma kupitia Vyama vya Kitume mbalimbali kwa kuzingatia karama zao, pamoja na kuanzisha shule na vyuo ili kutoa elimu bora.
Akizungumzia kiini cha eneo hilo kuanzishwa ujenzi wa kanisa, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Walei Parokia hiyo, Leonard Masige anasema kuwa ni kutokana na ongezeko la watu katika eneo la Kibamba lililoleta wito wa uinjilishaji, ndicho kikawa chanzo cha kuanzishwa kwa Parokia hiyo.
Mwenyekiti huyo anabainisha kuwa shauku ya kuwaleta watu karibu na Kristu, ndiyo ikawa sababu ya uwepo wa Parokia hiyo ambayo ilizaliwa kutoka Parokia ya Kibaha, kwani ilikuwa mbali kwa Waamini kuweza kupata huduma za kiroho.
Asili uasisi jina la Kibamba:
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Leonard Masige, neno Kibamba ni neno la Kizaramo lenye maana ya mmea unaofanana na mkonge ambao pia huitwa mkonge, pori. Mmea huo hupatikana mahali penye dalili za kichaka na bondeni kidogo.
“Chanzo cha Kibamba tulipo inaanzia eneo la Kibamba kwa Mangi ukitokea Kibaha upande wa kushoto, ukielekea bondeni kidogo kulikuwa na kichaka kidogo na kisima kidogo cha maji. Ilikuwa mtu akichota maji, akiulizwa amechota wapi, anasema ni pale kwenye Kibamba, na hapo ndipo ikawa chanzo cha jina Kibamba, lakini kabla ya hapo, inasemekana eneo lote hili la Kibamba lilijulikana Kibwegere,” anasema Mwenyekiti wa Parokia hiyo, Leonard Masige.
Changamoto zinazoikabili
“Sisi kwa kweli tunamshukuru Mungu, kwani hatuna tatizo la kurudi nyuma hadi sasa. Hii inatokana na mikakati mbalimbali tunayoifanya, hususani ushirikiano katika sala, kupitia Jumuiya Ndogo Ndogo, Kanda, na hata Parokia. Waamini wanashirikishwa katika kila kinachofanyika katika Parokia yao, na kweli wanayaona matunda ya kazi yao,”anasema Masige
Shughuli za kiuchumi Kibamba:
Kuhusu shughuli kubwa za kuwaingizia kipato chao Waamini wa Kibamba, Masige anabainisha kwamba Waamini hao wana shughuli nyingi za kiuchumi, ikiwa ni pamoja na kufanya biashara ndogo ndogo na kubwa, wakulima, wafugaji, waajiriwa wa taasisi mbalimbali za Serikali na Binafsi, pamoja na wajasiriamali.
Anasema kuwa ushirikiano wao pamoja na watu wa imani nyingine, ni mkubwa, akiongeza kwamba wanatoa huduma mbalimbali kupitia Waamini ambazo zinatolewa kwa watu wote bila kujali imani zao, ikiwemo huduma ya afya bila malipo, pamoja na msaada wa kisheria.
“Kwa ujumla, ushirikiano ni mzuri sana. Tunashirikiana vizuri, mfano mzuri ni wiki hii tulikwenda kufanya uinjilishaji kwenye Kanisa la SDA Kwembe, ambapo kwaya yetu ya Mtakatifu Vincent wa Paulo ilialikwa kwenye ujirani mwema na kushiriki vizuri,” alisema Mwenyekiti.
Parokia ya Mtakatifu Vincent wa Paulo – Kibamba, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, inapatikana katika Halmashauri ya Wilaya ya Ubungo, mkoani Dar es Salaam, huku ikiwa na Waamini takribani 6,000, Jumuiya 103, Kanda 15, pamoja na Kigango kimoja cha Mtakatifu Fransisko Ksaveri.

Waamini wa Parokia ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli, Bunju, Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, wakisali katika viwanja vya Parokia hiyo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sikukuu ya Ekaristi Takatifu iliyoadhimishwa parokiani hapo hivi karibuni.

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, akipokea zawadi kutoka kwa Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Maria De Mathias,  Mivumoni, Padri Edwin Kigomba wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti ya Kipaimara iliyoadhimishwa parokiani hapo hivi karibuni.